Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 12/1 kur. 20-23
  • Mwenye Umri wa Miaka Mia Moja na Mwenye Nguvu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwenye Umri wa Miaka Mia Moja na Mwenye Nguvu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Badiliko la Mtazamo
  • Kukabili Majaribu
  • Ziara ya Kustaajabisha
  • Kukabili Hali Baada ya Upotezo
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Nimefurahia Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 12/1 kur. 20-23

Mwenye Umri wa Miaka Mia Moja na Mwenye Nguvu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RALPH MITCHELL

Baba yangu, mwanamume wa kimo cha kadiri, alikuwa mhubiri Mmethodisti. Alihamishwa kutoka kanisa hadi kanisa baada ya kila miaka miwili au mitatu kwa mfululizo hasa katika miji midogo, kutia ndani Asheville, North Carolina, Marekani, ambako nilizaliwa katika Februari 1895. Hivyo nilikua nikijua Jumuiya ya Wakristo vizuri.

NAKUMBUKA nikiwa kijana mchanga nikipelekwa kwenye “benchi ya waombolezaji wa dhambi” kwenye mikutano ya kuhuisha ili nikajazwe roho takatifu—ili “nipate dini,” kama walivyoliita jambo hilo. Niliambiwa nitubu dhambi zangu, nishike Amri Kumi, na niwe mwema. Basi, ningeweza kwenda mbinguni ninapokufa. ‘Basi,’ nikajiambia, ‘nafikiri nitaenda helo kwa sababu siwezi kuwa mwema vya kutosha kwenda mbinguni.’ Nilifikiri kwamba ni watu wazima tu—hasa wahubiri—ndio waliokuwa wakiishi kulingana na viwango vya Biblia.

Lakini hata kabla ya miaka yangu ya utineja, nilianza kuona unafiki katika dini. Kwa kielelezo, baba yangu angedhabihu mahitaji ya kimwili ya familia yake ili tu aweke kiasi kikubwa cha pesa katika hazina ya askofu kwenye mkutano wa makasisi. Alitumaini kwamba jambo hilo lingemwezesha kupewa cheo katika kanisa lenye watu wengi zaidi. Nakumbuka mhubiri mmoja wa kwetu aliyekuwa pia mkulima wa pamba. Alitamani kupata cheo cha umashuhuri, hivyo akauza mabunda mia moja ya pamba na kwenda kwenye huo mkutano akiwa na pesa chungu nzima. Ilipoonekana kwamba wametwaa pesa zote walizoweza kupata kutoka kwa wahudhuriaji—wengi wao wakiwa wahubiri—mhubiri huyo aliyekuwa mkulima wa pamba akaruka juu na kupaaza sauti akisema: “Je, hizi tu ndizo mnazompa askofu wenu? Kila mhubiri anayetoa dola tano, nitatoa dola kumi!” Zaidi ya dola elfu moja zikakusanywa, naye askofu akaweka mtu huyo kuwa mzee msimamizi juu ya baba yangu. Sikuweza kuamini kwamba kuwekwa huko kulitoka kwa Mungu. Tangu wakati huo na kuendelea nikawa na mashaka kuhusu chochote kinachohusu dini.

Nilitwaliwa kwa nguvu wakati Marekani iliingia katika vita ya ulimwengu ya kwanza. Nakumbuka vizuri nikisikia makasisi wa jeshi wakituhubiria sisi wanajeshi kuhusu kupigania nchi yetu kwa uaminifu-mshikamanifu, nalo jambo hilo liliongeza tu chuki yangu kuelekea dini. Miradi yangu ilikuwa niokoke vita, nimalize masomo yangu, kisha nioe. Dini haikuwa katika mipango yangu ya wakati ujao.

Badiliko la Mtazamo

Katika 1922, nilimpenda mwanamke mchanga aitwaye Louise. Ikawa kwamba alikuwa Mkatoliki aliyejitoa, na tulipoamua kuoana, alitaka ndoa ya Kikatoliki. Mimi sikutaka sherehe ya kidini ya aina yoyote, hivyo alikubali kwamba tungeoana kwenye jengo la manispaa katika New York City.

Mwanzoni hatukuwa na mabishano juu ya dini. Nilimweleza tu kwamba sikutumaini dini na kwamba tungepatana ikiwa tu haingetajwa. Kisha, kati ya miaka ya 1924 na 1937, tukazaa watoto—wakafuatana, mpaka tukawa na wavulana watano na wasichana watano! Louise alitaka watoto wetu wahudhurie shule ya Kikatoliki. Sikutaka wapate mazoezi yoyote ya kidini, hivyo tuligombania hilo.

Mapema katika 1939 jambo fulani likatendeka ambalo lingebadili mtazamo wangu kwa ujumla juu ya dini. Henry Webber na Harry Piatt, Mashahidi wa Yehova wawili, walikuja nyumbani mwangu katika Roselle, New Jersey. Upesi ikaonekana kwamba walitaka kuongea juu ya habari nisiyotaka kuizungumza—dini. Imani yangu bado ilikuwa ina uchungu kwa sababu makasisi jeshini walisema, ‘Pigania nchi yako,’ huku makasisi nyumbani wakisema ‘Usiue.’ Unafiki kama nini! Nilifikiri nitawarekebisha sawasawa hao Mashahidi wawili. “Acheni niwaambie kitu,” nikasema, “Ikiwa dini yenu ni ya kweli, basi nyingine zote ni za uwongo. Na ikiwa moja tu ya nyinginezo ni ya kweli, basi zile nyingine zote, kutia ndani yenu, ni za uwongo. Kunaweza kuwa na dini moja tu ya kweli.” Kwa kushangaza, walikubaliana nami!

Kisha, wakaniomba nilete Biblia yangu na kufungua 1 Wakorintho 1:10. Humo nikasoma hivi: “Basi, ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala msifarakane; bali muunganishwe pamoja katika akili moja na hukumu moja.” (King James Version) Nilishangazwa na andiko hilo. Wakati uleule, niliogopa kwamba watu hao wawili walikuwa wakijaribu kunihusisha katika aina fulani ya madhehebu. Hata hivyo nilikuwa nimejifunza jambo fulani—kwamba hakupaswi kuwa na migawanyiko miongoni mwa Wakristo. Nilikuwa na maswali mengine mengi akilini mwangu. Kwa kielelezo, Ni nini hutokea kwa nafsi wakati wa kufa? Jinsi ningependa kuzungumza swali hilo pamoja nao! Lakini, nikafikiri, hilo lingeleta ubishi mwingi sana wa kidini nyumbani.

Kisha mmoja wa watu hao wawili akasema: “Tungependa kurudi na kusema nawe tena juma lijalo.” Kwa busara nikajaribu kuwakomesha, lakini mke wangu akasema. “Ralph,” akasema, “wanataka kujua wakati wanaweza kurudi.” Hilo lilinishangaza, kwa kuwa mke wangu alikuwa Mkatoliki mwenye bidii! Hata hivyo, nikafikiri, ‘Huenda tunaweza kupata mambo fulani ya kukubaliana juu ya dini.’ Hivyo nikakubali Henry Webber na Harry Piatt warudi Ijumaa iliyofuata.

Hivyo ndivyo nilivyoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Muda si muda baada ya hilo, nilialikwa kuhudhuria mkusanyiko katika Madison Square Garden katika New York City. Nakumbuka vizuri hotuba ya Joseph F. Rutherford “Serikali na Amani,” iliyotolewa katika Juni 25, 1939. Nilikuwa mmoja wa watu 18,000 waliokuwapo. Kwa hakika, watu 75,000 walisikia hotuba hiyo, ukitia ndani waliokuwa wameunganishwa kwa mitambo ya kimataifa kwa waya za redio na simu.

Hata hivyo mambo hayakuendelea kwa urahisi. Wafuasi wa kasisi wa Katoliki Charles Coughlin walikuwa wametisha kuvunja kusanyiko hilo, na kusema kweli, kufikia karibu nusu ya mwisho wa hotuba ya Ndugu Rutherford, mamia ya watu waliokuwa wamekasirika wakaanza kudhihaki na kupiga kelele za shime kama vile, “Heil Hitler!” na “Viva Franco!” Kulikuwa na msukosuko mwingi hivi kwamba ghasia ilisikika kupitia kamba za simu! Iliwachukua walinda-lango karibu dakika 15 kunyamazisha umati huo. Wakati huo wote, Ndugu Rutherford, kwa ujasiri, aliendelea kuongea, huku makofi ya kurudia-rudia yakimuunga mkono.

Sasa nikawa na udadisi sana. Je, kwa nini kasisi Mkatoliki achochee uadui mwingi namna hii dhidi ya Mashahidi wa Yehova? Niliwazia kwamba ni lazima kuwe na kweli fulani kuhusu yale Rutherford alikuwa akihubiri—ambayo kasisi hakutaka watu kama mimi wasikie. Hivyo nikaendelea kujifunza Biblia na kufanya maendeleo. Mwishowe, katika Oktoba 1939, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Baadhi ya watoto wangu wakabatizwa mwaka uliofuata, na mke wangu, Louise, akabatizwa katika 1941.

Kukabili Majaribu

Muda mfupi baada ya kuikubali kweli, mama yangu akafa, ikanibidi nirudi North Carolina kwa maziko yake. Nilihisi kwamba singeweza kwa dhamiri safi kuhudhuria ibada za maziko ambazo zingefanyiwa ndani ya kanisa Methodisti. Hivyo nikampigia baba yangu simu kabla ya kufunga safari nikamwambia aweke sanduku la maiti kwenye chumba cha kuhifadhia maiti. Alikubali, lakini nilipofika huko, walikuwa njiani kuelekea kanisani, ambako walifikiri bila shaka nitajiunga nao.

Sikufanya hivyo, na jambo hilo likasababisha mvurugo mkubwa katika familia yetu. Ingawa sikuzote tulikuwa marafiki wa karibu na dada yangu Edna, baada ya maziko ya mama yangu hangenisemesha. Niliandika barua nyingi, lakini hakuzijibu. Kila kiangazi Edna alipokuja New York kuhudhuria mazoezi ya ualimu kwenye City College, nilijaribu kumwona. Lakini angekataa kuniona, akisema kwamba alikuwa na shughuli nyingi. Mwishowe nikakata tamaa, kwa kuwa ilionekana kana kwamba nilikuwa ninamsumbua tu. Miaka mingi ingepita kabla ya kusikia tena kutoka kwake.

Kwa sababu ya kukataa kusalimu bendera, watoto wangu sita walifukuzwa shule katika 1941, kama ilivyokuwa kwa watoto wengine wengi katika Marekani na Kanada. Ili kutimiza matakwa ya kisheria ya elimu, Mashahidi hao walifanya mpango wa shule zao wenyewe zilizoitwa Shule za Ufalme. Ile iliyokuwa hoteli katika Lakewood, New Jersey, ikawa mahali pa shule ambapo watoto wangu walihudhuria. Jumba la Ufalme lilikuwa katika orofa ya kwanza, pamoja na darasa la shule, jikoni, na chumba cha kulia. Sehemu ya kulala ya wasichana ilikuwa kwenye orofa ya pili, na chumba cha kulala cha wavulana kilikuwa katika orofa ya tatu. Ilikuwa shule nzuri. Wengi wa watoto waliokuwa wakilala humo walienda nyumbani miisho juma pekee. Walioishi mbali zaidi walienda nyumbani kila baada ya miisho juma miwili.

Tangu miaka yangu ya mapema katika kweli, nilikuwa na tamaa yenye nguvu ya kuwa painia, kama waeneza-evanjeli wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova walivyojulikana. Kwenye mkusanyiko wa 1941 katika St. Louis, Missouri, ndugu fulani aliyeshiriki kwenye programu alieleza jinsi aliweza kupainia huku akilea watoto 12. Nikafikiri, ‘Ikiwa anaweza kupainia akiwa na 12, naweza kupainia nikiwa na 10.’ Hata hivyo, hali zangu hazikuniruhusu kuanza upainia hadi miaka 19 baadaye. Mwishowe, katika Oktoba 1, 1960, niliweza kuanza kumtumikia Yehova nikiwa painia wa kawaida.

Ziara ya Kustaajabisha

Katika 1975, nilipokea simu kutoka kwa dada yangu Edna. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 80, nami sikuwa nimemwona wala kusikia sauti yake kwa miaka 20 hivi. Alikuwa akipiga simu kutoka uwanja wa ndege, na akaniambia niende niwachukue pamoja na mumeye. Nilifurahi kumwona Edna tena, lakini jambo la kustaajabisha zaidi lilikuwa bado. Tukielekea nyumbani, mumeye alisema, “Una mwongofu.” Sikujua alimaanisha nini. Tulipofika nyumbani, mara nyingine tena akasema, “Una mwongofu hapa.” Mke wangu akaelewa mara moja. Akimgeukia dada yangu, akamuuliza, “Edna, wewe ni Shahidi?” “Ndiyo, mimi ni Shahidi,” Edna akajibu.

Edna alipataje kuikubali kweli? Katika 1972, kwa jitihada ya kurudisha uhusiano wetu uliokuwa umevunjika, nilikuwa nimemtumia zawadi ya uandikishaji wa Mnara wa Mlinzi. Karibu mwaka mmoja baadaye, Edna akawa mgonjwa naye hangeweza kutoka nyumbani. Yale magazeti bado yalikuwa juu ya dawati lake yakiwa yamefungwa. Kwa udadisi Edna alifungua moja yayo na kuanza kusoma. Baada ya kulimaliza, akifikiria, ‘Hii ni kweli!’ Kufikia wakati Mashahidi wa Yehova walipomtembelea nyumbani kwake, alikuwa amesoma magazeti yote ya Mnara wa Mlinzi na kuyamaliza. Alikubali funzo la Biblia, na muda si muda akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Kukabili Hali Baada ya Upotezo

Mwishowe, mke wangu, Louise, akashikwa na ugonjwa wa sukari, nayo hali yake ikazidi kuwa mbaya mpaka akafa katika 1979, akiwa na umri wa miaka 82. Louise alipokufa, sehemu yangu fulani ilikufa vilevile. Ulimwengu wangu wote ni kana kwamba ulisimama. Sikujua la kufanya. Sikuwa na mipango ya wakati ujao, nami nilihitaji kitia-moyo upesi. Mwangalizi asafiriye, Richard Smith, alinitia moyo niendelee na upainia. Niliona kwamba faraja yangu kubwa ilitokana na kuwafariji wengine waliokuwa wamepoteza wapendwa katika kifo.

Katika 1979, Watch Tower Society ilikuwa ikifanya mpango wa kuzuru Israel, hivyo nikapeleka jina langu. Safari hiyo ilinichochea sana, na niliporudi nyumbani, nikaendelea kufanya kazi ya utumishi wa painia. Tangu wakati huo kila mwaka nimelifanya kuwa zoea langu kusaidia katika eneo lisilogawiwa mtu au lisilofanyiwa kazi mara nyingi katika sehemu nyingine ya nchi. Ujapokuwa umri wangu mkubwa, bado naweza kujitoa kwa ajili ya pendeleo hili.

Nakadiria kwamba kwa miaka yote, nimepata shangwe ya kusaidia kama watu 50 kuingia kwenye barabara ya uhai. Wengi wa watoto wangu wako katika kweli. Wawili wa binti zangu wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida. Binti mwingine, Louise Blanton, anatumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, pamoja na mumeye, George, na mmoja wa wana wangu ametumikia akiwa mzee kwa miaka mingi.

Bila shaka, kwa sababu ya kutokamilika kulikorithiwa kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu, sisi sote tunaweza kuwa wagonjwa na kufa. (Warumi 5:12) Kwa hakika maisha yangu hayajawa bila maumivu na uchungu. Wakati huu naugua ugonjwa wa yabisi-kavu katika mguu wangu wa kushoto. Nyakati nyingine hunisumbua sana, lakini haujanizuia kuwa mtendaji. Nami naomba kwamba usinizuie. Nataka kuendelea kutenda. Tamaa yangu kubwa ni kuendelea katika utumishi wa painia hadi mwisho, nikifanya yote niwezayo kujulisha jina na kusudi la Yehova.

[Picha katika ukurasa wa23]

Nikiwa pamoja na binti yangu Rita

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki