Tumeungana Katika Utumishi wa Mungu Kupitia Nyakati Nzuri na Mbaya
Kama ilivyosimuliwa na Michel na Babette Muller
“NINA habari mbaya za kuwaambia,” daktari akasema. “Msahau maisha yenu ya umishonari katika Afrika.” Akimtazama mke wangu aitwaye Babette, daktari alisema, “Una kansa ya matiti.”
Tulishtuka tukakosa la kusema. Mambo mengi yakapita akilini mwetu. Tulifikiri kwamba ziara yetu kwa daktari wakati huu ingekuwa tu uchunguzi wa mwisho. Tikiti zetu za kurudi Benin, Afrika Magharibi, zilikuwa zimenunuliwa. Tulikuwa tumetumaini kurudi huko wakati wa juma hilo. Wakati wa miaka yetu 23 ya ndoa, tulikuwa tumeona mambo mazuri na mabaya. Tukiwa tumevurugika akili na tukiwa na hofu, sasa tulijitayarisha kwa ajili ya vita dhidi ya kansa.
Acha tuanze mwanzoni. Michel alizaliwa mwezi wa Septemba 1947, Babette mwezi wa Agosti 1945. Tulikulia Ufaransa na tukaoana mwaka wa 1967. Tuliishi Paris. Asubuhi moja mapema mwaka wa 1968, Babette alichelewa kwenda kazini. Bibi mmoja alikuja mlangoni akamtolea broshua ya kidini; aliichukua. Kisha yule bibi akasema: “Je, naweza kurudi nikiwa na mume wangu ili tuongee na wewe na mume wako?”
Babette alikuwa akifikiria kazi yake. Alitaka mwanamke huyo aende, kwa hiyo akasema, “Sawa, Sawa.”
Michel asimulia: “Sikupendezwa na dini, lakini hiyo broshua ilivuta uangalifu wangu nikaisoma. Siku chache baadaye, yule bibi aitwaye Joceline Lemoine, alirudi na mume wake, aitwaye Claude. Alikuwa stadi sana katika kutumia Biblia. Aliyajibu maswali yangu yote. Nilivutiwa sana.
“Babette alikuwa Mkatoliki lakini hakuwa na Biblia, jambo lililokuwa kawaida kwa Wakatoliki. Alisisimuka sana kuona na kusoma Neno la Mungu. Kutokana na funzo letu tulijifunza kwamba mawazo mengi ya kidini tuliyokuwa tumefundishwa yalikuwa ya uwongo. Tulianza kuongea na watu wetu wa ukoo na rafiki zetu juu ya mambo tuliyokuwa tukijifunza. Mwezi wa Januari 1969 tukawa Mashahidi wa Yehova waliobatizwa. Tisa kati ya watu wetu wa ukoo na marafiki walibatizwa upesi baada ya hapo.”
Kutumikia Mahali Palipokuwa na Uhitaji wa Wahubiri
Upesi baada ya ubatizo wetu, tuliwaza: ‘Hatuna watoto wowote. Kwa nini tusichukue utumishi wa wakati wote?’ Kwa hiyo mnamo 1970 tuliacha kazi zetu, tukajiandikisha kuwa mapainia wa kawaida, na kuhamia mji mdogo wa Magny-Lormes, karibu na Nevers, katikati ya Ufaransa.
Ulikuwa mgawo mgumu. Ilikuwa vigumu kupata watu waliotaka kujifunza Biblia. Tulishindwa kupata kazi ya kuajiriwa, kwa hiyo tulikuwa na fedha kidogo. Wakati mwingine tulikula viazi tu. Wakati wa kipupwe halijoto zilienda chini sana hadi digrii 22 Selsiasi kupita sufuri. Tuliita wakati tuliokuwa huko wakati wa ng’ombe saba waliokonda.—Mwanzo 41:3.
Lakini Yehova alitutegemeza. Siku moja tulipokuwa karibu tuishiwe na chakula, mtu mwenye kuleta barua alituletea sanduku kubwa la jibini kutoka kwa dada ya Babette. Siku nyingine tulikuja nyumbani kutoka mahubiri na kupata baadhi ya rafiki kadhaa ambao walikuwa wamekuja kwa gari kilometa 500 kutuona. Waliposikia jinsi mambo yalivyokuwa magumu, ndugu hawa walijaza magari yao mawili kwa chakula kwa ajili yetu.
Baada ya mwaka mmoja na nusu, Sosaiti ilituweka kuwa mapainia wa pekee. Zaidi ya miaka minne iliyofuata, tulitumikia katika Nevers, kisha Troyes, na hatimaye katika Montigny-lès-Metz. Mwaka wa 1976, Michel aliwekwa kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko upande wa kusini-magharibi mwa Ufaransa.
Miaka miwili baadaye, wakati wa shule ya waangalizi wa mzunguko, tulipata barua kutoka Watch Tower Society ikitualika twende ng’ambo tukiwa wamishonari; barua hiyo ilisema kwamba tunaweza kuchagua kati ya Chad na Burkina Faso (iliyokuwa ikiitwa Upper Volta). Tulichagua Chad. Upesi tukapata barua nyingine, ikitupa mgawo wa kutumikia chini ya tawi la Tahiti. Tulikuwa tumeomba kwenda Afrika, bara kubwa sana, lakini upesi tukajipata wenyewe kwenye kisiwa kidogo!
Kutumikia Katika Pasifiki Kusini
Tahiti ni kisiwa maridadi cha kitropiki cha Pasifiki Kusini. Tulipofika, ndugu wapatao mia moja walitulaki kwenye uwanja wa ndege. Walitukaribisha wakiwa na shada za maua, na ingawa tulikuwa tumechoka baada ya safari ndefu kutoka Ufaransa, tulifurahi sana.
Miezi minne baada ya kufika Tahiti, tulipanda mashua ndogo iliyojazwa mizigo ya nazi zilizokauka. Siku tano baadaye tulifika kwenye mgawo wetu mpya—kisiwa cha Nuku Hiva katika Visiwa vya Marquesas. Watu wapatao 1,500 waliishi katika kisiwa hicho, lakini hakukuwa na ndugu. Sisi tu.
Hali zilikuwa za kikale wakati huo. Tuliishi katika nyumba ndogo iliyotengenezwa kwa saruji na mianzi. Hakukuwa na umeme. Tulikuwa na mfereji wa maji uliokuwa ukifanya kazi nyakati nyingine, lakini maji yalikuwa yenye tope-tope. Mara nyingi, tulitumia maji ya mvua tuliyodunduliza kwenye tangi. Hakukuwa na barabara zilizotengenezwa vizuri, kulikuwa na njia za mchanga tu.
Ili kufika sehemu za mbali za kisiwa, ilitubidi tukodishe farasi. Matandiko yalifanyizwa kwa mbao—yasiyostarehesha kabisa, hasa kwa Babette, ambaye hakuwa amepata kuendesha farasi kamwe. Tulikuwa tukibeba mundu ili kukata mianzi iliyokuwa ikianguka njiani. Lilikuwa badiliko kubwa na maisha ya Ufaransa.
Tulifanya mikutano ya Jumapili, ijapokuwa ni sisi wawili tu tuliohudhuria. Mara ya kwanza, hatukuwa na mikutano mingine kwa kuwa tulikuwa sisi wawili tu. Badala yake tulisoma habari ya mkutano pamoja.
Baada ya miezi michache, tuliamua kwamba haikuwa vizuri twendelee kwa njia hii. Michel asimulia: “Nilimwambia Babette, ‘Lazima tuvae vizuri. Wewe keti pale, nami nitaketi hapa. Nitaanza kwa sala, kisha tutakuwa na mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Nitauliza maswali, nawe utajibu, hata kama wewe tu ndiye mtu aliye chumbani.’ Ilikuwa vizuri kufanya hivyo kwa sababu ni rahisi kuwa walegevu kiroho wakati ambapo hakuna kutaniko.”
Ilichukua muda kupata watu ili waje kwenye mikutano yetu ya Kikristo. Sisi wawili tulikuwa peke yetu kwa miezi minane ya kwanza. Baadaye, mtu mmoja, wawili, au wakati mwingine watatu walijiunga nasi. Mwaka mmoja, sisi wawili tu tulianzisha ule mwadhimisho wa kila mwaka wa Mlo wa Jioni wa Bwana. Baada ya dakika kumi, watu wengine wakaja, kwa hiyo nikatua na kuanza hotuba tena.
Leo, kuna wahubiri 42 na makutaniko 3 katika Visiwa vya Marquesas. Ingawa sehemu kubwa zaidi ya kazi ilifanywa na waandamizi wetu, watu wengine tuliowatembelea huko nyuma sasa wamebatizwa.
Ndugu Zetu Ni Wenye Thamani
Tulijifunza subira katika Nuku Hiva. Ilitubidi tungojee kila kitu ila mahitaji yetu ya lazima zaidi. Kwa mfano, kama ulitaka kitabu, uliandika, kisha ungoje kwa miezi miwili au mitatu kabla hakijafika.
Somo jingine tulilojifunza lilikuwa kwamba ndugu zetu ni wenye thamani. Tulipozuru Tahiti na kuhudhuria mkutano na kusikia ndugu wakiimba, tuliguswa moyo mpaka tukatoa machozi. Huenda ikawa kweli kwamba ni vigumu kupatana na ndugu wengine, lakini unapokuwa peke yako, unatambua jinsi udugu ulivyo mzuri. Katika mwaka wa 1980 Sosaiti iliamua kwamba tunapaswa kurudi Tahiti na kutumikia katika kazi ya mzunguko. Huko tulitiwa moyo sana na ukaribishaji-wageni wenye uchangamfu wa akina ndugu na upendo wao kwa kazi ya kuhubiri. Tulifanya kazi ya mzunguko Tahiti kwa miaka mitatu.
Kisiwa kwa Kisiwa
Halafu tukapewa mgawo wa makao ya mishonari katika Raïatéa, kisiwa kingine cha Pasifiki, tukakaa hapo kwa karibu miaka miwili. Baada ya Raïatéa, tulipewa mgawo wa kufanya kazi ya mzunguko katika kikundi cha visiwa Tuamotu. Tulitembelea visiwa 25 kati ya 80 kwa mashua. Ilikuwa vigumu kwa Babette. Kila wakati aliposafiri kwa mashua alikuwa mgonjwa.
Babette asema: “Hali ilikuwa mbaya sana! Nilikuwa mgonjwa kila wakati tulipokuwa kwenye mashua. Ikiwa tulikuwa baharini siku tano, ningekuwa mgonjwa kwa siku tano. Hakuna dawa zilizonisaidia. Hata hivyo, japo ugonjwa wangu, niliona bahari kuwa maridadi. Ulikuwa mwono wenye kuvutia kwelikweli. Dolfini wangekimbiza mashua. Mara nyingi waliruka juu ya maji ukipiga makofi!”
Baada ya miaka mitano katika kazi ya mzunguko, tulipewa mgawo tena kwenda Tahiti kwa miaka miwili na tena tukawa na wakati mzuri katika kazi ya kuhubiri. Kutaniko letu liliongezeka maradufu kutoka watangazaji 35 hadi 70 kwa mwaka mmoja na nusu. Watu 12 kati ya wale tuliojifunza nao Biblia walibatizwa punde kabla ya sisi kuondoka. Wengine wao sasa ni wazee katika kutaniko.
Kwa ujumla tulikaa miaka 12 katika Pasifiki Kusini. Kisha tukapokea barua kutoka Sosaiti ikisema kwamba hawakuhitaji wamishonari kwenye visiwa hivi tena kwa kuwa makutaniko yalikuwa imara sasa. Kulikuwa na watangazaji wapatao 450 tulipofika Tahiti na zaidi ya 1,000 tulipoondoka.
Hatimaye Afrika!
Tulirudi Ufaransa, na baada ya mwezi mmoja na nusu, Sosaiti ikatupa mgawo mpya—Benin, Afrika Magharibi. Tulikuwa tumetaka kwenda Afrika miaka 13 iliyopita, kwa hiyo tulifurahi sana.
Tulifika Benin Novemba 3, 1990, na tulikuwa miongoni mwa wamishonari wa kwanza kufika baada ya marufuku ya utendaji wa kuhubiri Ufalme ya miaka 14 kuondolewa. Ilisisimua sana. Hatukuwa na matatizo kuzoea hali kwa sababu maisha yanafanana na yale ya visiwa vya Pasifiki. Watu ni wenye urafiki sana na wakaribishaji-wageni. Unaweza kusimama na kuongea na mtu yeyote barabarani.
Majuma machache tu baada ya kufika Benin, Babette aliona uvimbe kwenye titi lake. Kwa hiyo tulikwenda kwenye kliniki ndogo karibu na tawi jipya lililofunguliwa. Daktari alimchunguza na kusema kwamba alihitaji upasuaji haraka. Siku iliyofuata tulikwenda kwa kliniki nyingine ambapo tulimwona daktari Mzungu, wa magonjwa ya wanawake kutoka Ufaransa. Yeye pia alisema kwamba tulipaswa kwenda Ufaransa haraka ili Babette apasuliwe. Siku mbili baadaye tulikuwa kwenye ndege kuelekea Ufaransa.
Tulihuzunika kuondoka Benin. Kukiwa na uhuru mpya wa kidini katika nchi hiyo, akina ndugu walisisimuka kuwa na wamishonari wapya nasi tulifurahi kuwa huko. Kwa hiyo tulikasirika kwamba ilitulazimu kuondoka baada ya kuwa nchini kwa majuma machache tu.
Tulipofika Ufaransa, daktari-mpasuaji alimchunguza Babette na kuthibitisha kwamba alihitaji upasuaji. Madaktari walifanya haraka, wakafanya upasuaji mdogo, kumwachilia Babette atoke hospitalini siku iliyofuata. Tulifikiri kwamba mambo yalikuwa yamekwisha.
Siku nane baadaye, tulikutana na yule daktari-mpasuaji. Ulikuwa wakati huo ndipo alitoa habari ya kwamba Babette alikuwa na kansa ya matiti.
Akikumbuka alivyohisi wakati huo, Babette asema: “Kwanza, sikuwa na wasiwasi sana kama Michel. Lakini siku moja baada ya hiyo habari mbaya, sikuwa na hisia. Sikuweza kulia. Sikuweza kutabasamu. Nilifikiri nitakufa. Kwangu mimi, kansa ilikuwa ni kifo. Mtazamo wangu ulikuwa, Twapaswa kufanya yale tupaswayo.”
Kupigana na Kansa
Tulisikia hiyo habari mbaya Ijumaa, na Babette alikuwa ameratibiwa upasuaji wa pili mnamo Jumanne. Tulikuwa tukiishi na dada ya Babette, lakini naye pia alikuwa mgonjwa, kwa hiyo tulihuzunika hatukuweza kuendelea kukaa katika nyumba yake ndogo.
Tulijiuliza pale tungeweza kwenda. Kisha tukakumbuka Yves na Brigitte Merda, wenzi wa ndoa tuliokuwa tumekaa nao awali. Wenzi wa ndoa hawa walikuwa wametukaribisha sana. Kwa hiyo tulimpigia simu Yves na tukamwambia kwamba Babette alihitaji upasuaji na kwamba hatukuwa na mahali pa kukaa. Tulimwambia pia kwamba Michel alihitaji kazi.
Yves alimpa Michel kazi nyumbani kwake. Akina ndugu walitutegemeza na kututia moyo kwa matendo mengi ya fadhili. Pia walitusaidia kifedha. Sosaiti ililipia gharama ya matibabu ya Babette.
Ulikuwa ni upasuaji mkubwa. Madaktari walilazimika kuondoa tezi za limfu na hilo titi. Walianza tibakemili mara moja. Baada ya juma moja, Babette aliweza kuondoka hospitalini, lakini alipaswa kurudi baada ya kila majuma matatu kwa tiba ya kuendelea.
Wakati Babette alipokuwa akipata matibabu, akina ndugu kutanikoni walikuwa wenye kusaidia sana. Dada mmoja ambaye pia alikuwa amepatwa na kansa ya matiti alikuwa mwenye kitia moyo kikubwa sana. Alimwambia Babette jambo la kutazamia na akamfariji sana.
Hata hivyo, tulihangaikia wakati wetu ujao. Akifahamu hili, Michel na Jeanette Cellerier walitupeleka kwenye mkahawa tupate mlo.
Tuliwaambia kwamba ilitulazimu tuache utumishi wetu wa mishonari na kwamba hatuwezi kamwe kurudi Afrika. Hata hivyo, Ndugu Callerier akasema: “Nini? Nani asema lazima mwache? Baraza Linaloongoza? Akina ndugu katika Ufaransa? Ni nani amesema?”
“Hakuna,” nikajibu, “Ni mimi nisemaye hivyo.”
“La, la!” akasema Ndugu Cellerier. “Mtarudi!”
Tibakemili ilifuatiwa na mnururisho, uliomalizwa mwishoni mwa mwezi wa Agosti 1991. Madaktari walisema kwamba hawakuona tatizo kwetu kurudi Afrika, mradi tu Babette awe akirudi Ufaransa kufanyiwa uchunguzi wa kawaida.
Kurudi Benin
Kwa hiyo tuliandikia makao makuu Brooklyn, tukiwaomba ruhusa ya kurudi katika utumishi wa mishonari. Tulikuwa na hamu ya kusikia majibu yao. Siku zilisonga polepole. Hatimaye, Michel hakuweza kungoja tena, kwa hiyo alipiga simu Brooklyn na kuuliza kama walipokea barua yetu. Walisema kwamba walikuwa wameifikiria—tunaweza kurudi Benin! Tulimshukuru Yehova jinsi gani!
Familia ya Merda ilipanga kuwe na tafrija kubwa ya kusherehekea habari hiyo. Mwezi wa Novemba 1991 tulirudi Benin, na akina ndugu walitukaribisha kwa karamu!
Babette aonekana kuwa mzima sasa. Tumekuwa tukirudi Ufaransa pindi kwa pindi kwa uchunguzi kamili wa kitiba, na madaktari hawaoni dalili zozote za kansa. Twafurahia kurudi kwenye mgawo wetu wa mishonari. Twahisi tunahitajiwa Benin, na Yehova amebariki kazi yetu. Tangu tuliporudi tumesaidia watu 14 kufikia hatua ya ubatizo. Watano kati yao sasa ni mapainia wa kawaida, na mmoja amewekwa kuwa mtumishi wa huduma. Pia tumeona kutaniko letu dogo likikua na kugawanywa kuwa makutaniko mawili.
Kwa miaka mingi, tumemtumikia Yehova tukiwa mume na mke na tumefurahia baraka nyingi na tumepata kujua watu wengi wazuri sana. Lakini pia tumezoezwa na kuimarishwa na Yehova kuvumilia magumu kwa mafanikio. Kama Ayubu, sikuzote hatukuelewa ni kwa nini mambo yalitukia hivyo, lakini tulijua kwamba sikuzote Yehova alikuwapo ili kutusaidia. Ni kama vile Neno la Mungu linavyosema: “Tazama, mkono wa BWANA haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia.”—Isaya 59:1.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Michel na Babette Muller wamevalia mavazi ya kitamaduni katika Benin
[Picha katika ukurasa wa 25]
Kazi ya mishonari miongoni mwa Wapolinesia katika Tahiti yenye joto