Njia ya Maisha Yenye Kusudi
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MELVA A. WIELAND
Katika Machi 1940, miezi michache baada ya kubatizwa, dada yangu Phyllis alinijia na kuniuliza: “Kwa nini usichukue upainia?” “Upainia?” nikauliza. “Unamaanisha kuhubiri wakati wote, karibu kila siku?”
‘NAWEZAJE kuwa painia,’ nikawaza, ‘nikiwa na ujuzi kidogo wa Biblia na fedha kidogo hata zaidi katika benki?’ Hata hivyo, swali la Phyllis lilifanya nianze kufikiri. Pia nilisali juu ya jambo hilo.
Mwishowe nikasababu, ‘Kwa nini nisimtumaini Mungu anapoahidi kutuhangaikia tukiutafuta kwanza Ufalme wake?’ (Mathayo 6:33) Kwa hiyo, katika Juni 1940, nilitoa taarifa ya kuacha kazi yangu ya kushona nguo. Halafu nikaandikia ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Australia, nikiomba mgawo wa upainia.
Mgawo Wangu wa Maisha
Majuma kadhaa baadaye nilipata jibu, lililosema kwamba ningepewa mgawo baada ya kuhudhuria mkusanyiko uliokuwa ufanywe kwenye uwanja wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Strathfield, kiungani mwa jiji kubwa zaidi la Australia, Sydney. Asubuhi iliyofuata baada ya mkusanyiko, niliripoti ofisini ili nipate mgawo wangu.
Mtu aliyekuwa ofisini akanieleza: “Sasa hivi tuna kazi nyingi sana katika chumba cha kufua nguo. Je, waweza kubaki na kusaidia kwa majuma kadhaa?” Hiyo ilikuwa katika Agosti 1940—na bado ninafanya kazi katika chumba cha kufua nguo! Wakati huo familia ya makao makuu ilikuwa ya watu 35 tu; sasa kuna 276.
Lakini huenda unajiuliza sababu inayonifanya nione kufanya kazi katika chumba cha kufua nguo kuwa “njia ya maisha yenye kusudi,” hasa kwa sababu hii imekuwa kazi yangu kwa zaidi ya miaka 50 sasa. Kabla ya kusimulia, acha nieleze juu ya mapendezi yangu ya awali.
Michezo Ikawa Njia ya Maisha
Nilizaliwa Melbourne katika Januari 1, 1914, nikiwa wa kwanza kwa watoto watano. Tulikuwa na wazazi wenye kutupenda walioishi kwa kanuni za hali ya juu na kutoa nidhamu ilipohitajiwa. Pia tulikuwa na yale yawezayo kuitwa malezi ya kidini ya kivivihivi, maana wazazi wetu hawakuwa wakienda kanisani. Hata hivyo, walisisitiza kwamba sisi watoto tuhudhurie masomo ya shule ya Jumapili ya Kanisa la Uingereza.
Nilipoacha shule katika 1928 na kuanza kazi ya kushona nguo, niliamua kutumia muda mwingi sana wa wakati wangu wa kupumzika kucheza michezo, nikiamini kwamba hii yaweza kunisaidia nishinde kuona haya. Nilijiunga na klabu cha tenisi na kucheza kwa mwaka mzima. Wakati wa kipupwe nilicheza mpira wa vikapu na besiboli, na wakati wa kiangazi nilikuwa kwa timu ya wanawake ya kricketi. Niliipenda sana kricketi, na nilifanyia bidii ustadi wangu ili niwe mtupaji mpira wa kasi zaidi ili nistahili kucheza mechi za mikoa.
Kusudi Tofauti na Michezo
Mapema maishani nilisumbuliwa na fundisho la kwamba Mungu mwenye upendo ana mahali paitwapo helo ambapo wale waliofanya mambo mabaya wangeteswa milele. Hili halikuonekana kuwa jambo la akili kwangu. Basi ebu wazia furaha yangu nilipojifunza katika Biblia bila kutazamia maana ya kweli ya “helo.” Hivi ndivyo ilivyotokea:
Dada yangu Phyllis, aliye mdogo wangu kwa miaka mitano, alipenda michezo pia, na tulikuwa kwa timu ileile ya wanawake ya kricketi. Katika 1936 mchezaji mwenzetu alimfahamisha Phyllis kwa kijana mmoja aliyeitwa Jim aliyejulikana kuwa mtu wa kidini sana. Muda si muda Jim akaanza kuzungumza na Phyllis juu ya mafundisho ya Biblia. Alishangaa. Angeniambia, “Yanaeleweka vizuri sana nayo yanapatana na akili.”
Wakati huo Phyllis na mimi tulishiriki chumba kimoja nyumbani, naye alijaribu kunivutia kwa yale Jim aliyokuwa akimwambia juu ya Ufalme wa Mungu. “Utatimiza yale serikali za wanadamu zimeshindwa kutimiza,” akanieleza kwa furaha sana. Hata hivyo, nilimbisha, nikisema kwamba hii ni dini nyingine tu ya kututatanisha na kwamba hakuna aliyejua kabisa juu ya wakati ujao. Lakini Phyllis alikuwa mwerevu na kuacha fasihi mahali-mahali chumbani, akitumaini kwamba nitazisoma.
Nilikuwa na udadisi wa kujua ni kwa nini Phyllis alikuwa mwenye shauku jinsi hii juu ya imani hii mpya, kwa hiyo siku moja nilichukua kijitabu. Kilikuwa na kichwa chenye kuvuta fikira Hereafter. ‘Nilifungua masikio yangu’ nilipokuwa nikipitia kurasa zacho na kuona neno “helo.” Kwa mshangao wangu, nilijifunza kwamba neno la Biblia “helo” linarejezea hasa kaburi la ujumla la wanadamu na kwamba watu wazuri na wabaya wote huenda huko. Pia nilijifunza kwamba helo si mahali pa mateso; wafu hawana fahamu na hawawezi kuhisi chochote.—Mhubiri 9:5, 10; Zaburi 146:3, 4.
Hili lilinielea, hasa wakati kijitabu hicho kilipoeleza kwamba Mungu mwenye upendo na mwenye uwezo ameahidi kuwafufua wafu kwa mwujiza uitwao ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Sasa nilitaka pia kuchunguza zaidi mambo ambayo Jim amekuwa akimwambia Phyllis. Nilipata tafsiri ya King James Version ndogo ambayo baba yangu alikuwa amenipa nilipokuwa mtoto na nikatazama maandiko yaliyoorodheshwa ndani ya kijitabu hicho. Haya yalithibitisha yaliyosemwa kuhusu helo na hali ya wafu.
Jambo jingine lililonishangaza lilikuwa kujifunza kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova. (Zaburi 83:18) Pia ningeweza kuona kwamba Mungu alikuwa na kusudi, au sababu, ya mambo yote aliyofanya au aliyoruhusu kutendeka. Haya yalinifanya nijiulize, ‘Kusudi langu hasa ni nini maishani?’ Tangu wakati huo na kuendelea nilianza kujiuliza kama lilikuwa jambo la maana kabisa kwangu kufuata michezo kwa uzito sana—na kupuuza mengine yote.
Kutenda kwa Kupatana na Matendo
Jim na Phyllis hawakujua kwamba mtazamo wangu wa maisha ulikuwa umebadilika, lakini walitambua wakati familia yetu ilialikwa kwenye karamu ya rafiki. Siku hizo, katika pindi kama hizo, wote waliokuwapo wangesimama, na divai ingetolewa kumtakia afya njema Mfalme wa Uingereza, na wote wangeinua glasi zao ili kuinywa divai hiyo. Hata hivyo, niliamua kubaki nikiwa nimeketi pamoja na Jim na Phyllis. Hawakuamini macho yao waliponiona nikiwa ningali nimeketi! Bila shaka, hatukutaka kuonyesha ukosefu wa heshima, lakini tukiwa Wakristo tulihisi kwamba tunapaswa kutokuwamo bila kushiriki katika sherehe kama hizo za utukuzo wa taifa.—Yohana 17:16.
Hata hivyo, wazazi wangu na washiriki wale wengine wa familia walichukizwa sana. Walisema kwamba hatukuwa waaminifu, au tuna kichaa—au yote mawili! Halafu, Phyllis na mimi tulipohudhuria sherehe ya kila mwaka ya kutukuza timu ya wanawake ya kricketi, jambo kama hilo lilitukia wakati wa sherehe za utukuzo wa taifa. Matokeo yalikuwa kwamba sote wawili tulijiondoa kwa timu hiyo. Jambo hili halikuwa gumu kama nilivyodhani lingelikuwa, maana nilikuwa nimetambua kwamba utii na uaminifu mshikamanifu wangu ni kwa Kristo Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu.
Phyllis sasa akanieleza kwamba nilihitaji kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida ili niijenge imani yangu kwa ujuzi zaidi wa Biblia. Wakati huo kulikuwa na kutaniko moja tu katika Melbourne, hivyo nikaanza kuhudhuria mikutano huko kila Jumapili alasiri. Baada ya muda mfupi nilikuwa nimesadiki kwamba hili ni tengenezo la Mungu la kweli la kidunia.
Upesi nilialikwa kushiriki katika utendaji wa kutaniko wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Mara ya kwanza nilisitasita, lakini Jumapili moja asubuhi niliamua kwenda ili nione tu jinsi ilivyofanywa. Nilipendezwa nilipogawiwa kushiriki na Shahidi mwenye ujuzi wa muda mrefu aliyezungumza akiwa na uhakika mwingi kwenye mlango wa kwanza na kupata usikilizaji bora kutoka kwa mwenye nyumba. Nikafikiri, ‘Hilo si jambo gumu sana, lakini ninahitaji mazoezi kabla ya kufanya vizuri kama alivyofanya.’ Basi wazia mshangao wangu wakati Shahidi huyo baada ya mlango huo wa kwanza, aliponiambia, “Sasa unaweza kwenda peke yako.”
“Peke yangu?” nikauliza kwa mshangao! “Haiwezekani kwamba unamaanisha hilo! Nitasema nini mtu akiniuliza swali nisilojua jibu?” Lakini mwenzi wangu alisisitiza. Kwa hiyo, nikiwa natetemeka kihalisi, nilienda peke yangu yeye alipokuwa akiendelea kutolea watu ushahidi upande ule mwingine wa barabara. Kwa njia fulani nilifaulu asubuhi hiyo.
Kuanzia hapo na kuendelea nilianza kushiriki kazi ya kuhubiri kila Jumapili asubuhi. Mtu aliponiuliza mlangoni swali nisiloweza kujibu, ningesema, “Nitalichunguza halafu nirudi nikujibu.” Kwa furaha, Yehova aliendelea kunipa nguvu na ujasiri ili niweze kuendelea na njia yangu mpya ya maisha yenye kusudi. Nikaweka maisha yangu wakfu kwake, na Oktoba 1939, nikabatizwa katika vidimbwi vya jiji la Melbourne. Muda mfupi baadaye, Phyllis aliyekuwa wakati huo ameolewa na Jim, akaniuliza kwa nini sikuanza upainia.
Kutumika Katika Tawi
Katika Januari 1941, muda mfupi baada ya kuanza kufanya kazi katika Betheli, kama tulivyoita ofisi ya tawi, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku katika Australia. Baadaye majeshi yalichukua Makao ya Betheli yetu katika Strathfield, na nilitumwa katika shamba la Sosaiti katika Ingleburn, karibu kilometa 48 nje ya jiji. Katika Juni 1943 mahakama yaliondolea Watch Tower Society shtaka hilo na kuondoa marufuku. Kufikia mwisho wa mwaka huo, watu 25 kati yetu tulialikwa tena kurudi Betheli ya Strathfield. Huko niliendelea kufanya kazi katika chumba cha kufua nguo, pamoja na kushiriki kazi nyinginezo kwenye makao.
Mwongo uliofuata ulionekana kupita haraka. Halafu katika 1956, niliolewa na Ted Wieland, mfanyakazi mwenzi katika Betheli. Ted alikuwa mtu mtulivu, mwenye saburi, na tulifurahi tulipopokea ukubali wa kuendelea kuishi Betheli tukiwa mume na mke. Sote wawili tulithamini njia yetu ya maisha yenye kusudi, tukifurahia pendeleo la kutumika katika tawi la Australia. Bila shaka, kutia na kazi yetu ya Betheli, tulikuwa na furaha ya kufanya kazi pamoja ya kusaidia wengine wawe wanafunzi wa Kristo. Unaweza kusoma mfano mmoja wa familia ya Weekes katika toleo la Amkeni! la Oktoba 22, 1993.
Maongezeko yenye kuendelea ya kuhubiri Ufalme yalihitaji kuongeza watu 10 au 12 tu kwa wafanyakazi wetu katika kipindi changu cha kwanza cha miaka 30 ya kukaa Betheli. Lakini hali zilibadilika haraka katika miaka ya 1970 tulipoanza kuchapa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! hapa. Ujenzi wa jengo jipya la matbaa ulianza katika Januari 1972. Baada ya muda mfupi matbaa ya tani 40 ilifika kutoka Japani, na kufikia 1973 tulikuwa tukichapa karibu magazeti 700,000 kila mwezi. Familia yetu ya Betheli sasa ikaanza kuwa kubwa kwelikweli.
Miaka ya 1970 iliniletea huzuni pia. Kwanza katika 1975, mume wangu mpendwa, Ted, akafa akiwa na umri wa miaka 80. Halafu, baadaye kabla ya mwaka mmoja kuisha, baba yangu aliyekuwa amezeeka akalala katika kifo. Nilipata faraja kubwa kutoka kwa Yehova na Neno lake, Biblia, na kutoka kwa ndugu na dada zangu wa kiroho. Katika wakati huu wenye huzuni maishani mwangu nilifaidika sana kwamba nilikuwa mwenye shughuli nyingi katika Betheli katika utendaji wangu wenye kusudi.
Hata hivyo, maisha yanaendelea, na kwa mara nyingine tena ninaanza kuhisi kuridhika na kupata baraka, sasa nikiwa mjane. Katika 1978, nilihudhuria mkusanyiko katika London, Uingereza, na baadaye nikatembelea makao makuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York. Kuwaona mamia ya ndugu na dada zangu wakifanya kazi kwa furaha hapo katika Betheli ya Brooklyn kumenichochea sana kufikia leo hii.
Miaka ya 1970 ilipofika mwisho, tulijulishwa kwamba mpanuko zaidi wa jengo tata la Betheli ya Australia ulikuwa ukipangwa. Hata hivyo, mpanuko haukuwa ufanyike katika Strathfield, ambapo hapakuwa na ardhi ya kutosha. Badala ya hivyo, jengo tata jingine kubwa zaidi lilikuwa lijengwe katika ardhi yetu katika Ingleburn, mahali nilipokuwa nimefanya kazi wakati wa marufuku mapema miaka ya 1940.
Kuendelea na Njia ya Maisha Yenye Kusudi
Tulichachawa jinsi gani katika Januari 1982 tulipohamia jengo letu jipya! Kwa kweli mwanzoni tulihuzunika kidogo kuacha mazingira tuliyoyazoea, lakini muda si muda tulisisimukia makao yetu mapya yenye vyumba vya kulala 73 vyenye kupendeza. Sasa badala ya kuona kuta za mawe na barabara za pambizoni, tunaona mashamba ya majani mabichi na miti, ng’ombe wanaolisha, na macheo na machweo matukufu ya jua—kikao chenye kupendeza sana.
Katika Machi 19, 1983, tulikuwa na wakfu wenye kufurahisha sana wa jengo tata jipya wakati wa vuli yenye kupendeza. Lloyd Barry wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kuchochea sana. Mimi binafsi nilithamini sana kuwa naye pamoja na mkeye wakati wa programu ya kuwekwa wakfu, maana nilikuwa nimefanya kazi pamoja nao katika Betheli ya Strathfield wakati sisi sote tulikuwa wachanga sana.
Maongezeko yenye kuendelea ya utendaji wa kuhubiri Ufalme yalifanya iwe lazima tupanue majengo yetu hapa katika Ingleburn. Katika 1987 ofisi ilipanuliwa. Halafu, katika Novemba 25, 1989, jengo jipya la makao la orofa tano na kiwanda kipya cha orofa tatu zilizoongezwa ziliwekwa wakfu. Tumeongezeka sana—kutoka wahudumu chini ya 4,000 katika Australia nilipoanza kuhudumu hadi kiasi kipatacho 59,000!
Karibuni zaidi tawi la Australia limefanywa kuwa moja ya Ofisi za Uhandisi za Kimkoa za Sosaiti tatu, pamoja na Japani na Ujerumani. Hii imefanya iwe lazima hata zaidi kupanua jengo tata la Betheli. Jengo jingine la ofisi la orofa tatu sasa limemalizika, na kazi inaendelea vizuri katika makao ya orofa tano, ambalo litakuwa na vyumba 80 zaidi kuwapa makao familia yetu inayoongezeka daima.
Katika chumba cha kufua nguo, tuna wafanyakazi wa kutosha, lakini mara nyingi mimi hukumbuka hiyo siku ya Agosti katika 1940 nilipoalikwa kusaidia katika idara hii kwa majuma mawili. Pia nafurahi sana kwamba majuma hayo mawili yameongezeka kuwa zaidi ya miaka 50 na kwamba Yehova Mungu aliongoza hatua zangu kwenye njia ya maisha yenye kusudi kama hii.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Nilipokuwa na umri wa miaka 25
[Picha katika ukurasa wa 23]
Siku yetu ya harusi katika 1956
[Picha katika ukurasa wa 24]
Katika 1938 dada yangu na mimi tulikuwa tumejitia sana katika michezo, lakini maisha yangu sasa ni yenye matokeo zaidi