Maskini Watalazimika Kungoja Hata Lini?
“Ikiwa jamii yenye uhuru haiwezi kuwasaidia wengi walio maskini, basi haiwezi kuwalinda wachache walio matajiri.”—John F. Kennedy.
“NINGEPENDA wakati ujao uwe mwangavu kwa kila mtu—bila umaskini, bila yeyote kukosa makao, paradiso!” Hivyo ndivyo mvulana wa miaka 12 kutoka São Paulo, Brazili, alivyosema. Lakini je, inawezekana kumaliza umaskini? Maskini watalazimika kungoja hata lini?
Watu fulani hujiona maskini kwa sababu hawawezi kununua vitu wanavyotaka. Hata hivyo, wazia hali yenye kusikitisha ya wale ambao wamekumbwa na umaskini kweli-kweli. Je, unaweza kuwazia jinsi watu hao wanavyopata magumu sana na jinsi wanavyokosa furaha? Wengine hulazimika kushindana na ndege na panya, wakitafuta chakula katika takataka! Umaskini kama huo utataabisha binadamu hata lini? Himizo la Federico Mayor, aliye mkurugenzi-mkuu wa UNESCO (Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, na Tamaduni), lafaa: “Tuacheni uvumilivu huu bandia utufanyao tuvumilie yasiyovumilika—ule umaskini, njaa na kuteseka kwa mamilioni ya wanadamu.”
Je, ndoto ya hali njema ya ulimwengu wote mzima itatimizwa? Maskini wana tumaini gani?
Maskini Wana Fursa Zipi?
Viongozi wenye nia nzuri huahidi kazi nyingi zaidi, mishahara bora, programu bora zaidi za kusaidia jamii, na ugawaji wa mashamba. Huenda wakakubaliana na aliyekuwa rais wa Marekani John F. Kennedy: “Ikiwa jamii yenye uhuru haiwezi kuwasaidia wengi walio maskini, basi haiwezi kuwalinda wachache walio matajiri.” Hata hivyo, makusudio mema hayatoshi kuondoa umaskini. Kwa kielelezo, je, ukuzi wa kiuchumi utaweza kuwasaidia wote walio maskini? Si lazima. Aliyekuwa kiongozi wa India Jawaharlal Nehru alisema hivi: “Nguvu za jamii ya ubepari, zikiachiliwa, zinaelekea kufanya walio matajiri kuwa matajiri zaidi na walio maskini kuwa maskini zaidi.” Hata hivyo, mbali na magumu na ukosefu, hali ya kuhisi kutofaa kitu huongezea mzigo walio maskini. Je, viongozi wa kibinadamu wanaweza kusaidia walio maskini kushinda hisia za kutoweza kusaidika na kukosa matumaini?
Kwa kweli, wengi walio maskini hoi wamejifunza kukabiliana na umaskini na kushinda hisia za kujiona kutofaa kitu wajapokabili matatizo makubwa sana, kama vile kupanda sana kwa maisha na ukosefu wa kazi ya kuajiriwa. Zaidi ya hayo, njaa kuu, ukosefu wa makao, na taabu zitaondolewa kabisa. Je, hili linakushangaza? Twakukaribisha usome makala ifuatayo: “Karibuni, Hakuna Atakayekuwa Maskini!”