Mwenye Furaha Katika Udugu wa Kweli wa Ulimwenguni Pote
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WILLIE DAVIS
Katika 1934 ule Mshuko Mkuu wa Kiuchumi ulikuwa umebana ulimwengu, na Marekani ilikuwa na matatizo mengi ya kiuchumi. Nje ya Kituo cha Kutoa Msaada cha Prospect katika Cleveland, Ohio, kulikuwa na pambano kati ya polisi na Mkomunisti mmoja shupavu. Polisi huyo alimpiga risasi na kumuua Mkomunisti huyo na msimama-kando fulani, aliyekuwa nyanya yangu, Vinnie Williams.
WAKOMUNISTI walijaribu kufanya vifo hivyo viwe tukio la ubaguzi wa rangi, kwa kuwa nyanya yangu alikuwa mweusi na yule polisi alikuwa mweupe. Waligawanya makaratasi ya habari yaliyokuwa na vichwa kama “Polisi wa Cleveland Wenye Ubaguzi wa Rangi” na “Lipizeni Kisasi cha Vifo Hivi.” Wakomunisti walipanga na kushughulikia mazishi ya nyanya yangu. Nina picha za wabebaji wa jeneza—wote wakiwa weupe na wote wakiwa wanachama wa chama cha Ukomunisti. Kila mmoja ana ngumi iliyokunjwa na kuinuliwa juu kwa njia ambayo baadaye ilikuja kuwa ishara ya Uwezo wa Weusi.
Nyanya yangu alipokufa, binti yake alikuwa amenibeba tumboni mwake, na miezi minne baadaye nilizaliwa. Nililelewa nikiwa na matatizo ya usemi. Nisingeweza kuongea bila kugugumiza, kwa hiyo masomo yangu ya mapema yalitia ndani mazoezi ya usemi.
Wazazi wangu waliachana nikiwa na umri wa miaka mitano, na dada yangu nami tulilelewa na mama yetu. Nilipokuwa na miaka kumi, nilianza kuuza bidhaa baada ya saa za shule ili kusaidia familia kugharamia matumizi. Miaka miwili baadaye nilianza kufanya kazi kabla na baada ya saa za shule, hivyo nikawa mruzuku mkuu wa familia yetu. Mama alipolazwa hospitalini na kuhitaji mfululizo wa upasuaji, niliacha shule na kuanza kufanya kazi kwa wakati wote.
Najulishwa kwa Udugu
Katika 1944 mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimwachia mke wa binamu yangu kitabu “The Truth Shall Make You Free,” nami nikajihusisha na funzo la Biblia lililoanzishwa naye. Mwaka uo huo nilianza kuhudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika Kutaniko la Eastside. Mfunzi wa shule, Albert Cradock, vilevile alikuwa na tatizo lilelile la usemi nililokuwa nalo, lakini alikuwa amejifunza kulidhibiti. Alikuwa kitia moyo kama nini kwangu!
Majirani wetu sanasana walikuwa Waitalia, Wapoland, Wahungaria, na Wayahudi, na kutaniko lilifanyizwa na watu kutoka jamii hizo na hata jamii nyinginezo. Mke wa binamu yangu pamoja nami tulikuwa miongoni mwa Wamerekani Waafrika wa kwanza kushirikiana na kutaniko hilo ambalo hasa lilijaa weupe, lakini Mashahidi hawakutuonyesha ubaguzi wa rangi. Hakika, walikuwa wakinialika kwa ukawaida nikiwa mgeni kwa ajili ya mlo.
Katika 1956, nilihamia sehemu ya kusini mwa Marekani ili nitumike sehemu yenye uhitaji zaidi wa wahudumu. Pindi moja niliporudi kaskazini katika kipindi cha kiangazi kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya, ndugu wengi wa Cleveland walinijia na kuonyesha upendezi wao mchangamfu kwa utendaji wangu. Hangaiko lao lilinifundisha somo muhimu: Nyakati zote ‘usiangalie mambo yako mwenyewe, bali kuangalia mambo ya wengine.’—Wafilipi 2:4.
Kupanua Huduma ya Wakati Wote
Baada ya kutumika miaka mitatu katika kazi ya kuhubiri wakati wote nikiwa painia, katika Novemba 1959, nilialikwa kufanya kazi katika Betheli ya Brooklyn, makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika New York. Nilipewa mgawo wa kufanya kazi katika Idara ya Usafirishaji. Mwangalizi wa idara yangu, Klaus Jensen, na mshiriki wangu wa chumba, William Hannan, wote wawili wakiwa weupe, wakawa baba za kiroho kwangu. Kila mmoja wao alikuwa ametumika kwa karibu miaka 40 katika Betheli kufikia wakati nilipofika.
Katika miaka ya mapema ya 1960, kulikuwa na washiriki wapatao 600 wa familia ya Betheli, na karibu 20 walikuwa Wamarekani Waafrika. Kufikia wakati huo, Marekani ilikuwa imeanza kujawa na mizozo ya ubaguzi wa rangi, na hakukuwa na uhusiano mzuri kati ya jamii. Hata hivyo, Biblia yafundisha kwamba “Mungu hana upendeleo,” nasi pia hatupaswi kuwa na upendeleo. (Matendo 10:34, 35) Mazungumzo ya kiroho ambayo tulikuwa nayo mezani kila asubuhi katika Betheli yaliimarisha azimio letu la kukubali maoni ya Mungu kwa mambo kama hayo.—Zaburi 19:7.
Nilipokuwa nikitumika katika Betheli ya Brooklyn nilikutana na Lois Ruffin, painia mmoja kutoka Richmond, Virginia, nasi tukafunga ndoa katika 1964. Tuliazimia kubaki katika huduma ya wakati wote, kwa hiyo baada ya arusi yetu tulirudi sehemu ya kusini mwa Marekani. Kwanza tulitumika tukiwa mapainia wa pekee, na kisha katika 1965, niliombwa kufanya kazi ya mzunguko. Kwa miaka kumi iliyofuata, tulizuru makutaniko katika majimbo ya Kentucky, Texas, Louisiana, Alabama, Georgia, North Carolina, na Mississippi.
Jaribu kwa Udugu Wetu
Hiyo ilikuwa miaka ya mabadiliko makubwa. Kabla ya kuhamia Kusini, jamii za rangi tofauti zilikuwa zimetenganishwa. Weusi hawakukubaliwa na sheria kuhudhuria shule zilezile, kula katika mikahawa ileile, kulala katika hoteli zilezile, kununua vitu katika maduka yaleyale, au hata kunywa katika mifereji ileile ya maji pamoja na weupe. Lakini katika 1964 Bunge la Marekani lilipitisha Sheria ya Haki za Wananchi iliyopiga marufuku ubaguzi wa rangi katika sehemu za umma, kutia ndani hali ya usafiri. Kwa hiyo hakukuwa tena msingi wowote wa kisheria wa kuwa na ubaguzi wa rangi.
Basi maswali yalikuwa ni, Je, ndugu na dada zetu katika makutaniko ya weusi pekee na katika makutaniko ya weupe pekee wangechanganyikana na kuonyeshana upendo na shauku au mikazo kutoka jumuiya zao na hisia zilizokazwa ndani yao kutoka zamani zingewafanya wakatae kuchanganyikana kirangi? Ulikuwa mwito mgumu kutii amri hii ya Kimaandiko: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.”—Warumi 12:10.
Kwa kadiri kila mtu angeweza kukumbuka, maoni yaliyoenea, hasa katika sehemu ya Kusini, yalikuwa kwamba weusi walikuwa wa hali ya chini. Maoni hayo yalikuwa yamekazwa kikiki ndani ya akili za watu kwa karibu kila sehemu ya jumuiya, kutia na makanisa. Kwa hiyo haikuwa rahisi kwa weupe wengine kuona weusi kuwa wa hali sawa nao. Kwelikweli, huo ulikuwa wakati wa kutahini udugu wetu—kwa wote weusi na weupe.
Kwa furaha, kwa ujumla kulikuwa na itikio zuri sana kwa habari ya kuchanganyikana kwa makutaniko yetu. Maoni ya ukuu wa kijamii yaliyofundishwa kwa kukaziwa sana kwa karne nyingi yaliondolewa upesi. Lakini kuchanganyikana kulipoanza, akina ndugu walifurahi, wengi wao wakishangilia kwa kuweza kukutana pamoja.
Kwa kupendeza, hata watu wasio Mashahidi mara nyingi walishirikiana na hali ya kuchanganyikana katika makutaniko yetu. Kwa kielelezo, katika Lanett, Alabama, majirani waliokuwa karibu na Jumba la Ufalme waliulizwa ikiwa hawataki weusi waje kwenye mikutano yetu. Mama mmoja mweupe aliye mzee-mzee alitikisa mkono wa ndugu mweusi, akisema: “Karibu katika ujirani wetu na uabudu Mungu wako kama upendavyo!”
Ndugu Waaminifu Katika Ethiopia
Katika 1974 tulifurahi kupokea mazoezi ya mishonari kwa muda wa miezi mitano na nusu katika Watchtower Bible School of Gilead katika New York City. Wakati huo tulipewa mgawo wa kwenda nchi ya Afrika ya Ethiopia. Maliki, Haile Selassie, alikuwa tu ndipo amepinduliwa na kupata kifungo cha nyumbani. Kwa kuwa kazi yetu ya kuhubiri ilipigwa marufuku, tulithamini uhusiano wa karibu wenye uchangamfu wa udugu wetu wa Kikristo.
Tuliishi na kutumika pamoja na wengi wa wale ambao baadaye walifungwa gerezani kwa sababu ya kushikamana kwao na ibada ya kweli. Baadhi ya marafiki wetu wapendwa hata waliuawa. Adera Teshome alikuwa mzee mwenzangu katika kutaniko moja la jiji kuu la Ethiopia, Addis Ababa.a Baada ya kukaa gerezani kwa miaka mitatu, aliuawa. Ni wazi, mke wake alihuzunika sana. Lakini ilifurahisha kama nini miaka kadhaa baadaye kumwona akiwa mwenye shangwe akitumika akiwa painia!
Worku Abebe, ndugu mwingine mwenye imani, alihukumiwa kifo mara nane.b Lakini yeye hakutishika! Nilipomwona mara ya mwisho, alinionyesha masikio yake ambayo walinzi wa gereza walikuwa wamepiga-piga kwa sehemu za nyuma za bunduki zao. Yeye alisema kwa ucheshi kwamba kupigwa kwa sehemu za nyuma za bunduki kulikuwa kiamsha-kinywa, chakula cha mchana, na chakula cha jioni. Ingawa sasa amekufa, akina ndugu wangali wanamkumbuka sana kwa upendo.
Hailu Yemiru ni ndugu mwingine ninayemkumbuka kwa upendo sana.c Yeye alimwonyesha mke wake upendo mwingi sana. Mke wake alikamatwa, lakini kwa kuwa alikuwa mja mzito naye angejifungua karibuni, Hailu aliwaomba wakuu wa gereza achukue mahali pake katika jela. Baadaye, alikataa kuridhiana imani yake, naye akauawa.—Yohana 15:12, 13; Waefeso 5:28.
Kwa sababu ya hali ya kisiasa iliyokuwa ikidhoofika nchini Ethiopia, tulihamia Kenya katika 1976. Kwa miaka saba tulitumika katika kazi ya kusafiri, tukizuru ndugu katika nchi nyingi za Afrika Mashariki—kutia na Kenya, Ethiopia, Sudan, Shelisheli, Uganda, na Tanzania. Pia nilisafiri kwenda Burundi na Rwanda mara kadhaa nikiwa sehemu ya msafara wa kuongea na wakuu wa serikali kuhusu kuhalalishwa kwa kazi yetu katika nchi hizo.
Nilifurahi kurudi Ethiopia mnamo Januari 1992 kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa kwanza uliopata kufanywa huko baada ya kuondolewa kwa marufuku juu ya kazi yetu. Wengi wa wale watu zaidi ya 7,000 waliokuwapo hawakujuana, kwa kuwa awali ndugu walikuwa wakikutana katika vikundi vidogo pekee. Kila siku ya mkusanyiko, walio wengi walikuwapo muda wa saa mbili kabla programu haijaanza na kubaki mpaka jioni sana, wakifurahia udugu wetu wenye upendo.
Ukabila Washindwa
Kwa karne nyingi ukabila umeenea sana katika Afrika. Kwa kielelezo, katika Burundi na Rwanda, makabila makubwa zaidi, Wahutu na Watutsi, wamechukiana kwa muda mrefu. Tangu nchi hizo zipate uhuru kutoka Ubelgiji mwaka 1962, watu wa makabila hayo mawili wamekuwa wakichinjana pindi kwa pindi kwa maelfu. Kwa hiyo ilifurahisha kama nini kuona watu wa makabila hayo mawili ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova wakifanya kazi pamoja kwa amani! Upendo wa kweli wanaoonyeshana umetia wengine moyo wasikilize kweli za Biblia.
Vivyo hivyo, makabila katika Kenya yamekuwa na tofauti zao. Lakini kuna tofauti kama nini katika udugu wa Kikristo wa watu wa Yehova katika Kenya! Waweza kuona watu wa makabila tofauti-tofauti wakiabudu Mungu pamoja katika Majumba ya Ufalme. Imekuwa furaha yangu kuwaona wengi wa hao wakiacha chuki zao za kikabila na kuonyesha upendo wa kweli kwa ndugu na dada zao wa makabila mengine.
Nafurahia Udugu Wetu
Nitazamapo nyuma zaidi ya miaka 50 ya kushirikiana na tengenezo la Mungu, shukrani nyingi kwa Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo, hujaza moyo wangu. Kwa kweli imekuwa ajabu kuona mambo waliyoleta duniani! Hali hazijawa kamilifu miongoni mwa watu wa Mungu, wala haziko hivyo leo. Lakini haiwezi kutazamiwa kwamba mamia ya miaka ya mafundisho ya ubaguzi ya ulimwengu wa Shetani yaweza kufutwa mara moja tu. Kwani, tungali wasiokamilika.—Zaburi 51:5.
Nilinganishapo tengenezo la Yehova pamoja na ulimwengu, moyo wangu hujawa kwa uthamini sana kwa ajili ya udugu wetu wa kweli wa ulimwenguni pote. Ningali nakumbuka kwa upendo wale ndugu katika Cleveland, wote wakiwa weupe, walionilea katika kweli. Na nilipowaona ndugu katika sehemu ya kusini mwa Marekani, wote weupe kwa weusi, wakibadili hisia zao za ubaguzi na kutwaa upendo wa kidugu utokao moyoni, moyo wangu ulishangilia sana. Kisha kwenda Afrika na kujionea mwenyewe jinsi Neno la Yehova liwezavyo kufutilia chuki za kikabila kumenifanya nithamini hata zaidi udugu wetu wa ulimwenguni pote.
Kwa kweli, Mfalme Daudi alilitaja jambo hilo vema aliposema hivi: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”—Zaburi 133:1.
[Maelezo ya Chini]
a Picha za Adera Teshome na Hailu Yemiru zipo katika ukurasa wa 177 wa Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1994; maono ya Worku Abebe yasimuliwa katika kurasa 178-81.
b Picha za Adera Teshome na Hailu Yemiru zipo katika ukurasa wa 177 wa Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1994; maono ya Worku Abebe yasimuliwa katika kurasa 178-81.
c Picha za Adera Teshome na Hailu Yemiru zipo katika ukurasa wa 177 wa Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1994; maono ya Worku Abebe yasimuliwa katika kurasa 178-81.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mazishi ya nyanya yangu
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mashahidi Watutsi na Wahutu wakifanya kazi pamoja kwa amani
[Picha katika ukurasa wa 25]
Nikiwa na mke wangu, Lois