Je! Haidhuru Jinsi Unavyoabudu?
MJI mmoja mdogo wa Afrika unachomwa na jua la adhuhuri. Kuna makelele ya ngoma zinazopigwa sana, ya nyimbo, na ya makofi yenye furaha kutoka kwenye bonde lililo karibu. Lakini hiyo si kitumbuizo cha kirafiki. Ni ibada ya kidesturi ya Kiafrika. Lakini makelele hayo yashindana na mchanganyiko wa sauti zinazotoka kwenye kanisa moja la karama lililo karibu. Huko, waabudu wenye kuchachawa “waponyesha” kimuujiza na kusema katika lugha. Kwenye mwisho mwingine wa mji kuna aina nyingine ya ibada. Ile sauti kubwa ya mwadhini akiwaita Waislamu wenzake waende kuswali.
Naam, ujitoaji wa kidini wa aina nyingi waweza kuonwa katika majiji na miji mingi ya Kiafrika. Kwa vizazi vingi, Waafrika waliridhika kufuata desturi zao wenyewe za kidini. Lakini wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wakaja, wakifuata majeshi ya mataifa tofauti-tofauti ya Ulaya, na wakajaribu kwa ukatili kufanya kila mtu “awe Mkristo”—kutia ndani hata majina yao.
Matokeo yakawa nini? Aina ya dini iliyochanganya mazoea na itikadi za kidesturi za Kiafrika na imani za kigeni za kidini. Kufikia leo waabudu wengi “Wakristo” hutumia hirizi na talasimu za kidesturi. Isitoshe, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo hawakuonyesha kabisa Ukristo wa kweli, nao wakaacha nyuma vizazi vilivyochukizwa. Kwa sehemu kubwa, wao wana hatia ya ule mtazamo ulioko miongoni mwa baadhi ya Waafrika leo, wa kutotaka kusikiliza Biblia.
Hata hivyo, aina nyingi za “Ukristo” zingali zinafuatwa sana leo. Katika miaka ya karibuni vikundi vya kidini vyenye karama hasa vimekuja kupendwa sana; dini za kuponya kupitia imani zimejaa. Mwandikaji mmoja wa gazeti alieleza juu ya uvutio wa makanisa hayo kwa kusema kwamba ‘wazo la Mwafrika la dini sanasana ni kwamba dini ni kumridhisha mtu. Kwa akili za Mwafrika, ni lazima dini iwe na uwezo wa kutosheleza binadamu moja kwa moja kimwili. Kwa hiyo, kwa Mwafrika anayeamini kwamba njia fulani za kiroho zinahitajika kwa karibu kila jambo, njia za dini za kiroho [au zenye kuponya kwa imani] zapatana na mahitaji ya njia yake ya maisha.’ Hata hivyo, inasikitisha kwamba makanisa mengi yenye karama yameanzishwa kwa wazi kuwa shughuli za kibiashara.
Kuna madhehebu ya kidini zaidi ya 6,000 leo yanayotenda katika Afrika. Labda umepata kuhisi kwamba dini hizo na madhehebu hayo yote yanaleta wokovu. Lakini swali kubwa ni hili, Mungu huhisije?
Je! Dini Yoyote Inaweza Kumpendeza Mungu?
Kwa kweli, Muumba wa ulimwengu wote mzima hangetuacha bila mwelekezo kwa habari hiyo. (Amosi 3:7; Matendo 17:26, 27) Na kuna ushuhuda mwingi sana kwamba mwelekezo wa kimungu waweza kupatikana katika Biblia. La, Biblia si kitabu cha wazungu, jinsi wengine wakiitavyo. Kwa kweli, hakuna mtu yeyote—Mwafrika au Mzungu—awezaye kusema Biblia ni kitabu chake. ‘Kila Andiko ni lenye pumzi ya Mungu,’ chasema 2 Timotheo 3:16. Mafundisho ya Biblia ya kweli na ya unyoofu, ukale wayo, kuokoka kwayo dhidi ya mashambulizi ya kikatili, unabii wayo wenye usahihi kabisa na kuenezwa kwayo duniani pote kusiko na kifani—hayo yote ni mathibitisho ya wazi kwamba iliandikwa kimungu.
Kitabu hicho chatufundisha nini? Kwanza, chatuambia kwamba kuna ‘Mungu mmoja wa pekee wa kweli.’ (Yohana 17:3) Basi ikiwa hivyo, dini zote zingewezaje kuwa na kweli? Je! vikundi vya kidini havipingani kwa mambo kama Mungu ni nani? Mwandikaji wa Biblia Yakobo alitaja “dini iliyo safi na ya kweli.” (Yakobo 1:27, Today’s English Version) Kama kuna uhitaji wa kutambua dini ya kweli, basi lazima pia kuwepo dini isiyo ya kweli au ya bandia. Jambo hilo lingepinga wazo la kwamba dini zote ni njia tofauti tu za kumfikia Mungu.
Viwango vya Muumba vya Ibada
Ni ipi njia ifaayo ya kumwabudu Mungu? Biblia yatufundisha kwamba ibada ya kweli inategemea ujuzi sahihi. Pindi moja nabii mkuu Yesu Kristo alimwambia mwanamke Msamaria hivi: “Ninyi mnaabudu msichokijua.” (Yohana 4:22) Je! yawezekana kwamba ndivyo ilivyo na wewe pia? Je! umepata kufundishwa kwamba Mungu Mweza Yote ana jina lake binafsi, Yehova? (Zaburi 83:18) Je! wajua makusudi yake ni nini kuhusu mwanadamu na dunia? (Mathayo 6:9, 10; Waefeso 1:9, 10; 3:11) Je! dini yako yakutolea tumaini halisi la wakati ujao ulio bora zaidi? Na ikiwa wajiona kuwa Mkristo, je, waweza kueleza itikadi zako kutoka kwenye Maandiko, ama hizo ni mapokeo tu ambayo hujachunguza vizuri?
Ukijikuta kwamba huna ujuzi sahihi, waweza kuupata kupitia funzo la Neno la Mungu, Biblia. Yehova Mungu atazamia waabudu wake wa kweli wafahamu yale ambayo Kitabu Kitakatifu chafundisha. Zaidi ya hayo, anawatazamia wakitumie kitabu hicho maishani mwao. Mtazamo wetu wapaswa kuwa kama ule wa mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zaburi 119:105) Dini yako imekusaidia kwa kadiri gani kujua na kuelewa Biblia?
Jambo jingine kuu katika ibada ya kweli ni imani katika Yesu Kristo, si akiwa tu nabii mkuu bali akiwa Mwana mzaliwa wa pekee wa Mungu. Maandiko yasema waziwazi kwamba Yesu ndiye “Mkuu wa uzima.” (Matendo 3:15; 4:12) Wengi husema kwamba wana imani kwa Yesu, lakini imani yao ni halisi kadiri gani? Imani ya kweli kwa Kristo yamaanisha kutii maagizo yake. Mungu mwenyewe alitia moyo jambo hilo aliposema hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.” (Marko 9:7) Hivyo, waabudu wa kweli hujitahidi kufuata nyayo za Yesu kwa ukaribu kadiri wawezavyo. (1 Petro 2:21) Njia moja wafanyavyo hivyo ni kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri peupe iliyoanzishwa na Yesu. (Mathayo 4:17; 10:5-7) Je! dini yako inakutia moyo ushiriki binafsi katika kazi hiyo?
Upendo ni takwa jingine la ibada ya kweli. Yehova Mungu atajwa kuwa wonyesho halisi wa upendo, na Yesu aliwaeleza wafuasi wake kwamba wangetambuliwa kwa upendo ambao wangeonyeshana. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 4:8) Kwa kufikiria yale mamilioni mengi ya watu wanaodai kuwa Wakristo leo, je, ulimwengu usingejaa upendo kabisa? Hata hivyo, kwa hakika ulimwengu wetu umekuwa mahali pasipo na upendo kabisa. Vita vimeua mamilioni ya watu katika karne hii pekee. Uhalifu na jeuri zaendelea kuongezeka. Kwa hiyo jiulize hivi, ‘Kama kila mtu angekuwa wa dini yangu, je, ulimwengu ungekuwa mahali penye upendo zaidi?’
Hatimaye, Biblia yaonyesha kwamba ni lazima waabudu wa kweli wasiwe sehemu ya ulimwengu usiomjua Mungu. Mungu alipotenga taifa la kale la Israeli lihifadhi ibada iliyo safi, aliwaonya watu wake waepuke kushirikiana kwa ukaribu na mataifa jirani yaliyopotoka. (Kumbukumbu la Torati 7:1-6) Kwenye Yohana 17:16, Kristo Yesu vilevile aliwaambia wafuasi wake hivi: “Wao si wa ulimwengu kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” Waabudu wa kweli wa Mungu hawashiriki katika siasa, ukosefu wa adili, biashara yenye pupa, au falsafa zozote zisizomheshimu Mungu. (Yohana 18:36; 1 Yohana 2:15-17) Wao hutii ile amri iliyoandikwa kwenye Warumi 12:2: “Msiifuatishe namna ya dunia hii.” Je! dini yako hukutia moyo ufanye hivyo?
Kuna Msaada
Naam, kwa kweli Mungu hufikiria jinsi unavyoabudu. Kwa maoni yake, kuna dini moja tu ya kweli. (Waefeso 4:4-6) Mazungumzo yetu mafupi yamegusia baadhi ya mambo makuu ya mafundisho ya Biblia. Mbona usijitahidi kujifunza hata mengi zaidi?
Haidhuru ulilelewa katika dini gani, Mashahidi wa Yehova waweza kukusaidia kwa habari hiyo ya dini. Wao wanajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya kazi yao kubwa ya kufundisha Biblia. Wao wamejitolea kusaidia watu wa jamii zote na wa malezi yote ya kidini wapate uelewevu wa kina zaidi wa Biblia. (Mithali 2:1-6) Wao huchapisha fasihi za Biblia zinazofanyiwa utafiti sana.a Kwa kweli, wao hata watakuja nyumbani mwako na kukufundisha wewe Biblia bila malipo. Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wakati huu wananufaika kutokana na programu hiyo ya kufundisha Biblia. Mbona usifanye hivyo wewe mwenyewe? Kwa kweli, ni muhimu ujifunze kwa sababu ni jambo la kufikiriwa sana jinsi unavyoabudu.
[Maelezo ya Chini]
a Kichapo kimoja kama hicho ni Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kilichotangazwa katika 1992 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Watu wengi wamethamini mazungumzo yacho ya akili na ya kisomi juu ya dini kuu za ulimwengu.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo hawakuonyesha kabisa Ukristo wa kweli
[Picha katika ukurasa wa 5]
Makanisa mengi yenye karama ni shughuli za kibiashara
[Picha katika ukurasa wa 6]
Imani kwa Yesu ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mashahidi wa Yehova husaidia mamilioni ya watu wapate ujuzi sahihi kupitia mafunzo ya Biblia nyumbani bila malipo