Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 9/1 kur. 22-26
  • ‘Upendo Haupungui Wakati Wowote’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Upendo Haupungui Wakati Wowote’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kikundi cha Funzo la Biblia Chaanzishwa
  • Upinzani wa Makasisi
  • Utendaji Wetu wa Kuhubiri
  • Miaka ya Vita
  • Kiwango cha Yehova cha Ndoa Chadhihirishwa Wazi
  • Mapendeleo ya Utumishi
  • Upendo wa Kweli Haupungui Wakati Wowote
  • Nilikuwa Mwana Mpotevu
    Amkeni!—2006
  • Familia Iliyonipenda Kikweli
    Amkeni!—1995
  • ‘Mdogo Akawa Elfu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Yehova ni Ngome Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 9/1 kur. 22-26

‘Upendo Haupungui Wakati Wowote’

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA SAMUEL D. LADESUYI

Nastaajabu nitazamapo miaka iliyopita na kuona yote yaliyotimizwa. Yehova amekuwa akifanya mambo ya ajabu duniani pote. Katika Ilesha, Nigeria, wachache wetu tulioanza kuhubiri katika 1931 tumekuwa makutaniko 36. Wale waliokuwa wahubiri karibu 4,000 katika Nigeria wakati wahitimu wa kwanza wa Watchtower Bible School of Gilead walipofika katika 1947 wameongezeka hadi zaidi ya 180,000. Katika siku za mapema, hatukutazamia wala kufikiri, mpanuko ambao ungetokea. Nashukuru kama nini kwamba nimeshiriki katika kazi hii ya ajabu! Acha niwaeleze juu yayo.

BABA yangu alikuwa muuza-bunduki na baruti kutoka mji mmoja hadi mwingine; mara nyingi hakuwa nyumbani. Alikuwa na wake saba niliowajua, lakini si wote walioishi naye. Baba yangu alirithi mama yangu kutoka kwa ndugu yake aliyekufa. Akawa mke wake wa pili, nami niliishi naye.

Siku moja baba alikuja nyumbani akitoka kumtembelea mke wake wa kwanza, aliyeishi katika kijiji jirani. Alipokuwa huko, aligundua kwamba ndugu-nusu wangu alikuwa akienda shuleni. Huyo ndugu-nusu wangu alikuwa na umri wa miaka kumi, umri niliokuwa nao. Hivyo baba akaamua kwamba ni lazima niende shuleni pia. Akanipa senti tisa—senti tatu za kununua kitabu cha mafundisho na senti sita za kununua kibao cha kuandikia. Hiyo ilikuwa katika 1924.

Kikundi cha Funzo la Biblia Chaanzishwa

Tangu miaka yangu ya mapema zaidi, nilipenda Neno la Mungu, Biblia. Nilifurahia mafundisho ya Biblia shuleni nami sikuzote nilisifiwa na walimu wangu wa shule ya Jumapili. Hivyo katika 1930, nilitwaa fursa ya kuhudhuria hotuba iliyotolewa na Mwanafunzi wa Biblia aliyetuzuru, aliyekuwa mmoja wa wale wa kwanza kuhubiri katika Ilesha. Baada ya hotuba hiyo, aliniangushia nakala ya kitabu The Harp of God katika lugha ya Kiyoruba.

Nilikuwa nimehudhuria shule ya Jumapili kwa ukawaida. Sasa nikaanza kubeba The Harp of God na kukitumia kupinga mafundisho fulani yaliyokuwa yakifundishwa huko. Mabishano yakaanza, nami nikaonywa mara nyingi na viongozi wa kanisa dhidi ya kufuata hilo ‘fundisho jipya.’

Mwaka uliofuata, nilipokuwa nikitembea-tembea barabarani, nilikutana na kikundi cha watu waliosikiliza mtu fulani aliyekuwa akiwatolea hotuba. Msemaji alikuwa J. I. Owenpa, Mwanafunzi wa Biblia. Alikuwa ametumwa huko na William R. Brown (aliyeitwa mara nyingi Bible Brown), aliyekuwa mwangalizi wa kazi ya kuhubiri Ufalme kutoka Lagos.a Nilitambua kwamba kikundi kidogo cha funzo la Biblia kilikuwa kimeundwa katika Ilesha ili wasome The Harp of God, hivyo nikajiunga nao.

Nilikuwa ndiye mchanga zaidi katika kikundi hicho—kijana wa shule tu, nikiwa na umri upatao miaka 16. Kama ilivyo kawaida ningeona haya, hata kuogopa, kushiriki karibu-karibu na watu wenye umri wa miaka 30 na zaidi. Lakini walifurahi sana kuwa pamoja nami miongoni mwao, nao walinitia moyo. Walikuwa kama baba zangu.

Upinzani wa Makasisi

Muda si muda tukaanza kukabili upinzani mkali kutoka kwa makasisi. Wakatoliki, Waanglikana, na wengineo, ambao walikuwa wakipigana wao kwa wao mbeleni, sasa waliungana dhidi yetu. Walitunga hila na machifu wa mahali petu wachukue hatua ya kutuvunja moyo. Walituma polisi kutunyang’anya vitabu, wakidai kuwa vilidhuru watu. Hata hivyo, ofisa wa utawala alionya kwamba hawakuwa na haki ya kuchukua vitabu hivyo, na majuma mawili baadaye vitabu hivyo vikarudishwa.

Baada ya hilo tuliitwa kwenye mkutano ambapo tulikutana na oba, au chifu mkuu, pamoja na watu wengine mashuhuri wa mji huo. Tulikuwa watu wapatao 30 wakati huo. Kusudi lilikuwa kutukomesha kusoma vitabu hivyo “hatari.” Waliuliza ikiwa tulikuwa wageni, lakini walipochunguza vizuri nyuso zetu, wakasema, “Hawa ni wana wetu, ingawa kuna wageni miongoni mwao.” Walituambia kwamba hawakutaka tuendelee kusoma vitabu hivyo vya dini ambayo ingetudhuru.

Tulirudi nyumbani bila kusema lolote, kwa kuwa tulikuwa tumeamua kutowasikiliza hata kidogo hao watu mashuhuri. Wengi wetu tulipendezwa sana na yale tuliyokuwa tukijifunza nasi tulikuwa tumeazimia kuendelea kujifunza. Hivyo, ingawa wachache waliogopa na kuacha kikundi chetu, wengi wetu tuliendelea na funzo katika duka la seremala. Hatukuwa na mwenye kuongoza. Tulianza kwa sala kisha tukasoma mafungu ya kitabu kwa zamu. Baada ya karibu muda wa saa moja, tulisali tena kisha tukarudi nyumbani. Lakini tulikuwa tukipelelezwa, na machifu na wakuu wa kidini wakaendelea kutuita kila baada ya majuma mawili na kutuonya dhidi ya kujifunza fasihi ya Wanafunzi wa Biblia.

Wakati uo huo, tulijaribu kutumia ujuzi kidogo tuliokuwa nao kusaidia watu, na wengi walikuwa wakikubaliana nasi. Watu mmoja-mmoja walikuwa wakiungana nasi. Tulifurahi sana, lakini bado hatukujua mengi kuhusu dini tuliyokuwa tukishirikiana nayo.

Mapema katika 1932 ndugu mmoja alifika kutoka Lagos kusaidia kutupanga kitengenezo, na katika Aprili “Bible” Brown pia akaja. Alipoona kwamba kulikuwa na kikundi chenye idadi ya karibu watu 30, Ndugu Brown akauliza juu ya maendeleo tuliyokuwa tukifanya katika kusoma kwetu. Tulimwambia yote tuliyojua. Akasema kwamba tulikuwa tayari kwa ubatizo.

Kwa kuwa kilikuwa kipindi cha ukame, ilitubidi kusafiri umbali wa kilometa 14 kutoka Ilesha hadi mtoni na karibu watu 30 miongoni mwetu wakabatizwa. Tangu wakati huo na kuendelea tulihisi tumehitimu kuwa wahubiri wa Ufalme na tukaanza kwenda nyumba kwa nyumba. Hatukutarajia kufanya hivyo, lakini sasa tulikuwa na shauku nyingi ya kushiriki na wengine yale tuliyoyajua. Ilitubidi kujitayarisha vizuri ili tupate utegemezo wa Biblia wa kukanusha mafundisho ya uwongo tuliyokabili. Hivyo kwenye mikutano yetu, tulizoea kuzungumza juu ya mafundisho, tukisaidiana kwa yale tuliyoyajua.

Utendaji Wetu wa Kuhubiri

Tulihubiri kotekote mjini. Watu walitudhihaki na kutupaazia sauti, lakini hatukujali hayo. Shangwe yetu ilikuwa kubwa kwa sababu tulikuwa tumepata kweli, ingawa bado tulikuwa na mengi ya kujifunza.

Tulienda nyumba kwa nyumba kila Jumapili. Watu wangeuliza maswali, nasi tungejaribu kuyajibu. Jumapili jioni tulitoa hotuba ya watu wote. Hatukuwa na Jumba la Ufalme, hivyo tulifanyia mikutano mahali peupe. Tulikusanya watu pamoja, tukatoa hotuba, na kuwaomba waulize maswali. Nyakati nyingine tulihubiri makanisani.

Pia tulisafiri kwenye sehemu ambapo watu hawakuwa wamesikia kamwe juu ya Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi, tulisafiri kwa baiskeli, lakini wakati mwingine tungekodisha basi. Tufikapo kijijini, tungepiga mbiu kwa sauti kubwa. Kijiji kizima kingetusikia! Watu walikimbia kuona ni nini kilichokuwa kikitendeka. Kisha tulitoa ujumbe wetu. Baada ya kumaliza, watu walisongamana kuchukua nakala za fasihi yetu. Tuliangusha nyingi sana.

Tulitazamia kwa hamu nyingi kuja kwa Ufalme wa Mungu. Nakumbuka kwamba tulipopokea Kitabu-Mwaka cha 1935, (Kiingereza) mmoja wa ndugu, alipoona ratiba iliyojaa ya mazungumzo ya andiko la mwaka huo, aliuliza hivi: “Je, hii inamaanisha kwamba tutamaliza mwaka mwingine mzima kabla Har–Magedoni haijaja?”

Katika kujibu mwenye kuongoza akauliza: “Je, ndugu unafikiri kwamba Har–Magedoni ikija kesho, tutaacha kusoma Kitabu-Mwaka?” Ndugu huyo aliposema la, mwenye kuongoza akauliza: “Basi kwa nini una wasiwasi?” Tulikuwa, na bado tunangoja kwa hamu siku ya Yehova.

Miaka ya Vita

Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, kuingiza vitabu vyetu nchini kulipigwa marufuku. Ndugu mmoja katika Ilesha alimtolea polisi kitabu Riches bila kujua. Polisi huyo akauliza: “Nani mwenye kitabu hiki?” Ndugu huyo akasema kilikuwa chake. Polisi huyo akasema kitabu hicho kilikuwa kimekatazwa, akampeleka katika kituo cha polisi, na kumfunga jela.

Nilienda katika kituo cha polisi, na baada ya kuulizia, nikamtoa ndugu huyo kwa dhamana. Kisha nikampigia simu Ndugu Brown katika Lagos kumweleza yaliyotokea. Pia nikauliza ikiwa kulikuwa na sheria yoyote iliyopiga marufuku kugawanywa kwa vitabu vyetu. Ndugu Brown akaniambia kwamba ni kuingiza tu nchini vitabu vyetu, si kugawanya, kulikopigwa marufuku. Siku tatu baadaye, Ndugu Brown akatuma ndugu mmoja kutoka Lagos aone ni nini kilichokuwa kikitendeka. Ndugu huyo akaamua kwamba sisi sote tunapaswa kwenda katika kazi ya kuhubiri siku iliyofuata tukiwa na magazeti na vitabu.

Tulienda sehemu tofauti-tofauti. Baada ya karibu muda wa saa moja, nililetewa habari kwamba akina ndugu walio wengi walikuwa wameshikwa. Hivyo ndugu aliyetembelea pamoja nami tukaenda kwenye kituo cha polisi. Polisi wakakataa kusikiliza maelezo yetu kwamba vitabu havikuwa vimepigwa marufuku.

Wale ndugu 33 waliokuwa wameshikwa walipelekwa kwenye mahakama ya Hakimu Mkuu katika Ife, nami nikaandamana nao. Watu wa mji waliotuona tukichukuliwa wakapaaza sauti, “Kazi ya watu hawa sasa imekwisha. Hawatarudi hapa tena.”

Shtaka lilitajwa mbele ya hakimu mkuu, Mnigeria. Vitabu vyote na magazeti yalitolewa. Akauliza ni nani aliyempa ruhusa mkubwa wa polisi kushika watu hawa. Mkubwa huyo wa polisi akajibu kwamba alikuwa amefuata maagizo kutoka kwa ofisa wa utawala. Hakimu mkubwa akamwita mkubwa wa polisi na wanne wa wawakilishi wetu, kutia ndani mimi, kwenye ukumbi wake.

Akauliza Bw. Brown ni nani. Tukamwambia kwamba alikuwa mwakilishi wa Watch Tower Society katika Lagos. Kisha akatuambia kwamba alikuwa amepokea habari kwa simu kutoka kwa Bw. Brown kutuhusu. Akaahirisha kesi siku hiyo na kuwapa ndugu dhamana. Siku iliyofuata akawaachilia ndugu hao, na kuwaamuru polisi warudishe vitabu.

Tulirudi Ilesha, tukiimba. Watu wakaanza tena kupaaza sauti, lakini wakati huo walikuwa wakisema, “Wamerudi tena!”

Kiwango cha Yehova cha Ndoa Chadhihirishwa Wazi

Ilikuwa katika 1947 kwamba wahitimu wa kwanza watatu wa Gileadi walifika Nigeria. Mmoja wa ndugu hawa, Tony Attwood, bado yupo hapa, akitumika katika Betheli ya Nigeria. Tangu wakati huo na kuendelea, tuliona mabadiliko makubwa katika tengenezo la Yehova katika Nigeria. Moja la mabadiliko makubwa lilikuwa maoni yetu juu ya kuoa wake wengi.

Nilimwoa Olabisi Fashugba katika Februari 1941 nami nilikuwa na ujuzi wa kutosha kutoongeza wake wengine. Lakini hadi 1947 wamishonari walipokuja, kuoa wake wengi kulikuwa jambo la kawaida katika makutaniko. Ndugu waliokuwa na wake wengi waliambiwa kwamba walikuwa wameoa zaidi ya mke mmoja bila kujua ni vibaya. Hivyo ikiwa walikuwa na wake wawili au watatu au wanne au watano, wangekaa nao, lakini hawapaswi kuongeza zaidi. Huo ndio mwongozo tuliokuwa nao.

Watu wengi walitaka sana kuungana nasi, hasa Jamii ya Cherubim na Seraphim katika Ilesha. Walisema kwamba Mashahidi wa Yehova ndio watu pekee waliofundisha kweli. Walikubaliana na mafundisho yetu na walitaka kugeuza makanisa yao yawe Majumba ya Ufalme. Tulifanya bidii ili kuwezesha muungano huo. Hata tulikuwa na vituo vya kuzoeza wazee wao.

Kisha kukaja mwongozo mpya kuhusu kuoa wake wengi. Mmoja wa wamishonari akatoa hotuba kwenye kusanyiko la mzunguko katika 1947. Akazungumza juu ya mwenendo mwema na tabia nzuri. Halafu akanukuu 1 Wakorintho 6:9, 10, lisemalo kwamba wasio waadilifu hawatarithi Ufalme wa Mungu. Kisha akaongeza hivi: “Na wenye wake wengi hawataurithi Ufalme wa Mungu!” Wasikilizaji wakapiga kelele hivi: “Ati, wenye wake wengi hawataurithi Ufalme wa Mungu!” Mgawanyiko ukatokea. Ilikuwa kama vita. Wapya wengi walioshiriki wakaacha kushiriki, wakisema: “Asante Mungu, hatujajiingiza sana kwa tengenezo hilo.”

Hata hivyo, wengi wa ndugu, wakaanza kurekebisha njia zao kwa kuwaacha huru wake zao. Waliwapa pesa na kusema, ‘Ikiwa wewe ni mchanga, nenda ukatafute mume mwingine. Nilifanya kosa kukuoa. Sasa ni lazima niwe mume wa mke mmoja.’

Haraka tatizo jingine likatokea. Wengine baada ya kuamua kukaa na mke mmoja na kuacha huru wengineo, walibadili mawazo yao na kuamua kutoka kurudisha mmoja wa wake wale wengine na kuacha huru yule waliyekuwa naye mbeleni! Hivyo shida ikaanza tena.

Mwongozo mwingine ukaja kutoka makao makuu katika Brooklyn, uliotegemea Malaki 2:14, ambalo hurejezea “mke wa ujana wako.” Mwongozo ulikuwa kwamba waume wanapaswa kukaa na mke wa kwanza waliyekuwa wameoa. Hivyo ndivyo swali hilo lilivyosuluhishwa hatimaye.

Mapendeleo ya Utumishi

Katika 1947 Sosaiti ikaanza kuimarisha makutaniko na kuyapanga kwa mizunguko. Walitaka kuweka rasmi ndugu wakomavu waliokuwa na ujuzi mkubwa kuwa ‘watumishi kwa ndugu,’ sasa waitwao waangalizi wa mzunguko. Ndugu Brown akaniuliza ikiwa ningekubali kuwekwa rasmi huko. Nikasema kwamba sababu iliyofanya nibatizwe ilikuwa kufanya mapenzi ya Yehova, nikiongeza hivi: “Hata ulinibatiza. Sasa ambapo kuna nafasi ya kumtumikia Yehova kwa ukamili zaidi, wafikiri nitakataa?”

Katika Oktoba mwaka huo, saba kati yetu tuliitwa kwenda Lagos na kuzoezwa kabla ya kutumwa katika kazi ya mzunguko. Katika siku hizo mizunguko ilikuwa mikubwa sana. Nchi nzima iligawanywa kwa mizunguko saba tu. Makutaniko yalikuwa machache.

Kazi yetu tukiwa watumishi kwa akina ndugu ilikuwa ngumu. Tulitembea kilometa nyingi kila siku, mara nyingi tukipitia misitu ya kitropiki yenye joto jingi. Kila juma ilitubidi kusafiri kutoka kijiji hadi kijiji. Mara nyingine nilihisi miguu yangu imekwisha. Mara nyingine nilihisi kana kwamba ninakufa! Lakini kulikuwa na shangwe nyingi pia, hasa kwa kuona idadi yenye kuongezeka ya watu waliokubali kweli. Kwa miaka saba tu, idadi ya wahubiri katika nchi hiyo ikaongezeka mara nne!

Nilishiriki katika kazi ya mzunguko hadi 1955 wakati afya mbaya iliponilazimisha kurudi Ilesha, nilipowekwa kuwa mwangalizi wa jiji. Kuwa nyumbani kuliniwezesha kuweka fikira zaidi katika kusaidia familia yangu kiroho. Leo watoto wangu wote sita wanamtumikia Yehova kwa uaminifu.

Upendo wa Kweli Haupungui Wakati Wowote

Nikumbukapo miaka mingi iliyopita, nina mengi sana ya kutolea shukrani. Kulikuwa na kuvunjika moyo, mahangaiko, na magonjwa, lakini kulikuwepo pia shangwe nyingi. Ingawa ujuzi na uelewevu wetu umekua baada ya miaka mingi, nimejifunza kupitia kwa mambo niliyoona maana ya 1 Wakorintho 13:8, (NW) lisemalo: ‘Upendo haupungui wakati wowote.’ Ikiwa unampenda Yehova na kushikamana kwa uimara katika utumishi wake, atakusaidia kupita matatizo yako na atakubariki sana.

Nuru ya kweli inazidi kung’aa zaidi na zaidi. Katika siku zile tulipoanza mara ya kwanza, tulifikiri Har–Magedoni ingekuja haraka; hiyo ndiyo sababu tuliharakisha kufanya yote tuliyoweza. Lakini yote hayo yalikuwa kwa faida yetu. Hiyo ndiyo sababu nakubaliana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Nitamsifu BWANA muda ninaoishi, nitamwimbia Mungu wangu ningali ni hai.”—Zaburi 146:2.

[Maelezo ya Chini]

a Ndugu Brown alikuwa akiitwa Bible Brown kwa sababu ya desturi yake ya kutaja Biblia kuwa mamlaka ya mwisho.—Ona “Mavuno ya Mweneza-Evanjeli wa Kweli” katika Mnara wa Mlinzi wa Septemba 1, 1992, ukurasa 32.

[Picha katika ukurasa wa23]

Samuel akiwa na Milton Henschel katika 1955

[Picha katika ukurasa wa24]

Samuel akiwa na mkeye, Olabisi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki