Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 7/15 kur. 3-4
  • “Tufundishe Sisi Kusali”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Tufundishe Sisi Kusali”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mifano na “Watakatifu-Wafadhili”
  • Chanzo cha Rozari
  • Je! Wakristo Wapaswa Kutumia Tasbihi (Rozari)?
    Amkeni!—1990
  • Je, Tunapaswa Kusali kwa Watakatifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Watakatifu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Usali kwa Bikira Maria?
    Amkeni!—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 7/15 kur. 3-4

“Tufundishe Sisi Kusali”

“BWANA, tufundishe sisi kusali.” Ombi hilo lilitolewa na mmoja wa wanafunzi wa Yesu Kristo. (Luka 11:1) Ni wazi kwamba mwanafunzi huyo asiyetajwa kwa jina alikuwa mtu aliyethamini sala kwa kina. Vivyo hivyo waabudu wa kweli leo hutambua umaana wa sala. Iwayo yote, sala ndiyo njia ambayo kwayo twapata fursa ya kusikiwa na Mtu wa Juu Zaidi katika ulimwengu wote mzima! Na ebu wazia! “Msikiaji wa sala” (NW) hutolea mahangaiko na masumbufu yetu uangalifu wa kibinafsi. (Zaburi 65:2) La maana hata zaidi, kupitia sala, sisi humtolea Mungu shukrani na sifa.—Wafilipi 4:6.

Hata hivyo, maneno “tufundishe sisi kusali” hutokeza maswali fulani mazito. Ulimwenguni pote njia nyingi za kumfikia Mungu hutumiwa na dini tofauti-tofauti. Lakini je, kuna njia ifaayo na isiyofaa ya kusali? Ili kujibu, acheni kwanza tuchunguze baadhi ya desturi za kidini zipendwazo na watu wengi zinazohusisha sala. Tutakazia uangalifu desturi zinazofuatwa katika Amerika ya Latini.

Mifano na “Watakatifu-Wafadhili”

Kwa ujumla, nchi za Amerika ya Latini hufuatia dini sana. Kwa kielelezo, kotekote Mexico mtu aweza kuona lile zoea lipendwalo na watu wengi la kusali kwa “watakatifu-wafadhili.” Kwa kweli, ni desturi kwa miji ya Mexico kuwa na “watakatifu-wafadhili” wanaofanyiwa misherehekeo siku fulani-fulani. Wakatoliki wa Mexico pia husali kwa mifano ya namna nyingi. Hata hivyo, uamuzi juu ya ni “mtakatifu” yupi wa kuelekezewa sala wategemea aina ya ombi ambalo mwabudu ataka kutoa. Ikiwa mtu anamtafuta mtu wa kumwoa, aweza kumwashia mshumaa “Mtakatifu” Anthony. Mtu atakayefunga safari kwa gari aweza kujikabidhi mikononi mwa “Mtakatifu” Christopher, mfadhili wa wasafiri, hasa wa wale wasafirio kwa magari.

Lakini, desturi hizo zilianzia wapi? Historia huonyesha kwamba Wahispania walipofika Mexico, walikuta watu waliojitoa kwa ibada ya miungu ya kipagani. Katika kitabu chake Los Aztecas, Hombre y Tribu (Waazteki, Mtu na Kabila), Victor Wolfgang von Hagen asema hivi: “Kulikuwa na miungu ya kibinafsi, kila mmea ulikuwa na mungu wao, kila utendaji ulikuwa na mungu au mungu wa kike wao, hata kujiua kulikuwa na mungu wako. Yacatecuhtli alikuwa mungu wa wanabiashara. Katika ulimwengu huu wenye kuamini miungu mingi, miungu yote ilikuwa na mielekeo na kazi mbalimbali zilizokuwa dhahiri.”

Ufanani kati ya miungu hiyo na “watakatifu” wa Katoliki ulitokeza sana hivi kwamba washindi Wahispania walipojaribu “kuwafanya Wakristo” wenyeji wa huko, hao waligeuza tu utii wao kutoka sanamu zao na kuuelekeza kwa “watakatifu” wa kanisa. Makala katika The Wall Street Journal ilikiri kwamba Ukatoliki unaozoewa katika sehemu fulani za Mexico una mizizi katika desturi za watu wasioamini Mungu wala Biblia. Ilionyesha kwamba katika eneo moja, wengi wa wale “watakatifu” 64 waliostahiwa na watu, walifanana na “miungu hususa ya Kimaya.”

Buku New Catholic Encyclopedia labisha kwamba “kifungo imara chenye ukaribu wa uhakika kinafanyizwa kati ya mtakatifu na wale wanaomwelekezea sala, . . . kifungo ambacho, badala ya kupunguza uhusiano pamoja na Kristo na pamoja na Mungu, huutia nguvu na kuukuza.” Lakini kifungo ambacho kwa wazi ni alama ya upagani kingeweza kuukuzaje uhusiano wa mtu pamoja na Mungu wa kweli? Je, sala zitolewazo kwa “watakatifu” hao zingeweza kwa kweli kumpendeza Mungu?

Chanzo cha Rozari

Desturi nyingine ipendwayo na watu wengi huhusisha matumizi ya rozari. Kitabu Diccionario Enciclopédico Hispano-Americano (Kamusi ya Kiensaiklopidia ya Kihispania na Kiamerika) hufafanua rozari kuwa “uzi wenye shanga hamsini au mia moja na hamsini zilizotenganishwa katika vikundi vya kumi-kumi kwa nyinginezo zilizo kubwa zaidi na kuunganishwa na kisalaba kwenye miisho, ambacho kwa sasa chatanguliwa na shanga tatu.”

Kikieleza jinsi rozari hutumiwa, kichapo kimoja cha Katoliki chasema: “Ile Rozari Takatifu ni aina ya sala ya sauti na ya akili juu ya Mafumbo ya ukombozi wetu. Hufanyizwa na vikundi kumi na vitano. Kila kikundi hutia ndani kuikariri ile Sala ya Bwana, Salamu Mariamu kumi, na Utukufu Uwe wa Baba. Katika kila kikundi, kuna kutafakari juu ya fumbo fulani.” Hayo mafumbo ni mafundisho ambayo Wakatoliki wapaswa kujua, katika kisa hiki yakirejezea uhai, kuteseka, na kifo cha Kristo Yesu.

Buku The World Book Encyclopedia lasema hivi: “Njia za mapema za kusali kwa kutumia rozari zilianza katika Ukristo wakati wa Enzi za Kati, lakini ni katika miaka ya 1400 na 1500 tu zilipoenea.” Je, rozari hutumiwa katika Ukatoliki pekee? La. Kitabu Diccionario Enciclopédico Hispano-Americano chataarifu: “Shanga za aina iyo hiyo hutumiwa katika Ibada ya Kiislamu, Kilama na Kibuddha.” Kwa kweli, Encyclopedia of Religion and Religions yaonyesha kwamba: “Imedokezwa kwamba Waislamu walipokea Rozari kutoka kwa Wabuddha, na Wakristo kutoka kwa Waislamu wakati wa zile Krusedi.”

Wengine hubisha kwamba rozari hutumika tu ikiwa kikumbusha wakati sala kadhaa zinapohitaji kurudiwa-rudiwa. Lakini je, Mungu hupendezwa na matumizi yayo?

Hatuhitaji kukisia-kisia au kujadiliana juu ya kufaa kwa desturi hizo au uhalali wazo. Yesu alitoa itikio lenye mamlaka kwa ombi la kuwafundisha wafuasi wake jinsi ya kusali. Yale aliyosema yatatuelimisha na huenda hata yakashangaza wasomaji wengine.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Wakatoliki kwa kawaida hutumia shanga za rozari. Chanzo chazo ni nini?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki