Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/15 kur. 2-6
  • Je, Kweli ya Kidini Yaweza Kupatikana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kweli ya Kidini Yaweza Kupatikana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Falsafa na Ile Kweli
  • Je, Kweli Inahitaji Kufunuliwa?
  • Dini na Ile Kweli
  • ‘Ngano na Magugu’
  • Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kwa Nini Utafute Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kumwiga Mungu wa Ukweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • “Kweli Itawaweka Nyinyi Huru”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/15 kur. 2-6

Je, Kweli ya Kidini Yaweza Kupatikana?

KATIKA Sweden mtu mmoja mdadisi wa mambo ya kiroho katika mji wenye chuo kikuu wa Uppsala aliamua kuchunguza itikadi za dini mbalimbali katika mji wake, hata kutembelea mahali pao pa ibada. Alisikiliza makasisi wao walipokuwa wakihubiri, naye akawauliza washiriki fulani maswali. Yeye alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova peke yao ndio walioonekana kuwa na hakika kwamba walikuwa “wameipata kweli.” Akifikiria maoni mbalimbali ya kidini yaliyopo, alishangazwa na jinsi Mashahidi wangedai hivyo.

Je, wewe binafsi unafikiri kwamba inawezekana kuijua ile kweli kuhusu dini? Je, yawezekana hata kuijua ile ambayo huenda ikaitwa kweli yenyewe?

Falsafa na Ile Kweli

Wale waliojifunza falsafa wamekuza maoni ya kwamba binadamu hawezi kuipata kweli yenyewe. Huenda unajua kwamba falsafa imefafanuliwa kuwa “sayansi inayojaribu kueleza chanzo cha kuwapo na uhai.” Hata hivyo, kwa hakika, falsafa hiyo haipiti hapo. Katika Filosofins Historia (Historia ya Falsafa), mwandikaji Msweden Alf Ahlberg aliandika hivi: “Maswali mengi ya kifalsafa ni ya hali fulani ambayo haiwezekani kuyatolea jibu kamili. . . . Watu wengi wana maoni ya kwamba matatizo yote ya asili [yanayohusu kanuni za asili za vitu] yanatiwa ndani ya . . . kundi hili.”

Kama tokeo, wale ambao wamejaribu kutafuta jibu la maswali ya maana sana ya maisha kupitia falsafa mara nyingi wamepata kuwa hawaridhiki au kujikuta katika majonzi. Katika kitabu chake Tankelinjer och trosformer (Njia za Kufikiri na Imani za Kidini), mwandikaji Msweden Gunnar Aspelin alisema hivi: “Jambo moja tunaloliona ni kwamba maumbile hayajali mwanadamu kuliko vipepeo na mbu . . . Hatuna uwezo, hatuna uwezo kabisa, mbele ya uvutano huo unaoingiliana katika ulimwengu na katika ulimwengu wetu wa ndani. Hayo ndiyo maoni kuelekea maisha ambayo yamepatikana mara nyingi katika vitabu vingi kuelekea mwisho wa karne ambayo watu wameendeleza imani yao kwayo na kuota juu ya wakati ujao ulio bora.”

Je, Kweli Inahitaji Kufunuliwa?

Ni wazi kwamba jitihada za binadamu peke yazo za kutafuta kweli juu ya maisha hazijafaulu, na zaonekana hazitafaulu kamwe. Basi, kuna sababu nzuri kuamua kwamba aina fulani ya ufunuo wa kimungu ni ya lazima. Kile wengi huita kitabu cha maumbile kinatoa ufunuo wa kadiri fulani. Hata ikiwa hakitoi maelezo kamili juu ya chanzo cha uhai, kinaonyesha kabisa kuwa kuna kitu fulani chenye kuridhisha zaidi kuliko maelezo ya kilimwengu ya mambo ya asili ya maisha. Kijani kimeacho kuelekea juu kwa kweli hufuata sheria tofauti na zile za rundo la mawe ndani ya shimo lenye kudidimia. Vitu vilivyo hai kwa asili hujijenga na kujipanga katika njia ambayo vitu visivyo hai havifanyi. Mwanafunzi mmoja ajulikanaye wa sheria na dini alikuwa na msingi wa kusema: “Mambo [ya Mungu] yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake.”—Warumi 1:20.

Lakini ili kujua ni nani anayehusika na uumbaji na mpangilio huu, tunahitaji ufunuo zaidi. Je, hatupaswi kutazamia ufunuo kama huo kuwapo? Je, halingekuwa jambo la akili kutazamia kwamba yule Mmoja aliyeanzisha uhai duniani angejitambulisha kwa viumbe vyake?

Biblia inadai kuwa ndiyo ufunuo huo. Katika gazeti hili mara nyingi tumetoa sababu nzuri za kukubali dai hili, na watu wengi wenye kufikiri wamekubali dai hili. Uhakika wa kwamba wanaume walioandika Biblia walitaka ifahamike kuwa yale waliyoandika hayakutokana nao, ni jambo lenye kutokeza sana. Zaidi ya mara 300, tunapata manabii wa Biblia wakitumia semi kama vile, “BWANA asema hivi.” (Isaya 37:33; Yeremia 2:2; Nahumu 1:12) Yamkini unajua kwamba wanaume na wanawake wanaoandika vitabu au makala mara nyingi hutamani sana kujitambulisha. Hata hivyo, walioandika Biblia hawakujitambulisha; wakati mwingine ni vigumu kujua ni nani aliyeandika sehemu fulani za Biblia.

Jambo jingine la Biblia ambalo huenda ukapata kuwa la maana ni upatano wayo. Hili ni jambo lenye kutokeza sana, ukifikiria kwamba vitabu 66 vya Biblia viliandikwa kwa kipindi cha miaka 1,600. Tuseme umeenda katika maktaba ya umma na kuchagua vitabu vya kidini 66 vilivyoandikwa zaidi ya kipindi cha karne 16. Kisha uvijalidi pamoja vitabu hivyo kimoja-kimoja kuwa buku moja. Je, ungetazamia buku hilo kuwa na habari yenye kichwa kimoja na ujumbe wenye kupatana? Sivyo hata kidogo. Jambo hilo lingehitaji muujiza. Fikiria hili: Vitabu vya Biblia vina habari yenye kichwa kimoja, navyo huthibitishana. Hili laonyesha kwamba ni lazima kuwe mbuni mmoja, au mtungaji, aliyeelekeza yale waandikaji wa Biblia waliyorekodi.

Hata hivyo, utapata sehemu inayothibitisha Biblia kuwa chanzo cha kimungu kuliko kitu kinginecho chote. Unabii mbalimbali—habari iliyoandikwa kimbele kuhusu yale ambayo kwa hakika yangetokea wakati ujao. Semi kama vile, “Itakuwa katika siku hiyo” na, “Itakuwa katika siku za mwisho” zapatikana katika Biblia pekee. (Isaya 2:2; 11:10, 11; 23:15; Ezekieli 38:18; Hosea 2:21-23; Zekaria 13:2-4) Mamia mengi ya miaka kabla Yesu Kristo atokee hapa duniani, unabii mwingi katika Maandiko ya Kiebrania ulieleza mambo mengi madogo-madogo juu ya maisha yake—tangu kuzaliwa kwake hadi kifo chake. Hatuwezi kufikia mkataa mwingine mzuri kuliko kwamba Biblia ndiyo chanzo cha kweli kuhusu maisha. Yesu mwenyewe athibitisha jambo hili akisema: “Neno lako ndiyo kweli.”—Yohana 17:17.

Dini na Ile Kweli

Hata wengi wanaodai kuwa na imani katika Biblia wanaamini kwamba ile kweli haiwezi kupatikana. Kasisi Mmarekani John S. Spong alieleza hivi: “Ni lazima . . . tuache kufikiri tunayo kweli na wengine lazima wakubaliane na maoni yetu ya kwamba hakuna awezaye kuipata ile kweli yenyewe.” Mwandikaji wa Katoliki ya Kiroma, Christopher Derrick, anatoa sababu moja ya maoni hayo yasiyofaa kuhusu kuipata kweli: “Mtajo wowote wa ‘kweli’ ya kidini unaonyesha dai la aina fulani kujua . . . Unamaanisha kwamba mtu mwingine huenda akawa amekosea; na hilo halikubaliki hata kidogo.”

Hata hivyo, ukiwa mtu mwenye kufikiri, utafanya vema kufikiria maswali fulani yenye maana. Ikiwa kweli haiwezi kupatikana, kwa nini Yesu Kristo angesema: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru”? Na kwa nini mmoja wa mitume wa Yesu angesema kwamba mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli”? Kwa nini neno “kweli” linapatikana zaidi ya mara mia moja katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuhusiana na imani? Ndiyo, kwa nini, ikiwa kweli haiwezi kupatikana?—Yohana 8:32; 1 Timotheo 2:3, 4.

Kwa kweli, Yesu hakuonyesha tu kwamba kweli yaweza kupatikana bali alionyesha kwamba kuitafuta kunatakiwa ikiwa ibada yetu itakubaliwa na Mungu. Yule mwanamke Msamaria aliposhindwa kujua ni nini iliyokuwa ibada ya kweli—ile ibada iliyokuwa ya Wayahudi katika Yerusalemu au ile iliyokuwa ya Wasamaria kwenye Mlima Gerizimu—Yesu hakujibu kwa kusema kwamba kweli haiwezi kupatikana. Badala ya hilo, alisema hivi: “Waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24, Italiki ni zetu.

Watu wengi hudai, ‘Biblia yaweza kutafsiriwa kwa njia mbalimbali, kwa hiyo mtu hawezi kuwa na hakika ni ipi iliyo kweli.’ Lakini, je, kweli Biblia imeandikwa kwa njia isiyoeleweka hivi kwamba huwezi kuwa na hakika jinsi inavyopaswa kueleweka? Ni kweli kwamba semi fulani za kiunabii na za ufananisho huenda zikawa ngumu kuelewa. Kwa kielelezo, Mungu alimwambia nabii Danieli kwamba kitabu chake, kilicho na semi nyingi za kiunabii, hakingeeleweka wazi hadi “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:9) Na ni wazi kwamba mifano fulani na mifananisho inahitaji kufasiriwa.

Hata hivyo, inaeleweka kwamba Biblia inaeleza waziwazi mafundisho ya msingi ya Kikristo na kanuni za maadili zilivyo muhimu kwa ibada ya Mungu katika kweli. Hairuhusu fasiri zinazopingana. Katika barua kwa Waefeso, imani ya Kikristo inasemwa kuwa “moja,” ikionyesha kwamba hakukupaswa kuwe na imani mbalimbali. (Waefeso 4:4-6) Labda huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Biblia haiwezi kwa kufaa kufasiriwa kwa njia nyingi tofauti, kwa nini kuna dini nyingi tofauti za “Kikristo”?’ Tunapata jibu tuangaliapo nyuma muda mfupi baada ya mitume wa Yesu kufa na wakati uasi-imani kutoka kwa imani ya kweli ya Kikristo ulipokuwa umeanza kutokea.

‘Ngano na Magugu’

Yesu alitabiri uasi-imani huu katika mfano wake wa ngano na magugu. Yesu mwenyewe alieleza kwamba “ngano” inawakilisha Wakristo wa kweli; “magugu” yanawakilisha Wakristo wa uongo, au waasi-imani. “Lakini watu walipolala,” Yesu akasema, “adui” angepanda magugu katika shamba la ngano. Kupanda huku kulianza baada ya mitume kulala usingizi katika kifo. Mfano huo unaonyesha kwamba kutotambua Wakristo wa kweli na wa uongo kungeendelea hadi “umalizio wa mfumo wa mambo,” (New World Translation). Hivyo, katika karne zote, utambulishi wa Wakristo wa kweli umefichika kwa sababu shamba la kidini limetawalwa na walio Wakristo wa jina tu. Hata hivyo, kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo,” badiliko lingetokea. “Mwana wa Adamu” “atawatuma malaika zake” kubagua Wakristo wa uongo kutoka kwa Wakristo wa kweli. Hili lilimaanisha kwamba ingekuwa rahisi basi kulitambua kutaniko la Kikristo, likiwa na cheo lililokuwa nacho wakati wa mitume.—Mathayo 13:24-30, 36-43.

Unabii wa Isaya na vilevile wa Mika unatabiri huko kukusanywa tena kwa waabudu wa kweli “katika siku za mwisho.” Isaya asema: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” Kuchunguza kwa makini uhakika wa mambo kwaonyesha kwamba unabii wa Isaya unatimizwa wakati wetu.—Isaya 2:2, 3; Mika 4:1-3.

Lakini, ukuzi wa kutaniko la Kikristo, hautokezwi na jitihada fulani za kibinadamu. Yesu alitabiri kwamba ‘angewatuma malaika zake’ kufanya kazi ya ukusanyaji. Yeye pia alionyesha kusudi la pekee sana kwa jambo hilo: “Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao.” (Mathayo 13:43) Hili laonyesha kwamba kazi ya kuelimisha, au ya kufundisha, ingefanywa ulimwenguni pote na kutaniko la Kikristo.

Mashahidi wa Yehova wanaona utimizo wa unabii huu katika kazi ya kuelimisha wanayoifanya leo katika nchi 232. Kwa kulinganisha itikadi, viwango vya mwenendo, na tengenezo la Mashahidi pamoja na Biblia, watu wasio na upendeleo wanaweza kuona waziwazi kwamba mambo haya yanapatana na yale ya kutaniko la Wakristo la karne ya kwanza. Mashahidi huzungumza juu ya imani yao kuwa ‘ile kweli’ bila kusukumwa na kimbelembele cha aina fulani cha kujitukuza. Badala ya hilo, wanafanya hivyo kwa sababu wamejifunza kindani sana Neno la Mungu, Biblia, nao huifuata ikiwa kiwango cha pekee ambacho dini yaweza kwa kufaa kupimwa.

Wakristo wa mapema walirejezea imani yao kuwa ‘ile kweli.’ (1 Timotheo 3:15; 2 Petro 2:2; 2 Yohana 1) Yaliyokuwa kweli kwao lazima pia yawe kweli kwetu leo. Mashahidi wa Yehova wanaalika kila mmoja kujihakikishia jambo hilo kwa kujifunza Biblia. Tunatumaini kwamba kwa kufanya hivyo wewe pia utapata shangwe iletwayo si kutokana tu na kupata dini ipitayo nyingine bali kwa kuipata ile kweli!

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

FALSAFA KADHAA DHIDI YA KWELI

POSITIVISM: Maoni ya kwamba mawazo yote ya mambo ya kidini ni upuzi usioweza kuthibitishwa na kwamba lengo la falsafa ni kuunganisha sayansi chanya na kuzifanya kuwa kitu kimoja.

EXISTENTIALISM: Wateteaji wayo waliathiriwa sana na ukatili wa Vita ya Ulimwengu 2 na kwa hiyo wakawa na maoni hasi juu ya maisha. Inakazia kuchunguza huzuni ya mwanadamu mbele ya kifo na utupu wa maisha. Mfuasi wa existentialism Jean-Paul Sartre alisema kwamba, kwa kuwa hakuna Mungu, mwanadamu ameachwa naye anaishi katika ulimwengu wote mzima usiojali kabisa.

SKEPTICISM: Inaamini kwamba kupitia uchunguzi na kusababu haiwezekani kufikia lengo lolote, ujuzi wa ulimwengu wote mzima—kweli yoyote—kuhusu kuwapo.

PRAGMATISM: Inakadiria thamani ya kweli ya usadikisho kwa msingi wa uhusiano wayo na mapendezi ya binadamu, kama vile kuirekebisha elimu, maadili, na siasa. Haiioni kweli yenyewe ikiwa na thamani yoyote.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Ukurasa 3: Pili kutoka kushoto: Kwa hisani ya The British Museum; Kulia: Sung Kyun Kwan University, Seoul, Korea

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki