Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 11/1 kur. 4-8
  • Ukweli Kuhusu Malaika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukweli Kuhusu Malaika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupuuza Fungu la Shetani
  • Sala kwa Nani?
  • Je, Malaika Hawana Dini?
  • ‘Baba wa Uwongo’
  • Je, Ni Kuwafikia Malaika au Roho Waovu?
  • “Malaika wa Nuru”
  • ‘Malaika Akiruka Katika Mbingu ya Kati’
  • Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Namna Malaika Wanavyoweza Kukusaidia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Malaika—Je! Wao Wanaathiri Maisha Yako Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 11/1 kur. 4-8

Ukweli Kuhusu Malaika

Kufahamu mtu mara nyingi hutia ndani kujua jambo fulani kuhusu familia ya mtu huyo. Ndivyo ilivyo na kupata kumjua Yehova Mungu. Mengi zaidi yanahusika kuliko tu kujifunza jina lake. Ni lazima tujue pia jambo fulani kuhusu “familia” yake mbinguni. (Linganisha Waefeso 3:14, 15, “New World Translation.”) Biblia huwaita malaika “wana” wa Mungu. (Ayubu 1:6) Tufikiriapo fungu lao la maana katika Biblia, ni lazima tutake kujua mengi kuwahusu ili tufahamu mahali pao katika kusudi la Mungu.

JAMII fulani mpya inaanza kutokea. Watu walio wengi hawasemi tu kwamba wanaamini katika malaika; bali idadi inayoongezeka inadai kuwa imeathiriwa na malaika kwa kadiri fulani. Wamarekani 500 walipoulizwa, “Je, wewe mwenyewe umewahi kuhisi kuwapo kwa malaika katika maisha yako?” karibu theluthi moja walijibu ndiyo. Jambo la kushangaza pia ni idadi ya vijana wanaodai kuitikadi katika malaika—asilimia 76 kamili kulingana na uchunguzi mmoja katika Marekani! Ni dhahiri kwamba watu wanapendezwa na malaika. Lakini je, kufikiri huku kwa sasa kuhusu malaika kwapatanaje na kweli ya Biblia?

Kupuuza Fungu la Shetani

Tuzungumzapo juu ya malaika, hatupaswi kuwapuuza malaika waovu, viumbe vya kimbingu ambavyo Biblia husema viliasi dhidi ya Mungu. Wa kwanza kabisa ni Shetani. Kitabu kimoja kinachopendwa na wengi kiitwacho Ask Your Angels hudokeza kwamba Shetani ni “sehemu fulani ya Mungu” ambaye husaidia binadamu kuimarisha “misuli yao ya kiroho” kupitia majaribu ya kila wakati. Yajapokuwa “makusudio yenye upendo” ya Shetani, watungaji wa kitabu hicho wasema, kwa karne nyingi amehusianishwa kimakosa na uovu. Wao waongeza kwamba Shetani na Yesu, “ingawa hawakamilishani kabisa, angalau wako upande mmoja, wao ni sehemu muhimu za mtu mmoja.” Haya ni madai ya kushangaza, lakini Biblia yasema nini?

Biblia huonyesha wazi kwamba Shetani si “sehemu fulani ya Mungu” bali ni adui ya Mungu. (Luka 10:18, 19; Warumi 16:20) Yeye hupinga enzi kuu ya Yehova, na makusudio yake kuelekea wanadamu si yenye “upendo” hata kidogo. Bila huruma yeye humwaga hasira yake juu ya watumishi wa Mungu wa kidunia. Huwashtaki mbele ya Mungu mchana na usiku!a (Ufunuo 12:10, 12, 15-17) Kusudi la Shetani ni kuwapotosha kwa vyovyote. Kumnyanyasa bila huruma Ayubu mwaminifu kulidhihirisha wazi mtazamo wake usio na huruma kuelekea kuteseka kwa binadamu.—Ayubu 1:13-19; 2:7, 8.

Mbali na kuwa “upande mmoja,” Shetani na Yesu ni tofauti na ni maadui kabisa. Kwani, bila shaka Shetani ndiye aliyemwongoza Herode kuidhinisha mauaji makubwa ya watoto—yote hayo katika jitihada za kumuua mtoto mchanga Yesu! (Mathayo 2:16-18) Na mashambulizi ya Shetani yasiyokoma yaliendelea hadi kifo cha Yesu. (Luka 4:1-13; Yohana 13:27) Hivyo badala ya kuwa “sehemu muhimu za mtu mmoja,” Yesu na Shetani wametofautiana kabisa. Unabii wa Biblia huonyesha kwamba uadui wao hauwezi kuondoleka. (Mwanzo 3:15) Kwa kufaa, ni Yesu aliyefufuliwa atakayemharibu Shetani wakati wa Mungu ufikapo.—Ufunuo 1:18; 20:1, 10.

Sala kwa Nani?

Watu fulani wateteao utendaji wa malaika miongoni mwetu hupendekeza njia ya kutafakari na njia nyinginezo za ufundi ili kuwasiliana na malaika. “Ombi la unyofu la kuwasiliana na mshiriki yeyote wa familia hiyo ya kimbingu halitakosa kutimizwa,” chasema kitabu kimoja. “Uliza nawe utajibiwa.” Mikaeli, Gabrieli, Urieli, na Rafaeli, ni miongoni mwa malaika ambao kitabu hicho chapendekeza kuwaendea.b

Hata hivyo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kusali kwa Mungu, si kwa malaika. (Mathayo 6:9, 10) Vilevile, Paulo aliandika: ‘Katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.’ (Wafilipi 4:6) Hivyo, katika sala zao, Wakristo hawamwendei mwingine yeyote isipokuwa Yehova, nao hufanya hivyo katika jina la Yesu Kristo.c—Yohana 14:6, 13, 14.

Je, Malaika Hawana Dini?

Kulingana na Eileen Elias Freeman, asimamiaye AngelWatch Network, “malaika hupita kila dini, kila falsafa, kila itikadi ya kidini. Kwa kweli, malaika hawana dini kama tuijuayo.”

Hata hivyo, Biblia hueleza wazi kwamba malaika waaminifu wana dini; wao humwabudu Mungu wa kweli, Yehova, asiyevumilia ushindani wowote kutoka kwa miungu mingine. (Kumbukumbu la Torati 5:6, 7; Ufunuo 7:11) Hivyo, malaika fulani kama hao alijifafanua kwa mtume Yohana kuwa ‘mtumwa tu mwenzi’ wa wale wazitiio amri za Mungu. (Ufunuo 19:10, NW) Hakuna popote katika Biblia tusomapo juu ya malaika waaminifu wakitegemeza aina nyingineyo yote ya ibada. Wao humpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine.—Kutoka 20:4, 5.

‘Baba wa Uwongo’

Visa vingi vionwavyo eti ni kukutana na malaika vyatia ndani kuwasiliana na wafu. “Nilikuwa na hisia kwamba mjomba wangu alikuwa amepata njia ya kunifikia na kunijulisha kwamba alipata furaha mwishowe,” asema mwanamke mmoja aitwaye Elise baada ya kupokea kile alichohisi kuwa ishara. Vilevile Terri akumbuka rafiki mpendwa aliyekufa. “Juma moja baada ya maziko,” yeye asema, “alinijia katika kile nilichodhani kuwa ndoto. Aliniambia nisiombolezee kuondoka kwake, kwa sababu alikuwa na furaha na katika amani.”

Lakini Biblia hueleza kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Pia yasema kwamba mtu afapo, ‘siku hiyo mawazo yake yapotea.’ (Zaburi 146:4) Hata hivyo, Shetani, ni ‘baba wa uwongo.’ (Yohana 8:44) Ndiye aliyeanzisha uwongo wa kwamba nafsi ya kibinadamu huokoka kifo. (Linganisha Ezekieli 18:4.) Watu walio wengi leo wanaamini hivyo, jambo ambalo linafaana na kusudi la Shetani, kwa kuwa linakana uhitaji wa imani katika ufufuo—fundisho la Kikristo la msingi. (Yohana 5:28, 29) Hivyo, kutafuta habari kutoka kwa wafu au kuonekana kama unapokea ujumbe mbalimbali kutoka kwao bado ni sehemu nyingine ya utendaji wa malaika usiokubaliwa na Mungu.

Je, Ni Kuwafikia Malaika au Roho Waovu?

Utendaji mwingi wa sasa wa malaika huloweshwa katika mafumbo ya kishetani. Fikiria ono la Marcia. “Tangu Septemba hadi Desemba 1986,” yeye asema, “Nilianza kupokea ujumbe mbalimbali kutoka ‘ulimwengu usio wa asili.’ Niliona maono nikawa na ndoto za ajabu za ‘maisha ya awali.’ Nilikutana na marafiki waliokuwa wamekufa na kuwa na maono mengine mengi yasiyo ya asili ambapo nilipata kujua mambo kuhusu watu niliotoka tu kukutana nao. Pia nilibarikiwa na kipawa cha uandikaji usiohitaji jitihada na kupeleka ujumbe mbalimbali kutoka sehemu zisizo za asili. Watu fulani, ambao sikukutana nao kamwe maishani mwao duniani, wangepeleka ujumbe mbalimbali kwa wengine kupitia kwangu.”

Kutumia uaguzi kuwa njia ya “kuwasiliana” na malaika ni jambo la kawaida. Kitabu kimoja hutia moyo waziwazi wasomi wacho watumie mawe ya uchawi, kadi za ubashiri, kitabu fulani cha uaguzi cha Mashariki, sarafu, kusoma viganja, na unajimu. “Ruhusu utu wako wa ndani kabisa ukuongoze kwenye mwasiliani-roho afaaye,” watungaji wa kitabu hicho waandika, “na utumaini kwamba malaika atakutana nawe huko.”

Hata hivyo, kulingana na Biblia chochote ‘kitakacho kutana nawe huko’ kwa hakika si mmoja wa malaika wa Mungu. Kwa nini? Kwa sababu uaguzi unakaidi kabisa Mungu, na waabudu wa kweli—mbinguni na duniani—usijihusishe nao. Hata katika Israeli uaguzi ulikuwa kosa zito! “Mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA,” Sheria ikasema.—Kumbukumbu la Torati 13:1-5; 18:10-12.

“Malaika wa Nuru”

Haipasi kutushangaza kwamba Ibilisi aweza kufanya uaguzi uonekane kuwa na manufaa, hata wa kimalaika. Biblia husema kwamba Shetani “hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Hata anaweza kuunda mambo ya ajabu kisha afanye yatendeke, akidanganya watazamaji wafikiri kwamba mambo hayo ya ajabu yanatoka kwa Mungu. (Linganisha Mathayo 7:21-23; 2 Wathesalonike 2:9-12.) Lakini kazi zote za Shetani—ziwe zinaonekana nzuri au mbaya jinsi gani—hutumikia moja la makusudi haya mawili: kugeuza watu dhidi ya Yehova au kupofusha tu akili zao ili “isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Njia hii ya pili ya udanganyifu mara nyingi ndiyo yenye matokeo zaidi.

Fikiria hili simulizi la Biblia la msichana fulani mtumishi katika karne ya kwanza. Matabiri yake yaliwaletea mabwana-wakubwa wake faida nyingi. Kwa siku nyingi aliwafuata wanafunzi, akisema: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi Sana, wanaowatangazia nyinyi njia ya wokovu.” Maneno yake yalikuwa ya kweli. Hata hivyo, simulizi hilo hutuambia kwamba alikuwa amepagawa, si na malaika fulani, bali na “roho mwovu wa uaguzi.” Mwishowe, Paulo “akageuka na kumwambia huyo roho: ‘Nakuagiza wewe katika jina la Yesu Kristo umtoke yeye.’ Naye akatoka saa ileile.”—Matendo 16:16-18, NW.

Kwa nini Paulo alimfukuza roho huyo? Isitoshe, aliwapa faida nyingi mabwana-wakubwa wa msichana huyo mwenye kupagawa na roho mwovu. Akiwa na nguvu zisizo za asili, msichana huyo mtumishi, huenda aliwaambia wakulima wakati wa kupanda, wanawali wakati wa kuolewa, na wachimba-madini mahali pa kutafuta dhahabu. Roho huyo hata alimsukuma msichana huyo kuzungumza maneno fulani ya kweli, akiwasifu wanafunzi waziwazi!

Hata hivyo, alikuwa ‘roho mwovu wa uaguzi.’ Basi, hakuwa na haki ya kutangaza juu ya Yehova na uandalizi wake wa wokovu. Maneno yake ya kusifu, labda yakisemwa ili kusadikisha matabiri ya msichana huyo mtumishi, yalikengeusha fikira za watazamaji kutoka kwa wafuasi wa kweli wa Kristo. Akiwa na sababu nzuri, Paulo aliwaonya Wakorintho hivi: “Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana [“Yehova,” NW] na katika meza ya mashetani.” (1 Wakorintho 10:21) Si ajabu, Wakristo wa karne ya kwanza waliharibu vitabu vyao vyote vilivyohusiana na uaguzi.—Matendo 19:19.

‘Malaika Akiruka Katika Mbingu ya Kati’

Kama vile tumeona, Biblia hufunua utendaji ulio mwingi wa sasa wa malaika kuwa na uhusiano wa karibu na Mpinzani wa Mungu, Shetani Ibilisi. Je, hilo lamaanisha kwamba malaika watakatifu hawahusiki na mambo ya kibinadamu? Sivyo ilivyo, sasa wanatimiza kazi yenye nguvu nyingi duniani. Ni ipi hiyo? Ili kujibu, ni lazima tutazame kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Malaika wanatajwa mara nyingi katika kitabu hiki kuliko kitabu kinginecho cha Biblia.

Kwenye Ufunuo 14:6, 7, twasoma rekodi ya mtume Yohana ya ono hili la kiunabii alilopokea: ‘Nikaona malaika mwingine, akiruka katika mbingu ya kati, mwenye Injili ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa, akasema kwa sauti kuu, Mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja. Msujudieni yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji.’

Andiko hilo lakazia kazi iliyo kuu ya malaika leo. Wanahusika katika mgawo muhimu kabisa—ule wa kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Ni kuhusu kazi hii kwamba Yesu aliwaahidi wafuasi wake hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mathayo 28:18-20) Yesu yupo pamoja na wafuasi wake jinsi gani? Njia moja ni kwa kuwaandalia msaada wa kimalaika ili kazi hii kubwa sana iweze kutimizwa.

Mashahidi wa Yehova hutumia zaidi ya saa bilioni moja kila mwaka wakihubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Huku wakitimiza kazi hii, wao huona uthibitisho wa mwongozo wa kimalaika. Katika huduma yao ya mlango kwa mlango, mara nyingi imetokea kwamba wanakuta watu fulani waliokuwa wametoka tu kusali ili mtu fulani awasaidie kufahamu makusudi ya Mungu. Mwongozo wa kimalaika, pamoja na ujianzilishi wa Mashahidi, umefanya mamia ya maelfu wapate ujuzi wa Yehova kila mwaka!

Je, wewe unamsikiliza malaika arukaye katika mbingu ya kati? Wakati mwingine Mashahidi wa Yehova wakutembeleapo kwa nini usizungumze nao kwa kirefu zaidi ujumbe huu wa kimalaika?

[Maelezo ya chinis]

a Maneno “Shetani” na “Ibilisi” humaanisha “mkinzani” na “mchongezi.”

b Huku Mikaeli na Gabrieli wakitajwa katika Biblia, majina ya Rafaeli na Urieli yapatikana katika vitabu vya Kiapokrifa, ambavyo si sehemu ya vitabu vya Biblia vinavyokubaliwa.

c Ona kwamba sala inapitia kwa Yesu, wala haimwendei yeye. Sala hutolewa katika jina la Yesu kwa sababu damu yake iliyomwagwa ilifungua njia ya kumkaribia Mungu.—Waefeso 2:13-19; 3:12.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

MALAIKA NI AKINA NANI?

KINYUME cha itikadi za wengi, malaika si nafsi zilizoondoka za binadamu waliokufa. Biblia husema waziwazi kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Basi, malaika walitoka wapi? Biblia huonyesha kwamba kila mmoja wao aliumbwa na Mungu kabla ya kuwekwa msingi kwa dunia. (Ayubu 38:4-7) Ukubwa wa familia ya kimbingu ya Mungu huenda ukawa mamia ya mamilioni ya malaika, labda mabilioni au zaidi! Malaika kadhaa walijiunga na Shetani katika uasi wake.—Danieli 7:10; Ufunuo 5:11; 12:7-9.

Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa utaratibu, si ajabu kwamba familia yake kubwa sana ya kimalaika ina utaratibu.—1 Wakorintho 14:33.

• Malaika mkubwa zaidi, katika uwezo na mamlaka, ni malaika mkuu, Yesu Kristo, aitwaye pia Mikaeli. (1 Wathesalonike 4:16; Yuda 9) Chini ya mamlaka yake kuna maserafi, makerubi, na malaika.

• Maserafi wanatumikia kwenye kiti cha ufalme cha Mungu. Kwa wazi mgawo wao unatia ndani kutangaza utakatifu wa Mungu na kudumisha usafi wa watu wake.—Isaya 6:1-3, 6, 7.

• Makerubi pia wanaonekana mahali Yehova alipo. Wakiwa wasaidizi au wasimamizi wa kiti cha ufalme cha Mungu, wao hushikilia utukufu wa Yehova.—Zaburi 80:1; 99:1; Ezekieli 10:1, 2.

• Malaika (maana yake “wajumbe”) ni mawakili wa Yehova. Wao hutekeleza mapenzi ya kimungu, yawe yanatia ndani kuokoa watu wa Mungu au kuharibu waovu.—Mwanzo 19:1-26.

[Picha katika ukurasa w7]

Je, wewe unamsikiliza malaika arukaye katika mbingu ya kati?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki