Misiba ya Asili-Ni Ishara ya Nyakati?
“TAIFA litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali. Hayo yote ndiyo mwanzo wa utungu.” Kwa maneno hayo Yesu Kristo aliwaeleza wanafunzi wake karne 19 zilizopita kwamba matukio hayo yenye kuleta msiba, pamoja na ongezeko la uasi-sheria na kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote, yangeanzisha ishara yenye mambo mengi ikitia alama “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 24:3-14, linganisha na New World Translation.
Kwa sababu ya yale yaliyotajwa juu, ni lazima tuulize hivi, Je! tunaona matetemeko ya dunia, vimbunga, mafuriko, ukame, na njaa kali yenye kuleta msiba mkuu zaidi kuliko vizazi vilivyopita? Na kujapokuwa maendeleo katika sayansi na tekinolojia, je, watu wengi zaidi kwa kulinganisha wanateseka kwa sababu hiyo?
Kwa wengi jibu ni ndiyo. Kwa kielelezo, gazeti New Scientist laonya kwamba “ulimwengu waweza kutazamia misiba zaidi katika miaka ya 1990 kuliko katika miongo iliyopita.” Vivyo hivyo, katika jarida UN Chronicle la Juni 1991, mkurugenzi wa Shirika la Kimeteorolojia (upimaji wa hali ya hewa) Ulimwenguni alisema hivi: “Mwelekeo waonekana wazi kabisa. Kuanzia miaka ya 1960 hadi miaka ya 1980 . . . , kumekuwa na ongezeko la mara tano katika matukio ya misiba mikubwa ya asili, na ongezeko la mara tatu katika jumla ya hasara za kiuchumi.” Likiandaa maelezo zaidi kidogo juu ya habari hiyo, World Health, gazeti la Shirika la Afya Ulimwenguni la UM, lilionelea hivi: “Vielelezo vya misiba ya asili na matokeo yayo yenye uharibifu vyaweza kufuatishwa muda wote wa historia. Hata hivyo, karne ya 21 ikaribiapo, twakabili mchanganyiko wenye kubadilika katika hali za idadi ya watu, za kimazingira, na za kitekinolojia ambazo huenda zikafanya vikundi vingi vya watu vipatwe kwa urahisi na athari za maafa makuu ya asili na pia yenye kusababishwa na binadamu.”
Yeyote aelekezaye uangalifu kwenye matukio ya sasa hashangai kusikia taarifa kama hizo. Vyombo vya habari havipungukiwi kamwe na masimulizi yenye msisimuko, iwe ni mlipuko wa volkano katika Ufilipino, tetemeko la dunia katika Kalifornia, furiko katika Bangladesh, njaa kali katika Somalia, kimbunga katika Hawaii, au mawimbi makubwa mno katika Nikaragua. Hata mwezi haupiti bila ripoti juu ya msiba katika sehemu moja au nyingine ya ulimwengu.
Watu fulani hawaoni hilo kuwa jambo la maana. Wao hutoa hoja kwamba lile linaloonekana kuwa ongezeko katika misiba wakati wetu ni kwa sababu habari huripotiwa vizuri zaidi au rekodi huwekwa vizuri zaidi. Juu ya hayo wao hutoa hoja kwamba watu zaidi wanateseka kutokana na misiba kwa sababu tu kuna watu zaidi leo. Je! hoja hizo zasimulia mambo yote?
Angalia lile linalosemwa katika makala ya New Scientist iliyonukuliwa juu. “Kulikuwa na misiba 523 iliyoripotiwa katika miaka ya 1960 na 767 katika miaka ya 1970. Kufikia miaka ya 1980, idadi ilikuwa imefika 1387.” Laendelea kueleza kwamba “sehemu ya lile linaloonekana kuwa ongezeko katika mwongo uliopita yaweza kuwa kwa sababu ya ule unyoofu wa kadiri kubwa zaidi katika kuripoti misiba katika Uchina na Muungano wa Sovieti.” Kisha laongeza hivi: “Hata hivyo, idadi [ya misiba] inaongezeka.” Ongezeko la ghafula katika idadi ya misiba haliwezi kupunguziwa maana kwa kusemwa ni kwa sababu tu habari huripotiwa vizuri zaidi au rekodi huwekwa vizuri zaidi.
Zaidi ya hayo, jarida UN Chronicle la Machi 1992 laripoti hivi: “Katika miongo miwili iliyopita, watu wapatao milioni 3 wamepoteza uhai wao na milioni 800 zaidi wameathiriwa na ‘hasara, ugumu na kuteseka’ ambako kumeletwa na msiba wa asili.” Hilo lamaanisha kwamba karibu mtu 1 kati ya kila watu 7 wanaoishi duniani ameathiriwa na msiba au afa la aina fulani. Hilo lashtua kwelikweli na laacha msingi mdogo sana wa kuwa na shaka kwamba enzi yetu ni yenye msukosuko na mchafuko.
Kwa kuwa Biblia hutabiri wakati kama huo wenye msononeko mkuu, je, yamaanisha kwamba Mungu ndiye husababisha misiba na kule kuteseka kunakotokana nayo? Watu wengi hufikiri hivyo. Lakini mambo ya hakika huonyesha nini? Na la maana zaidi, Biblia huonyesha nini?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Cover: W. Faidley/Weatherstock
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Picha ya katikati: Mark Peters/Sipa Press
WHO/League of Red Cross