Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
‘Mlango Mkubwa Uongozao Kwenye Utendaji Umefunguliwa’ Katika Kuba
MTUME Paulo alikuwa mhubiri mwenye kutokeza wa habari njema ya Ufalme wa Mungu. Alitumia kila fursa ili kushiriki na wengine ahadi za Muumba za uhai udumuo milele kwa ajili ya wanadamu watiifu. Alipokuwa akizuru Efeso la kale, Paulo alitambua hali mpya ambayo ingemruhusu asaidie watu wengi hata zaidi. Alisema hivi: “Ninakaa katika Efeso . . . ; kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.”—1 Wakorintho 16:8, 9, NW.
Mashahidi wa Yehova katika Kuba wanajipata pia wakiwa katika hali mpya. Ingawa bado hawajasajiliwa kirasmi, sasa Mashahidi wanaweza kushiriki tumaini lao la Biblia pamoja na wananchi wenzao hadharani. Juzijuzi serikali ya Kuba ilionyesha kwamba inapendezwa sana kuruhusu vikundi mbalimbali vya kidini kutenda bila kizuizi. Rais Castro amewataja Mashahidi wa Yehova hadharani kuwa kikundi cha kidini ambacho sasa kina uhusiano bora zaidi pamoja na serikali ya Kuba.
Hali hiyo mpya ‘imewafungulia Mashahidi mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.’ Kwa kielelezo, juzijuzi Mashahidi wa Yehova walifungua ofisi Kuba, inayowasaidia waratibu kazi yao ya kuhubiri katika nchi hiyo. Mashahidi zaidi ya 65,000 wanasaidia watu kujifunza na kuelewa Biblia. Wanatumia fasihi za Biblia, kama magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wakuba wengi wenye mwelekeo wa uadilifu wananufaika na kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.
Mashahidi wanafanya pia mikutano ya kawaida katika vikundi vidogo kotekote katika hicho kisiwa. Nyakati nyingine wanafurahia hata lile pendeleo la kufanya makusanyiko makubwa zaidi katika vikundi vya watu wapatao 150. Wanathamini kikweli ruhusa ambayo wamepokea kutoka kwa wenye mamlaka wa Kuba, inayowapa fursa ya kukusanyika pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho, wakiimba sifa kwa Mungu, na kusali pamoja.
Juzijuzi “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya ulifanywa zaidi ya mara 1,000 katika miisho-juma mitatu tu. Ripoti moja husema kwamba “utaratibu, nidhamu, na amani” zilidhihirika kwenye kila mkusanyiko. Wenye mamlaka waliwapa Mashahidi heko kwa ajili ya jambo hilo.
Ulimwenguni pote, Wakristo wa kweli hujitahidi kutimiza amri waliyopewa na Mungu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wakati uleule, wanajitahidi kudumisha uhusiano wenye amani pamoja na wenye mamlaka wa serikali. (Tito 3:1) Mashahidi wa Yehova hufuata shauri la mtume Paulo aliyeandika hivi: “Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.”—1 Timotheo 2:1, 2.