Sababu kwa Nini Ibada ya Kweli Hupokea Baraka ya Mungu
“Sifuni Yah, nyinyi watu! Wokovu na utukufu na nguvu ni za Mungu wetu, kwa sababu hukumu zake ni za kweli na za uadilifu.”—UFUNUO 19:1, 2, NW.
1. Babiloni Mkubwa atafikiaje mwisho wake?
“BABILONI MKUBWA” ameanguka machoni pa Mungu na sasa anakabili utokomeo. Unabii wa Biblia waonyesha kwamba kahaba huyu wa kidini wa ulimwenguni pote karibuni atafishwa na hawara zake wa kisiasa; mwisho wake utakuja ghafula na kwa kasi. Ufunuo wa Yesu kwa Yohana ulikuwa na maneno haya ya kiunabii: “Malaika mwenye nguvu akainua jiwe kama jiwe kubwa la kusagia na kulivurumisha ndani ya bahari, akisema: ‘Hivyo kwa mtupo wa kasi sana atavurumishwa chini Babiloni lile jiji kubwa, na hatapatikana tena kamwe.’”—Ufunuo 18:2, 21, NW.
2. Watumishi wa Yehova wataitikiaje uharibifu wa Babiloni?
2 Uharibifu wa Babiloni Mkubwa utaombolezwa na visehemu vya ulimwengu wa Shetani lakini kwa hakika hautaombolezwa na watumishi wa Mungu, wa kimbingu au wa kidunia. Sauti zao kubwa zenye shangwe kwa Mungu zitakuwa: “Sifuni Yah, nyinyi watu! Wokovu na utukufu na nguvu ni za Mungu wetu, kwa sababu hukumu zake ni za kweli na za uadilifu. Kwa maana ametekeleza hukumu juu ya kahaba mkubwa aliyeifisidi dunia kwa uasherati wake, na amelipiza kisasi cha damu ya watumwa wake mkononi mwake.”—Ufunuo 18:9, 10; 19:1, 2, NW.
Ni Lazima Dini ya Kweli Itokeze Matunda Gani?
3. Ni maswali gani yanayohitaji kujibiwa?
3 Kwa kuwa ni lazima dini isiyo ya kweli iondolewe kabisa kutoka duniani, ni aina gani ya ibada itakayobaki? Twaweza kutambuaje leo ni kikundi kipi cha kidini kitakachookoka uharibifu wa milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli ya Shetani? Ni nini matunda yenye uadilifu ambayo ni lazima kikundi hiki kitokeze? Kuna angalau ishara kumi za kutambulisha ibada ya kweli ya Yehova.—Malaki 3:18; Mathayo 13:43.
4. Ni jipi lililo takwa la kwanza kwa ibada ya kweli, na Yesu aliwekaje kielelezo kulihusu?
4 Kwanza kabisa, Wakristo wa kweli lazima wategemeze enzi kuu aliyoifia Yesu—enzi kuu ya Baba yake. Yesu hakutoa uhai wake kwa sababu ya kusudi lolote la kisiasa, kikabila, au kijamii. Alitanguliza Ufalme wa Baba yake mbele ya tamaa zote za kisiasa au za kimapinduzi za Kiyahudi. Yeye alijibu toleo la Shetani la kumpa mamlaka ya ulimwengu wote kwa maneno haya: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” Yeye alijua kutokana na Maandiko ya Kiebrania kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa kweli juu ya dunia yote. Ni kikundi kipi cha kidini ambacho bila shaka yoyote kinaunga mkono utawala wa Yehova badala ya mifumo ya kisiasa ya ulimwengu huu?—Mathayo 4:10; Zaburi 83:18.
5. (a) Waabudu wa kweli wapaswa kulionaje jina la Mungu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova huliheshimu jina hilo?
5 Takwa la pili ni kwamba ibada ya kweli lazima itukuze na kutakasa jina la Mungu. Mweza Yote alifunua jina lake, Yehova (lililotafsiriwa Yahweh katika tafsiri fulani za Biblia), kwa watu wake Israeli, nalo latumiwa maelfu ya mara katika Maandiko ya Kiebrania. Hata kabla ya hilo, Adamu, Hawa, na wengine walijua hilo jina, ingawa hawakuliheshimu sikuzote. (Mwanzo 4:1; 9:26; 22:14; Kutoka 6:2) Wakati ambapo watafsiri wa Jumuiya ya Wakristo na wa Kiyahudi mara nyingi wameondoa jina la kimungu kutoka kwenye Biblia zao, Mashahidi wa Yehova wamelipa jina hilo hadhi na staha yalo ifaayo katika New World Translation of the Holy Scriptures. Wao huheshimu jina hilo, kama walivyofanya Wakristo wa mapema. Yakobo alitoa ushuhuda hivi: “Simioni amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwayo watu kwa ajili ya jina lake. Na pamoja na hili maneno ya Manabii yapatana, . . . ‘ili wale wabakio kati ya watu wapate kumtafuta Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu waitwao kwa jina langu, asema Yehova, anayefanya mambo haya.’”—Matendo 15:14-17 NW; Amosi 9:11, 12.
6. (a) Ni nini lililo takwa la tatu kwa ibada ya kweli? (b) Yesu na Danieli walikaziaje utawala wa Ufalme? (Luka 17:20, 21)
6 Takwa la tatu kwa ibada ya kweli ni kwamba inapaswa kutukuza Ufalme wa Mungu kuwa ndio suluhisho pekee la haki na lenye kudumu la matatizo ya wanadamu ya utawala. Yesu alifundisha wazi wafuasi wake wasali Ufalme huo uje, ili utawala wa Mungu uchukue uongozi wa dunia. Danieli alipuliziwa kutoa unabii kuhusu siku za mwisho: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . utavunja falme hizi zote [za kilimwengu na za kisiasa] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Ni nani ambao wameonyesha kwa mwenendo wao katika karne hii ya 20 kwamba wao waunga mkono kikamili Ufalme huo—je, ni dini za Babiloni Mkubwa au ni Mashahidi wa Yehova?—Danieli 2:44; Mathayo 6:10; 24:14.
7. Waabudu wa kweli huonaje Biblia?
7 Takwa la nne kupata kibali cha Mungu ni kwamba watumishi wa kweli wa Mungu wanapaswa kutegemeza Biblia ikiwa Neno la Mungu lililopuliziwa. Basi wao hawawezi kushindwa na uhakiki wa Biblia, ambao hujaribu kuonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha kibinadamu tu chenye mapungufu mengi yawezayo kutokea. Mashahidi wa Yehova waamini Biblia kuwa Neno lililopuliziwa la Mungu, kama vile Paulo alivyomwandikia Timotheo: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”a Basi, Mashahidi wa Yehova huchukua Biblia kuwa mwongozo wao, kitabu chao cha mafundisho kwa maisha ya kila siku, na chanzo chao kikuu cha tumaini kwa ajili ya wakati ujao.—2 Timotheo 3:16, 17.
Dini ya Upendo, Si ya Chuki
8. Ni nini lililo takwa la tano kwa ibada ya kweli?
8 Yesu alibainishaje wafuasi wake wa kweli? Jibu lake latuleta kwenye ishara muhimu ya tano ya kutambulisha ibada ya kweli. Yesu alisema: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35, italiki ni zetu.) Yesu alionyeshaje upendo wake? Kwa kutoa uhai wake ukiwa dhabihu ya fidia. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Kwa nini upendo wa kweli ni sifa muhimu kwa Wakristo wa kweli? Yohana alieleza: “Wapenzi, na mpendane; kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, . . . Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:7, 8.
9. Ni nani wameonyesha upendo wa kweli, na kwa jinsi gani?
9 Ni nani ambao wameonyesha aina hiyo ya upendo katika nyakati zetu, hata wajapokabiliwa na chuki ya kijamii, kitaifa, au kikabila? Ni nani ambao wamepita ule mtihani mkuu zaidi, hata kufikia kifo, ili upendo wao ushinde? Je, twaweza kusema kwamba ni makasisi na watawa wa kike wa Katoliki ambao kwa kweli wameshiriki lawama fulani kwa mauaji ya jamii nzima yaliyotokea Rwanda katika 1994? Je, ni Waothodoksi wa Serbia au Wakatoliki wa Kroatia ambao wamejiingiza katika “utakasaji wa kikabila” na matendo mengine yasiyo ya Kikristo katika vita hiyo ya wenyewe kwa wenyewe katika yale mataifa ya Balkani? Au ni makasisi wa Katoliki au wa Protestanti ambao wamechochea ubaguzi na chuki katika Ireland Kaskazini katika miongo michache iliyopita? Hakika Mashahidi wa Yehova hawawezi kushtakiwa kuwa walishiriki katika yoyote ya mapambano hayo. Wao wameteseka katika magereza na kambi za mateso, hata kufikia kifo, badala ya kusaliti upendo wao wa Kikristo.—Yohana 15:17.
10. Kwa nini Wakristo wa kweli hudumisha kutokuwemo?
10 Takwa la sita kwa ibada inayokubalika kwa Mungu ni kule kutokuwamo kuhusu mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu. Kwa nini Wakristo wanapaswa kudumisha kutokuwamo katika siasa? Paulo, Yakobo, na Yohana hutupa sababu nzuri ya kuchukua msimamo huo. Mtume Paulo aliandika kwamba Shetani ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo,” apofushaye akili za wasioamini kwa kila njia iwezekanayo, kutia ndani siasa zenye kuleta migawanyiko. Mwanafunzi Yakobo alisema kwamba “kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu,” na mtume Yohana alisema kwamba ‘dunia yote hukaa katika yule mwovu.’ Basi, Mkristo wa kweli hawezi kuridhiana ujitoaji wake kwa Mungu kwa kujihusisha na ulimwengu mfisadi wa siasa na mamlaka wa Shetani.—2 Wakorintho 4:4, NW; Yakobo 4:4; 1 Yohana 5:19.
11. (a) Wakristo huonaje vita? (b) Kuna msingi gani wa Kimaandiko kwa msimamo huo? (2 Wakorintho 10:3-5)
11 Kwa kupatana na hayo matakwa mawili yanayotangulia, takwa la saba ni la wazi, yaani, waabubu wa kweli walio Wakristo hawapaswi kushiriki katika vita. Kwa kuwa dini ya kweli ni udugu wa ulimwenguni pote wenye kutegemea upendo, basi hakuna chochote kiwezacho kugawanya au kuharibu “ushirika mzima wa ndugu . . . katika ulimwengu.” Yesu alifundisha upendo, si chuki; amani, si vita. (1 Petro 5:9, NW; Mathayo 26:51, 52) “Mwovu” yuleyule, Shetani, aliyemchochea Kaini amwue Abeli aendelea kuchochea chuki miongoni mwa wanadamu na kuanzisha mapambano na umwagikaji wa damu kwa msingi wa migawanyiko ya kisiasa, kidini, na kikabila. Wakristo wa kweli ‘hawajifunzi vita tena,’ hata iwe nini. Kitamathali, tayari wao ‘wamefua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.’ Wao hutokeza matunda ya amani ya roho ya Mungu.—1 Yohana 3:10-12; Isaya 2:2-4; Wagalatia 5:22, 23.
Mungu Hubariki Usafi wa Mwenendo na Mafundisho
12. (a) Ni nini lililo takwa la nane, lakini unaweza kutaja migawanyiko gani ya kidini? (b) Paulo alikaziaje takwa hili la nane?
12 Muungano wa Kikristo ni takwa la nane kwa ibada ya kweli. Hata hivyo, dini zenye kuleta migawanyiko za Jumuiya ya Wakristo hazijasaidia kwa habari hii. Nyingi za zile zinazoitwa dini mashuhuri zimegawanyika na kuwa mafarakano mbalimbali, matokeo yakiwa ni mvurugo. Kwa kielelezo, fikiria dini ya Baptisti katika Marekani, ambayo imegawanyika kuwa Wabaptisti wa Kaskazini (American Baptist Churches katika Marekani) na Wabaptisti wa Kusini (Southern Baptist Convention), pamoja na vikundi vingine vingi vya Baptisti ambavyo vimetokana na migawanyiko. (World Christian Encyclopedia, ukurasa 714) Migawanyiko mingi imetokea kwa sababu ya tofauti za mafundisho au usimamizi wa kanisa (kwa kielelezo, Kipresbiteri, Kiepiskopali, Kikongrigeshonali). Migawanyiko iliyo katika Jumuiya ya Wakristo inafanana na ile iliyo katika dini zisizo za Jumuiya ya Wakristo—iwe ni Dini ya Buddha, Uislamu, au Dini ya Hindu. Mtume Paulo aliwashauri nini Wakristo wa mapema? “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”—1 Wakorintho 1:10; 2 Wakorintho 13:11.
13, 14. (a) Ni nini kinachomaanishwa na ‘kuwa watakatifu’? (b) Ibada ya kweli hudumishwaje ikiwa safi?
13 Ni lipi takwa la tisa kwa dini inayokubaliwa na Mungu? Kanuni ya Biblia ionyeshwayo kwenye Mambo ya Walawi 11:45 (NW): “Ni lazima mthibitike kuwa watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” Mtume Petro alirudia kutaja takwa hili alipoandika hivi: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.”—1 Petro 1:15, italiki ni zetu.
14 Ni nini kinachodokezwa na uhitaji huu wa kuwa mtakatifu? Kwamba waabudu wa Yehova wapaswa kuwa safi kiroho na kiadili. (2 Petro 3:14) Hakuna nafasi kwa watenda-dhambi wa kimakusudi wasiotubu ambao kwa mwenendo wao waonyesha kudharau dhabihu ya fidia ya Kristo. (Waebrania 6:4-6) Yehova hutaka kwamba kutaniko la Kikristo lidumishwe likiwa safi na takatifu. Hilo hutimizwaje? Kwa sehemu hilo hutimizwa kwa tendo la kihukumu la kutenga na ushirika wale ambao wangechafua kutaniko.—1 Wakorintho 5:9-13.
15, 16. Wakristo wengi wamefanya mabadiliko gani maishani mwao?
15 Kabla ya kujua kweli ya Kikristo, wengi waliishi maisha mapotovu, yenye anasa yasiyo na uzuifu, na yenye ubinafsi. Lakini lile neno kuhusu Kristo liliwabadili, nao wamepata msamaha wa dhambi zao. Paulo alitaja jambo hilo kwa mkazo alipoandika: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa.”—1 Wakorintho 6:9-11, italiki ni zetu.
16 Ni dhahiri kwamba Yehova huwakubali wale wanaotubu mwenendo wao usio wa kimaandiko, na kugeuka, na kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo na mafundisho yake. Kwa kweli wao huwapenda majirani wao kama wanavyojipenda na kuonyesha hilo kwa njia nyingi sana, kama vile kwa kudumu katika huduma itoayo ujumbe wa uhai kwa wote wanaousikia.—2 Timotheo 4:5.
“Kweli Itawaweka Huru”
17. Ni nini lililo takwa la kumi kwa ibada ya kweli? Toa vielelezo.
17 Kuna takwa la kumi ambalo Yehova anataka wale wamwabuduo kwa roho na kweli watimize—fundisho safi. (Yohana 4:23, 24) Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Kweli ya Biblia hutuweka huru kutokana na mafundisho yenye kumshushia Mungu heshima, kama vile nafsi isiyoweza kufa, moto wa helo, na purgatori. (Mhubiri 9:5, 6, 10; Ezekieli 18:4, 20) Hiyo hutuweka huru kutokana na fumbo la Kibabiloni la “Utatu Mtakatifu Zaidi” wa Jumuiya ya Wakristo. (Kumbukumbu la Torati 4:35; 6:4; 1 Wakorintho 15:27, 28) Kutii kweli ya Biblia hutokeza watu wenye upendo, wenye rehema, wenye kujali na wenye fadhili. Ukristo wa kweli haujapata kamwe kutokeza watesaji wenye kisasi wasiovumilia kama vile Tomás de Torquemada, au wachochea vita wenye chuki kama wale papa wenye kuendeleza zile Krusedi. Lakini Babiloni Mkubwa ametokeza matunda ya aina hii katika historia yote, angalau tangu wakati wa Nimrodi mpaka sasa.—Mwanzo 10:8, 9.
Jina Linalotambulisha
18. (a) Ni nani wanaopatana na hayo matakwa kumi kwa ibada ya kweli na jinsi gani? (b) Ni lazima sisi mmoja-mmoja tufanye nini ili turithi baraka zilizo mbele yetu?
18 Ni nani leo ambao kwa kweli wanatimiza matakwa hayo kumi ya ibada ya kweli? Ni nani wanaojulikana na kutambuliwa na wengine kwa rekodi yao ya uaminifu-maadili na amani yao? Duniani pote Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14, 16; 18:36) Watu wa Yehova wamepewa heshima ya kubeba jina lake na kuwa Mashahidi wake, jinsi Yesu Kristo alivyokuwa shahidi mwaminifu kwa Baba yake. Sisi hubeba jina hilo takatifu, tukifahamu daraka letu la kuishi kulingana na kile kinachowakilishwa na jina hilo. Na, tukiwa Mashahidi wake, tuna matazamio matukufu kama nini mbele yetu! Yaani, kuwa sehemu ya familia ya kibinadamu iliyoungana, na kuabudu Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima katika paradiso iliyorudishwa hapa duniani. Ili kupokea baraka hiyo, na tuendelee kujitambulisha wazi kuwa upande wa ibada ya kweli na kubeba kwa fahari jina Mashahidi wa Yehova “kwa kuwa hukumu zake ni za kweli na za haki”!—Ufunuo 19:2; Isaya 43:10-12; Ezekieli 3:11.
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri zenyewe za Biblia si zenye upulizio wa Mungu. Tafsiri zenyewe zaweza kuonyesha utofauti wa kuelewa lugha za awali zilizotumiwa kurekodi Biblia.
Ungejibuje?
◻ Watumishi wa Yehova wauonaje uharibifu wa Babiloni Mkubwa?
◻ Ni yapi yaliyo matakwa muhimu kwa ibada ya kweli?
◻ Kweli hukuwekaje huru?
◻ Tumepewa heshima gani ya kipekee tukiwa Mashahidi wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mashahidi wa Yehova wanahubiri na kufundisha habari njema za Ufalme wa Mungu
[Picha katika ukurasa wa 18]
Sikuzote Wakristo wa kweli wamedumisha kutokuwamo kwa siasa za kilimwengu na vita
[Hisani]
Ndege: Kwa hisani ya Ministry of Defense, London