Mtu Mwenye Husuda
LUGHA ya Kiebrania ina neno moja tu la asili limaanishalo “wivu.” Linaporejezea wanadamu wenye dhambi, neno la Kiebrania laweza kutafsiriwa “husuda” au “ushindani.” (Mwanzo 26:14; Mhubiri 4:4, NW) Lakini, lugha ya Kigiriki ina maneno zaidi ya moja yamaanishayo “wivu.” Neno zeʹlos, kama ilivyo na kifanani chalo cha Kiebrania, laweza kurejezea wivu wa uadilifu na pia wivu wenye dhambi. Neno jingine la Kigiriki, phthoʹnos, hasa lina maana hasi. Katika New World Translation, sikuzote hilo hutafsiriwa kuwa “husuda.”
Neno phthoʹnos lilitumiwaje katika Kigiriki cha kale? The Anchor Bible Dictionary yaeleza: “Kama isivyo na mtu mwenye pupa, mtu mwenye phthonos si lazima atake vitu ambavyo hataki mwingine awe navyo; yeye hataki tu mwingine awe navyo. Yeye hutofautiana na mtu mwenye ushindani kwa njia ya kwamba kusudi lake, kama isivyo na mtu mwenye ushindani, si kushinda bali kuzuia wengine wasishinde.”
Mara nyingi mtu mwenye husuda hajui kwamba mtazamo wake ndio kisababishi kikubwa cha matatizo yake. “Mojawapo tabia za phthonos,” kamusi iyo hiyo yaeleza, “ni ukosefu wayo wa kujitambua. Mtu aliye phthoneros, akiombwa atetee mwenendo wake, sikuzote atajiambia na kuambia wengine kwamba wale anaowashambulia wanastahili kushambuliwa na kwamba ni hali ya ukosefu wa haki inayomfanya awachambue. Akiulizwa anawezaje kusema juu ya rafiki kwa njia hiyo, yeye atasema kwamba uchambuzi wake utamnufaisha rafiki huyo.”
Waandikaji wa Gospeli, Mathayo na Marko watumia neno la Kigiriki phthoʹnos kufafanua nia ya wale waliofanya Yesu auawe kimakusudi. (Mathayo 27:18; Marko 15:10) Ndiyo, walisukumwa na husuda. Hisia iyo hiyo yenye kudhuru imewafanya waasi-imani kuwa wenye chuki yenye ukatili dhidi ya ndugu zao wa zamani. (1 Timotheo 6:3-5) Si ajabu kwamba watu wenye husuda wamezuiwa kuingia katika Ufalme wa Mungu! Yehova Mungu ameamuru kwamba wote wanaoendelea ‘kujawa na husuda’ ni wenye ‘kustahili mauti.’—Warumi 1:29, 32; Wagalatia 5:21.
[Picha katika ukurasa w7]
Usiache husuda iharibu maisha yako