Wakaraite na Utafutaji Wao wa Kweli
“CHUNGUZA kwa makini katika [Maandiko] nawe usitegemee maoni yangu.” Maneno hayo yalisemwa na kiongozi Mkaraite wa karne ya nane W.K. Wakaraite walikuwa akina nani? Je, twaweza kujifunza lolote la maana kutokana na kielelezo chao? Kujibu maswali haya, lazima turudi nyuma katika historia kwenye bishano la muda mrefu lililoongoza kwenye harakati ya Karaite.
Bishano Hilo Lilianzaje?
Katika karne za kumalizia kabla ya Wakati wa Kawaida, falsafa mpya ilianza katika Dini ya Kiyahudi. Ilikuwa wazo la kwamba Mungu alitoa Sheria mbili kwenye Mlima Sinai, moja iliyoandikwa na nyingine ya maneno.a Kufikia karne ya kwanza W.K., kulikuwa na mabishano makali kati ya wale waliokubali fundisho hili jipya na wale waliolikataa. Mafarisayo ndio waliokuwa waanzilishi, kwa upande mwingine Masadukayo na Waessene walikuwa miongoni mwa wapinzani.
Katikati ya bishano hili lenye kuendelea, Yesu wa Nazareti akatokea akiwa Mesiya aliyeahidiwa. (Danieli 9:24, 25; Mathayo 2:1-6, 22, 23) Yesu alikabili vikundi hivyo vyote vyenye kupingana vya Wayahudi. Katika kusababu pamoja nao, alizungumza dhidi ya kubatilisha neno la Mungu kwa sababu ya pokeo lao. (Mathayo 15:3-9) Yesu pia alifundisha kweli za kiroho katika njia awezayo tu Mesiya. (Yohana 7:45, 46) Zaidi ya hayo, wafuasi wa kweli wa Yesu pekee ndio waliotoa ushuhuda wa kutegemezwa kimungu. Wakajulikana kuwa Wakristo.—Matendo 11:26.
Wakati hekalu la Yerusalemu lilipoharibiwa katika mwaka wa 70 W.K., Mafarisayo ndio waliokuwa dhehebu la kidini pekee lililookoka likiwa nzima. Sasa bila ukuhani, dhabihu, na hekalu, Dini ya Wayahudi ya Kifarisayo ingeanzisha vibadala vya haya yote, wakiruhusu mapokeo na ufasiri kuzidi Sheria iliyoandikwa. Hili lilitolea nafasi “vitabu vitakatifu” vipya kuandikwa. Kwanza Mishna kikatokea, kikiwa na maongezeo na mafasiri yacho ya sheria yao ya maneno. Baadaye, maandishi mengine yalikusanywa yakaongezwa na kuitwa Talmud. Wakati uleule, Wakristo waasi-imani wakaanza kugeuza mafundisho ya Yesu. Vikundi hivyo vikaanzisha mifumo ya kidini yenye nguvu nyingi—mamlaka ya kirabi upande mmoja na mamlaka ya kanisa upande mwingine.
Kwa sababu ya ubishi wa Wayahudi pamoja na Warumi wapagani na baadaye pamoja na Warumi “Wakristo,” kitovu cha Dini ya Wayahudi mwishowe kikahamia Babiloni. Ilikuwa huko kwamba maandishi ya Talmud yalichapishwa katika njia yayo iliyokamilika zaidi. Ijapokuwa marabi walidai kwamba Talmud ilifunua mapenzi ya Mungu kwa njia kamili zaidi, Wayahudi wengi walihisi uzito wenye kuongezeka wa mamlaka ya kirabi nao wakatamani neno la Mungu walilopelekewa kupitia Musa na manabii.
Katika nusu ya mwisho ya karne ya nane W.K., Wayahudi katika Babiloni waliopinga mamlaka na itikadi za kirabi katika sheria yao ya maneno walimkubali kiongozi aliyesoma aliyeitwa Anan ben David. Yeye alitangaza haki isiyozuiliwa ya kila Myahudi ya kujifunza Maandiko ya Kiebrania kuwa chanzo pekee cha dini ya kweli, bila kujali fasiri ya kirabi au Talmud. Anan alifundisha hivi: “Chunguza kwa makini katika Tora [sheria ya Mungu iliyoandikwa] nawe usitegemee maoni yangu.” Kwa sababu ya kukaziwa huku kwa Andiko, wafuasi wa Anan wakajulikana kuwa Qa·ra·ʼimʹ, neno la Kiebrania limaanishalo “wasomi.”
Wakaraite na Marabi Wagongana
Ni vielelezo vipi kadhaa vya mafundisho ya Wakaraite yaliyoleta tisho katika vikundi vya kirabi? Marabi walikataza kula nyama na maziwa pamoja. Walitoa hili kuwa maelezo ya sheria ya maneno ya Kutoka 23:19, isemayo: “Usimtokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake.” Kwa upande mwingine, Wakaraite walifundisha kwamba mstari huu ulimaanisha vile tu ulivyosema—hakuna zaidi, hakuna upungufu. Walidai kwamba makatazo ya kirabi yalikuwa ya mwanadamu.
Kulingana na fasiri yao ya Kumbukumbu la Torati 6:8, 9, marabi walishikilia kwamba wanaume Wayahudi walipaswa kusali wakivalia tefillin, au filakteri, na kwamba mezuzah ilipaswa iwekwe kwa kila mwimo.b Wakaraite waliona mistari hii kuwa na maana ya kitamathali na ufananisho tu hivyo wakakataa amri kama hizo za kirabi.
Katika mambo mengine Wakaraite walikuwa na makatazo mengi zaidi kuliko marabi. Kwa kielelezo, fikiria maoni yao ya Kutoka 35:3, isemayo: “Hamtawasha moto katika nyumba zenu kwa siku ya sabato.” Wakaraite walikataza kuacha taa au stima ikiwaka hata ikiwa iliwashwa kabla ya Sabato.
Hasa baada ya kifo cha Anan, viongozi wa Karaite mara nyingi hawakupatana juu ya digrii na hali ya vizuizi fulani, na ujumbe wao kwa kawaida haukueleweka. Wakaraite walikosa umoja kwa sababu hawakutambua kiongozi yeyote hususa bali walikazia usomaji na fasiri ya kibinafsi ya Maandiko, tofauti na njia ya mamlaka ya kirabi. Hata hivyo, ijapokuwa hilo, harakati ya Karaite ilijulikana na kuwa na uvutano mwingi sana kupita jumuiya ya Kibabiloni ya Wayahudi na kuenea kuzunguka pote Mashariki ya Kati. Hata kitovu kikubwa cha Karaite kilianzishwa Yerusalemu.
Wakati wa karne za tisa na kumi W.K., wasomi wa Karaite walishinda katika funzo lililofanywa upya la lugha ya Kiebrania nao wakawa na kipindi cha ufanisi. Waliona mstari wa Andiko la Kiebrania likiwa takatifu, wala si mapokeo ya maneno. Wakaraite fulani wakawa wanakiliji wenye umakini wa Maandiko ya Kiebrania. Kwa hakika, ilikuwa sai ya Karaite iliyosukuma funzo la Maandiko la Kimasora miongoni mwa Wayahudi wote, likihakikisha kuhifadhiwa kwa andiko la Biblia lililo sahihi zaidi leo.
Wakati wa kipindi hiki cha ukuzi wa haraka, Wakaraite wa Dini ya Kiyahudi waliingia katika kazi ya mishonari ya waziwazi miongoni mwa Wayahudi wengine. Hilo lilitokeza tisho la wazi kwa Dini ya Kiyahudi ya kirabi.
Marabi Waliitikiaje?
Shambulizi la marabi lilikuwa vita vikali vya maneno, kwa kurekebisha kwa werevu na kubadili fundisho lao ili kufikia lengo lao. Wakati wa karne iliyofuata shambulizi la Anan, Dini ya Kiyahudi ya kirabi ilifuata taratibu kadhaa za Karaite. Marabi wakawa wenye ujuzi zaidi wa kunukuu Maandiko, wakiambatanisha njia na utaratibu wa Karaite katika ufasaha wao.
Kiongozi aliyetambuliwa wa mfululizo wa utendaji huu wa Karaite alikuwa Saʽadia ben Joseph, aliyekuja kuwa kiongozi wa jumuiya ya Wayahudi katika Babiloni katika nusu ya kwanza ya karne ya kumi W.K. Kitabu kikubwa cha Saʽadia, The Book of Beliefs and Opinions, kilitafsiriwa kwa Kiingereza na Samuel Rosenblatt, aliyesema hivi katika utangulizi wacho: “Ingawa . . . alikuwa na mamlaka juu ya Talmud katika siku yake, [Saʽadia] anaitumia kidogo sana kwa kulinganisha, inaonekana ni kwa sababu ilikuwa tamaa yake kushinda Wakaraite kwa kinga yao wenyewe, Sheria Iliyoandikwa waliyoikubali kuwa ya maana.”
Ikifuatia hatua za Saʽadia, Dini ya Kiyahudi ya kirabi mwishowe ilipata uongozi na uvutano mwingi sana. Ilitimiza hili kwa kuchukua mambo ya kutosha kutoka kwa Sheria Iliyoandikwa ili kupata ushuhuda wenye nguvu nyingi kutoka kwa ubishi wa Karaite. Tendo la mwisho lilifanywa na Musa Maimonidi, msomi wa Talmud aliyejulikana wa karne ya 12. Kwa mtazamo wake wa uvumilivu kuelekea Wakaraite aliokaa nao Misri, na vilevile njia yake ya usomi yenye kusadikisha, walimheshimu naye akadhoofisha uongozi wao wenyewe.
Harakati ya Karaite Yapoteza Uwezo
Sasa ikiwa haina umoja na bila muungano wa kujikinga, harakati ya Karaite lilipoteza uwezo na wafuasi. Mwishowe, Wakaraite wakarekebisha maoni na kanuni zao. Leon Nemoy, mwandishi wa harakati ya Karaite, aandika hivi: “Ingawa Talmud ilipigwa marufuku, maneno mengi ya kitalmud yalipatanishwa kisiri na njia ya Karaite ya kufuata sheria na desturi.” Kilichoko ni kwamba, Wakaraite walipoteza kusudi lao la awali nao wakachukua mengi ya Dini ya Kiyahudi ya kirabi.
Bado kuna karibu Wakaraite 25,000 katika Israeli. Maelfu kadhaa wengine waweza kupatikana katika jumuiya nyinginezo, hasa katika Urusi na Marekani. Hata hivyo, wakiwa na mapokeo yao wenyewe ya maneno, wanatofautiana na Wakaraite wa kwanza.
Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa historia ya Wakaraite? Kwamba ni kosa zito ‘kulitangua [‘kubatilisha,’ NW] neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo.’ (Mathayo 15:6) Kuwekwa huru kutokana na mapokeo yenye kulemaza ya wanadamu kwahitaji ujuzi sahihi wa Maandiko. (Yohana 8:31, 32; 2 Timotheo 3:16, 17) Ndiyo, wale watafutao kujua na kufanya mapenzi ya Mungu hawategemei mapokeo ya wanadamu. Badala ya hivyo, wao huchunguza Biblia kwa makini na kutumia maagizo ya muhimu ya Neno la Mungu lililopuliziwa.
[Maelezo ya chinis]]
a Kwa maelezo ya ile iliyoitwa sheria ya maneno, ona kurasa 8-11 za broshua Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Tefillin ni visanduku vidogo viwili vya ngozi vilivyo na vikaratasi vyenye mistari ya Maandiko. Visanduku hivi vilivaliwa kidesturi kwenye mkono wa kushoto na kichwani wakati wa sala za siku ya juma. Mezuzah ni kunjo dogo lililoandikwa Kumbukumbu la Torati 6:4-9 na 11:13-21, iliyowekwa ndani ya kisanduku na kutiwa kwenye mwimo.
[Picha katika ukurasa wa30]
Kikundi cha Wakaraite
[Hisani]
Kutoka kitabu The Jewish Encyclopedia, 1910