Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 5/15 kur. 29-31
  • Je, Wewe ni Painia Mwenye Usawaziko?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Wewe ni Painia Mwenye Usawaziko?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Dumu Ukiwa Mwenye Nguvu Kiroho!
  • Kusawazisha Madaraka ya Familia
  • Usawaziko wa Kiuchumi
  • Mapainia Wenye Usawaziko Ni Baraka Kwelikweli
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kutoa Utegemezo kwa Mapainia
    Huduma Yetu ya Ufalme—1992
  • Roho ya Huduma ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 5/15 kur. 29-31

Je, Wewe ni Painia Mwenye Usawaziko?

MACHO ya baba yang’aa akisubiri akiwa amenyosha mikono ili binti yake achukue hatua za kwanza za kusitasita. Aangukapo kwa ghafula, yeye amtia moyo ajaribu tena. Yeye ajua kuwa upesi atapata usawaziko na nguvu.

Kwa njia sawa na hiyo, mhudumu painia mpya huenda akahitaji wakati na kitia moyo kabla ya kupata usawaziko unaohitajiwa ili kufanikiwa akiwa mpiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote. Mapainia wengi huendelea kutumikia kwa shangwe kwa miongo mingi. Mabadiliko yasiyotazamiwa katika hali zao hufanya wachache wapoteze usawaziko wao. Wengine hata hupoteza shangwe yao. Katika nchi moja, asilimia 20 ya wale waanzao upainia huacha utumishi wa wakati wote katika miaka miwili ya kwanza. Ni nini kiwezacho kumfanya painia aache utumishi huu wenye shangwe zaidi? Je, lolote laweza kufanywa ili kuepuka matokeo mabaya hayo?

Ingawa afya mbaya, mahitaji ya kifedha, na madaraka ya familia yaweza kufanya wengine waache huduma ya wakati wote, kikwazo kwa wengi kimekuwa kushindwa kudumisha usawaziko mzuri kati ya majukumu mbalimbali ya Kikristo. Usawaziko hurejezea “hali ambayo hakuna sehemu yoyote inayolemea zile nyingine au haisawaziki na nyinginezo.”

Yesu Kristo alionyesha wanafunzi wake jinsi kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ilipaswa kufanywa. Katika huduma yake mwenyewe, alionyesha pia jinsi usawaziko hudumishwa. Yesu alionyesha kuwa viongozi wa kidini Wayahudi walikosa usawaziko, akiwaambia: “Mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.”—Mathayo 23:23.

Kanuni hiyo hutumika leo vilevile, hasa katika huduma ya upainia. Wakichochewa na idili na makusudio mazuri, wengine wameuchukua upainia kabla ya kujitayarishia kikamili au kufikiria yale yahusishwayo. (Luka 14:27, 28) Wengine wamejitoa sana katika huduma ya shambani hivi kwamba wamepuuza mambo mengine muhimu ya Kikristo. Wao wawezaje kupata na kudumisha usawaziko?

Dumu Ukiwa Mwenye Nguvu Kiroho!

Yesu hakupuuza hali yake ya kiroho. Ingawa umati uliokuja kumsikiliza na kuponywa ulichukua muda wake mwingi isivyo kawaida, yeye alipanga wakati wa kutoa sala ya kutafakari. (Marko 1:35; Luka 6:12) Kuusawazisha upainia leo pia hutaka mtu atumie vya kutosha maandalizi yote ya kuendelea kuwa mwenye nguvu kiroho. Paulo alisababu: “Basi wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe?” (Warumi 2:21) Bila shaka lingekuwa kosa kwa mtu kuutumia wakati wake wote akihubiria wengine huku akipuuza kupanga wakati wa kutosha kwa ajili ya funzo la kibinafsi na sala ya ukawaida.

Kumiko amekuwa painia kwa miongo miwili. Ingawa ana watoto watatu na mume asiyeamini, amegundua kutokana na mambo aliyojionea kuwa wakati umfaao kuisoma Biblia ni kabla tu ya kwenda kitandani. Ajifunzapo, yeye hasa huandika hoja awezazo kutumia katika huduma ya shambani ili aweze kufanya huduma yake ya kila siku iwe mpya na ya kupendeza. Mapainia wengine wenye mafanikio huamka kabla ya wengine katika familia kuamka ili kujilisha kiroho wakati wa zile saa za asubuhi zenye utulivu. Huenda ukawa na nyakati nyingine zifaazo zilizowekwa kando kwa ajili ya kutayarisha mikutano na kusoma vichapo vya karibuni zaidi vya Kikristo. Ukitamani kudumisha shangwe ya huduma, funzo la kibinafsi si jambo liwezalo kufanywa haraka-haraka au kupuuzwa.

Kusawazisha Madaraka ya Familia

Wazazi wanaopainia wahitaji kukumbuka kuwa sehemu kubwa ya “mapenzi ya Bwana” kwao hutia ndani kutunza mahitaji ya kimwili, kihisia-moyo, na kiroho ya familia yao wenyewe. (Waefeso 5:17; 6:1-4; 1 Timotheo 5:8) Nyakati nyingine hata mwenzi anayeamini na washiriki wa familia huhofu kuwa hawatastareheshwa na kutegemezwa na mke na mama mara tu huyo aanzapo kupainia. Hisia kama hizo hutokeza itikio lisilo changamfu kuelekea tamaa yake ya kuwa painia. Hata hivyo, kwa kupanga vizuri na kufikiri kimbele, usawaziko waweza kudumishwa.

Mapainia wengi hujitahidi kuhubiri sana wakati washiriki wa familia hawako nyumbani. Kumiko, aliyetajwa mapema, huwa na familia yake wakila kiamsha kinywa, huaga mume na watoto wake asubuhi waondokapo naye hurudi nyumbani kabla hawajarejea. Yeye hutumia siku za Jumatatu ili kupika vyakula mbalimbali mapema ili aweze kupumzika na kula milo pamoja na familia yake badala ya kujishughulisha mno jikoni. Kufanya zaidi ya kazi moja kwa wakati mmoja, kama vile kazi nyingine za nyumbani huku akitayarisha milo, pia husaidia. Kwa njia hiyo Kumiko hata hupata nafasi ya kukaribisha marafiki wa watoto wake nyumbani na kuwaandalia vitu vya kuwafurahisha.

Watoto wakuapo na kuingia katika miaka yao ya utineja, mara nyingi wao huhitaji uangalifu mwingi kutoka kwa wazazi katika kukabiliana na mambo mapya yawakumbayo kama hisia, tamaa, shaka, na woga. Hili hutaka mzazi aliye painia awe chonjo na kubadili ratiba. Mfikirie Hisako, painia aliye mama ya watoto watatu. Yeye alifanya nini wakati binti yake mkubwa zaidi alipoanza kukosa shangwe na uchangamfu kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na huduma ya shambani kwa sababu ya uvutano wa marafiki walimwengu shuleni? Uhitaji halisi ulikuwa binti yake kuufanya ukweli kuwa wake mwenyewe na kuwa na hakika kabisa kuwa kujitenga na ulimwengu ndiyo njia bora zaidi.—Yakobo 4:4.

Hisako asema: “Niliamua kujifunza tena naye mafundisho ya msingi katika kitabu Kuishi Milele kila siku. Mwanzoni tuliweza kujifunza kwa dakika chache tu, mara nyingi binti yangu akilalamika kuwa na maumivu makali ya tumbo na kichwa wakati wa funzo ulipofika. Lakini niliongoza hilo funzo kwa ukawaida. Baada ya miezi michache, mwelekeo wake ulibadilika sana, ukielekeza kwenye kujiweka kwake wakfu na kubatizwa baada ya muda mfupi.” Sasa Hisako anafurahia huduma ya wakati wote pamoja na binti yake.

Akina baba wanaopainia pia wahitaji kuwa waangalifu ili wasijikute wakijihusisha sana katika kutunza wanaopendezwa shambani na wajibu wao mbalimbali wa kutaniko hivi kwamba wanashindwa kuwapa watoto wao wanaokua utegemezo na mwongozo wa kihisia-moyo wenye nguvu ambao wanahitaji. Hili si jambo ambalo mwanamume apaswa kumsukumia mke wake. Mzee Mkristo mwenye shughuli nyingi ambaye amekuwa painia kwa muda mrefu na ambaye pia ana biashara ndogo hupanga wakati wa kujifunza na kila mmoja wa watoto wake wanne. (Waefeso 6:4) Kwa kuongezea, yeye hutayarisha mikutano ya kila juma pamoja na familia yake. Mapainia wenye usawaziko hawaziachilii familia zao kimwili au kiroho.

Usawaziko wa Kiuchumi

Mtazamo ufaao wa mahitaji ya kila siku ni eneo jingine ambalo mapainia wapaswa kujitahidi kudumisha usawaziko mzuri. Hapa tena, twaweza kujifunza mengi kutoka kwa kielelezo na shauri zuri la Yesu. Alionya dhidi ya kusumbukia mahitaji ya kimwili kupita kiasi. Badala ya hilo, aliwatia wanafunzi wake moyo kuutanguliza Ufalme, akiahidi kuwa Mungu atawatunza kama atunzavyo uumbaji mwingine wote. (Mathayo 6:25-34) Kwa kufuata shauri hilo zuri, mapainia wengi wameweza kubaki katika utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi, na Yehova amebariki jitihada zao za kutafuta “riziki.”—Mathayo 6:11.

Mtume Paulo aliwashauri Wakristo wenzake kwamba ‘[“ukubalifu,” NW] wao na ujulikane na watu wote.’ (Wafilipi 4:5) Kwa kweli ukubalifu hutaka tutunze ifaavyo afya yetu. Mapainia wenye usawaziko hujitahidi kuonyesha ukubalifu katika njia yao ya maisha na katika mtazamo wao kuelekea vitu vya kimwili, wakijua kuwa wengine huutazama mwenendo wao.—Linganisha 1 Wakorintho 4:9.

Vijana wachukuao utumishi wa upainia wapaswa kuepuka kutumia vibaya ukarimu wa wazazi wao. Ikiwa wanaishi katika nyumba ya wazazi wao, ungekuwa wonyesho wa usawaziko mzuri na uthamini kushiriki katika kazi za nyumbani na kuwa na kazi isiyo ya muda wote ambayo itawawezesha kuchangia gharama za nyumbani.—2 Wathesalonike 3:10.

Mapainia Wenye Usawaziko Ni Baraka Kwelikweli

Huenda ukawa painia anayejitahidi sana kuwa na usawaziko mzuri. Uwe na hakika kwamba waweza kuwa na usawaziko. Kama tu vile mtoto mdogo huhitaji wakati ili kujifunza kujisawazisha na kutembea, mapainia wengi waliokomaa husema kuwa ilichukua wakati kupata usawaziko katika kutunza wajibu wao mbalimbali.

Kuwa na funzo la kibinafsi, kutunza washiriki wa familia, na kujiandalia mahitaji yao wenyewe ya kimwili ni baadhi ya maeneo ambayo mapainia hujitahidi kuwa na usawaziko. Ripoti huonyesha kwamba mapainia wengi hutimiza madaraka yao kwa njia ya kutokeza sana. Wao ni baraka kwelikweli kwa jumuiya nao humletea Yehova na tengenezo lake sifa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki