Kutimiza Uhitaji wa Msingi wa Binadamu kwa Kutoa Pongezi
MANENO “Umefanya vizuri!” “Nimefurahia mafanikio yako!” au “Ulifanya kadiri uwezavyo; hongera” ya moyo mweupe huongeza sana hali ya kujiheshimu, hasa yatokapo kwa mtu unayemstahi sana. Wanadamu hufurahi wakipongezwa. Wakipongezwa, wao hufanya maendeleo na huwa wenye furaha. Hakika, pongezi linalostahiliwa ni muhimu sana kwa akili na moyo kama chakula bora kilivyo muhimu kwa mwili.
Kamusi moja yafafanua pongezi kuwa “kukubaliwa kwa mtu kuwa anastahili kufikiriwa au kupewa uangalifu” na “kuonwa au kupewa uangalifu kwa njia ya kipekee.” Neno hilo lahusiana kwa ukaribu na staha, hisia ya heshima sana, ambayo ikitolewa hutoa maana ya kadirio au changanuo lifaalo la mtu na kadiri ya pongezi astahiliyo.
Pongezi—Uhitaji wa Msingi
Kutoa pongezi inapostahiliwa ni jambo la akili na lifaalo. Yesu aliweka kigezo katika kielezi chake cha watumwa ambao bwana-mkubwa wao alikuwa amewapa mali zake. Akishukuru kwa ajili ya usimamizi mzuri kwa mali zake, yeye alisema: “Vema, mtumwa mwema na uaminifu.” (Mathayo 25:19-23) Hata hivyo, uungwana huu hupuuzwa mara nyingi sana. Kukosa kutoa pongezi hukandamiza shauku na hali ya kujifanyia mambo. Iona asema hivi: “Kupongezwa hukufanya uhisi unahitajika, unatakikana, na kuthaminiwa . . . Hukufanya uwe mwenye ujianzilishi. Ukipuuzwa, unahisi vibaya na kuvunjika moyo.” Patrick aongezea hivi: “Basi inakuwa vigumu kudumisha hali au matokeo bora.” Kwa hiyo, ni muhimu kama nini kwamba tujifunze jinsi na namna ya kutoa pongezi. Sisi sote hutamani ule usalama wa kujua kwamba twakubalika na watu. Hilo ni uhitaji wa msingi wa binadamu.
Neno la kutoa sifa, madaraka yaliyoongezwa, au hata zawadi ya kimwili hukuchochea uendelee kufanya kadiri uwezavyo. Hilo ni kweli uwe mzazi, mume, mke, mtoto, mshiriki wa kutaniko, au mwangalizi. “Nipongezwapo,” asema Margaret, “mimi hufurahi, huona nahitajika, na kuwa na tamaa ya kufanya vema zaidi.” Andrew akubaliana na hilo, akisema: “Roho yangu huchachawa, ikinichochea kufanya kazi kwa bidii hata zaidi.” Hata hivyo, kutoa pongezi na kumstahi mtu huhitaji ufikirio wenye uangalifu na uamuzi mzuri.
Iga Kigezo cha Yehova Katika Kutoa Pongezi
Mfano mzuri zaidi wa kutambua hadhi ya wengine ni Yehova Mungu. Yeye hutakabali wale wanaostahili pongezi. Yeye alitakabali watu kama Abeli, Henoko, na Noa. (Mwanzo 4:4; 6:8; Yuda 14) Yehova alimtakabali Daudi kwa uaminifu wake wenye kutokeza sana. (2 Samweli 7:16) Samweli, aliyemheshimu Yehova kwa miaka mingi akiwa nabii, naye aliheshimiwa na Mungu, ambaye aliitikia haraka kwa sala ya Samweli ya kutaka msaada wa kushinda Wafilisti. (1 Samweli 7:7-13) Je, hungehisi kuwa umeheshimiwa kwa kutakabaliwa hivyo kimungu?
Shukrani na uthamini ni maneno yanayokaribiana sana na pongezi. Biblia hutuhimiza ‘tuwe watu wa shukrani’ na kuwa wenye uthamini kwa mambo yanayofanywa kwa niaba yetu. (Wakolosai 3:15; 1 Wathesalonike 5:18) Ingawa hili larejezea hasa kuwa mwenye shukrani kwa Yehova, ndivyo ilivyo na mambo ya kila siku ya maisha. Mtume Paulo alithamini hiyo. Yeye alimpongeza Fibi kuwa “msaidizi wa watu wengi” na kwa Priska na Akila kwa ‘kuwa tayari hata kukatwa kichwa’ kwa niaba yake na kwa niaba ya wengine. (Warumi 16:1-4) Ebu wazia jinsi lazima walihisi baada ya kupokea shukrani kama hiyo iliyotajwa waziwazi. Pia ilikuwa vema kwa Paulo kuwa na furaha ya kutoa pongezi, heshima, na kitia-moyo. Sisi vilevile twaweza kumwiga Yehova na waabudu wake wenye uthamini kwa kutoa pongezi ifaayo kwa wale wanaoistahili.—Matendo 20:35.
Kutoa Pongezi Katika Familia
“Pongezi kidogo hufanya maisha yafurahishe sana,” asema Mitchell, mume aliye pia mzee Mkristo. “Inakufanya umpende, labda kwa milele, yule anayekupongeza.” Kwa mfano, mume Mkristo huwa na mzigo mzito wa daraka na kufanya maamuzi mazito yanayohusu hali njema ya familia. Ni lazima aandae mahitaji ya kiroho, kimwili na ya kihisia-moyo ya familia. (1 Timotheo 5:8) Ana shukrani kama nini wakati anapopewa pongezi inayostahiliwa kwa mgawo wake aliopewa na Mungu akiwa kichwa cha familia na mkeye amwonyeshapo ‘staha’!—Waefeso 5:33.
Kitu kisichopasa kupuuzwa ni kazi ya mke wa nyumbani, ambayo haionwi na wengi. Mawazo ya kisasa yaweza kushusha kazi hiyo na kuinyang’anya staha na ustahili wayo. Lakini, ni kazi inayompendeza Mungu. (Tito 2:4, 5) Inafariji kama nini mume mwenye utambuzi amsifupo mke wake, hasa katika pande zote za maisha ambazo mke huyo hufanya vema zaidi, akimpa pongezi chini ya ukichwa wake! (Mithali 31:28) Rowena asema hivi juu ya mume wake: “Aonyeshapo shukrani kwa kile ninachofanya, napata ikiwa rahisi kumnyenyekea na kumheshimu na kumstahi.”
Pindi moja mwelimishaji Mmarekani Christian Bovee alisema hivi: “Sifa nzuri kwa watoto ni kama jua kwa maua.” Ndiyo, hata mtoto mchanga zaidi huhitaji uhakikisho wa kila mara kwamba yeye ni mshiriki wa familia anayethaminiwa. Katika miaka ya ukuzi wa utineja, iliyojawa mabadiliko ya kihisia-moyo na kimwili, kuna kujiona kulikoongezeka juu ya jinsi sura ilivyo, pamoja na tamaa ya kuwa huru na kupongezwa. Wakati huo hasa, tineja huhitaji kuhisi amependwa na wazazi wake na kutendewa kwa ufahamu na fadhili ya kibinadamu. Wazazi na babu na nyanya wanaozeeka vilevile huhitaji uhakikisho kwamba wao wangali ni wenye msaada na kupendwa, kwamba ‘hawajatupwa wakati wa uzee.’ (Zaburi 71:9; Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 23:22) Kuridhisha kabisa uhitaji wa kutoa pongezi huleta furaha iliyoongezeka na mafanikio kwa maisha ya familia.
Kutoa Pongezi Katika Kutaniko la Kikristo
Kuna thamani kubwa katika kusitawisha upendezi wa moyo mweupe kwa wengine katika kutaniko la Kikristo na kutoa pongezi kwa ukarimu kwa kuthamini kazi zao na jitihada zao. Wazee wa Kikristo wapaswa kuchukua uongozi kwa kutoa shukrani kwa matimizo na jitihada za wengine kutanikoni. “Ilikuwa baada tu ya kupokea ziara kadhaa za uchungaji ndipo nilipotambua kadiri [maneno yao ya pongezi] yalivyomaanisha kwa habari ya kitia-moyo, uradhi, na furaha,” akasema Margaret. “Nikang’amua yale mambo ambayo mtu hukosa asipopongezwa kwa ujumla.” Hiyo ni sababu nzuri kama nini ya kuonyesha upendezi wa binafsi ulio wa kweli na wenye upendo kwa wote kutanikoni! Tambua kazi yao nzuri. Pongeza na kutia moyo sana. Katika makutaniko mengi kuna wazazi wasio na wenzi wanaofanya kazi kwa bidii ili kukazia kikiki maadili ya kiroho kwa watoto wao. Wazazi kama hawa wanahitaji pongezi la pekee. Kazia mambo yafaayo badala ya mambo yasiyofaa. Acha wengine waone shauku yako ya kidugu kwao. Acha waone kwamba unajali. Kwa njia hiyo, waangalizi wenye upendo hufanya kazi ya bidii ili kujenga kutaniko. (2 Wakorintho 10:8) Washiriki mmoja-mmoja nao hutoa pongezi na staha istahiliwayo kwa waaminifu kama hao wanaofanya kazi kwa niaba yao.—1 Timotheo 5:17; Waebrania 13:17.
Lakini kuna upande mwingine wa jambo hili. Ni kweli kwamba tamaa ya kutaka kupongezwa huwa na nguvu sana. Katika siku za Yesu hiyo ilikuwa ndiyo kazi kubwa ya viongozi wa kidini. Ilikuwa lazima Yesu arekebishe maoni mabaya ya wanafunzi wake juu ya jambo hilo. (Marko 9:33-37; Luka 20:46) Wakristo huhitaji kuwa wenye ufikirio mzuri na wenye usawaziko. Isipoangaliwa, tamaa ya kutaka kupongezwa yaweza kuhatarisha kiroho. (Yakobo 3:14-16) Kwa mfano, laweza kuwa jambo lenye msiba kama nini ikiwa mzee anakuwa mwenye kiburi na kuanza kudai kwamba wengine wakubali jinsi anavyojitukuza mwenyewe!—Warumi 12:3.
Mtume Paulo aliwaonya kwa hekima Wakristo wenzi katika Roma: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.” (Warumi 12:10) Maneno haya hasa yanarejezea wazee wa Kikristo, ambao ni lazima siku zote watambue Kristo kuwa Kichwa cha kutaniko. Unyenyekeo kwa mkono wake wa kuume wenye mamlaka waonyeshwa kwa kutafuta kujua mwelekezo wa Kristo kwa njia ya roho takatifu, kanuni za Biblia, na uongozi utolewao na Baraza Linaloongoza la “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”—Mathayo 24:45-47; ona Ufunuo 1:16, 20; 2:1.
Kwa hiyo, wazee wakutanapo, nao wakisali wapate mwongozo wa Yehova wa kuchunga kundi la Mungu, wao watajitahidi kufanya maamuzi ambayo yanafaa Kimaandiko. Kiasi, upole, na unyenyekevu wa Kikristo utazuia mzee yeyote asijaribu kujitukuza mwenyewe, kutawala ndugu zake, na kuweka maoni yake katika mikutano hiyo. (Mathayo 20:25-27; Wakolosai 3:12) Iwezekanapo, ingefaa mwenyekiti wa baraza la wazee aombe maoni kwanza kutoka kwa wazee wenzake na kisha kutoa mapema sana orodha ya mambo ya kujadiliwa ili kuruhusu wakati wa ufikirio wenye uangalifu na sala kwa kila jambo lililoorodheshwa. Katika mikutano ya wazee, yeye hangejaribu kushawishi maoni ya wazee, bali angewatia moyo kutumia “uhuru mwingi wa usemi” kwa mambo yanayojadiliwa. (1 Timotheo 3:13) Wazee wenzi nao wapaswa kusikiliza kwa uangalifu maelezo ya mmoja na mwenzake na kunufaika kwa furaha kutokana na ufahamu wa ndani wa wazee ambao wana miaka mingi ya ujuzi wa Kikristo.—Kutoka 18:21, 22.
Hata hivyo, waangalizi wanaelewa kwamba Kristo aweza kutumia mzee yeyote katika baraza hilo kutumia kanuni za Biblia zinazohitajika kukabiliana na hali au kufanya uamuzi muhimu. Roho nzuri itaenea miongoni mwa baraza hilo wakati pongezi istahiliyo itolewapo kwa kila mzee kwa ajili ya mchango wake katika kutunza masilahi ya kiroho ya kutaniko.—Matendo 15:6-15; Wafilipi 2:19, 20.
Jitahidi Kutoa na Kupata Pongezi Linalostahiliwa
Pongezi hujenga. Hutia moyo nayo hupendeza. “Hata kama tunahisi sisi ni watu wa kawaida tu,” asema Mary, “twahitaji kitia-moyo kwa ajili ya ustahi wetu wenyewe.” Kwa moyo mweupe toa shukrani kwa jitihada za kila siku za wengine. Kufanya hivyo hufanya maisha yafae zaidi na kuwafurahishe. Wazazi, watoto, waangalizi, na washiriki wa kutaniko la Kikristo, mwaweza kupongezwa kwa jinsi mnavyosema na kutenda. Biblia husema kwa njia nzuri juu ya watu wanyenyekevu walio wenye bidii na kiasi. (Mithali 11:2; 29:23; Waebrania 6:1-12) Jifunze kutoa shukrani ya rehema kwa ustahili wa wengine. Fikiria hisia za wengine ufanyapo kazi pamoja nao. Mtume Petro alitoa onyo hili: “Mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitivu, wanyenyekevu.” (1 Petro 3:8) Hilo lahitaji kuwapa wengine pongezi, na hivyo kutimiza uhitaji wa msingi wa binadamu.