Kukusanyika Pamoja na Wale Wanaomhofu Mungu
“WATU kila mahali hutamani kupata uhuru kutoka katika hali ya kuhofu—kuhofu jeuri, hofu ya kutokuwa na kazi ya kuajiriwa, na kuhofu ugonjwa mahututi. Sisi sote tuna tamaa hiyo. . . . Basi, kwa nini tunazungumzia jinsi ya kusitawisha hofu?” Swali hilo lenye kuvutia lilizushwa na msemaji wa hotuba ya msingi katika kila mmoja wa “Hofu ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya iliyoanza Juni 1994.
Mamilioni waliohudhuria—kwanza katika Amerika Kaskazini, halafu baadaye katika Ulaya, Amerika ya Kati na ya Kusini, Afrika, Asia, na visiwa vya bahari—walitamani sana kujifunza jinsi ya kusitawisha hofu ya aina hiyo. Kwa nini? Kwa sababu kushiriki kwetu baraka ambazo Yehova Mungu anazo kwa watu wake kwategemea kuwa kwetu na hofu ya kimungu. Ilikuwa kujifunza kuhusu hofu ya kimungu kwamba wakusanyikaji walikuja pamoja, na wakati wa programu hiyo ya siku tatu, walijifunza mengi kuhusu sifa hii muhimu ya Kikristo.
‘Umhofu Mungu na Kushika Amri Zake’
Hicho kilikuwa ndicho kichwa cha siku ya kwanza ya mkusanyiko, kikitegemea Mhubiri 12:13. Inamaanisha nini kumhofu Mungu? Katika sehemu ya kwanza kabisa ya programu, mwenyekiti wa mkusanyiko alielezea kwamba hofu ya kimungu huonyesha kicho na staha nyingi kuelekea Yehova na vilevile ogofyo lifaalo la kutompendeza. Hofu hiyo ya kimungu si mbaya; inafaa na yastahili.
Hofu hii ifaayo hutunufaishaje? Hotuba iliyofuata “Usichoke na Kukata Tamaa,” ilielezea kuwa hofu ya kimungu itatuchochea tushike amri za Mungu kwa shangwe. Pamoja na upendo kwa Mungu na jirani, hofu hiyo itatia ndani yetu nishati ya kiroho. Ndiyo, hofu ya kimungu yaweza kutusaidia kuepuka kupunguza mwendo katika lile shindano la mbio la uhai wa milele.
Yaliyofuata katika programu yalikuwa mahoji yakitoa uthibitisho halisi kwamba hofu ya kimungu yaweza kututegemeza. Waliohojiwa walieleza jinsi hofu ya Mungu yenye kicho ilivyowaathiri waendelee katika huduma japo ubaridi, kutojali kwa watu, na mnyanyaso na kuwasaidia kuvumilia hata katika majaribu magumu ya kibinafsi.
Lakini, kwa nini watu wengine wana hofu ya kimungu hali wengine hawana? Katika hotuba “Kusitawisha na Kunufaishwa na Hofu ya Kimungu,” msemaji wa hotuba ya msingi alieleza kuwa katika Yeremia 32:37-39, Yehova aliahidi Yeye angewapa watu Wake moyo wa kumhofu Mungu. Yehova huingiza hofu ya kimungu mioyoni mwetu. Kwa njia gani? Kupitia roho takatifu yake na Neno lake lililopuliziwa, Biblia. Hata hivyo, kwa wazi twapaswa kuweka jitihada kubwa ili kujifunza Neno la Mungu na kutumia kwa ukamili maandalizi mengi ya kiroho ambayo amefanya. Haya yatia ndani mikusanyiko na mikutano yetu, ambayo hutusaidia kujifunza kumhofu.
Programu ya alasiri ilifungua kwa himizo la kumtumaini Yehova na Neno lake. Hili lilifuatiwa na mazungumzo ya njia za msingi ambazo kwazo Ufalme wapaswa kuathiri maisha zetu tukiwa Wakristo.
Halafu ukaja mfululizo wa kwanza wa ile mifululizo mitatu iliyotolewa katika mkusanyiko. “Hofu ya Kimungu Hutusukuma Tutii Matakwa ya Kimungu” kilikuwa kichwa cha mfululizo huu, ambao ulikazia uangalifu kwenye familia. Ifuatayo ni namna moja ya shauri la Kimaandiko na linalotumika lililotolewa.
□ Kwa waume: Hofu ya kimungu yapaswa kumsukuma mwanamume kumpenda mke wake kama mwili wake mwenyewe. (Waefeso 5:28, 29) Mtu haujeruhi mwili wake kimakusudi, kujiaibisha mbele ya rafiki zake, au kupiga porojo juu ya makosa yake mwenyewe. Hivyo basi, apaswa kumtendea mke wake kwa adabu na heshima ambayo yeye hujipa mwenyewe.
□ Kwa wake: Hofu ya kimungu ya Yesu ilimsukuma ‘kumpendeza Mungu sikuzote.’ (Yohana 8:29) Huu ni mwelekeo ufaao kwa wake kuiga katika kushughulika na waume zao.
□ Kwa wazazi: Wazazi Wakristo waweza kuonyesha hofu ya kimungu kwa kuchukulia kwa uzito madaraka yao ya kiuzazi, wakiwaona watoto wao kuwa urithi kutoka kwa Yehova. (Zaburi 127:3) Lengo kuu la wazazi lapaswa liwe kuwalea watoto wao waje kuwa Wakristo wa kweli.
□ Kwa watoto: Yehova hufunza watoto wawatii wazazi wao “katika muungano na Bwana.” (Waefeso 6:1, NW) Hivyo, kuwatii wazazi wao ni kumtii Mungu.
Hotuba ya mwisho ya siku hiyo iligusa hisia zetu, kwa kuwa ilizungumzia hisia za ndani ambazo sisi sote hupata tupotezapo mpendwa katika kifo. Hata hivyo, kufikia nusu ya hotuba hivi, kulikuwa na jambo la kustaajabisha. Msemaji alifanya wasikilizaji watereme kwa kutangaza kutolewa kwa broshua mpya Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa. Kichapo hiki cha kurasa 32, chenye rangi kamili chasema mengi yawezayo kusaidia wale waombolezao wafahamu na kushughulikia hisia na mahangaiko ya moyo yatokeayo kufuatia kifo cha mpendwa. Je, umewahi kushindwa na lile utakalosema kwa mtu aliyefiwa? Sehemu ya broshua hii yazungumzia jinsi tuwezavyo kusaidia wale wanaoomboleza. Hali wakisikiliza msemaji, wengi katika wasikilizaji walikuwa wakiwazia mtu fulani ambaye angenufaika kutokana na broshua hii mpya.
‘Toa Utumishi Mtakatifu kwa Hofu ya Kimungu na Kicho’
Hicho kilikuwa ndicho kichwa cha siku ya pili, kikitegemea Waebrania 12:28. Wakati wa progamu ya asubuhi ukaja mfululizo wa pili “Makutaniko Yanayotembea Katika Hofu ya Yehova.” Sehemu ya kwanza ilishughulikia uhudhuriaji wa mikutano. Kuwapo kwetu mikutanoni huonyesha staha yetu kwa Mungu na kwa maandalizi yake ya kiroho. Kwa kuhudhuria, twaonyesha kwamba twaogopa jina lake na twatamani kutii mapenzi yake. (Waebrania 10:24, 25) Msemaji wa pili alielezea kwamba ili kutaniko kwa ujumla litembee katika hofu ya Yehova, ni lazima kila mmoja afanye sehemu yake katika kudumisha mwenendo mzuri. Msemaji wa mwisho alizungumza kuhusu pendeleo na wajibu ambao Wakristo wote wanao—kutangaza zile habari njema bila kuacha. Tutaendelea kuhubiri hadi lini? Hata Yehova atakaposema imetosha.—Isaya 6:11.
“Shangwe ya Yehova Ni Ngome Yako” kilikuwa kichwa cha hotuba iliyofuata, kama kinavyozungumziwa katika makala za funzo za gazeti hili. (Nehemia 8:10) Kwa nini watu wa Yehova ni wenye shangwe? Msemaji alielezea kifupi sababu kadhaa. Yenye kutokeza sana ni kwamba uhusiano wa karibu pamoja na Mungu hutufanya kuwa watu wenye shangwe zaidi ya wote duniani. Ebu wazia, msemaji aliwakumbusha wakusanyikaji, tuna pendeleo la kuwa miongoni mwa watu ambao Yehova amewavuta kwa Yesu Kristo. (Yohana 6:44) Ni sababu yenye nguvu kama nini ya kuwa na shangwe!
Jambo kuu katika kila mkusanyiko ni ubatizo, na Mikusanyiko ya “Hofu ya Kimungu” haikuwa tofauti. Katika hotuba “Wakfu na Ubatizo Katika Hofu ya Yehova,” msemaji alieleza kwamba wajibu wa kibinafsi wa wote waliobatizwa unahusisha mambo manne: (1) Ni lazima tujifunze Neno la Mungu kwa msaada wa vichapo vitusaidiavyo kulielewa na kulitumia; (2) ni lazima tusali; (3) ni lazima tushirikiane na waamini wenzetu kwenye mikutano ya kutaniko; na (4) ni lazima tutoe ushahidi juu ya jina la Yehova na Ufalme wake.
Programu ya Jumamosi alasiri ilianza na habari yenye kutumainisha “Kikundi cha Watu Wasioachwa Kabisa na Yehova.” Karne 35 zilizopita, wakati taifa la Israeli lilikabili nyakati ngumu, Yehova alitoa uhakikisho kupitia Musa, akisema hivi: “BWANA Mungu wako . . . hatakupungukia wala kukuacha.” (Kumbukumbu la Torati 31:6) Yehova alithibitika kusema kweli kuhusu uhakikisho huo kwa kuhami Waisraeli walipoingia Bara la Ahadi na kulimiliki. Leo, tunapokabili majaribu magumu, sisi pia twaweza kuwa na uhakika kamili kwamba Yehova hatatuacha, maadamu twashikamana naye kwa ukaribu na kutii shauri la Neno lake.
Waweza kupataje furaha katika kuisoma Biblia? Katika hotuba “Soma Neno la Mungu, Biblia Takatifu, Kila Siku,” msemaji alipendekeza kuisoma kwa akili yenye kudadisi na kuuliza maswali kama haya: Usimulizi huu wanifundisha nini kuhusu sifa na njia za Yehova? Nawezaje kuwa kama Yehova kuhusiana na sifa hizi? Kuisoma Biblia katika njia hii ni jambo lenye kufurahisha na la kuthawabisha.
Halafu fikira zilielekezwa kwenye mfululizo wa tatu wa programu, “Maandalizi ya Kusaidia Wale Wanaomhofu Yehova.” Ingawa huenda Yehova asifanye miujiza kwa niaba ya watu wake leo, kwa hakika yeye hutoa msaada kwa wale wanaomhofu. (2 Petro 2:9) Mfululizo huu ulizungumzia maandalizi manne kutoka kwa Yehova ya kutusaidia katika siku hizi zilizo hatari: (1) Kupitia roho yake, Yehova hutupa nguvu za kutimiza kazi zipitazo sana nguvu zetu wenyewe. (2) Kupitia Neno lake, yeye hutuandalia shauri na mwongozo. (3) Kupitia fidia, yeye hutupa dhamiri safi. (4) Kupitia tengenezo lake, kutia ndani wazee, yeye hutuandalia mwelekezo na ulinzi. (Luka 11:13; Waefeso 1:7; 2 Timotheo 3:16; Waebrania 13:17) Kwa kutumia kikamili maandalizi haya, tutaweza kuvumilia na hivyo kupata kibali cha Yehova.
Hotuba ya mwisho Jumamosi alasiri ilikuwa na kichwa “Siku ya Yehova Yenye Kutia Hofu Iko Karibu,” ikitegemea unabii wa Malaki. Kumekuwako siku zenye kutia hofu katika historia iliyopita, kama wakati hukumu ilipotekelezwa juu ya Yerusalemu katika 70 W.K. Lakini siku inayotisha zaidi ya yote katika yote waliyopata kuyaona wanadamu itakuwa siku ya Yehova inayokuja wakati ambapo ‘kisasi kitaletwa juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.’ (2 Wathesalonike 1:6-8, NW) Hilo litatokea karibuni kadiri gani? Msemaji alitaarifu hivi: “Mwisho uko karibu! Yehova ajua ile siku na saa. Yeye hatabadili ratiba yake. Tunatolewa wito wa kuvumilia kwa subira.”
Ilikuwa vigumu kuamini kuwa tayari siku mbili zilikuwa zimepita. Siku ya mwisho ingeleta nini?
“Hofuni Mungu na Kumpa Utukufu”
Kichwa cha siku ya tatu kilitegemea Ufunuo 14:7. Wakati wa programu ya asubuhi, mfuatano wa hotuba ulikazia mafundisho ya kimsingi yanayotofautisha Mashahidi wa Yehova na matengenezo mengine yote ya kidini.
Katika hotuba “Kutakuwa na Ufufuo wa Waadilifu,” msemaji alitokeza swali lenye kupendeza: “Wale waliokufa wakiwa waaminifu katika hii miaka ya mwisho-mwisho ya mfumo wa mambo wa Shetani watafufuliwa lini katika hiyo Siku ya Hukumu ya kipindi cha miaka elfu?” Jibu? “Biblia haisemi,” msemaji alieleza. “Hata hivyo, je, si jambo linalopatana na akili nzuri kwamba wale wanaokufa katika siku yetu wafufuliwe mapema ili kushiriki pamoja na ule umati mkubwa wa waokokaji wa Har–Magedoni katika ile kazi kubwa sana ya kielimu itakayofanywa muda wote wa Siku ya Hukumu? Bila shaka ndiyo!” Je, kutakuwako waokokaji? Hakika kutakuwako. Mafundisho na vielezi vya Biblia vinavyotuhakikishia kuhusu jambo hili vilielezewa waziwazi katika hotuba iliyofuata, “Waokolewa Wakiwa Hai Kupitia Dhiki Kubwa.”
Mashahidi wa Yehova wamefahamu kwa muda mrefu kwamba Biblia yatoa matokeo mawili—uhai wa milele katika paradiso duniani kwa ajili ya mamilioni yasiyohesabika na uhai wa kimbingu usioweza kufa kwa idadi ndogo ambao watatawala pamoja na Kristo katika Ufalme wake. Tumaini la kimbingu lilizungumziwa katika hotuba “Msiwe na Hofu, Kundi Dogo.” (Luka 12:32) Kwa sababu ya hali ya sasa ya ulimwengu, kundi dogo lazima liwe bila hofu; kila mmoja wao lazima avumilie hadi mwisho kabisa. (Luka 21:19) “Kuwa kwao bila hofu” msemaji alisema, “kwawatia moyo wale wa umati mkubwa. Wao wapaswa pia kusitawisha mtazamo wa kuwa bila hofu watazamiapo kukombolewa katika ule wakati wenye taabu kuu zaidi ambao dunia haijawahi kupata.”
Katika umalizio wa programu ya asubuhi, wasikilizaji walitazama kwa furaha drama ya Biblia Machaguo Unayokabili. Katika siku za Yoshua, na pia za nabii Eliya, Waisraeli walipaswa kukata shauri. Ilikuwa lazima chaguo lifanywe. Eliya alisema hivi: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? BWANA akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! mfuateni yeye.” (1 Wafalme 18:21) Leo pia, wanadamu wapaswa kukata shauri. Hakuna wakati wa kusita-sita katika mawazo mawili yaliyo tofauti. Chaguo sahihi ni jipi? Ni lilelile alilofanya Yoshua wa kale. Yeye alisema hivi: “Lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.”—Yoshua 24:15.
Ghafula, ilionekana, ilikuwa Jumapili alasiri na wakati wa hotuba ya watu wote iliyokuwa na kichwa “Kwa Nini Umhofu Mungu wa Kweli Sasa.” Katika Ufunuo 14:6, 7 (NW) wanadamu wote wasihiwa: “Hofuni Mungu na kumpa utukufu.” Kwa nini ni muhimu kumhofu Mungu sasa? Kwa sababu, kama andiko liendeleavyo kusema, “saa ya hukumu yake imewasili.” Kupitia Mwana wake, aliyetawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu, Yehova ataleta kwa umalizio mfumo wa mambo wa sasa ulio mchafu na wenye uasi. Msemaji alieleza kwamba hii ndiyo njia pekee ya kuleta kitulizo kwa wale wanaomhofu Mungu na vilevile kuokoa na kuhifadhi makao yetu ya kidunia. Kwa kuwa hizi ni siku za kumalizia za huu mfumo wa mambo, ni muhimu kwamba tumhofu Mungu wa kweli sasa!
Kufuatia muhtasari wa funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo, msemaji wa mwisho alipanda jukwaani. Kama tokeo la programu ya mkusanyiko, hofu ya kimungu imekuwa na umaana mkubwa zaidi kwa wakusanyikaji, alieleza. Alikazia manufaa nyingi zinazokuja kwa wale wanaomhofu Mungu. Msemaji alitangaza kutolewa kwa vidio mpya—United by Divine Teaching. Hiyo yakazia sehemu za kipekee za “Ufundishaji wa Kimungu” Mikusanyiko ya Kimataifa iliyofanywa katika 1993-94. Hotuba ilipokuwa ikimalizika, wengi walijiuliza, ‘Tutazamie nini mwaka ujao?’ Mikusanyiko ya wilaya ya siku tatu katika sehemu nyingi.
Kwa umalizio, msemaji alirejezea Malaki 3:16, ambayo husema hivi: “Ndipo wale waliomcha [“waliomhofu,” NW] BWANA waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha [“waliomhofu,” NW] BWANA, na kulitafakari jina lake.” Wakusanyikaji waliondoka wakiwa na azimio la kutafakari juu ya jina la Yehova na kumtumikia wakiwa na hofu ya kimungu.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wataka-kubatizwa wahitaji kuendelea kudhihirisha hofu ya kimungu
[Picha katika ukurasa wa 25]
Ile Drama “Machaguo Unayokabili” ilivutia wasikilizaji wenye uhitaji wa kukata shauri kuhusu kutumikia Yehova
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wakusanyikaji waliterema kupata ile broshua mpya “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa”