Je, Kuna Malaika Miongoni Mwetu?
Jambo hilo lilifanyika haraka sana. Akiwa na mawazo mengi bila kufikiria alipo, Marilynn alitembeatembea katika kijia cha gari-moshi. Kwa ghafula, alisikia mgurumo mkubwa. Akainua kichwa, na mara akagundua kwamba alikuwa amesimama moja kwa moja mbele ya gari-moshi lililokuwa likija! Marilynn akashindwa kwenda kwa sababu ya hofu. Gari-moshi hilo lilikuwa karibu sana hivi kwamba angeona macho ya buluu na uso uliojawa na hofu nyingi wa dereva walo. Baadaye Marilynn hakusahau kamwe yaliyotokea. “Ilikuwa kana kwamba jitu lilinisukuma kutoka nyuma,” yeye akasema. “Niliruka kutoka kwenye reli hiyo na kuanguka kwenye ukoko wa makaa-mawe kando tu ya reli hiyo.” Akiwa na majeraha madogo, Marilynn akainuka kumshukuru mwokozi wake—lakini hapakuwa na mtu yeyote! Akaamua nini? “Malaika mlinzi wangu aliokoa uhai wangu,” Marilynn asema. “Kwani ingalikuwa ni nani mwingine?”
ULIMWENGU wenye mashaka kwa ghafula waonekana ukijawa na malaika. Katika miaka ya majuzi, viumbe vya kimbingu vimekuwa habari za maonyesho ya televisheni, sinema, na hata michezo ya kuigiza ya Hadharani. Vitabu vinavyohusu malaika ni vingi sana kwenye orodha ya vitabu vya kidini vinavyouzwa kwa wingi. Kuna vyama, mikutano, na vijitabu vyenye habari za malaika. Mikutano ya mijadala imefanywa ili kukusaidia—kama makala moja isemavyo—upate “utegemezo wa kimalaika.”
Watumiao fursa ipatikanayo ya utendaji wa malaika ni wafanya biashara watengenezao bidhaa nyingi sana za matumizi. “Chochote chenye malaika juu yacho hununuliwa sana,” asema mtu fulani anayemiliki duka pamoja na mwenzake Marekani. Kuongezea uuzaji wa vitabu vingi, yeye huorodhesha “sanamu za malaika, pini, wanasesere, T-shati, vibandiko vya matangazo na kadi za salamu”—zote zikijumlika kuwa kile ambacho mwandishi mmoja wa gazeti aziita “faida za kimbingu.”
Lakini huu si msisimuko tu, wasisitiza wale wateteao wazo la kuwako kwa malaika miongoni mwetu. Ili kuthibitisha dai lao, wao hutoa ushuhuda mmoja baada ya mwingine—“maono halisi” ya kukutana na malaika. Wengine husema waliona malaika katika umbo la kibinadamu. Wengine waliona nuru, wakasikia sauti, wakahisi kuwapo kwa kitu fulani, au wakahisi msukumo fulani waaminio kuwa wa kimalaika. Wengi, kama vile Marilynn, husema kwamba malaika aliokoa uhai wao.
Ni jambo gani linatendeka? “Nafikiri kuna uhuisho wa hali ya kiroho,” asema Joan Wester Anderson, ambaye ameandika vitabu viwili kuhusu kukutana na “viumbe vyenye uwezo upitao wa binadamu.” Alma Daniel, aliyesaidia kuandika kitabu kingine, aeleza zaidi. Yeye asema kwamba malaika “sasa wameagizwa wajijulishe ili kwamba watu wengi zaidi na zaidi waweze kufikiwa. Jambo linalofanya tuwaone kwa wingi ni kwa sababu wanataka iwe hivyo. Wanajidhihirisha wenyewe.”
Je, ndivyo ilivyo kweli? Au kuna kitu kingine zaidi kinachochochea uvutio wa sasa kwa malaika? Ili kujua jambo hilo, ni lazima tuchunguze Neno la Mungu. Biblia ina ukweli kuhusu malaika, kama tutakavyoona.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Kurasa 3 na 4: The New Testament: A Pictorial Archive from Nineteenth-Century Sources, by Don Rice/Dover Publications, Inc.