Je, Nafsi ni Isiyoweza Kufa?
MARAFIKI na familia watembea kimya-kimya kando ya jeneza lililo wazi. Wanautazama mwili, ule wa kijana mwenye umri wa miaka 17. Ni vigumu kwa marafiki wake wa shuleni kumtambua. Amepoteza nywele nyingi kwa sababu ya tiba ya kemikali; kansa imemfanya apunguke uzito sana. Je, kweli huyu aweza kuwa rafiki yao? Majuma kadhaa tu kabla ya hapo, alikuwa amejaa mawazo mengi, maswali mengi, nishati nyingi—uhai mwingi! Mama ya kijana huyo arudia-rudia maneno haya akiwa na machozi: “Tommy ni mwenye furaha zaidi sasa. Mungu alitaka Tommy awe mbinguni naye.”
Mama huyo mwenye kuvunjika moyo apata kadiri fulani ya tumaini na faraja katika wazo la kwamba mwana wake angali hai kwa njia fulani. Amefundishwa kanisani kwamba nafsi ni isiyoweza kufa, kwamba hiyo ni kitovu cha utu, mawazo, kumbukumbu—mtu “binafsi.” Yeye aamini kwamba nafsi ya mwana wake, haikufa hata kidogo; ikiwa roho iliyo hai, iliondoka mwili wake alipokufa, ikaenda mbinguni ili kuwa pamoja na Mungu na malaika.
Wakati wa msiba, moyo wa kibinadamu hushikamana sana na ishara yoyote ya tumaini, kwa hiyo si vigumu kuona ni kwa nini itikadi hiyo huvutia watu wengi sana. Kwa mfano, ona vile mwanatheolojia J. Paterson-Smyth anavyojieleza katika kitabu The Gospel of the Hereafter: “Kifo ni jambo dogo sana kwa kulinganishwa na kile kifuatacho—ulimwengu ule wa ajabu, sana sana, ambamo Kifo hutuingiza.”
Kotekote ulimwenguni na katika dini na desturi nyingi, watu huamini kwamba mwanadamu ana nafsi ndani yake isiyoweza kufa, roho yenye ufahamu iendeleayo kuishi baada ya mwili kufa. Itikadi hiyo imeenea karibu kotekote katika yale maelfu ya dini na mafarakano ya Jumuiya ya Wakristo. Hilo ni fundisho rasmi katika Dini ya Kiyahudi. Wahindu huamini kwamba atman, au nafsi, iliumbwa mwanzoni kabisa, imefungiwa mwilini wakati wa kuzaliwa, na huhamia mwili mwingine wakati wa kifo katika duru (kawaida) yenye kuendelea ya kuzaliwa upya katika umbo jingine. Waislamu huamini kwamba nafsi inakuja kuwako pamoja na mwili wakati wa kuzaliwa na huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Imani nyinginezo—waabudu-maumbile Waafrika, Washinto, hata Wabuddha kwa njia fulani—hufundisha mambo mbalimbali juu ya habari hiyohiyo.
Maswali Fulani Yenye Kusumbua
Ingawa ni wazi kwamba dhana ya nafsi isiyoweza kufa ni yenye kuvutia watu wengi sana, hata hivyo inatokeza maswali fulani yenye kusumbua. Kwa kielelezo, watu hujiuliza nafsi ya mpendwa inakwenda wapi ikiwa yeye hakuonyesha kielelezo kizuri maishani mwake. Je, yeye atazaliwa upya katika umbo jingine la kiumbe chenye hali ya chini? Au je, anatumwa purgatori, ambako atasafishwa kwa utaratibu fulani wenye moto mpaka aonwe kuwa astahili kwenda mbinguni? Kwa ubaya zaidi, je, yeye apasa kuteswa milele katika helo yenye moto? Au je, yeye ni roho apaswaye kutulizwa, kama vile dini nyingi za waabudu-maumbile hufundisha?
Dhana hizo hutokeza matarajio yenye kuwalemea walio hai. Je, tutulize roho za wapendwa wetu waliokufa wasije wakatulipiza kisasi? Je, twapaswa kuwasaidia kutoka katika purgatori fulani yenye kutisha? Au tutetemeke tu tukihofu sana tufikiriapo kuteseka kwao katika helo? Au tuwatendee wanyama fulani walio hai kana kwamba ndani yao wana nafsi za wanadamu waliokufa?
Maswali yanayotokea kumhusu Mungu mwenyewe ni yenye kusumbua pia. Kwa mfano, wazazi wengi, kama yule mama anayetajwa mwanzoni, hufarijiwa kwanza na dhana ya kwamba Mungu “alichukua” nafsi isiyoweza kufa ya mtoto wao ili awe naye mbinguni. Lakini upesi wengi huanza kujiuliza ni Mungu wa aina gani ambaye angemtesa mtoto asiye na hatia kwa ugonjwa wenye kuchukiza sana, akimtwaa kwa ghafula mtoto huyo anayethaminiwa sana kutoka kwa wazazi wenye kuvunjika moyo ili tu kumhamisha mtoto huyo mbinguni kupitia kifo kisichotarajiwa. Je, Mungu wa jinsi hiyo ana haki, upendo, na rehema? Watu fulani hata hutilia shaka hekima ya Mungu wa jinsi hiyo. Wao huuliza kwa nini Mungu mwenye hekima aweke nafsi hizi zote duniani mwanzoni ikiwa zote zapaswa kuwa mbinguni hatimaye? Je, hilo halingemaanisha kwamba uumbaji wa dunia ulikuwa jitihada ya bure sana?—Linganisha Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 103:8; Isaya 45:18; 1 Yohana 4:8.
Basi, ni wazi kwamba fundisho la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, hata lifundishweje, hutokeza maswali ya kutatanisha, hata mambo yenye kupingana. Kwa sababu gani? Tatizo hasa linahusisha machimbuko ya fundisho hilo. Huenda ukaliona kuwa jambo lenye kuelimisha kuchunguza vyanzo hivyo kifupi; na huenda ukashangaa kujifunza yale ambayo Biblia yenyewe husema kuhusu nafsi. Inatoa tumaini zuri zaidi la uhai baada ya kifo kuliko lile lifundishwalo kwa kawaida na dini za ulimwengu.