Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Maadui wa Zamani Wameungana Katika Kumtumikia Yehova
“MARA ya kwanza niliposikia jambo kuhusu Mashahidi wa Yehova ilikuwa nilipokuwa nikitumikia nikiwa mlinzi aliyejihami Bosnia,” aeleza Branko.a
Branko alikuwa akishika doria ya kulinda kwenye hospitali ambapo majeruhi walikuwa wakitibiwa. Mmojawapo madaktari alikuwa anajifunza Biblia pamoja na Mashahidi, na wakati wa zamu ya usiku, alimwelezea Branko mengi ya yale aliyojifunza kuhusu Biblia.
Yale aliyosikia Branko usiku huo yalimchochea sana hivi kwamba akaacha silaha zake. Aliwasiliana na Mashahidi, ili ajifunze mengi zaidi. Wakati mwingine baadaye, baada ya kuhamia nchi moja ya Ulaya, Branko alitafuta Jumba la Ufalme na kuhudhuria mkutano wa kutaniko la Kiyugoslavia la Mashahidi wa Yehova. Huko ndiko Branko alikomkuta Slobodan.
Slobodan pia alikuja kutoka Bosnia na alikuwa amejitolea kutumikia katika vita hiyohiyo kama Branko—lakini akiwa katika upande ule mwingine wa vita. Slobodan alipigania Waserbia dhidi ya Wakroati. Wakati hao wawili walipokutana, Slobodan alikuwa amekuwa Shahidi wa Yehova aliyebatizwa. Alijitolea kujifunza Biblia pamoja na Branko, adui wake wa zamani. Kadiri funzo lilivyofanya maendeleo, Branko alijifunza mengi kuhusu Yehova, na upendo wake kwa Mungu ukakua. Jambo hilo lilimsukuma Branko ajiweke wakfu kwa Muumba. Katika mwezi wa Oktoba 1993 alionyesha wakfu wake kwa ubatizo wa maji.
Slobodan alikujaje kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Alikuwa ameondoka eneo la vita la Bosnia mbeleni. Alikuwa amesoma vichapo kadhaa vya Mashahidi, lakini upendezi wake kwa Neno la Mungu haukua hadi Mashahidi wawili walipotembelea nyumbani kwake mapema 1992. Ni nani aliyemtembelea Slobodan, akijitolea kujifunza Biblia pamoja naye? Alikuwa Mujo, ambaye pia alitoka Bosnia, lakini aliyelelewa akiwa Mwislamu. Funzo la Biblia lilipoendelea, Mujo na Slobodan, waliokuwa maadui zamani, walitumia wakati pamoja kila siku ili kuimarishana imani.
Vita katika Yugoslavia ya zamani imeua mamia ya maelfu ya watu. Lakini Branko, Slobodan, na Mujo sasa wanatumikia wakiwa wahubiri wa habari njema wa wakati wote wakiwa katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Wao wameshinda mzozo wa kikabila na kijamii, na sasa wanatafuta amani wakijitiisha kwa Muumba, Yehova.
Lakini ni nini kilicholeta mabadiliko hayo? Ulikuwa upendo wao kwa Yehova, staha yao kwa Biblia, na bidii yao ya kutumia kweli ya Biblia maishani mwao. Kama vile Maandiko Matakatifu yasemavyo, “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, . . . tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”—Waebrania 4:12.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yasiyo halisi yametumiwa.