Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/15 kur. 10-14
  • Mchapishaji Aliyepata Sifa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mchapishaji Aliyepata Sifa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vulgate Iliyorekebishwa
  • Mchapishaji wa Kifalme
  • Ile Sorbonne Dhidi ya Marekebisho
  • Ile Sorbonne Yashambulia
  • Wanatheolojia Wapiga Marufuku Biblia Zake
  • Ashtakiwa Kuwa Mzushi
  • Mchapishaji wa Kigeni
  • Je, Wakumbuka?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Sura na Mistari​—Ni Nani Aliiweka katika Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Funzo Namba 6—Maandishi-awali ya Kigiriki ya Kikristo ya Maandiko Matakatifu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/15 kur. 10-14

Mchapishaji Aliyepata Sifa

JE, ULIPATA kujaribu kutafuta fungu fulani katika Biblia lakini ukasahau mahali lilipo? Lakini, kwa kukumbuka tu neno moja, uliweza kulipata kwa kutumia konkodansi ya Biblia. Au labda umepata kuhudhuria kusanyiko la Wakristo ambapo mamia, au hata maelfu, waliohudhuria waliweza kufungua Biblia zao kusoma andiko sekunde chache tu baada ya kutajwa.

Katika kila mojayapo mambo hayo, yote ni kwa sababu ya mtu fulani ambaye huenda humjui. Alifanya funzo lako la Biblia kuwa rahisi, naye pia alichangia kuhakikisha kwamba sisi leo tuna Biblia zilizo sahihi. Hata alikuwa na uvutano kwa jinsi Biblia nyingi zinavyofanana.

Mtu huyo alikuwa Robert Estienne.a Alikuwa mchapishaji, aliyekuwa mwana wa mchapishaji, katika Paris, Ufaransa, karibu na mwanzo wa karne ya 16. Hicho kilikuwa kipindi cha ule Mvuvumko na yale Marekebisho. Matbaa ikawa chombo cha harakati hizo mbili. Henri Estienne, baba ya Robert, alikuwa mchapishaji mashuhuri, akitokeza baadhi ya chapa bora zaidi ya vitabu katika kipindi cha ule Mvuvumko. Kazi yake ilitia ndani vitabu vya usomi na vya Kibiblia kwa ajili ya Chuo Kikuu cha Paris na chuo chao cha theolojia—ile Sorbonne.

Lakini ebu tukazie fikira mwana huyo, Robert Estienne. Ni machache yajulikanayo juu ya masomo yake. Lakini, tangu umri wa mapema, alijifunza vizuri Kilatini na upesi akajifunza Kigiriki na Kiebrania vilevile. Robert alijifunza ustadi wa uchapishaji kutoka kwa baba yake. Alipochukua usimamizi wa matbaa ya Henri katika 1526, tayari Robert Estienne alikuwa amejulikana kuwa msomi wa lugha wa ngazi ya juu. Ingawa alichapisha chapa za fasihi za Kilatini pamoja na vitabu vinginevyo vya uchunguzi, upendo wake wa kwanza usiotilika shaka ulikuwa Biblia. Akitamani kutimizia Biblia ya Kilatini kile kilichokuwa kimetimizwa tayari katika vitabu vya kale vya Kilatini, Estienne alitaka kurudisha kwa kadiri iwezekanavyo lile andiko la awali la karne ya tano la Biblia ya Latin Vulgate ya Jerome.

Vulgate Iliyorekebishwa

Jerome alikuwa ametafsiri kutoka kwa lugha za awali za Kiebrania na Kigiriki, lakini kufikia siku za Estienne, Vulgate ilikuwa imekuwapo kwa miaka elfu moja. Makosa mengi na mipotoko mingi ilikuwa imepenyeza kwa sababu ya vizazi vingi kunakili Vulgate. Na zaidi, katika zile Enzi za Kati, maneno ya Biblia yaliyopuliziwa kimungu yalikuwa yamefunikwa na chungu nzima ya hekaya za enzi za kati, mafungu yaliyofasiriwa, na mabadiliko mabaya. Hayo yalikuwa yamechanganyana sana na andiko la Biblia hivi kwamba yalianza kuonwa kuwa maandiko yaliyopuliziwa.

Ili kuondoa yale yote ambayo hayakuwa awali, Estienne alitumia njia uhakiki wa andiko iliyokuwa ikitumiwa katika funzo la fasihi za kale. Yeye alitafuta hati-mkono za kale na zilizo bora zaidi zilizopatikana. Katika maktaba zilizopo Paris na viungani vyalo na katika mahali kama Évreux na Soissons, yeye aligundua hati-mkono nyingi za kale, mojapo yaonekana ikiwa ya karne ya sita. Kwa uangalifu, Estienne alilinganisha maandiko tofauti-tofauti ya Kilatini fungu kwa fungu, akichagua mafungu pekee yaliyoonekana kuwa na mamlaka zaidi. Matokeo ya kazi hiyo, Biblia ya Estienne, ilichapishwa kwa mara ya kwanza katika 1528, nayo ilikuwa hatua kubwa katika kurekebisha usahihi wa kimaandiko wa Biblia. Chapa zilizoboreshwa za Estienne zikafuata. Wengine kabla yake walikuwa wamejaribu kusahihisha Vulgate, lakini yake ilikuwa ndiyo chapa ya kwanza ya kuandaa habari kamili za funzo. Pambizoni, Estienne alionyesha mahali alikuwa ameacha nje mafungu fulani yenye kutilika shaka au mahali ambapo pangeweza kuwa na maana zaidi ya moja. Pia alitaja hati-mkono zilizofanya marekebisho hayo yawekwe.

Estienne alianzisha mambo mengine mengi yaliyokuwa mapya katika karne ya 16. Yeye alitofautisha vitabu vya Apokrifa na Neno la Mungu. Aliweka kitabu cha Matendo baada ya zile Gospeli na kabla ya barua za Paulo. Juu ya kila ukurasa, aliweka maneno machache makuu ya kusaidia wasomaji kupata mafungu fulani hususa. Hicho kilikuwa kielelezo cha awali zaidi cha kile kiitwacho kwa ukawaida kichwa cha kila ukurasa. Badala ya kutumia chapa nzito ya Kigothi, au chapa-nyeusi, iliyotoka Ujerumani, Estienne alikuwa mmoja wa watu wa kwanza kuchapisha Biblia nzima katika chapa-nyepesi ya kiroma iliyo rahisi kusoma inayotumiwa sana siku hizi. Pia aliandaa marejezo mengi na maandishi ya kilugha ya kusaidia kuelewesha mafungu fulani.

Watu wengi wa tabaka ya juu na viongozi wa kidini walithamini Biblia ya Estienne, kwa kuwa ilikuwa bora kuliko chapa nyingine yoyote ya Vulgate. Kwa umaridadi, ustadi wa kazi, na utumizi, chapa yake ikawa kigezo cha kutumiwa na upesi ilikuwa ikiigwa kotekote Ulaya.

Mchapishaji wa Kifalme

“Je! wamwona mtu mwenye bidii [“ustadi,” NW] katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme,” yasema Mithali 22:29. Ustadi wenye ubuni wa Estienne na uwezo wake wa kilugha ulionwa na Francis 1, mfalme wa Ufaransa. Estienne akaja kuwa mchapishaji wa mfalme katika Kilatini, Kiebrania, na Kigiriki. Akifanya hivyo, Estienne alitokeza kile kinachoonwa kuwa bora zaidi hadi leo katika uchapishaji wa Ufaransa. Katika 1539 alianza kutokeza Biblia nzima ya kwanza na iliyo bora zaidi ya Kiebrania iliyochapishwa katika Ufaransa. Katika 1540 aliingiza michoro katika Biblia yake ya Kilatini. Lakini badala ya ile michoro ya kuvutia ya matukio ya Biblia iliyokuwa kawaida katika Enzi za Kati, Estienne aliandaa michoro yenye kufundisha iliyotegemea uthibitisho wa kiakiolojia au vipimo na mafafanuzi yaliyopatikana katika Biblia yenyewe. Chapa hizo za mbao zilionyesha kindani zaidi mambo kama sanduku la agano, mavazi ya kuhani mkuu, tabenakulo, na hekalu la Sulemani.

Akitumia aina ya pekee ya chapa ya Kigiriki aliyokuwa ameagiza achapishie hati-mkono ya mfalme, Estienne aliendelea kutokeza chapa ya kwanza ya funzo ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Ingawa chapa mbili za kwanza za andiko la Kigiriki za Estienne hazikushinda sana zile za Desiderius Erasmus, katika chapa ya tatu ya 1550, Estienne aliongeza milinganisho na marejezo kutoka hati-mkono zipatazo 15, kutia ndani ile Kodeksi ya Bezae ya karne ya tano W.K. na Biblia ya Septuagint. Chapa hiyo ya Estienne ilikubaliwa sana hivi kwamba baadaye ikawa msingi wa ile iitwayo Textus Receptus, au Andiko Lililopokewa, ambalo tafsiri nyingi za baadaye zilitegemea, kutia ndani King James Version ya 1611.

Ile Sorbonne Dhidi ya Marekebisho

Huku mawazo ya Luther na Warekebishaji wengine yakienea kotekote Ulaya, Kanisa Katoliki lilijaribu kudhibiti mawazo ya watu kwa kuchanganua yale waliyosoma. Katika Juni 15, 1520, Papa Leo 10 alikuwa ametoa amri iliyoamuru kwamba kitabu chochote chenye “uzushi” kisichapishwe, kuuzwa, wala kusomwa katika nchi yoyote ya Kikatoliki na kudai kwamba mamlaka za kilimwengu zifuate amri hiyo katika maeneo zilizotawala. Katika Uingereza, Mfalme Henry 8 aliachia askofu wa Katoliki Cuthbert Tunstall kazi ya ukaguzi wa vitabu. Hata hivyo, katika sehemu kubwa ya Ulaya, mamlaka kuu katika mambo ya fundisho, baada tu ya papa, ilikuwa kitivo cha wanatheolojia katika Chuo Kikuu cha Paris—ile Sorbonne.

Ile Sorbonne ilikuwa sauti ya Ukatoliki wa kawaida. Kwa karne nyingi ilikuwa imeonwa kuwa nguzo ya imani ya Katoliki. Wakaguzi wa vitabu wa ile Sorbonne walipinga chapa zote za vitabu vyenye uchambuzi na tafsiri za kilugha za Vulgate, wakiziona kuwa “bure na vilevile zenye kudhuru kanisa.” Hilo halikushangaza wakati ambapo Warekebishaji walikuwa wakitilia mashaka mafundisho, sherehe, na mapokeo ya kanisa ambayo hayakuwa na msingi wa Maandiko. Hata hivyo, wanatheolojia wengi katika ile Sorbonne waliona mafundisho yaliyotukuzwa ya kanisa kuwa muhimu zaidi ya usahihi wa Biblia yenyewe. Mwanatheolojia mmoja alisema hivi: “Mara mafundisho yapatikanapo, Maandiko ni kama ngazi inayotolewa baada ya ukuta kujengwa.” Walio wengi katika kitivo hicho hawakuelewa Kiebrania na Kigiriki, na bado walidharau uchunguzi wa Estienne na wasomi wengine wa ule Mvuvumko ambao walikuwa wakitafuta maana ya asili ya maneno yaliyotumiwa katika Biblia. Profesa mmoja wa ile Sorbonne hata alijasiri kusema kwamba “kueneza ujuzi wa Kigiriki na Kiebrania kungeharibu dini yote.”

Ile Sorbonne Yashambulia

Ingawa chapa za mapema za Vulgate ya Estienne ilipita wakaguzi wa vitabu wa kitivo hicho, haijakosa kuwa na mzozo. Kule nyuma katika karne ya 13, Vulgate ilikuwa imekuwa takatifu ikiwa Biblia rasmi ya chuo kikuu hicho, na kwa maoni ya watu wengi, maandishi yayo hayakuwa na makosa kamwe. Kitivo hicho hata kilikuwa kimeshutumu msomi Erasmus aliyeheshimiwa kwa sababu ya kazi yake katika Vulgate. Jambo la kwamba mchapishaji wa kawaida tu wa mahali hapo angejasiri kusahihisha andiko rasmi lilishtua wengine.

Labda jambo lililohangaisha wanatheolojia hao kuliko jambo jingine lolote ni maandishi ya pambizoni ya Estienne. Maandishi hayo yalitilia shaka uhalali wa andiko la Vulgate. Tamaa ya Estienne kuelewesha mafungu fulani ilifanya tu ashtakiwe kuingilia mambo ya theolojia. Alikanusha shtaka hilo, akidai kwamba maandishi yake yalikuwa tu ufupisho au ya aina ya uchunguzi. Kwa kielelezo, andiko lake kwenye Mwanzo 37:35 lilieleza kwamba neno “helo” [Kilatini, infernum] halimaanishi hapo kuwa mahali ambapo waovu wanateswa. Kitivo hicho kilimshtaki kwamba alikana kutokufa kwa nafsi na uwezo wa “watakatifu” wa kuombea watu.

Hata hivyo, Estienne alipata upendeleo na ulinzi wa mfalme. Francis 1 alipendezwa sana na uchunguzi wa ule Mvuvumko, hasa kazi ya mchapishaji wake wa kifalme. Yaripotiwa kwamba Francis 1 hata alikuwa akimzuru Estienne na pindi moja alingoja kwa saburi Estienne alipokuwa akifanya marekebisho fulani ya dakika ya mwisho katika andiko fulani. Akiungwa mkono na mfalme, Estienne aliishinda ile Sorbonne.

Wanatheolojia Wapiga Marufuku Biblia Zake

Lakini katika 1545, matukio yalifanya kitivo cha ile Sorbonne kielekeze ghadhabu yote kwa Estienne. Zikiona manufaa za kupinga Warekebishaji kwa umoja, Vyuo vikuu vya Katoliki vya Cologne (Ujerumani), Louvain (Ubelgiji), na Paris vilikuwa vimekubaliana mapema kushirikiana katika kukagua vitabu vyenye mafundisho yasiyo ya kawaida. Wanatheolojia wa Chuo Kikuu cha Louvain walipoandikia ile Sorbonne wakishangaa kwamba Biblia za Estienne hazikuwa katika orodha ya Paris ya vitabu vilivyoshutumiwa, ile Sorbonne ilijibu kwa uwongo kwamba hakika wangalizishutumu ikiwa wangaliziona. Maadui wa Estienne sasa wakawa na uhakika kwamba mamlaka zilizounganika za vitivo vya Louvain na Paris zingetosha kumsadikisha Francis 1 juu ya makosa ya mchapishaji wake.

Wakati uo huo, baada ya kuonywa juu ya makusudi ya maadui wake, Estienne akawa wa kwanza kumwendea mfalme. Estienne alipendekeza kwamba ikiwa wanatheolojia hao wangetokeza orodha ya makosa yoyote waliyopata, alikuwa tayari kabisa kuchapisha makosa hayo pamoja na masahihisho ya wanatheolojia hao na kuyatia ndani ya kila Biblia ya kuuzwa. Mfalme alipendelea suluhisho hilo. Akamwambia Pierre du Chastel, msomaji wake wa kifalme, kushughulikia jambo hilo. Katika Oktoba 1546 kitivo hicho kiliandikia Du Chastel kikilalamika kwamba Biblia za Estienne zilikuwa “chakula cha wale wanaokana Imani yetu na kuunga mkono uzushi . . . wa sasa” nazo zilijaa sana makosa kiasi cha kwamba “zote [zilistahili] kuondolewa na kuharibiwa.” Akikosa kusadikishwa, sasa mfalme mwenyewe akaagiza kitivo hicho kitokeze makosa hayo ili yachapishwe pamoja na Biblia za Estienne. Waliahidi kufanya hivyo, lakini kwa hakika walifanya kila jitihada wawezavyo kuepuka kutokeza orodha ya mambo mengi ya yale yaonwayo kuwa makosa.

Francis 1 akafa katika Machi 1547, Estienne akapoteza mwenzi mwenye nguvu zaidi aliyemwunga mkono dhidi ya uwezo wa ile Sorbonne. Henry 2 alipotwaa mamlaka, alirudia tena amri ya baba yake kwamba kile kitivo kitoe makosa. Lakini, akiona jinsi wakuu wa Ujerumani walivyokuwa wakitumia Marekebisho ili kutimiza miradi ya kisiasa, Henry 2 hakuhangaikia mazuri na mabaya ya Biblia za mchapishaji huyo wa kifalme kama kudumisha Ukatoliki katika Ufaransa na kuiunganisha chini ya mfalme wayo mpya. Katika Desemba 10, 1547, Kamati ya Faragha ya mfalme iliamua kwamba Biblia za Estienne zizuiwe mpaka wanatheolojia watokeze orodha yao ya makosa.

Ashtakiwa Kuwa Mzushi

Kitivo hicho sasa kilitafuta njia za kupeleka kesi ya Estienne katika mahakama ya kipekee ambayo ilikuwa imeanzishwa ili ifanye kesi za uzushi. Estienne alijua vizuri hatari aliyokabili. Baada ya miaka miwili tangu ianzishwe, mahakama hiyo ikaja kuitwa chambre ardente, au “chumba cha kuchoma.” Watu wapatao 60 waliwekwa mtini, kutia ndani wachapishaji na wauzaji vitabu fulani waliochomwa wakiwa hai katika Place Maubert, mwendo wa mguu wa dakika chache tu kutoka mlango wa mbele wa Estienne. Nyumba ya Estienne ilisakwa-sakwa kutafuta angalau uthibitisho wa shtaka dhidi yake. Zaidi ya mashahidi 80 walihojiwa. Wapeleka-habari waliahidiwa zawadi ya robo ya mali yake ikiwa angalipatikana na hatia ya uzushi. Na bado uthibitisho wao wa pekee ulikuwa yale ambayo Estienne alikuwa amechapisha waziwazi katika Biblia.

Tena mfalme akaamuru kwamba orodha ya kitivo hicho ya makosa ipelekwe kwa Kamati ya Faragha yake. Kwa ufidhuli, kitivo hicho kikajibu kwamba ‘wanatheolojia hawapendi tabia ya kuandika sababu zao za kushutumu jambo kuwa uzushi bali hujibu kwa mdomo pekee, ambayo ni lazima uamini, au kama sivyo kuandika hakutakoma.’ Henry akakubali. Marufuku ya mwisho ikawekwa. Karibu kila kitabu cha Kibiblia ambacho Estienne alipata kutokeza kilipigwa marufuku. Ingawa alikuwa ameokoka moto wa Place Maubert, aliamua kutoka Ufaransa kwa sababu ya marufuku kabisa ya Biblia zake na uwezekano wa kudhulumiwa zaidi.

Mchapishaji wa Kigeni

Katika Novemba 1550, Estienne alihamia Geneva, Uswisi. Kile kitivo kilifanya kuwa jambo lisilo halali katika Ufaransa kuchapisha Biblia yoyote ila Vulgate. Sasa akiwa huru kuchapisha chochote alichotaka, Estienne alichapisha upya “Testamenti Mpya” yake ya Kigiriki katika 1551, pamoja na tafsiri mbili za Kilatini (Vulgate na ya Erasmus) katika safu zinazoambaana. Katika 1552, alifuatisha kwa tafsiri ya Kifaransa ya Maandiko ya Kigiriki katika safu zinazoambaana na andiko la Kilatini la Erasmus. Katika chapa hizo mbili, Estienne alianzisha mfumo wake wa kugawanya andiko la Biblia katika mistari yenye nambari—mfumo ule unaotumiwa ulimwenguni pote leo. Ingawa wengine walikuwa wamejaribu hapo awali njia mbalimbali za kugawanya mistari, mtindo wa Estienne ulikuja kukubaliwa. Biblia yake ya Kifaransa ya 1553 ilikuwa Biblia nzima ya kwanza ya kuandaa migawanyiko ya mistari.

Biblia ya tafsiri mbili ya Kilatini ya 1557 ya Estienne yajulikana pia kwa kutumia jina la binafsi la Mungu, Jehova, kotekote katika Maandiko ya Kiebrania. Katika pambizo ya zaburi ya pili, alitaja kwamba kuwekwa kwa maneno ʼAdho·naiʹ badala ya Tetragramatoni ya Kiebrania (יהוה) kulitegemea tu ushirikina wa Kiyahudi na hivyo kwapaswa kukataliwa. Katika chapa hiyo, Estienne alitumia italiki kuonyesha maneno ya Kilatini yaliyoongezwa ili kukamilisha maana ya Kiebrania. Mtindo huo uliowekwa ulikuja kutumiwa katika Biblia nyinginezo, jambo ambalo limetatanisha wasomaji wa leo ambao wamezoea matumizi ya kisasa ya italiki kuonyesha mkazo.

Akiwa ameazimia kutumia usomi wake kusaidia wengine, Estienne alitoa maisha yake kwa uchapishaji wa Maandiko Matakatifu. Wale leo wanaothamini Neno la Mungu waweza kushukuru jitihada zake na kazi za wengine waliojikakamua kufunua maneno ya Biblia kama yalivyoandikwa awali. Mwendo walioanzisha waendelea tupatapo ujuzi sahihi zaidi wa lugha za kale na kugundua hati-mkono za kale na zilizo sahihi zaidi za Neno la Mungu. Muda mfupi kabla ya kifo chake (1559), Estienne alikuwa akifanyia kazi tafsiri mpya ya Maandiko ya Kigiriki. Yeye aliulizwa: “Nani atainunua? Nani ataisoma?” Yeye alijibu kwa hakika: ‘Watu wote waliosoma wenye ujitoaji wa kimungu.’

[Maelezo ya Chini]

a Aliitwa pia kwa jina lake lililofanywa Kilatini, Stephanus, na jina lake lililofanywa Kianglikana, Stephens.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jitihada za Robert Estienne zimesaidia vizazi vya wanafunzi wa Biblia

[Hisani]

Bibliothèque Nationale, Paris

[Picha katika ukurasa wa 12]

Michoro ya kufundisha ya Estienne iliigwa kwa vizazi

[Hisani]

Bibliothèque Nationale, Paris

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki