Kuchukuliwa Mbinguni—Je! Ni Fundisho Lililofunuliwa na Mungu?
UCHUKULIWA Mbinguni—fundisho kwamba Mariamu, mama wa Yesu alipaa mbinguni katika mwili wa nyama—hupendwa sana na mamilioni ya Wakatoliki Roma. Mwanahistoria George William Douglas asema hivi: “Kuchukuliwa Mbinguni kwa Bikira Mariamu kumeheshimiwa [kwa muda mrefu] kuwa mojayapo sikukuu zake kuu zaidi na mojayapo desturi kuu za mwaka wa Kanisa.”
Lakini, wanatheolojia Wakatoliki hukiri kwamba Biblia haisemi kwamba Mariamu alipaa mbinguni jinsi hiyo. Kwa kweli, Wakatoliki wachache hung’amua kwamba fundisho hilo lenye kupendwa sana limekuwa habari ya ubishi na jadiliano kali kwa muda wa karne nyingi. Kwa hiyo kanisa lilikujaje hasa kukubali fundisho la Kuchukuliwa Mbinguni kwa Mariamua? Je! kuna sababu yoyote ya kuliona kuwa limefunuliwa kimungu? Majibu ya maswali hayo si ya kiakili tu. Yana umaana wenye kina sana kwa wowote wapendao kweli.
Mageuzi ya Fundisho Fulani
Huenda ikakushangaza kujua kwamba katika karne za kwanza baada ya kifo cha Yesu, wazo la Kuchukuliwa Mbinguni kwa Mariamu halikujulika na hata kidogo na Wakristo. Mwanatheolojia Mkatoliki Jean Galot aandika hivi katika L’Osservatore Romano: “Mwanzoni, ukumbusho wa kifo cha Mariamu haukushirikishwa hata kidogo na jamii ya Kikristo.”
Hata hivyo, baada ya fundisho la Utatu kuwa fundisho rasmi la kanisa, Mariamu alianza kupewa fungu la maana zaidi na zaidi. Alianza kuitwa majina matukufu kama vile “Mama ya Mungu,” “mwenye kuchukuliwa mimba bila dhambi,” “Mpatanishi wa kike,” na “Malkia wa Mbingu.” Baadaye, mwanatheolojia Galot asababu hivi, “kutoelezwa sana kwa kifo cha Mariamu katika mapokeo ya kale hakungeweza kuwaridhisha kikamili wale Wakristo waliotambua ukamilifu wa Mariamu na waliotaka kumpa heshima ya kidini. Hivyo, masimulizi juu ya Kuchukuliwa Mbinguni, yaliyokuwa tokeo la mawazio-wazio ya wengi, yakafanyizwa.”
Karibu karne ya nne W.K., yale maandishi yaliyoitwa eti apokrifa za kuchukuliwa mbinguni yalianza kuenea. Maandishi hayo yalitoa masimulizi ya kuwazika tu juu ya kule kulikodhaniwa kuwa kupaa kwa Mariamu mbinguni. Kwa kielelezo, chukua maandishi yaitwayo “Kulala Usingizi kwa Mama Mtakatifu wa Mungu.” Yameonwa kuwa yaliandikwa na mtume Yohana mwenyewe, lakini yaelekea zaidi kwamba yaliandikwa karibu miaka 400 baada ya kifo cha Yohana. Kulingana na masimulizi hayo ya uwongo, mitume wa Kristo walikusanywa kwa Mariamu kimuujiza, ambako walimwona akiponya vipofu, viziwi, na vilema. Hatimaye, kama ilivyodaiwa hapo, mitume walimsikia Bwana akimwambia Mariamu hivi: “Tazama, tokea sasa mwili wako wenye thamani kubwa utahamishwa paradisoni, na nafsi yako takatifu itakuwa mbinguni katika hazina za Baba yangu katika uangavu wa kupita wote, ambako kuna amani na kushangilia kwa malaika watakatifu, na kuendelea kwa [kushangilia huko].”
Waamini waliitikiaje maandishi hayo? Mchunguzi wa Fundisho la Mariamu René Laurentin aeleza hivi: “Maitikio yalikuwa tofauti sana. Wale wepesi kuamini walidanganywa na uvutio wa simulizi hilo zuri, bila kufikiria zaidi. Wengine huchukia masimulizi hayo yasiyopatana, ambayo mara nyingi hupingana na hayana mamlaka.” Hivyo nadharia ya Kuchukuliwa Mbinguni haikukubaliwa rasmi kwa urahisi. Jambo jingine lililoongezea mvurugo huo ni kwamba yale yaliyodhaniwa kuwa masalio ya mwili wa Mariamu yalikuwa yakipewa heshima ya kiibada katika sehemu fulani-fulani. Haikuwa rahisi kupatanisha hilo na imani ya kwamba mwili wake wa nyama ulikuwa umechukuliwa mbinguni.
Katika karne ya 13, Thomas Aquinas, kama vile wanatheolojia wengi, aliendelea kuonyesha kwamba haikuwezekana kufasili kule Kuchukuliwa Mbinguni kuwa fundisho, kwa kuwa “Andiko halifundishi hilo.” Bado, imani hiyo iliendelea kupendwa na wengi zaidi, na michoro ya wasanii mashuhuri kama vile Raphael, Correggio, Titian, Carracci, na Rubens, iliyoonyesha kule kulikodhaniwa kuwa kuchukuliwa kwa Mariamu mbinguni, iliongezeka.
Suala hilo lilibaki likiwa halijasuluhishwa hadi hivi karibuni. Kulingana na Myesuiti Giuseppe Filograssi, baadaye sana kufikia sehemu ya kwanza ya karne yetu, wasomi Wakatoliki waliendelea kutangaza kwa chapa “mafunzo na mazungumzo ambayo hayakupendelea sikuzote” ile nadharia ya Kuchukuliwa Mbinguni. Hata papa wengi, kama vile Leo wa 13, Pius wa 10, na Benedict wa 15, “hawakusema mengi juu ya hilo.” Lakini katika Novemba 1, 1950, kanisa lilichukua msimamo thabiti hatimaye. Papa Pius wa 12 alitangaza hivi: “Twalifasili kuwa fundisho lililofunuliwa na Mungu kwamba Mama wa Mungu Mkingwa Dhambi ya Asili, Mariamu aliye Bikira sikuzote, alichukuliwa mwili na nafsi hadi katika utukufu wa mbingu, wakati mwendo wa uhai wake wa kidunia ulipofika mwisho.”—Munificentissimus Deus.
Imani katika safari ya Mariamu kwenda mbinguni katika mwili haikuwa ya hiari tena miongoni mwa Wakatoliki—sasa lilikuwa fundisho la Kanisa. Papa Pius wa 12 alijulisha kwamba “mtu yeyote . . . akithubutu kukanusha au kutilia shaka kwa hiari lile ambalo Sisi tumefasili, yeye apaswa ajue kwamba amepungukiwa na Imani ya Kimungu na ya Katoliki.”
Yale Ambayo Maandiko Husema Hasa
Kanisa lilichukua msimamo huo wenye ujasiri kwa msingi gani? Papa Pius wa 12 alidai kwamba fundisho la Kuchukuliwa Mbinguni lina “msingi walo hasa katika Andiko Takatifu.”[21a] Miongoni mwa maandiko yanayotajwa mara nyingi kuwa uthibitisho wa kuchukuliwa mbinguni kwa Mariamu ni Luka 1:28, 42. Mistari hiyo husema hivi juu ya Mariamu: “Salamu, mwenye neema nyingi, Bwana yu pamoja nawe: umebarikiwa miongoni mwa wanawake . . . , na zao la tumbo lako la uzazi limebarikiwa.” (Douay) Wale waaminio fundisho la kuchukuliwa mbinguni husababu kwamba kwa sababu Mariamu alikuwa “mwenye neema nyingi,” ni lazima awe hakupatwa kamwe na kifo. Na akiwa ‘amebarikiwa’ kama vile ‘zao la tumbo lake la uzazi,’ ni lazima awe ana mapendeleo yaliyo sawa na yale ya Yesu—kutia na kupaa kwake kimbingu. Je! waona hilo kuwa kusababu kuzuri?
Kwanza, wasomi wa lugha husema kwamba maneno “mwenye neema nyingi” ni tafsiri isiyo sahihi na kwamba maneno ya Kigiriki cha awali yaliyotumiwa na Luka yanafasiriwa kwa usahihi zaidi kuwa “kitu kilichoelekezewa upendeleo wa Mungu.” Hivyo Jerusalem Bible ya Katoliki hufasiri Luka 1:28 hivi: “Shangilia, mwenye kupendelewa sana!” Hakuna sababu ya kukata maneno kwamba Mariamu alichukuliwa mbinguni kimwili kwa sababu tu ‘alipendelewa sana’ na Mungu. Katika Biblia Katoliki ya Douay, Mkristo shahidi-mfia-imani wa kwanza, Stefano, alisemwa pia kuwa mwenye kupendelewa sana, au “mwenye neema nyingi”—naye hajapata kuonwa kuwa alifufuliwa kimwili.—Matendo 6:8.
Lakini, je, Mariamu hakubarikiwa au kupendelewa? Ndiyo, lakini kwa kupendeza, yule mwanamke aliyeitwa Yaeli huko nyuma katika siku za waamuzi wa Israeli alionwa kuwa “mwenye kubarikiwa miongoni mwa wanawake.” (Waamuzi 5:24, Dy) Kwa hakika hakuna mtu ambaye angetoa hoja kwamba Yaeli pia alichukuliwa mbinguni kimwili. Isitoshe, wazo lenyewe la Kuchukuliwa Mbinguni lategemea dhana la kwamba Yesu mwenyewe alipaa mbinguni katika mwili wa nyama. Hata hivyo, Biblia husema kwamba Yesu “alihuishwa,” au alifufuliwa, “katika roho.” (1 Petro 3:18, Dy; linganisha 1 Wakorintho 15:45.) Mtume Paulo asema zaidi kwamba “mwili wa nyama na damu haviwezi kumiliki ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 15:42-50, Dy.
Ni kweli, Biblia husema juu ya ufufuo wa kimbingu kwa ajili ya Wakristo waaminifu wapakwa kwa roho. Hata hivyo, 1 Wathesalonike 4:13-17 laonyesha wazi kwamba ufufuo huo usingeanza mpaka “kuwapo kwa Bwana,” (NW) katika siku za mwisho za enzi hii mbovu. Hadi wakati huo, Mariamu angelala usingizi katika kifo, pamoja na maelfu mengine ya Wakristo waaminifu.—1 Wakorintho 15:51, 52.
Mariamu—Mwanamke wa Imani
Hakikishiwa kwamba katika kusema yaliyotangulia hatukusudii kumvunjia heshima Mariamu. Bila shaka, Mariamu alikuwa mwanamke mwenye kielelezo kizuri—ambaye imani yake yastahili kuigwa. Alikubali kwa utayari pendeleo la kuwa mama wa Yesu, pamoja na majaribu na dhabihu ambazo zingetiwa ndani yalo. (Luka 1:38; 2:34, 35) Pamoja na Yusufu, yeye alimlea Yesu katika hekima ya kimungu. (Luka 2:51, 52) Alikaa pamoja na Yesu wakati wa kuteseka kwake juu ya mti. (Yohana 19:25-27) Na akiwa mwanafunzi mwaminifu, alibaki Yerusalemu kwa utiifu akapata kujionea kumwagiliwa kwa roho ya Mungu katika Pentekoste.—Matendo 1:13, 14; 2:1-4.
Maoni yasiyo sahihi juu ya Mariamu hayamheshimu wala Muumbaji wala Mariamu. Fundisho la Kuchukuliwa Mbinguni lakazia lile dai lisilo na msingi kwamba Mariamu ni mwombezi kwa Mungu. Lakini je, Yesu Kristo alipata kukubali fundisho la jinsi hiyo wakati wowote? Tofauti na hilo, yeye alisema hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya.” (Yohana 14:6, 14; linganisha Matendo 4:12.) Ndiyo, Yesu Kristo peke yake, wala si Mariamu, ndiye mwombezi kwa Muumbaji. Ni kupitia Yesu—wala si Mariamu—kwamba sisi twapaswa tumwendee Mpaji-Uhai wetu ili kupata “msaada wakati wa uhitaji.”—Waebrania 4:16, Revised Standard Version, Catholic Edition.
Kukubali kweli kuhusu Mariamu kwaweza kuwa jambo la kuumiza wengine. Angalau, huenda hilo likamaanisha kuacha imani fulani za tangu zamani sana na mawazo yaliyothaminiwa sana. Hata hivyo, ingawa hiyo huumiza nyakati nyingine, kweli ‘humweka mtu huru’ hatimaye. (Yohana 8:32) Yesu alisema kwamba Baba yake alikuwa akitafuta wale ambao wangeabudu “katika roho na katika kweli.” (Yohana 4:24, Dy) Kwa Wakatoliki wenye mioyo myeupe, maneno hayo ni kama mwito mgumu.
[Maelezo ya Chini]
a Fundisho katika Dini ya Katoliki, tofauti na imani sahili, husemwa kuwa kweli iliyofanyizwa kwa uzito ama na baraza la maaskofu ama na “mamlaka ya kufundisha [ya papa] isiyokosea.” Miongoni mwa mafundisho yaliyofasiliwa hivyo na Kanisa Katoliki, ya karibuni zaidi ni lile la Kuchukuliwa Mbinguni kwa Mariamu.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
JE! MARIAMU ALIKUFA?
Je! Mariamu alikufa kihalisi kabla ya kule kunakodhaniwa kuwa kupaa kwake mbinguni? Wanatheolojia Wakatoliki hujipata wenyewe wakikabili mambo mawili magumu kuhusu suala hilo. Nuovo dizionario di teologia laonyesha kwamba “ingekuwa vigumu kumpa Mariamu hali ya kutoweza kufa, ambayo hata Kristo hakuwa nayo.” Kwa upande ule mwingine, kusema kwamba Mariamu alikufa kwatokeza suala lililo gumu vilevile. Mwanatheolojia Kari Børresen aonyesha kwamba “kifo ni adhabu ya dhambi ya awali, ambayo, kulingana na [fundisho la “Kuchukuliwa Mimba Akiwa Mkingwa Dhambi ya Asili”], haikumwathiri Mariamu.” Basi, kwa msingi huo, je, yeye angalikufa? Si ajabu kwamba Papa Pius wa 12 aliepuka kwa uangalifu suala lote kuhusu kifo cha Mariamu alipofasili fundisho la Kuchukuliwa Mbinguni.
Kwa furaha, fundisho la Biblia halina mvurugo huo. Haifundishi popote—wala haidokezi—kwamba Mariamu alikuwa zao la “kuchukuliwa mimba akiwa mkingwa dhambi ya asili.” Tofauti na hilo, hiyo huonyesha kwamba Mariamu alikuwa binadamu asiye mkamilifu mwenye uhitaji wa ukombozi. Kwa sababu hiyo, baada ya kuzaliwa kwa Yesu, alikwenda hekaluni akafanya toleo la dhambi kwa Mungu. (Mambo ya Walawi 12:1-8; Luka 2:22-24) Kama vile wanadamu wote wasio wakamilifu, Mariamu alikufa hatimaye.—Warumi 3:23; 6:23.
Kweli hiyo sahili yatofautiana kabisa na yale maswali yasiyojibika yanayotokezwa na lile fundisho la Kuchukuliwa Mbinguni.
[Picha katika ukurasa wa 26]
‘Kuchukuliwa Mbinguni kwa Bikira,’ iliyochorwa kwa rangi na Titian (c. [karibu] 1488-1576)
[Hisani]
Giraudon/Art Resource, N.Y.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Kwa kuleta toleo la dhambi kwenye Hekalu baada ya kuzaliwa kwa Yesu, Mariamu alijitangaza kuwa mwenye dhambi aliyehitaji ukombozi