Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/1 kur. 21-25
  • Uamuzi Wangu wa Kuendelea Kufikia Ukomavu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uamuzi Wangu wa Kuendelea Kufikia Ukomavu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vita Yabadili Maisha Zetu
  • Vizuizi vya Maendeleo ya Kiroho
  • Kuingia Katika Utumishi wa Painia
  • Kufuatia Utumishi wa Mishonari
  • Kujipatanisha na Shamba la Kigeni
  • Kuzuru Marekani
  • Kuendelea Kufanya Maendeleo ya Kiroho
  • Familia Iliyonipenda Kikweli
    Amkeni!—1995
  • Kuhubiri Habari Njema Katika Nchi za Mbali
    Amkeni!—2008
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/1 kur. 21-25

Uamuzi Wangu wa Kuendelea Kufikia Ukomavu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA CARL DOCHOW

“Kuendelea Kufikia Ukomavu au Kurudia Dhambi, Lipi?” kilikuwa kichwa cha makala moja katika toleo la The Watchtower, la Juni 15, 1948. Makala hiyo ilinisukuma kubadilika kutoka hali ya hatari ya kiroho huko mashambani mwa Marekani hadi kazi ya mishonari katika Amerika Kusini ambayo imeendelea zaidi ya miaka 43.

NILIZALIWA Machi 31, 1914, nikiwa wa tatu katika familia ya wavulana wanne, katika nyumba ndogo ya mbao katika Vergas, Minnesota. Miaka yangu ya ujana ilikuwa yenye furaha. Nakumbuka nikivua samaki pamoja na baba. Hata hivyo, mama alikuwa mgonjwa mara kwa mara, ikanibidi niache shule nikiwa darasa la tano ili nimsaidie mama kazi za nyumbani. Nilipofika miaka 13, ugonjwa wa mama uligunduliwa kuwa kansa ya mapafu.

Mama alijua hangeweza kuishi muda mrefu, hivyo akaanza kunitayarisha nichukue nafasi yake. Yeye angeketi jikoni na kunionyesha jinsi ya kupika na kuoka mkate. Kuongezea hayo, alinifundisha kufua nguo, kutunza bustani, na kutunza kuku mia moja. Pia alinitia moyo kusoma sura moja ya Biblia kila siku, nilifanya hivyo ujapo uwezo wangu mdogo wa kusoma. Baada ya kunizoeza kwa miezi kumi, mama akafa katika Januari 27, 1928.

Vita Yabadili Maisha Zetu

Baada ya Vita ya Ulimwengu ya 2 kuanza katika Septemba 1939, sala zilitolewa kwa niaba ya wanajeshi kila Jumapili katika kanisa letu la Lutheri. Ndugu yangu mkubwa Frank alikuwa ameazimia kutoua, hivyo alipokataa kupigana akiwa mwanajeshi, alishikwa. Wakati wa kujaribiwa kwake yeye alisema: “Kabla sijaua watu wasio na hatia, mwaweza kunipiga risasi!” Alihukumiwa kutumikia kifungo cha mwaka mmoja katika jela katika Kisiwa cha McNeil pwani mwa Jimbo la Washington.

Huko Frank alikuta zaidi ya Mashahidi wa Yehova 300 waliokuwa wamefungwa kwa sababu walikataa kabisa kuhusika na vita. (Isaya 2:4; Yohana 17:16) Baada ya muda mfupi alianza kushirikiana nao naye akabatizwa hapohapo katika jela. Kwa ajili ya tabia nzuri, hukumu yake ilipunguzwa kwa miezi tisa. Katika Novemba 1942 tulipokea habari kwamba Frank aliachiliwa huru, na muda mfupi baadaye alitueleza juu ya habari njema za Ufalme wa Mungu. Baada ya kuchunguza ujumbe huo kwa makini katika Biblia zetu, sisi sote tungeweza kuona kwamba mambo ambayo Frank alikuwa akitufundisha yalikuwa kweli.

Vizuizi vya Maendeleo ya Kiroho

Katika 1944, nilihamia eneo la Malta, Montana, kuishi na mjomba wangu. Hali zetu zilifanana—sote wawili tulikuwa tumeoa na wake zetu wakatuacha baada ya miezi sita ya ndoa. Alifurahi kuwa nami nimsaidie katika ukulima na upishi, nasi tuligawana faida katikati. Mjomba wangu alisema ningerithi shamba lake la hektari 260 ikiwa ningekaa naye. Hiyo ilikuwa miaka yenye ufanisi ya ukulima, nami niliupenda kama nini! Kila mwaka tulikuwa na mazao mazuri sana, na ngano iliuzwa kwa zaidi ya dola 3.16 kwa kila mkebe.

Hata hivyo, mjomba wangu hakupenda nihudhurie mikutano ya kutaniko dogo la Mashahidi katika Malta. Katika Juni 7, 1947, bila mjomba wangu kujua, nilibatizwa katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova katika Wolf Point. Huko ndugu mmoja Mkristo alinialika niwe painia, au mhudumu wa wakati wote. Ingawa kutumia maisha yangu kwa njia hiyo kulikuwa tamaa ya moyo wangu, nilieleza kwamba mjomba wangu hangeniruhusu kamwe kutumia wakati huo wote katika huduma.

Muda mfupi baadaye, mjomba wangu alifungua bahasha na kusoma barua niliyokuwa nimetumiwa kutoka kwa rafiki aliyenisihi niwe mhudumu wa wakati wote. Akiwa amekasirika sana, mjomba wangu aliniamuru nifanye uamuzi—niache kuhubiri au niondoke. Amri hiyo ilikuwa nzuri kwa sababu nilipenda ukulima sana na sijui kama ningeliuacha kwa uamuzi wangu mwenyewe. Hivyo, nilirudi kwa familia yangu katika Minnesota, ambao wote walikuwa wamebatizwa nao walishirikiana na Kutaniko la Detroit Lakes.

Mwanzoni familia yangu ilinitia moyo kupainia, lakini katika 1948 walianza kupoa kiroho. Ndipo ile makala “Kuendelea Kufikia Ukomavu au Kurudia Dhambi, Lipi?” iliandaa nguvu za kiroho nilizohitaji. Ilionya kwamba “matokeo mabaya sana yatatokea ikiwa tutakataa kimakusudi kuendelea sambamba na ujuzi unaoongezeka.” Makala hiyo ilisema: “Hatuwezi kusimama tu na kurudi nyuma, bali ni lazima tufanye maendeleo katika uadilifu. Maendeleo, bila kusimama, ndiyo msukumo wenye nguvu zaidi dhidi ya kurudi nyuma.”

Ingawa familia yangu ilitoa visababu vinginevyo, naamini kwamba tatizo lao hasa lilikuwa tamaa ya kutajirika. Wangeweza kuona faida za kiuchumi za kutumia wakati mwingi katika ukulima na wakati mchache katika kuhubiri. Badala ya kuingia katika mtego wa tamaa ya mali, nilifanya mipango ili nipainie. Nilijua kwamba haingekuwa rahisi, na hata nilifikiri singeweza kupainia. Hivyo katika 1948, nilijijaribu kwa kunuia kuingia katika upainia katika wakati mbaya kabisa wa mwaka—Desemba.

Kuingia Katika Utumishi wa Painia

Yehova alibariki jitihada zangu. Kwa kielelezo, siku moja ilikuwa sentigredi 27 chini ya sufuri, bila kuhesabu upepo wenye baridi. Nilikuwa nikitoa ushahidi wa barabarani kama kawaida, nikibadilisha mikono yangu mara kwa mara—nikiweka mkono ulio baridi mfukoni na kushika magazeti na ule mwingine hadi huo ugande na kustahili kuwekwa mfukoni. Mtu fulani akaja. Akisema kwamba amekuwa akiangalia utendaji wangu kwa muda fulani, aliuliza: “Magazeti hayo yana nini yaliyo ya maana sana hivyo? Nipe hayo mawili ili niyasome.”

Wakati huohuo, ningeweza kuona kwamba kushirikiana na familia yangu kulitia hali yangu ya kiroho hatarini, baada ya kuomba Watch Tower Society, nikapewa mgawo mpya, katika Miles City, Montana. Huko nilitumika nikiwa mtumishi wa shirika, ajulikanaye kuwa mwangalizi-msimamizi sasa. Nikiishi ndani ya trela fulani yenye ukubwa wa meta mbili kwa tatu, nilijisimamia kifedha kwa kufanya kazi nusu siku katika mahali pa kufua nguo. Pindi kwa pindi niliajiriwa kufanya kazi niliyoipenda sana—kuvuna.

Kufikia wakati huo, niliendelea kusikia jinsi hali ya kiroho ya familia yangu ilivyokuwa ikiendelea kuharibika. Mwishowe, wao pamoja na wengineo katika Kutaniko la Deroit Lakes, wakawa wapinzani wa tengenezo la Yehova. Kati ya wahubiri wa Ufalme 17 katika kutaniko hilo, 7 peke yao ndio waliobaki waaminifu. Familia yangu ilikuwa imeazimia kunifanya niache tengenezo la Yehova pia, hivyo nilitambua kulikuwa na suluhisho moja tu, kufanya maendeleo zaidi. Lakini jinsi gani?

Kufuatia Utumishi wa Mishonari

Wakati wa mkusanyiko wa kimataifa katika New York City katika 1950, nilishuhudia kuhitimu kwa wanafunzi wa shule ya mishonari wa darasa la 15 la Watchtower Bible School of Gilead. ‘Ikiwa tu ningekuwa miongoni mwa wale wanaoenda kumtumikia Yehova katika mgawo wa kigeni,’ nikafikiri.

Nilipeleka ombi nami nikakubaliwa kuwa mshiriki wa darasa la 17 la Gileadi, lililoanza katika Februari 1951. Mahali pa shule kwenye shamba moja katika New York palikuwa penye kupendeza. Jinsi nilivyotaka kufanya kazi shambani baada ya saa za masomo, labda katika kibanda cha ng’ombe au nje kwenye mimea! Lakini John Booth, mwangalizi wa Kingdom Farm wakati huo, alieleza kuwa ni mimi peke yangu niliyekuwa na ujuzi katika kufua nguo. Hivyo nilipewa mgawo wa kufanya kazi hiyo.

Gileadi haikuwa rahisi kwa mtu aliyesoma hadi darasa la tano tu. Ingawa taa zilipaswa kuzimwa kufikia 4:30 usiku, mara nyingi nilisoma hadi usiku wa manane. Siku moja, mmoja wa wafunzi aliniita katika ofisi yake. “Carl,” akasema, “naona kwamba hupiti mtihani sana.”

‘Ole wangu,’ nikafikiri, ‘watanifukuza.’

Hata hivyo, mfunzi huyo akanishauri kwa upendo jinsi ningeweza kutumia wakati wangu vizuri zaidi bila kusoma usiku sana. Kwa hofu nikauliza: “Je, nafaa kuendelea kukaa hapa Gileadi?”

“Bila shaka, ndiyo,” yeye akajibu. “Lakini sijui kama utafaulu kupata diploma.”

Nilipata faraja kutoka kwa maneno ya msimamizi wa shule, Nathan H. Knorr. Hapo awali alikuwa amewaambia wanafunzi kwamba kupita mtihani hakukumvutia kama ‘udumifu’ wa wamishonari katika migawo yao.

Somo lililokuwa gumu zaidi kwangu lilikuwa Kihispania, lakini nilitumainia mgawo wa kwenda Alaska, ambapo hali-baridi ya hewa ndiyo niliyozoea huko nyumbani. Zaidi ya hilo, ningeweza kuhubiri kwa Kiingereza. Hivyo unaweza kuwazia mshangao wangu katikati ya mtaala, nilipopokea mgawo wangu Ekuado, Amerika Kusini. Ndiyo ingenibidi kusema Kihispania, na katika ikweta yenye joto jingi!

Siku moja kachero wa FBI alinitembelea katika Shule ya Gileadi. Aliniuliza juu ya mwana wa mtumishi wa shirika aliyekuwa ameacha tengenezo letu katika Detroit Lakes. Vita vya Korea vilikuwa vikianza, na kijana huyu alidai kuwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova na hivyo asiingizwe katika utumishi wa kijeshi. Nilieleza kwamba yeye hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena. Kachero huyo aliponiaga, yeye alisema: “Mungu wako na akubariki katika kazi yako.”

Baadaye nilisikia kwamba kijana huyo aliuawa katika mojapo vita vya kwanza katika Korea. Tokeo lenye huzuni kama nini kwa mtu ambaye angeliendelea kufikia ukomavu katika tengenezo la Mungu!

Mwishowe, siku yetu ya shangwe ya kuhitimu ikafika katika Julai 22, 1951. Bila shaka, hakuna mtu wa familia yangu aliyekuwapo, lakini furaha yangu ilikuwa imekamilika nilipopokea diploma kwa sababu ya maendeleo niliyokuwa nimefanya.

Kujipatanisha na Shamba la Kigeni

Mara nilipokuwa katika mgawo wangu, nilipata kwamba mazoezi ya mama yalikuwa yenye manufaa sana. Upishi, kufua nguo kwa mikono, na ukosefu wa maji ya mfereji hayakuwa mambo mapya kwangu. Lakini kuhubiri kwa Kihispania kulikuwa kupya! Nilitumia mahubiri yaliyochapishwa katika Kihispania kuhubiri kwa muda fulani. Ilinichukua miaka mitatu kabla ya kuweza kutoa hotuba kwa Kihispania na nilifanya hivyo kwa kutumia maandishi mengi sana.

Nilipofika katika Ekuado katika 1951, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme wanaopungua 200. Kwa miaka 25 hivi kufanya wanafunzi kulionekana kukikawia. Mafundisho yetu ya Biblia yalikuwa tofauti sana na mapokeo yasiyo ya kimaandiko ya Ukatoliki, na kushikamana kwetu na maagizo ya Biblia juu ya uaminifu kwa mwenzi mmoja wa ndoa hasa hakukupendwa kabisa.—Waebrania 13:4.

Hata hivyo, tuliweza kuangusha fasihi nyingi za Biblia. Huduma yetu katika Machala, iliyoko kitovuni mwa mashamba ya ndizi, inatoa kielezi bora cha jambo hili. Nicholas Wesley na mimi ndio tuliokuwa Mashahidi peke yetu huko tulipofika katika 1956. Tungeondoka asubuhi mapema kwa kilori cha takataka kilichotumiwa katika kazi ya barabara zilizokuwa zikitengenezwa siku hizo. Baada ya kusafiri kwa umbali fulani, tungeshuka na kutolea watu ushahidi mpaka tufike kule tulikokuwa tukiishi.

Siku moja hasa, Nick na mimi tuliweka maandishi ili kuona nani kati yetu angeangusha magazeti mengi. Nakumbuka kwamba nilikuwa nimeangusha magazeti mengi zaidi kuliko Nick kufikia adhuhuri, lakini kufikia jioni kila mmoja wetu alikuwa ameangusha magazeti 114. Kila mwezi tuliachia watu waliokuwa wakipokea magazeti kwa ukawaida mamia ya magazeti yetu. Mara sita niliangusha zaidi ya magazeti elfu moja kila mwezi. Ebu wazia ni watu wangapi wangeweza kujifunza kweli za Biblia katika magazeti hayo!

Katika Machala, tulikuwa pia na pendeleo la kujenga Jumba la Ufalme la kwanza la kutaniko katika Ekuado. Hiyo ilikuwa miaka 35 iliyopita, katika 1960. Katika siku hizo za mapema, tulikuwa na wahudhuriaji 15 tu kwenye mikutano yetu. Leo Machala una makutaniko 11 yanayositawi!

Kuzuru Marekani

Mwishoni mwa miaka ya 1970, nilirudi Marekani nikiwa likizoni na kutumia saa chache pamoja na ndugu yangu Frank. Alinibeba kwa gari lake hadi juu ya kilima ambapo tungeona Bonde la Mto Red kwa mbali. Palikuwa penye kupendeza, penye ngano nyingi iliyoiva sana. Kwa mbali Mto Sheyenne wenye miti kila upande ulikuwa ukionekana. Ile shangwe ya uzuri huo wenye utulivu ilikatizwa ndugu yangu alipoanza mazungumzo yake ya kawaida.

“Kama hungekuwa mpumbavu ukirandaranda huko katika Amerika Kusini, shamba hili lingekuwa lako pia!”

“Frank,” nikamkatiza haraka. “Achia mazungumzo hayo hapo.”

Hakusema neno jingine. Miaka michache baadaye, alikufa ghafula kutokana na ugonjwa wa ghafula wa moyo, akaacha mashamba matatu makubwa yenye kupendeza ya kufuga wanyama katika Dakota Kaskazini yakiwa na jumla ya zaidi ya hektari 400, pamoja na hektari 260 za shamba alilorithi la mjomba wangu katika Montana.

Sasa wote katika familia yangu wamekufa. Lakini nafurahi kwamba katika Detroit Lakes, mahali sote tulianzia tukiwa Mashahidi wa Yehova miaka mingi iliyopita, nina familia ya kiroho ya ndugu na dada Wakristo zaidi ya 90.

Kuendelea Kufanya Maendeleo ya Kiroho

Miaka 15 iliyopita imetokeza mazao katika mavuno ya kiroho hapa katika Ekuado. Kuanzia wahubiri wa Ufalme 5,000 katika 1980, sasa tuna zaidi ya 26,000. Nimepata baraka ya kusaidia zaidi ya mia moja kati yao kubatizwa.

Sasa, nikiwa na umri wa miaka 80, najitahidi zaidi kufanya saa 30 kila mwezi katika huduma kuliko nilivyofanya kutimiza saa zangu 150 kila mwezi katika 1951. Tangu 1989, nilipogundua nilikuwa na kansa ya tezi za kiume, nimetumia wakati wa kupata nafuu kusoma. Tangu mwaka huo, nimeisoma Biblia nzima mara 19 na kitabu Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom mara 6. Kwa njia hii ninaendelea kufanya maendeleo ya kiroho.

Ndiyo, nimekuwa na fursa za kuvuna faida za vitu vya kimwili katika mashamba ya Marekani. Lakini thawabu za utajiri wa kimwili ni bure zikilinganishwa na shangwe niliyopata katika mavuno ya kiroho. Ofisi ya tawi hapa Ekuado yanieleza kwamba nimeangusha zaidi ya magazeti 147,000 na vitabu 18,000 katika kazi yangu ya mishonari. Nayaona haya kuwa mbegu za kiroho, nyingi zazo tayari zimechipuka; nyingine bado zaweza kuchipuka ndani ya mioyo ya watu wasomapo juu ya kweli hizi za Ufalme.

Siwezi kufikiri juu ya kitu kingine bora kuliko kuendelea kufikia ulimwengu mpya wa Mungu pamoja na watoto wangu wote wa kiroho na mamilioni ya wengine waliochagua kutumikia Mungu wetu, Yehova. Pesa hazitaokoa mtu kupita mwisho wa ulimwengu huu mwovu. (Mithali 11:4; Ezekieli 7:19) Walakini, matunda ya kazi yetu ya kiroho yataendelea—ikiwa kila mmoja wetu atafanya maendeleo ya kufikia ukomavu.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa tayari kupainia katika Miles City, Montana, katika 1949

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kununua maji kwa ajili ya makao yetu ya mishonari, 1952

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kuhubiri katika Machala, 1957

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tangu niwe mgonjwa katika 1989, nimeisoma Biblia nzima mara 19

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki