Walipata Amani Katika Ulimwengu Wenye Msukosuko
JALADA la gazeti hili laonyesha picha ya vita kali kutoka Bosnia na Herzegovina. Je, amani yaweza kuwapo mahali kama hapo? Kwa kushangaza, jibu ni ndiyo. Huku jumuiya za Katoliki ya Kiroma, Othodoksi ya Mashariki, na za Kiislamu katika nchi hiyo yenye msiba zikipigania eneo, watu wengi hutamani amani, na wengine wameipata.
Akina Djorem walikuwa wakazi wa Sarajevo, nao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Kati ya msukosuko wote katika jiji hilo, wao walikuwa na mazoea ya kuzuru majirani wao ili kushiriki nao habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kwa nini? Kwa sababu familia ya akina Djorem ilijua kwamba Ufalme huu ni halisi, kwamba tayari umesimamishwa mbinguni, na kwamba huo ndio tumaini la pekee la wanadamu la kupata amani. Mashahidi wa Yehova wana uhakika kamili katika ile ambayo mtume Paulo aliita “habari njema ya amani.” (Waefeso 2:17, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa sababu ya watu kama Bozo na Hena Djorem, wengi wanapata amani katika Bosnia na Herzegovina.
Amani Halisi Itakuja
Kuna mengi zaidi ya kusema kuhusu akina Djorem. Lakini, kwanza ebu tuzungumze juu ya mume na mke wengine waliopata uhakika katika Ufalme wa Mungu. Majina yao ni Artur na Arina. Hao pamoja na wana wao wachanga zamani waliishi katika jamhuri moja katika eneo la ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Vita ya wenyewe kwa wenyewe ilipotokea, Artur alipigania moja ya pande zenye kupigana. Lakini, mara akajiuliza, ‘Kwa nini ninapigana na watu hawa ambao zamani walikuwa majirani wangu?’ Akaondoka nchi hiyo na baada ya kupata magumu mengi, alifika Estonia pamoja na familia yake changa.
Alipozuru St. Petersburg, Artur alikutana na Mashahidi wa Yehova akavutiwa na yale aliyojifunza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mapenzi ya Yehova ni kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakuwa ndio utawala pekee juu ya wanadamu. (Danieli 2:44) Kisha dunia itakuwa mahali pa amani, ikiwa haina tena vita za wenyewe kwa wenyewe au mapambano ya kimataifa. Isaya alitoa unabii kuhusu wakati huo: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.
Akiona picha ya dunia hiyo yenye amani ya wakati ujao katika kichapo cha kufundisha Biblia ambacho Shahidi fulani alimwonyesha, Artur alitaja kwamba zamani aliishi mahali palipofanana na picha hiyo. Lakini, sasa palikuwa pakiharibiwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe. Huko Estonia, Artur na familia yake wanajifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu kupitia funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.
Amani Kati ya Msukosuko
Zaburi 37:37 husema: “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani.” Kwa kweli, amani ya mtu mkamilifu na mnyoofu machoni pa Mungu haihusu wakati wake ujao pekee. Yeye anayo hata sasa. Hiyo yawezekanaje? Ebu fikiria ono la mtu mmoja aitwaye Paul.
Paul aishi katika kambi fulani ya wakimbizi iliyo mbali katika kusini-magharibi mwa Ethiopia, ingawa kwa hakika yeye atoka nchi moja ya jirani. Alipokuwa kwao, alikutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyefanya kazi katika kampuni moja ya mafuta, mtu huyo akampa kichapo cha kumsaidia kujifunza Biblia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.a Paul hakukutana na Shahidi huyo tena, lakini alijifunza kitabu hicho kwa makini. Vita ya wenyewe kwa wenyewe ilimfanya atorokee kambi ya wakimbizi katika Ethiopia, na huko alizungumza na wengine kuhusu yale aliyokuwa amejifunza. Kikundi kidogo kikakubali hayo kuwa kweli. Kwa kutegemea yale waliyokuwa wamejifunza, upesi walikuwa wakihubiria wengine katika kambi.
Paul aliandikia makao makuu ya Watch Tower Society akiomba msaada. Mhudumu mmoja aliyetumwa kutoka Addis Ababa alishangaa kupata watu 35 wakimngoja, wakiwa tayari kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mipango ilifanywa ya msaada kutolewa kwa ukawaida.
Yaweza kusemwaje kwamba watu kama Paul hufurahia amani? Hawaishi maisha rahisi, lakini wana imani katika Mungu. Wanapoathiriwa na msukosuko wa ulimwengu huu, wao hutumia hili shauri la Biblia: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.” Tokeo ni kwamba wana uradhi ambao ni vigumu kupatikana leo. Maneno ya mtume Paulo kwa kutaniko la Filipi yatumika kwao: “Amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” Hakika, wao huhisi wana uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, “Mungu wa amani.”—Wafilipi 4:6, 7, 9.
Amani ya Wakati Huu
Mfalme aliyetawazwa wa Ufalme wa Mungu ni Yesu Kristo, aitwaye katika Biblia “Mwana-Mfalme wa Amani.” (Isaya 9:6, New World Translation) Kumhusu, nabii wa kale alisema hivi: “Atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia.” (Zekaria 9:10) Maneno yaliyopuliziwa kama haya yalikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya maisha ya mtu fulani aitwaye José.
Wakati mmoja José alifungwa gerezani. Alikuwa haramia naye alikuwa ameshikwa akifanya matayarisho ya kubomoa kituo cha polisi. Alifikiri kwamba ni jeuri tu ingefanya serikali iboreshe hali katika nchi alimoishi. Alipokuwa gerezani, mke wake alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.
Baada ya José kufunguliwa, yeye pia alijifunza Biblia, na upesi maneno ya Zaburi 85:8 yakaanza kutumika kwake: ‘Nitasikia atakavyosema Mungu BWANA, maana atawaambia watu wake amani, naam, na watauwa wake pia.” Hata hivyo, mstari huo wamalizia kwa onyo hili: “Wasiurudie upumbavu [“hali ya kujitumaini,” NW] tena.” Hivyo, mtu anayetafuta amani ya Yehova hatathubutu kutenda mambo kivyake au kwa njia ya kupinga mapenzi Yake.
Leo, José na mke wake ni wahudumu Wakristo. Wao huelekeza wengine kwa Ufalme wa Yehova kuwa ndio suluhisho la matatizo ambayo awali José alijaribu kusuluhisha kwa kutumia mabomu ya kujitengenezea nyumbani. Wako tayari kutumaini Biblia, isemayo: “BWANA atatoa kilicho chema.” (Zaburi 85:12) Hakika, majuzi José alizuru kituo alichokuwa akipanga kuharibu. Kwa nini? Ili kuzungumza na familia za kituo hicho kuhusu Ufalme wa Mungu.
Watu Wenye Amani
Kwenye Zaburi 37:10, 11, Biblia husema: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Ni matazamio mazuri kama nini!
Hata hivyo, ona kwamba amani ya Yehova yapatikana kwa “wenye upole” pekee. Wale watafutao amani waweza kulazimika kujifunza kuwa wenye amani. Ndivyo ilivyokuwa kwa Keith, aishiye New Zealand. Keith alitajwa kuwa mtu “ambaye amejenga sana kimwili na mwenye nguvu sana kiutu, mchokozi, na mpenda ubishi.” Alikuwa mshiriki wa genge fulani naye aliishi katika nyumba iliyokuwa ngome kwelikweli, kukiwa na mbwa-walinzi watatu wakishika doria katika bustani yayo dhidi ya watu wasiotakikana. Mke wake, mama ya watoto wake sita, alikuwa amemtaliki.
Keith alipokutana na Mashahidi wa Yehova, habari njema ilikuwa na uvutano mkubwa sana kwake. Upesi yeye pamoja na watoto wake walikuwa wakihudhuria mikutano pamoja na Mashahidi. Alinyoa nywele zake zilizokuwa ndefu kufikia kiuno chake akaanza kuzungumza na washiriki wake wa zamani kuhusu Ufalme wa Mungu. Baadhi yao pia wakaanza kujifunza Biblia.
Kama mamilioni ya watu wenye mioyo minyoofu ulimwenguni pote, Keith alikuwa ameanza kutumia maneno ya mtume Petro: “Atakaye kupenda maisha, na kuona siku njema, . . . na aache mabaya, atende mema; atafute amani, aifuate sana.” (1 Petro 3:10, 11) Mke wa zamani wa Keith alikubali kuolewa naye tena, naye sasa anajifunza ‘kutafuta amani na kuifuatia.’
Amani ya Yehova imeokoa uhai wa wengi, kutia ndani mtu fulani ambaye wakati mmoja alikuwa mwanariadha aliyezaliwa katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Mtu huyu alishinda medali nyingi katika mashindano ya Olimpiki, lakini alikata tamaa akaanza kutumia dawa za kulevya na kileo. Baada ya miaka 19 yenye visa vingi vilivyotia ndani hukumu ya miaka mitatu katika kambi ya kazi ngumu katika Siberia, safari ya kujificha melini akielekea Kanada, na kunusurika kifo mara mbili kwa sababu ya tabia yake ya kutumia dawa za kulevya, alisali kwa Mungu kwa ajili ya msaada wa kupata kusudi la kweli la uhai. Funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova waliojua Kirusi lilimsaidia apate jibu la maswali yake. Leo, mtu huyu, kama mamilioni wengine, amejipatia amani na pia ana amani pamoja na Mungu.
Tumaini la Ufufuo
Hatimaye, ebu tuwarudie Bozo na Hena Djorem katika Sarajevo. Mume na mke hao walikuwa na binti, Magdalena, mwenye umri wa miaka mitano. Mwezi wa Julai uliopita, wote watatu walikuwa wakiondoka nyumbani ili kushiriki tena katika utendaji wa kuhubiri wakati ambapo wote waliuawa na kombora lililolipuka. Vipi juu ya amani ambayo walihubiria wengine? Je, kombora hilo lililowaua lilionyesha kwamba hiyo haikuwa amani halisi?
La hasha! Katika mfumo huu wa mambo, misiba hutokea. Watu huuawa kwa mabomu au makombora. Wengine hufa kwa ugonjwa au aksidenti. Wengi hufa kwa sababu ya umri wa uzee. Wale wafurahiao amani ya Mungu hawakosi kuathiriwa na mambo hayo, lakini jambo la kwamba matukio hayo yaweza kuwapata haliwafanyi wakose tumaini.
Yesu alimwahidi rafiki yake Martha: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.” (Yohana 11:25) Akina Djorem waliamini jambo hili, kama ilivyo na Mashahidi wa Yehova wengine wote. Na akina Djorem walikuwa na imani kwamba iwapo watakufa, wangefufuliwa katika dunia ambayo wakati huo kwa kweli ingekuwa mahali pa amani. Yehova Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
Kabla tu ya kufa, Yesu aliwaeleza wafuasi wake hivi: “Amani yangu nawapa. . . . Msifadhaike mioyoni mwenu.” (Yohana 14:27) Twashangilia pamoja na akina Djorem waliokuwa na amani hiyo na ambao kwa kweli wataifurahia kikamili zaidi katika ufufuo. Twafurahi kwa ajili ya wale wote wamwabuduo Yehova, Mungu wa amani. Hao wana amani ya akili. Wao hufurahia amani pamoja na Mungu. Wao husitawisha amani pamoja na wengine. Nao wana uhakika katika wakati ujao wenye amani. Ndiyo wamepata amani, ingawa wao waishi katika ulimwengu wenye msukosuko. Hakika, wote wamwabuduo Mungu kwa roho na kweli hufurahia amani. Wewe pia na upate amani hiyo.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wamepata amani wajapoishi katika ulimwengu wenye msukosuko