Wenye Shangwe Katika Ulimwengu Usio na Shangwe
“KWA vyovyote, hii imekuwa karne ya Shetani,” ukaanza uhariri katika The New York Times la Januari 26, 1995. “Watu hawakupata kuonyesha katika enzi nyingineyo iliyotangulia, mwelekeo, wala tamaa kubwa sana, ya kuua mamilioni ya watu wengine kwa sababu za rangi, dini au jamii.”
Ukumbusho wa 50 wa kuwekwa huru kwa watu wasio na hatia waliofungwa gerezani katika kambi za kifo za chama cha Nazi ulichochea uhariri kama huo uliotangulia. Hata hivyo, aina izo hizo za uuaji wa kikatili bado hutukia katika sehemu za Afrika na Ulaya Mashariki.
Mauaji ya kijamii, utakasaji wa kikabila, machinjo ya kikabila—vyovyote vile yanavyoitwa—hutokeza huzuni nyingi. Hata hivyo, miongoni mwa ujeuri huo usio na maana hutokea sauti za shangwe zenye nguvu. Kwa kielelezo, acheni tuangalie Ujerumani katika miaka ya 1930.
Kufikia Aprili wa 1935, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku na Hitler na chama chake cha Nazi, wasifanye kazi zozote za utumishi wa serikali. Mashahidi walikamatwa pia, wakafungwa gerezani, na kupelekwa kwenye kambi za mateso kwa sababu walidumisha kutokuwamo kwa Kikristo. (Yohana 17:16) Mwisho-mwisho wa Agosti 1936, vikundi vikubwa-vikubwa vya Mashahidi wa Yehova vilikamatwa. Maelfu ya hao yalipelekwa kwenye kambi za mateso, ambapo Mashahidi wengi walikaa hadi 1945 ikiwa waliokoka. Lakini Mashahidi waliitikiaje kutendwa huko kikatili kulikowapata katika hizo kambi? Ijapokuwa huenda ikashangaza, wao waliweza kudumisha shangwe yajapokuwa mazingira yao yasiyo na shangwe.
“Mwamba Matopeni”
Mwanahistoria Mwingereza Christine King alimhoji mwanamke Mkatoliki aliyekuwa katika hizo kambi. “Yeye alitumia fungu la maneno ambalo sijasahau kamwe,” akasema Dakt. King. “Alisema kinaganaga kuhusu maisha yenye kukirihi, hali zenye kuchukiza ambamo aliishi. Naye akasema kwamba alijua Mashahidi, na Mashahidi hao walikuwa mwamba matopeni. Walikuwa kama mahali imara katika tope hilo lote la kunata. Alisema kwamba wao walikuwa watu pekee ambao hawakutema mate wakati walinzi walipopita. Walikuwa watu pekee ambao hawakukabiliana na hali hiyo kwa chuki bali kwa upendo na tumaini na hisia ya kwamba kulikuwa na kusudi.”
Ni nini kilichowawezesha Mashahidi wa Yehova wawe ‘miamba matopeni’? Imani isiyotikisika katika Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo. Kwa hiyo, jitihada za Hitler zilishindwa kukomesha upendo na shangwe yao ya Kikristo.
Sikiliza wakati waokokaji wawili wa kambi hizo wakumbukapo yaliyotokea miongo mitano baada ya wao kukabiliana kwa mafanikio na mtihani huo wa imani. Mmoja asema hivi: “Nabubujika kwa shangwe nikijua kwamba nilikuwa na pendeleo lisilo na kifani la kuthibitisha upendo na shukrani yangu kwa Yehova nikiwa chini ya hali zenye ukatili zaidi. Hakuna mtu aliyenilazimisha nifanye hivyo! Kinyume cha hilo, wale waliojaribu kutulazimisha walikuwa maadui wetu waliojaribu kwa matisho kutufanya tumtii Hitler zaidi kuliko Mungu—lakini bila mafanikio! Nafurahi si wakati huu tu bali, kwa sababu ya dhamiri nzuri, nilifurahi hata nilipokuwa gerezani.”—Maria Hombach, umri wa miaka 94.
Shahidi mwingine asema hivi: “Nafikiria siku zangu za kufungwa gerezani kwa shukrani na shangwe. Miaka iliyotumiwa chini ya Hitler katika magereza na kambi za mateso ilikuwa migumu na ilijaa mitihani. Lakini nisingalitaka kuikosa, kwani ilinifundisha kumtumainia Yehova kabisa.”—Johannes Neubacher, umri wa miaka 91.
“Kumtumainia Yehova kabisa”—ndiyo iliyokuwa siri ya shangwe ambayo Mashahidi wa Yehova walikuwa nayo. Hivyo, wao ni wenye shangwe, ingawa wanazungukwa na ulimwengu usio na shangwe. Shangwe yao ilikuwa wazi kwenye “Wasifaji Wenye Shangwe” Mikusanyiko ya Wilaya katika miezi ya karibuni. Acheni tupitie kwa ufupi vikusanyiko hivyo vyenye shangwe.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Maria Hombach