Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 12/1 kur. 15-20
  • Vijana Wamkumbukao Muumba Wao

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana Wamkumbukao Muumba Wao
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu Yu Halisi Kadiri Gani Kwako?
  • Kinachomaanishwa na Kukumbuka
  • Elimu Yenye Kusudi
  • Sababu Gani Utumie Fedha Zako kwa Hekima?
  • Vijana Wanaostahili Kuigwa
  • Elimu Yenye Kusudi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Je, Biblia Inapinga Elimu?
    Amkeni!—1998
  • Elimu—Gharama Yake? Faida Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Elimu?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 12/1 kur. 15-20

Vijana Wamkumbukao Muumba Wao

“Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”—MHUBIRI 12:1.

1. Ni maneno gani ya kijana mwenye umri wa miaka 11 yanayoonyesha kwamba Muumba wetu yu halisi kwake?

NI VIZURI kama nini vijana wanaposema na kutenda katika njia inayoonyesha kwamba wanamwona Yehova Mungu kuwa mtu halisi wanayemstahi na wanayetaka kumpendeza! Mvulana wa miaka 11 alisema hivi: “Ninapokuwa peke yangu na kutazama nje dirishani, naona jinsi maumbile ya Yehova yalivyo ya ajabu. Kisha naota jinsi Paradiso itakavyokuwa nzuri wakati ujao na jinsi niwezavyo kuwagusa wanyama wakati huo.” (Isaya 11:6-9) Aliongeza hivi: “Ninapokuwa peke yangu, ninasali kwa Yehova. Najua hatanikasirikia kwa sababu ya kuzungumza naye nyakati zote. Najua yupo akinitazama sikuzote.” Je, Muumba wetu yu halisi kwako kama alivyo kwa mvulana huyo?

Mungu Yu Halisi Kadiri Gani Kwako?

2. (a) Muumba wako aweza kuwaje halisi kwako? (b) Wazazi waweza kuwa na fungu gani katika kuwasaidia watoto wao wathamini kwamba Mungu ni mtu halisi?

2 Ili Yehova na ahadi zake awe halisi kwako, lazima kwanza ujifunze juu yake na wakati ujao wa ajabu anaokutolea katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Biblia hufafanua. (Ufunuo 21:3, 4) Ikiwa wazazi wako wamekufundisha juu ya mambo hayo, una sababu ya kuwa na shukrani kwa sababu hilo hukuwezesha kutii amri hii iliyopuliziwa: ‘Mkumbuke Muumba wako.’ (Mhubiri 12:1) Kijana mmoja alisema hivi kuhusu mazoezi yake ya mapema kutoka kwa wazazi: “Kila jambo maishani lilimhusisha Yehova sikuzote. Huo ulikuwa ufunguo wa kumkumbuka kwangu Muumba wangu.” Mwanamke kijana mwingine alionelea hivi: “Nitakuwa mwenye shukrani kwa wazazi wangu milele kwa kunifundisha kwamba Yehova ni mtu halisi. Walinionyesha jinsi ya kumpenda na wakaniambia juu ya shangwe ya kumtumikia wakati wote.”

3, 4. Ni nini kiwezacho kukusaidia kumfikiria Yehova kuwa mtu halisi?

3 Hata hivyo, wengi huona vigumu kumwona Mungu kuwa mtu halisi anayependezwa nao. Je, wamwona hivyo? Kijana mmoja alisaidiwa kumfikiria Mungu katika njia ya kibinafsi kupitia taarifa hii katika Mnara wa Mlinzi: “Jinsi Yehova Mungu alivyo mkubwa kwa habari ya mwili wake, hatujui.” Bila shaka ukuu wa Mungu hautegemei ukubwa au umbo lake, kama vile sentensi inayofuata katika Mnara wa Mlinzi hilo ilivyosema: “Ukuu wake halisi uko katika kuwa aina ya Mungu aliye,” kwelikweli, Mungu mwaminifu, mwenye huruma, mwenye upendo, na mwenye kusamehe.a (Kutoka 34:6; Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 86:5; Yakobo 5:11) Je, umekuja kumwona Yehova kuwa mtu wa aina hiyo, rafiki mwenye kutumainika ambaye waweza kuwa na uhusiano wenye thamani pamoja naye?—Isaya 41:8; Yakobo 2:23.

4 Yesu aliwasaidia wafuasi wake wa mapema wafurahie uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Hivyo, mtume Yohana alipoandika juu ya kufufuliwa kwake kwenye uhai wa kimbingu alikotarajia, Yohana alionelea hivi: “Tutafanana naye [Mungu]; kwa maana tutamwona kama alivyo.” (1 Yohana 3:2; 1 Wakorintho 15:44) Vijana leo waweza pia kusaidiwa wamwone Mungu kuwa mtu halisi, mmoja ambaye waweza kupata kumjua vizuri ingawa hawawezi kumwona kibinafsi. Mwanamume kijana alisema hivi: “Wazazi wangu walinisaidia kumkumbuka Yehova kwa kuuliza maswali mengi, kama, ‘Yehova angesema nini? Ungeelezaje hilo katika maneno yako mwenyewe? Hilo lamaanisha nini?’” Je, maswali kama hayo hayafanyi tufikirie uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Mungu?

Kinachomaanishwa na Kukumbuka

5. Ni vielelezo gani vya Biblia vinavyoonyesha kwamba kumkumbuka mtu kwahusisha mengi zaidi ya kukumbuka jina lake?

5 Kutii amri hiyo, ‘Mkumbuke Muumba wako,’ kwamaanisha mengi zaidi ya kumfikiria Yehova tu. Kwahusisha utendaji, kufanya limpendezalo. Yule mhalifu alipomwomba sana Yesu, ‘Nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako,’ alitaka Yesu afanye zaidi ya kulikumbuka jina lake. Alitaka Yesu atende, amfufue. (Luka 23:42) Vivyo hivyo, Yosefu aliyefungwa gerezani alitarajia tendo fulani kwa niaba yake alipomwomba mnyweshaji wa Farao amkumbuke kwa Farao. Na Ayubu alipomwomba Mungu kwa unyenyekevu, ‘Unikumbuke,’ Ayubu alikuwa akiomba kwamba wakati fulani ujao, Mungu atende kwa kumfufua.—Ayubu 14:13; Mwanzo 40:14, 23.

6. Neno la Kiebrania “kumbuka” hudokezaje shauku kwa ajili ya kitu au mtu akumbukwaye?

6 Chanzo kimoja chenye mamlaka chasema kwamba neno la Kiebrania litafsiriwalo “kumbuka” mara nyingi hudokeza “ile shauku ya akili na tendo linaloandamana na kukumbuka.” Kudokezwa kwa “shauku” katika neno “kumbuka” kwaweza kuonekana katika manung’uniko ya “mkutano wa wafuasi” nyikani: ‘Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri.’ Sawa na vile Ayubu alivyoomba kwa unyenyekevu akumbukwe kwa upendeleo na Mungu, ndivyo Hezekia, Nehemia, Daudi, na mtunga-zaburi asiyetajwa kwa jina walivyoomba pia wakumbukwe kwa shauku na Yehova kwa kutambua uaminifu wao.—Hesabu 11:4, 5; 2 Wafalme 20:3; Nehemia 5:19; 13:31; Zaburi 25:7; 106:4.

7. Tukimkumbuka Mungu kwa shauku, hilo litaathirije mwenendo wetu?

7 Hivyo twaweza kujiuliza, ‘Je twamkumbuka Muumba wetu kwa shauku na kuepuka kufanya lolote la kumfanya ahisi umizo au umivu?’ Kijana mmoja alionelea hivi: “Katika umri mdogo sana, mama alinisaidia kutambua kwamba Yehova ana hisia, nilijua kwamba matendo yangu yalimwathiri.” (Zaburi 78:40-42) Kijana mwingine alieleza hivi: “Nilijua kwamba matendo yangu ama yangesaidia ama yangezuia katika kujibu dai ambalo Shetani alimtolea Yehova. Nilitaka kuufurahisha moyo wa Yehova, kwa hiyo hilo lilinisaidia nalo huendelea kunisaidia leo.”—Mithali 27:11.

8. (a) Ni ufuatiaji wa nini utakaoonyesha kwamba twamkumbuka Yehova kwa shauku? (b) Vijana watafikiria kwa hekima maswali yapi?

8 Yakubalika kwamba, katika ulimwengu huu mwovu, si rahisi sikuzote kumkumbuka Yehova kwa kushiriki kikamili katika utendaji umpendezao. Hata hivyo ingekuwa vema kama nini ikiwa ungeweza kumwiga kijana Timotheo wa karne ya kwanza—bila kutaja maelfu ya vijana wanaomhofu Mungu leo—kwa kufuatia utumishi wa Kikristo wa wakati wote ukiwa mhudumu painia! (Matendo 16:1-3; 1 Wathesalonike 3:2) Ingawa hivyo, yaweza kuulizwa, Je, ungeweza kujitegemeza mwenyewe katika huduma ya upainia? Na ikiwa ungeoa au ungeolewa, je, ungekuwa na stadi za kuandalia wale walio katika familia yako? (1 Timotheo 5:8) Hayo ni maswali ya maana, na ni muhimu uyafikirie kwa uzito.

Elimu Yenye Kusudi

9. Ni uamuzi gani unaowakabili vijana juu ya elimu ya kilimwengu?

9 Kadiri jamii ya kibinadamu izidivyo kuwa tata, kiwango kikubwa zaidi cha elimu huenda kikahitajiwa ili kupata kazi ya kutosha ya kujitegemeza katika kazi ya upainia. Huenda ikawa umeona kwamba hata wengine wenye elimu ya chuo kikuu wamelazimika kupata mafunzo ya ziada ili wapate stadi mpya zinazothaminiwa na waajiri leo. Kwa hiyo, nyinyi vijana mnaotaka kumpendeza Mungu mtafuatia kiwango gani cha elimu? Uamuzi wapasa kufanywa ifaavyo mkifikiria amri hii iliyopuliziwa: ‘Mkumbuke Muumba wako.’

10. Ni elimu gani bora zaidi tuwezayo kupokea?

10 Bila shaka, mtataka kufuatia kile ambacho hata wengi wa wenye mamlaka za kilimwengu huona kuwa elimu bora zaidi—ile ipatikanayo kutoka kwenye funzo lenye uangalifu la Neno la Mungu. Mwandikaji Mjerumani Johann Wolfgang von Goethe asema hivi: “Kadiri maendeleo ya kiakili [ya kikundi cha watu] yalivyo makubwa, ndivyo kunavyokuwa na uwezekano kamili zaidi wa kuitumia Biblia ikiwa msingi na pia kifaa cha elimu.” Ndiyo, funzo la Biblia litawaandalia vifaa bora maishani kuliko elimu nyingine yoyote itakavyoweza!—Mithali 2:6-17; 2 Timotheo 3:14-17.

11. (a) Ni kazi gani ya maana zaidi tuwezayo kufanya? (b) Kwa nini kijana mmoja aliamua kupata kiasi fulani cha elimu?

11 Kwa kuwa ujuzi juu ya Mungu hupa uhai, kazi ya maana zaidi uwezayo kufanya leo ni kushiriki ujuzi huo pamoja na wengine. (Mithali 3:13-18; Yohana 4:34; 17:3) Hata hivyo, ili kufanya hilo kwa matokeo zaidi, wahitaji kuelimishwa katika njia za msingi. Wahitaji kuweza kufikiri waziwazi, kusema kwa kutumia akili, na kusoma na kuandika vizuri—stadi zinazofundishwa shuleni. Kwa hiyo chukua kwa uzito mitaala yako ya shule, kama alivyofanya Tracy, kijana katika Florida, Marekani, aliyehitimu kutoka shule ya sekondari akiwa na tuzo za kielimu. Alieleza tumaini lake hivi: “Mradi wangu sikuzote umekuwa kuwa mtumishi wa wakati wote wa Mungu wangu Yehova, nami natumaini kwamba elimu yangu itanisaidia nifikie mradi huo.”

12. Ikiwa elimu ya kilimwengu ya ziada inachaguliwa, hiyo yaweza kusaidia kutimiza kusudi jipi?

12 Je, umefikiria ni kwa nini unaenda shuleni? Je, ni kwa kusudi hasa la kujiandalia vifaa ili uwe mhudumu mwenye matokeo wa Yehova? Ikiwa ndivyo, utataka kufikiria kwa uzito elimu yako inatimiza kusudi hilo vizuri kadiri gani. Baada ya kupata shauri kwa wazazi wako, yaweza kuamuliwa kwamba wapaswa kufuatia elimu kupita kiwango cha chini zaidi kinachotakwa na sheria. Elimu hiyo ya ziada yaweza kukusaidia kupata kazi ya kuajiriwa ili kujitegemeza na bado kukuacha ukiwa na wakati na nishati za kushiriki kikamili katika utendaji wa Ufalme.—Mathayo 6:33.

13. Wakristo Warusi wawili waliofuatia elimu ya ziada walionyeshaje kusudi lao maishani?

13 Watu fulani wanaofuatia elimu ya ziada wanashiriki katika huduma ya wakati wote hata wanapoendelea kupokea elimu zaidi. Wafikirie Nadia na Marina, wasichana wawili matineja katika Moscow, Urusi. Wote wawili walibatizwa katika Aprili 1994 wakaanza kutumika wakiwa wahudumu mapainia-wasaidizi. Muda mfupi baadaye walihitimu kutoka shule ya sekondari na wakajiandikisha katika programu ya miaka miwili ya somo la hesabu. Katika Mei 1995 walianza upainia wa kawaida, na bado walidumisha wastani wa A katika masomo yao ya hesabu. Zaidi ya hayo, wao wawili waliweza kuongoza wastani wa mafunzo ya Biblia 14 kila juma huku wakiendelea kwenda shuleni. Wasichana hao wanatarajia kwamba elimu yao katika hesabu itawawezesha kupata kazi ya kuajiriwa ya kutosha, ili waweze kujitegemeza katika huduma ya wakati wote.

14. Bila kujali kiasi cha elimu ya kilimwengu tunachochagua, jambo la maana zaidi maishani mwetu lapasa kuwa nini?

14 Ukifuatia elimu ya kilimwengu kupita inavyotakwa na sheria, chunguza kwa hekima sababu za kufanya hivyo. Je, ni ili kujifanyia jina na kupata mali za kimwili? (Yeremia 45:5; 1 Timotheo 6:17) Au mradi wako ni kutumia elimu ya ziada ili kushiriki kikamili zaidi katika utumishi wa Yehova? Lydia, kijana aliyechagua kufuatia elimu ya ziada, alionyesha kuelekeza fikira vizuri juu ya mambo ya kiroho, akieleza hivi: “Wengine hufuatia elimu ya juu na kuruhusu ufuatiaji vitu vya kimwili uwazuie, nao wamemsahau Mungu. Uhusiano wangu pamoja na Mungu ndilo jambo la maana zaidi kwangu kibinafsi.” Ni mtazamo ustahilio pongezi kama nini kwetu sote!

15. Ni viwango vipi mbalimbali vya kielimu vilivyokuwapo miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza?

15 Jambo la maana ni kwamba, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na viwango mbalimbali vya kielimu. Kwa kielelezo, mtume Petro na mtume Yohana, walionwa kuwa watu “wasio na elimu, wasio na maarifa” kwa kuwa hawakuwa wamezoezwa katika shule za kirabi. (Matendo 4:13) Kwa upande mwingine, mtume Paulo alipokea ile ambayo leo yalingana na elimu ya chuo kikuu. Hata hivyo, Paulo hakutumia elimu hiyo ili kujielekezea uangalifu; badala ya kufanya hivyo, ilimfaidi alipowahubiri watu wa matabaka mbalimbali ya maisha. (Matendo 22:3; 1 Wakorintho 9:19-23; Wafilipi 1:7) Vivyo hivyo, Manaeni, aliyekuwa “a[m]eelimishwa pamoja na Herode mtawala wa wilaya,” alikuwa miongoni mwa wale walioongoza katika kutaniko la Antiokia.—Matendo 13:1, NW.

Sababu Gani Utumie Fedha Zako kwa Hekima?

16. (a) Kwa nini yaweza kuwa vigumu zaidi kumkumbuka Muumba wetu tukijipasha deni? (b) Kimojawapo vielezi vya Yesu chafunuaje umaana wa kufikiri kabla ya kutumia fedha?

16 Ukishindwa kutumia fedha zako kwa hekima, yaweza kuwa vigumu zaidi kumkumbuka Muumba wako kwa kufanya yampendezayo. Kwa kuwa ukijipasha deni, yaweza kusemwa kwamba una bwana-mkubwa mwingine. Biblia hueleza hivi: “Azima fedha nawe ni mtumwa wa yule akuazimaye.” (Mithali 22:7, Today’s English Version) Kimojawapo vielezi vya Yesu hukazia umaana wa kufikiri kabla ya kutumia fedha. “Ni nani katika ninyi,” Yesu akasema, “kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia? Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki.”—Luka 14:28, 29.

17. Kwa nini mara nyingi ni vigumu kwa mtu kudhibiti matumizi yake ya fedha?

17 Kwa hiyo, utajaribu kwa hekima, kuishi kupatana na kanuni ya Kimaandiko ya ‘kutowiwa na mtu chochote, isipokuwa kupendana.’ (Warumi 13:8) Lakini ni vigumu kufanya hilo, hasa unapokabiliwa na ugavi wenye kuendelea wa vifaa vipya ambavyo wanaofanya matangazo ya biashara wanadai kwamba wavihitaji kwelikweli. Mzazi mmoja, ambaye amejaribu kuwasaidia watoto wake wadhihirishe utambuzi, alionelea hivi: “Tumetumia wakati mwingi tukizungumzia kinachohitajiwa ni nini na kinachotakwa ni nini.” Kwa ujumla shule zimeshindwa kufundisha mambo hayo, zikiandaa maagizo machache sana ikiwa zaandaa yoyote juu ya kushughulikia fedha katika njia nzuri. “Twahitimu kutoka shule ya sekondari tukijua mengi juu ya pembetatu pacha kuliko jinsi ya kuhifadhi fedha,” akasema mfanyakazi mmoja wa kijamii. Basi, ni nini kiwezacho kukusaidia kutumia fedha kwa hekima?

18. Ufunguo wa kutumia fedha kwa hekima ni nini, na kwa nini?

18 Kutii himizo hili, ‘Mkumbuke Muumba wako,’ ndio ufunguo wa matumizi yenye hekima ya fedha zako. Hilo ni kwa sababu unapotii amri hiyo, jambo unalotanguliza ni kumpendeza Yehova, na shauku yako kwake huwa na uvutano juu ya jinsi unavyotumia fedha zako. Kulingana na hayo, utajaribu kutoruhusu mahitaji ya kibinafsi yahitilafiane na kumtolea Mungu ujitoaji wa nafsi yote. (Mathayo 16:24-26) Utajitahidi kudumisha jicho lako likiwa “sahili,” yaani, likiwa limekaziwa Ufalme wa Mungu na kufanya mapenzi yake. (Mathayo 6:22-24, NW) Hivyo utakuja kuona onyo la upole la kimungu la ‘kumheshimu BWANA kwa mali yako’ kuwa pendeleo lenye shangwe.—Mithali 3:9.

Vijana Wanaostahili Kuigwa

19. Katika wakati uliopita vijana wamemkumbukaje Muumba wao?

19 Kwa furaha, vijana wengi, wakati uliopita na sasa, wamemkumbuka Muumba wao. Samweli mchanga alidumu akiwa imara katika utumishi wa tabenakulo licha ya uvutano usio wa adili wa wale aliokuwa akitumika pamoja nao. (1 Samweli 2:12-26) Mke wa Potifa, aliyekuwa mshawishi wa kike mwenye kuvutia, hakuweza kumshawishi kijana Yosefu afanye uasherati. (Mwanzo 39:1-12) Ingawa alikuwa “mtoto,” Yeremia alihubiri kwa moyo mkuu akikabili upinzani mkali. (Yeremia 1:6-8) Msichana Mwisraeli mdogo alimwelekeza bila hofu mkuu wa jeshi Msiria akatafute msaada katika Israeli, ambapo angeweza kujifunza juu ya Yehova. (2 Wafalme 5:1-4) Kijana Danieli na waandamani wake walidumisha imani yao walipotahiniwa juu ya sheria za Mungu juu ya chakula. Na wale vijana Shadraka, Meshaki, na Abednego walichagua kutupwa kwenye tanuru yenye moto badala ya kuridhiana uaminifu-mshikamanifu wao kwa Mungu kwa kusujudu mbele ya sanamu.—Danieli 1:8, 17; 3:16-18; Kutoka 20:5.

20. Vijana wengi wamemkumbukaje Muumba wao leo?

20 Leo vijana zaidi ya 2,000 wenye umri kati ya miaka 19 na 25 wanatumikia katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova huko New York State, Marekani. Wao ni sehemu ndogo tu ya makumi ya maelfu ya vijana wanaomkumbuka Muumba wao ulimwenguni pote. Sawa na Yosefu wa kale, wao wamekataa kuridhiana usafi wao wa kiadili. Wengi wamemtii Mungu badala ya wanadamu walazimishwapo kuchagua yule ambaye wangemtumikia. (Matendo 5:29) Mwaka wa 1946 katika Poland, Henryka Zur mwenye umri wa miaka 15 aliteswa alipokataa kufanya tendo la ibada ya sanamu ya kidini. “Fikiri lolote utakalo ndani yako,” akadokeza mmoja wa watesi wake, “fanya tu ishara ya Katoliki ya msalaba.” Kwa sababu alikataa, alikokotwa hadi msituni na kupigwa risasi, tumaini lake la uhai wa milele likiwa halijavunjwa!b

21. Ni mwaliko gani ambao lingekuwa jambo la hekima kuukubali, na tokeo likiwa nini?

21 Lazima moyo wa Yehova uwe unachangamshwa kama nini na vijana ambao wamemkumbuka katika karne hizo! Je, wewe utaitikia mwaliko wake, ‘Mkumbuke Muumba wako’? Kwa kweli anastahili kukumbukwa nawe! Fikiria kila siku juu ya yote ambayo amekufanyia na ambayo bado atafanya, na ukubali mwaliko wake: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”—Mithali 27:11.

[Maelezo ya Chini]

a Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 1953, ukurasa 750, la Kiingereza.

b Ona Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1994 (cha Kingereza), kurasa 217-218, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Je, Wakumbuka?

◻ Vijana wanaweza kusaidiwaje wamwone Mungu kuwa mtu halisi?

◻ Yamaanisha nini kumkumbuka Muumba wako?

◻ Elimu yetu iwe na kusudi jipi?

◻ Kwa nini ni muhimu kutumia fedha zetu kwa hekima?

◻ Ni vijana gani wanaostahili kuigwa nawe?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, umefikiria ni kwa nini unaenda shuleni?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, wewe unajifunza kutumia fedha kwa hekima?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki