Wameungana Katika Kifungo Kikamilifu cha Upendo
“[M]kiunganishwa katika upendo.”—WAKOLOSAI 2:2.
1, 2. Ni uvutano gani wenye kuleta mgawanyiko unaohisiwa leo hasa?
SIKILIZA! Sauti kubwa inayovuma kotekote mbinguni inasema: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Kila mwaka upitapo, ujumbe huo huzidi kuogofya wakazi wa dunia.
2 Mpinzani mkuu wa Yehova amejulikana kwa muda mrefu kuwa mkinzani (Shetani) na mchongezi (Ibilisi). Lakini mdanganyi huyu sasa amechukua fungu jingine baya—yeye amekuwa mungu mwenye hasira! Kwa nini? Kwa sababu alitupwa kutoka mbinguni na Mikaeli na malaika zake katika vita iliyoanza mbinguni katika 1914. (Ufunuo 12:7-9) Ibilisi anajua kwamba ana wakati mchache tu wa kuthibitisha wito wake wa ushindani kwamba anaweza kugeuza watu wote wasimwabudu Mungu. (Ayubu 1:11; 2:4, 5) Kwa kukosa njia ya kuponyokea, yeye na mashetani wake ni kama kundi la nyuki linalotoa ghadhabu yalo kwa umati mwingi usiotulia wa wanadamu.—Isaya 57:20.
3. Matokeo ya Shetani kushushwa yamekuwa nini katika wakati wetu?
3 Matukio hayo, yasiyoonekana kwa macho ya wanadamu, yaeleza sababu ya kuwapo kwa maadili mabaya miongoni mwa wanadamu. Hayo pia yanaeleza sababu ya jitihada kubwa za wanadamu za kuunganisha mataifa yanayogawanyika ambayo hayawezi kuishi pamoja kwa muungano. Vikundi vya kikabila hushambuliana kikatili, vikitokeza mamilioni ya watu wasio na makao. Si ajabu kwamba uhalifu unaongezeka kwa kiwango kisicho na kifani! Kama Yesu alivyotabiri, ‘upendo wa wanadamu wengi unapoa.’ Kila mahali uangaliapo, hakuna muungano na upendo katika wanadamu wasiotulia.—Mathayo 24:12.
4. Kwa nini watu wa Mungu wamo katika hatari ya kipekee?
4 Kwa sababu ya hali ya ulimwengu, sala ya Yesu kwa ajili ya wafuasi wake yawa na umaana zaidi: “Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Leo, “yule mwovu,” hasa anatoa hasira yake kwa wale “wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” (Ufunuo 12:17) Kama usingalikuwa utunzi wa Yehova wenye uangalifu na wenye upendo, Mashahidi wake waaminifu wangaliharibiwa kabisa. Uhai wetu wategemea kutumia kwetu kikamili maandalizi yote ambayo Mungu anaandaa kwa ajili ya usalama wetu na hali-njema yetu ya kiroho. Hilo latia kujikakamua kwetu kwa kupatana na utendaji Wake kupitia Kristo, kama vile mtume alivyohimiza katika Wakolosai 1:29, NW.
5, 6. Mtume Paulo alihisije juu ya Wakristo Wakolosai, na kwa nini andiko kuu la mwaka wa 1995 lafaa?
5 Ingawa yaelekea Paulo hakuwa amewaona uso kwa uso, yeye aliwapenda ndugu zake katika Kolosai. Yeye aliwaeleza hivi: “Natamani mngalijua hangaiko langu kubwa kwenu.” (Wakolosai 2:1, The New Testament in Modern English, cha J. B. Phillips) Kwa kuwa wafuasi wa Yesu si sehemu ya ulimwengu, “yule mwovu” angeendelea kujaribu kuvunja umoja wa akina ndugu kwa kupanda miongoni mwao roho ya ulimwengu. Habari ambazo Epafra alileta kutoka Kolosai zilionyesha kwamba jambo hili limekuwa likitendeka kwa kadiri fulani.
6 Mojapo mahangaiko makubwa ya Paulo kwa ndugu zake Wakristo yaweza kutajwa kifupi kwa maneno haya: “[M]kiunganishwa katika upendo.” Maneno yake yana umaana wa pekee leo, katika ulimwengu unaokosa kabisa umoja na upendo. Tukitii shauri la Paulo, tutafurahia utunzi wa Yehova. Pia tutapata nguvu ya roho yake maishani mwetu, ikituwezesha kukinza mikazo ya ulimwengu. Shauri hili ni lenye hekima kama nini! Kwa hiyo, Wakolosai 2:2 litakuwa andiko letu kuu la mwaka wa 1995.
7. Ni muungano gani unaopaswa kupatikana miongoni mwa Wakristo wa kweli?
7 Katika barua yake ya mapema kwa Wakorintho, mtume Paulo alitumia kielezi cha mwili wa binadamu. Yeye aliandika kwamba “kusiwe na faraka” katika kutaniko la Wakristo wapakwa-mafuta bali “viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe.” (1 Wakorintho 12:12, 24, 25) Ni kielezi kizuri kama nini! Viungo vyetu hutegemeana, kila kimoja kikiwa kimeunganishwa na mwili wetu mzima. Kanuni hiyo inatumika kwa ushirika wetu wa ulimwenguni pote wa akina ndugu, uliofanyizwa kwa watiwa-mafuta na mamilioni wanaotumaini kuishi katika dunia paradiso. Tusijiondoe kamwe kutoka kwa mwili wa Wakristo wenzetu tukaishi kivyetu! Ikitenda kupitia Kristo Yesu, roho ya Mungu hutububujikia sana kupitia ushirika pamoja na ndugu zetu.
Muungano Washikamana na Ujuzi
8, 9. (a) Ni nini jambo la msingi la kuchangia kwetu muungano kutanikoni? (b) Umepataje ujuzi kuhusu Kristo?
8 Mojapo mambo makuu ya Paulo lilikuwa kwamba muungano wa Kikristo washikamana na ujuzi, hasa ule unaohusu Kristo. Paulo aliandika kwamba Wakristo wapaswa ‘kuunganishwa katika upendo, wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri takatifu ya Mungu, yaani, Kristo.’ (Wakolosai 2:2) Tumetwaa ujuzi—mambo ya hakika—tangu tulipoanza kujifunza Neno la Mungu. Likiwa sehemu ya kufahamu jinsi mambo mengi hayo ya hakika yanavyopatana na kusudi la Mungu, twaona fungu muhimu la Yesu. “Ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa [“ujuzi,” NW] zimesitirika.”—Wakolosai 2:3.
9 Je, unahisi hivyo kuhusu Yesu na fungu lake katika kusudi la Mungu? Wengi katika Jumuiya ya Wakristo ni wepesi kutaja Yesu, wakidai kwamba wamemkubali na kwamba wameokolewa. Lakini kweli wao wamjua? Hasha, kwa kuwa walio wengi zaidi huamini fundisho lisilo la kimaandiko la Utatu. Wewe unajua kweli kwa habari hiyo na tena yaelekea sana una ujuzi mpana kuhusu mambo ambayo Yesu alisema na kufanya. Mamilioni ya watu wamesaidiwa kupata ujuzi huo kwa funzo lenye kuarifu kwa kutumia kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Na bado twahitaji kuongeza zaidi ujuzi wetu wa Yesu na njia zake.
10. Ujuzi uliositirika unapatikanaje kwetu?
10 Ile taarifa ya kwamba “hazina zote za hekima na ujuzi zimesitirika” katika Yesu haimaanishi kwamba hatuwezi kupata ujuzi kama huo. Badala ya hivyo, hiyo ni kama chimbo la madini lililochimbwa. Si lazima tuanze kutafuta eneo kubwa tukishindwa mahali tutakapoanza kuchimba. Tayari twajua—ujuzi kamili waanza na mambo yale yanayofunuliwa na Biblia kuhusu Yesu Kristo. Tuthaminipo kikamili zaidi fungu la Yesu katika kutimiza kusudi la Yehova, sisi hupata hazina ya hekima ya kweli na ujuzi sahihi. Kwa hiyo twahitaji kuendelea kuchimba kwa undani hata zaidi, tukitoa vito au vitu vya thamani zaidi vinavyopatikana kutoka chanzo hiki ambacho tayari tumechimba.—Mithali 2:1-5.
11. Tunaweza kuongezaje ujuzi wetu na hekima yetu kwa kutafakari juu ya Yesu? (Toa kielezi cha Yesu akiosha miguu ya wanafunzi wake, au tumia vielelezo vingine.)
11 Kwa mfano, huenda tukajua kwamba Yesu aliosha miguu ya mitume wake. (Yohana 13:1-20) Lakini, je, sisi tumepata kutafakari juu ya somo ambalo alikuwa akifundisha na mtazamo alioonyesha? Kwa kufanya hivyo, twaweza kutoa hazina ya hekima inayotusaidia—ndiyo, inayotuchochea—kubadili jinsi tunavyomtenda ndugu au dada ambaye utu wake umetuudhi kwa muda mrefu. Ama kama tumepewa mgawo ambao hatupendi sana, twaweza kuitikia kwa njia tofauti baada ya sisi kufahamu vizuri Yohana 13:14, 15. Hivyo ndivyo ujuzi na hekima huwa na uvutano kwetu. Kunaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine tujipatanishapo kwa ukaribu zaidi na ujuzi ulioongezeka wa Kristo? Labda kundi ‘litaunganishwa katika upendo.’a
Ukengeushi Waweza Kuharibu Muungano
12. Twahitaji kujilinda dhidi ya ujuzi gani?
12 Ikiwa ujuzi sahihi watusaidia ‘kuunganishwa katika upendo,’ matokeo yanakuwa nini kwa ule “uitwao ‘ujuzi’ isivyo kweli”? Jambo tofauti kabisa—ubishi, mzozo, na kuacha ile imani. Kwa hiyo ni lazima tulinde dhidi ya ujuzi wa uongo kama huo, kama Paulo alivyomwonya Timotheo. (1 Timotheo 6:20, 21, NW) Paulo aliandika vilevile: “Nasema neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”—Wakolosai 2:4, 8.
13, 14. (a) Kwa nini ndugu Wakolosai walikuwa hatarini kwa habari ya ujuzi? (b) Kwa nini wengine leo waweza kuhisi kwamba hawamo katika hatari kama hiyo?
13 Wakristo Wakolosai walizingirwa kwa uvutano hatari ambao kwa kweli uliitwa ujuzi isivyo kweli. Watu wengi waliokuwa ndani na viungani vya Kolosai waliheshimu sana falsafa za Kigiriki. Pia kulikuwa na Wayudaiza (wachanganyao Ukristo na itikadi za Dini ya Kiyahudi) waliotaka Wakristo wafuate Sheria ya Kimusa, kama vile siku zayo za sherehe na matakwa yayo ya ulaji. (Wakolosai 2:11, 16, 17) Paulo hakupinga ndugu zake wasipate ujuzi wa kweli, lakini wao walihitaji kuwa waangalifu ili mtu asiwafanye mateka, kwa kutumia maneno ya kushawishi ili kuwasadikisha wawe na mtazamo wa kibinadamu tu katika maisha na matendo. Unaelewa kwamba baadhi ya watu kutanikoni wakiacha ufikirio wao na maamuzi yao kuongozwa na mawazo na mitazamo kama hiyo ya maisha isiyo ya kimaandiko, hilo lingetenda dhidi ya muungano na upendo kati ya washiriki wa kutaniko.
14 ‘Ndiyo,’ huenda ukafikiri, ‘naona hatari iliyokabili Wakolosai, lakini mimi siko katika hatari ya kuvutiwa na mawazo ya Kigiriki, kama vile nafsi isiyoweza kufa au mungu aliye utatu; wala sioni hatari yoyote ya kushawishwa na sikukuu za kipagani za dini ya uongo niliyoacha.’ Sawa. Ni vizuri kusadiki kabisa ukuu wa kweli ya msingi inayofunuliwa kupitia Yesu na kupatikana katika Maandiko. Lakini, yawezekana kwamba tumo hatarini kwa falsafa nyinginezo au maoni ya kibinadamu yanayoenea leo?
15, 16. Ni mtazamo gani maishani uwezao kuathiri kufikiri kwa Mkristo?
15 Mtazamo mmoja kama huo umekuwapo kwa muda mrefu: “Sasa i wapi ahadi ya kuja kwake? Mababa zetu wamelala kwa pumziko lao, lakini kila kitu kinaendelea jinsi ambavyo tu imekuwa sikuzote.” (2 Petro 3:4, The New English Bible) Mtazamo huo waweza kuelezwa kwa maneno mengine, lakini ni uleule. Mathalani, mtu anaweza kusababu hivi, ‘Nilipojifunza kweli kwa mara ya kwanza miongo kadhaa iliyopita, mwisho “ulikuwa umekaribia sana.” Lakini bado haujafika, na ni nani ajuaye siku utakapokuja?’ Ni kweli kwamba hakuna mtu ajuaye mwisho utafika lini. Lakini, ebu ona maoni ambayo Yesu alituhimiza tuwe nayo: ‘Angalieni, kesheni, kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo.’—Marko 13:32, 33.
16 Lingekuwa hatari kama nini kuwa na maoni kama hayo, bila kujua siku ambayo mwisho utakuja, tukapangie kuwa na maisha kamili na yaliyo ya “kawaida”! Mtazamo huo waweza kuonyeshwa kwa njia tunayosababu, ‘Ni vizuri nichukue hatua itakayoniruhusu (au watoto wangu) kuwa na kazi-maisha yenye kuheshimika inayoleta mapato mazuri na kuniruhusu kufurahia maisha mazuri. Bila shaka, nitahudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki kadiri fulani katika kazi ya kuhubiri, lakini hakuna sababu ya kujikaza au kufanya dhabihu kubwa.’—Mathayo 24:38-42.
17, 18. Yesu na mitume walituhimiza tuwe na maoni gani?
17 Hata hivyo, haiwezi kukanwa kwamba Yesu na mitume wake walipendekeza tuishi kwa kujua umuhimu wa kufanya habari njema zihubiriwe, kujikakamua na kuwa tayari kujidhabihu. Paulo aliandika hivi: “Ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana, . . . na wale wanunuao, kama hawana kitu. Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.”—1 Wakorintho 7:29-31; Luka 13:23, 24; Wafilipi 3:13-15; Wakolosai 1:29; 1 Timotheo 4:10; 2 Timotheo 2:4; Ufunuo 22:20.
18 Bila kudokeza kamwe kwamba tuwe na mradi wa kuishi maisha yenye starehe, Paulo aliandika hivi akiwa amevuviwa: “Hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. . . . Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa, ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi.”—1 Timotheo 6:7-12.
19. Kutaniko huathiriwaje wakati wale waliomo ndani yalo wanapokubali maoni ambayo Yesu alitia moyo juu ya maisha?
19 Kutaniko likiwa limefanyizwa na Wakristo wenye bidii ambao wanajitahidi sana ‘kuungama maungamo mazuri ya peupe,’ matokeo ya kawaida ni muungano. Wao hawawi na mtazamo huu, ‘Una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi.’ (Luka 12:19) Badala ya hivyo, wao wameungana katika jitihada ileile, wakiwa tayari kujidhabihu ili wawe na ushiriki ulio kamili kwa kadiri iwezekanavyo katika kazi hii ambayo haitarudiwa tena.—Linganisha Wafilipi 1:27, 28.
Tutahadhari Dhidi ya Maneno ya Kushawishi
20. Ni eneo gani pia ambamo Wakristo waweza kudanganywa?
20 Bila shaka, kuna njia nyinginezo ambazo Wakristo waweza ‘kudanganywa kwa maneno yenye kushawishi’ au madanganyo matupu yanayovuruga ‘kuunganishwa kwetu katika upendo.’ Ofisi ya Watch Tower Society nchini Ujerumani iliandika hivi: “Kisa kimoja kilitokeza mzozano, huku wahubiri na hata wazee wakiunga mkono pande tofauti-tofauti juu ya aina za tiba zinazotumiwa na ndugu fulani.” Wao waliongezea hivi: “Kwa sababu ya njia nyingi zinazotumiwa na idadi kubwa za wagonjwa, hilo ni jambo la kubishaniwa na, ikiwa njia za therapiutiki zina madokezo ya uwasiliani-roho, hizo zaweza kuhatarisha.”—Waefeso 6:12.
21. Mkristo aweza kupotezaje uangalifu ufaao leo?
21 Wakristo wanataka kudumisha uhai na afya nzuri ili waweze kumwabudu Mungu. Hata hivyo, katika mfumo huu sisi huzeeka na kupatwa na magonjwa yanayotokana na kutokamilika. Badala ya kukazia mambo ya afya, twapaswa kukazia akili suluhisho kamili, kwetu na kwa wengine. (1 Timotheo 4:16) Kristo ndiye chanzo cha suluhisho hilo, kama alivyokaziwa fikira katika shauri la Paulo kwa Wakolosai. Lakini kumbuka, Paulo alionyesha kwamba wengine waweza kuja na “maneno ya kushawishi” wakiondoa uangalifu wetu kutoka kwa Kristo, labda kwa njia za kugundua magonjwa, tiba, au lishe.—Wakolosai 2:2-4.
22. Twapaswa kuwa na mtazamo gani wenye usawaziko kwa madai mengi yanayohusu njia za kugundua ugonjwa au za tiba?
22 Watu ulimwenguni pote hufurikwa kwa matangazo ya biashara na ushuhuda wa ubora wa aina zozote za tiba na njia za kutambua ugonjwa. Baadhi ya njia hizo zajulikana na kutumiwa sana; nyinginezo huchambuliwa sana au kutiliwa shaka.b Kila mtu ana daraka la kuamua kile atakachofanya kuhusu afya yake. Lakini wale wanaokubali shauri la Paulo linalopatikana kwenye Wakolosai 2:4, 8 watalindwa dhidi ya “maneno ya kushawishi” au “madanganyo matupu” yanayokengeusha wengi ambao, wakiwa hawana tumaini la Ufalme, wanatamani sana kupata kitulizo. Hata kama Mkristo amesadiki kabisa kwamba tiba ya aina fulani huonekana ikiwa nzuri kwake, yeye hapaswi kuendeleza hiyo katika udugu wa Kikristo, kwa kuwa hiyo itakuwa jambo la kujadiliwa sana na yenye kuleta mzozo. Kwa hiyo yeye aweza kuonyesha kwamba yeye anastahi sana umuhimu wa muungano katika kutaniko.
23. Kwa nini tuna sababu hasa ya shangwe?
23 Paulo alikazia kwamba muungano wa Kikristo ni msingi wa shangwe kamili. Katika siku yake idadi ya makutaniko kwa hakika ilikuwa ndogo kuliko leo. Lakini bado aliandikia Wakolosai: “Nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo.” (Wakolosai 2:5; ona pia Wakolosai 3:14.) Tuna sababu kubwa zaidi kama nini ya kushangilia! Twaweza kuona uthibitisho halisi wa muungano, utaratibu, na imara katika imani katika kutaniko letu lenyewe, jambo lionyeshalo hali ya ujumla ya watu wa Mungu duniani kote. Kwa hiyo kwa muda mfupi unaobaki katika mfumo wa sasa, kila mmoja wetu na aazimie ‘kuunganishwa katika upendo.’
[Maelezo ya Chini]
a Ingawa kuna mambo mengi sana tuwezayo kujifunza, kutokana na vielelezo vifuatavyo, ona kile ambacho wewe binafsi unaweza kujifunza kuhusu Yesu kinachoweza kuchangia muungano katika kutaniko lako: Mathayo 12:1-8; Luka 2:51, 52; 9:51-55; 10:20; Waebrania 10:5-9.
b Ona Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1982, kurasa 22-9, Kiingereza.
Je, Uliyaona Mambo Haya?
◻ Andiko la mwaka la 1995 la Mashahidi wa Yehova ni gani?
◻ Kwa nini Wakristo Wakolosai walihitaji kuunganishwa katika upendo, na kwa nini twakuhitaji leo?
◻ Ni mtazamo gani wa maisha ulio hatari ambao Wakristo wanahitaji hasa kujilinda nao leo?
◻ Kwa nini Wakristo wapaswa kuwa chonjo wasidanganywe na maneno ya kushawishi kuhusu afya na njia za kugundua magonjwa?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Je, mipango yako ya wakati ujao inategemea kuwapo kwa Yesu?