Mahali pa Muziki Katika Ibada ya Kisasa
KUIMBA ni zawadi itokayo kwa Mungu. Kuinua sauti zetu katika wimbo kwaweza kutuletea sisi na Muumba wetu raha. Kupitia muziki, twaweza kuonyesha hisia-moyo zetu, majonzi na pia shangwe. Hata zaidi ya hayo, twaweza kutaja upendo wetu, shauku yetu, na sifa yetu kwa Mwanzilishi wa wimbo, Yehova.
Mengi ya marejezo ya Biblia kwenye muziki yapatayo mia tatu huhusianisha ibada ya Yehova. Kuimba kunafungamanishwa pia na shangwe—si shangwe ya wale waimbao tu bali pia shangwe kwa upande wa Yehova. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wamwimbie. Kwa kuwa BWANA awaridhia watu wake.”—Zaburi 149:3, 4.
Lakini kuimba ni kwa maana jinsi gani katika ibada ya kisasa? Watu wa Yehova leo waweza kumpendezaje kwa kuinua sauti zao katika wimbo? Muziki wapaswa uwe na mahali gani katika ibada ya kweli? Kuchunguza historia ya muziki katika ibada kutasaidia kujibu maswali hayo.
Mahali pa Kihistoria pa Muziki Katika Ibada
Rejezeo la Kibiblia la kwanza kwenye muziki halitajwi hususani kuhusiana na ibada ya Yehova. Kwenye Mwanzo 4:21, Yubali ahesabiwa ule ambao huenda ukawa uvumbuzi wa ala za kwanza za kimuziki au labda mwanzo wa aina fulani ya maishilio ya muziki. Hata hivyo, muziki ulikuwa sehemu ya ibada ya Yehova hata kabla ya kuumbwa kwa wanadamu. Tafsiri kadhaa za Biblia hueleza malaika wakiimba. Ayubu 38:7 husimulia juu ya kulia kwa malaika kwa shangwe na ‘kupiga kelele.’ Hivyo, kuna sababu ya Kimaandiko kuamini kwamba kuimba katika ibada kwa Yehova kulikuwa zoea muda mrefu kabla ya mwanadamu kupata kuwako.
Wanahistoria fulani wamejadili kwamba muziki wa Kiebrania wa kale ulikuwa melodia tu, bila kuungwa mkono na ulinganifu wa sauti. Hata hivyo, sauti zaidi ya moja iliweza kupigwa kwa wakati mmoja kwenye kinubi, ala inayotajwa sana katika Biblia. Ni lazima wapiga-vinubi waliona ule ulinganifu wa sauti ulioweza kutokezwa na maunganisho ya namna za sauti kwenye ala. Badala ya kuwa wa kikale, pasipo shaka muziki wao ulikuwa wa hali ya juu sana. Na kwa kuchunguza ushairi na usemi wa kawaida wa Maandiko ya Kiebrania, twaweza kukata kauli kwamba muziki wa Kiisraeli ulikuwa wenye ubora wa juu. Bila shaka ujuzi wao ulikuwa kichocheo kwa mitungo ya kimuziki chenye ubora kuliko kile cha mataifa jirani.
Tengenezo la hekalu la kale liliandalia mipango yenye utata ya ala za muziki na sauti mbalimbali katika ibada ya hekalu. (2 Mambo ya Nyakati 29:27, 28) Kulikuwa na ‘viongozi,’ “wastadi,” ‘wanafunzi,’ na ‘wakuu wa waimbaji.’ (1 Mambo ya Nyakati 15:21; 25:7, 8; Nehemia 12:46) Akieleza juu ya stadi zao za muziki za hali ya juu, mwanahistoria Curt Sachs aliandika hivi: “Vikundi vya waimbaji na vikundi vya wapigao muziki vilivyohusianishwa na Hekalu katika Yerusalemu vyadokeza kiwango cha juu cha elimu, ya kimuziki, ustadi, na ujuzi. . . . Ingawa hatujui jinsi muziki huo wa kale ulivyosikika, tuna uthibitisho wa kutosha wa nguvu, adhama, na ubingwa wao.” (The Rise of Music in the Ancient World: East and West, 1943, kurasa 48, 101-102) Wimbo Ulio Bora ni kielelezo cha ubunifu na ubora wa mitungo ya kimuziki ya Kiebrania. Hiyo ni hadithi iliyoimbwa, sawa na maneno, au maandishi, ya drama ya waimbaji. Katika maandishi ya Kiebrania, wimbo huo unaitwa “Wimbo wa Nyimbo,” yaani, wimbo ulio bora kabisa. Kwa Waebrania wa kale, kuimba kulikuwa sehemu muhimu ya ibada. Na kuliruhusu wonyesho wa wazi wa kihisia-moyo katika kumsifu kwao Yehova.
Kuimba kwa Wakristo wa Karne ya Kwanza
Muziki uliendelea kuwa sehemu ya kawaida ya ibada miongoni mwa Wakristo wa mapema. Kwa kuongezea zile Zaburi zilizopuliziwa, yaonekana walijitungia muziki na maneno ya wimbo kwa ajili ya ibada, wakiwekea kielelezo utungaji wa nyimbo za Kikristo wa siku ya kisasa. (Waefeso 5:19) Kitabu The History of Music, cha Waldo Selden Pratt, chaeleza hivi: “Kuimba katika ibada ya hadharani na ya faraghani kulikuwa jambo la kidesturi kwa Wakristo wa mapema. Kwa wageuzwa-imani Wayahudi huko kulikuwa mwendelezo wa desturi za sinagogi . . . Kuongezea Zaburi za Kiebrania . . . , hiyo imani mpya ilielekea daima kutokeza nyimbo mpya za kidini, yaonekana hapo mwanzo zikiwa za namna ya [tenzi ziitwazo] rapsodi.”a
Kwa kukazia thamani ya kuimba, Yesu alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, yaelekea yeye na mitume wake waliimba nyimbo za Haleli. (Mathayo 26:26-30) Hizo zilikuwa nyimbo za kumsifu Yehova zilizorekodiwa katika Zaburi na kuimbwa kuhusiana na sherehe ya Sikukuu ya Kupitwa.—Zaburi 113-118.
Uvutano wa Ibada Isiyo ya Kweli
Kufikia zile ziitwazo kwa kawaida Enzi za Giza, muziki wa kidini ulishushwa hali ukawa uimbaji wenye huzuni. Mwaka wapata 200 W.K., Clement wa Aleksandria alisema hivi: “Twahitaji ala moja: neno lenye amani la kusifu, si vinubi au ngoma au ala za kupuliza au tarumbeta.” Vizuizi viliwekwa, vikiwekea muziki wa kanisa mipaka uwe wa kuimbwa. Mtindo huo ulipata kujulikana kuwa wimbo uimbwao mara nyingi au wimbo usio na muziki. “Miaka isiyozidi arobaini baada ya kusimamishwa kwa Konstantinopo, Baraza la Laodikia (A.D. 367) lilikataza ushiriki wa ala na wa makutaniko katika kawaida ya ibada. Muziki wa imani ya kidesturi umekuwa wa kuimbwa tu,” chasema kitabu Our Musical Heritage. (Italiki ni zetu.) Vizuizi hivyo havikuwa na msingi katika Ukristo wa mapema.
Katika Enzi za Giza, Biblia haikupatikana kwa watu wa kawaida. Wakristo waliothubutu kuwa na Biblia au kuisoma walinyanyaswa na hata kuuawa. Basi, si ajabu kwamba zoea la kumwimbia Mungu sifa lilitoweka kwa ujumla katika kipindi hicho cha giza. Kwa vyovyote, ikiwa watu wa kawaida hawakuweza kuyapata Maandiko, wangeweza kujuaje kwamba sehemu moja ya kumi ya Biblia nzima ni wimbo? Ni nani angewajulisha kwamba Mungu aliwaamuru waabudu wake ‘wamwimbie BWANA wimbo mpya, sifa zake katika kusanyiko la watauwa’?—Zaburi 149:1.
Kurudisha Muziki Mahali Pao Pafaapo Katika Ibada
Tengenezo la Yehova limechangia sana kurudisha muziki na kuimba mahali pazo pafaapo katika ibada. Kwa kielelezo, toleo la Februari 1, 1896, la Zion’s Watch Tower lilikuwa na nyimbo tu. Lilikuwa na kichwa “Nyimbo za Nderemo za Asubuhi za Zayoni.”
Mwaka wa 1938 kuimba kwenye mikutano ya kutaniko kuliachishwa kwa ujumla. Hata hivyo, hekima ya kufuata kielelezo na uelekeo wa kimitume ikashinda upesi. Kwenye mkusanyiko wa wilaya wa 1944, F. W. Franz alitoa hotuba “Wimbo wa Utumishi wa Ufalme.” Alionyesha kwamba nyimbo za kumsifu Yehova ziliimbwa na viumbe wa kimbingu wa Mungu muda mrefu kabla ya uumbaji wa mwanadamu, akasema hivi: “Yafaa na yampendeza Mungu kwa watumishi wake wa kidunia kuinua sauti zao katika wimbo halisi.” Baada ya kufafanua jadiliano lake juu ya kuimba katika ibada, alitangaza kutolewa kwa kitabu cha wimbo Kingdom Service Song Book cha kutumiwa kwenye mikutano ya utumishi ya kila juma.b Kisha Informant (sasa inaitwa Huduma ya Ufalme Yetu) ya Desemba 1944 ikatangaza kwamba ile mikutano mingine pia ingetia ndani nyimbo za kuanzia na za kumalizia. Kuimba kukawa tena sehemu ya ibada ya Yehova.
‘Kuimba Katika Mioyo Yetu kwa Yehova’
Thamani ya uimbaji wa kuhisiwa moyoni inatolewa kielezi na ndugu zetu katika Ulaya Mashariki na katika Afrika ambao wamepatwa na miaka kadhaa ya taabu na mnyanyaso. Lothar Wagner alikaa miaka saba katika kifungo cha kutengwa mbali. Alivumiliaje? Asema hivi: “Kwa majuma kadhaa nilikazia fikira kukamilisha kumbukumbu langu la nyimbo za Ufalme. Wakati ambapo sikuyajua maandishi barabara nilitunga tu ubeti mmoja au mbili. . . . Nyimbo zetu za Ufalme zina wingi ulioje wa mawazo yenye kutia moyo na yenye kujenga!”—Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1974, kurasa 226-228 (cha Kiingereza).
Katika miaka mitano ya kifungo cha kutengwa mbali kwa sababu ya msimamo wake mwaminifu, Harold King alipata faraja katika kutunga na kuimba nyimbo za kumsifu Yehova. Mitungo yake kadhaa hutumiwa sasa na Mashahidi wa Yehova katika ibada yao. Shangwe inayohusianishwa na kuimba ni yenye kutegemeza. Lakini hatuhitaji kupatwa na mnyanyaso ili kusadikishwa juu ya thamani ya kumwimbia Mungu sifa.
Watu wote wa Yehova waweza kupata shangwe katika wimbo. Hata ikiwa huenda tukawa na mazuio fulani katika kujieleza kwa maneno, hisia zetu kwa Yehova zaweza kuwa za wazi tunapozitaja katika wimbo. Mtume Paulo alionyesha jinsi twaweza kupata shangwe katika kuimba sifa alipowaonya Wakristo kwa upole wafulize “[ku]jisemesha nyinyi wenyewe kwa zaburi na sifa kwa Mungu na nyimbo za kiroho, mkiimba na kufuatanisha sauti zenu wenyewe na muziki katika mioyo yenu kwa Yehova.” (Waefeso 5:19) Mioyo yetu inapojaa mambo ya kiroho, twaona kuimba kuwa njia yenye nguvu ya kuonyesha hilo. Kwa hiyo ufunguo wa kuboresha kuimba ni kuwa na mtazamo wa moyoni ulio sawa.
Kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova huchangia roho yenye shangwe, ikitusukuma kusema, kuimba, na kupaaza sifa za Yehova. (Zaburi 146:2, 5) Twaimba kwa moyo wote kuhusu mambo tunayofurahia. Na ikiwa twaupenda wimbo, ni yamkini sana kwamba tutauimba tukiwa na hisia halisi.
Si lazima mtu aimbe kwa sauti kubwa ili kuimba na hisia. Kuimba kwa sauti kubwa hakumaanishi kuimba kwema; wala kuimba kwa sauti isiyosikika hakumaanishi kuimba kwema. Sauti fulani zenye mlio wa kiasili huenda zikatokeza ingawa uimbaji huenda ukawa mwororo. Sehemu ya ugumu wa kuimba katika kikundi ni kujifunza kupatana. Uwe unaimba kwa ulinganifu wa sauti au kwa umoja, kufanya kiasi cha sauti yako kifaane na cha wale walio karibu nawe, hufanyiza wimbo wenye kupendeza na wenye umoja. Sifa ya kiasi ya Kikristo na sikio lenye kusikia humsaidia mtu apate usawaziko wa kuimba kwa idili na bado kutowashinda wengine kwa sauti yake. Hata hivyo, wale waimbao kwa ustadi au walio na sauti nzuri sana hawapasi kamwe kuzuiwa wasiimbe kwa sauti kubwa. Sauti yenye kupendeza yaweza kuandalia kutaniko utegemezo wenye nguvu katika kumwimbia Yehova sifa.
Kuimba kwenye mikutano yetu huandaa pia kikao kifaacho cha kuimba sehemu za ulinganifu wa sauti za melodia mbalimbali. Wale wawezao kulinganisha sauti kwa kusikia tu au wawezao kusoma mistari ya ulinganifu wa sauti katika kitabu cha wimbo na kuiimba wanatiwa moyo waimbe kwa upatano na kuongezea uzuri wa muziki.c
Huenda wengine wakadai, ‘Siwezi kuimba wimbo vizuri’ au ‘nina sauti mbaya; hualika niimbapo sauti za juu.’ Hivyo, wao huona haya waimbapo, hata kwenye Jumba la Ufalme. Kweli ni kwamba hakuna sauti inayoinuliwa katika kumsifu Yehova iliyo “mbaya” kwa maoni yake. Sawa na vile sauti ya mtu ya kuongea iwezavyo kuboreshwa kwa mazoezi na kwa kufuata madokezo yenye kusaidia yanayotolewa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ndivyo kuimba kwa mtu kuwezavyo kuboreshwa. Watu fulani wameboresha sauti zao kwa kuvuma tu wimbo wafanyapo kazi za kila siku. Kuvuma wimbo kwasaidia kulainisha sauti. Na kwa nyakati zifaazo tunapokuwa peke yetu au tunapofanya kazi mahali ambapo tusingesumbua wengine, kuimba melodia za Ufalme ni mazoezi mazuri kwa sauti na ni njia ya kumtia mtu katika hali ya akilini yenye shangwe, na ya pumziko.
Twaweza pia kutia moyo kuimbwa kwa nyimbo chache za Ufalme kwenye vikusanyiko. Kuimba huko, kunakofuatanishwa na ala kama vile gitaa au piano au na mirekodi ya piano ya Sosaiti, huandalia vikusanyiko vyetu mazingira ya kiroho. Kuimba huandaa pia msaada wa kujifunza nyimbo na kuziimba vizuri kwenye mikutano ya kutaniko.
Ili kusaidia makutaniko yachochewe kuimba mikutanoni, Sosaiti imeandaa mifuatano ya kimuziki iliyorekodiwa. Hiyo inapochezwa, yule anayeshughulikia mfumo wa sauti apaswa kukazia uangalifu kiasi cha sauti. Sauti ya muziki isipokuwa ya juu vya kutosha, huenda kutaniko likaona haya kuimba kwa sauti. Ndugu anayedhibiti mfumo wa sauti aimbapo pamoja na kutaniko, ataweza kuona kama muziki unatoa uongozi wenye kutegemeza au la.
Mfanyie Yehova Melodia
Kuimba kunatupa sisi fursa ya kuonyesha hisia zetu kwa Muumba wetu. (Zaburi 149:1, 3) Si wonyesho wa ghafula wa kihisia-moyo tu, bali ni wonyesho uliodhibitiwa, wenye kiasi, na wenye shangwe wa sifa yetu. Kuimba kwa moyo wetu wote kutanikoni kwaweza kutuweka katika hali ifaayo ya akilini na moyoni kwa ajili ya programu inayofuata na kwaweza kutuchochea kwenye ushiriki mkubwa zaidi katika ibada ya Yehova. Ingawa kuimba kuna uvutano wa kihisia-moyo, maneno yaweza kutufundisha pia. Kwa kujieleza wenyewe hivyo kwa umoja na kwa ulinganifu wa sauti, tunatayarisha mioyo yetu kwa usikivu na kwa unyenyekevu ili tuweze kujifunza pamoja tukiwa watu waliokutanishwa.—Linganisha Zaburi 10:17.
Kuimba kutakuwa sehemu ya ibada ya Yehova sikuzote. Kwa hiyo tuna tazamio la kushiriki milele hisia hizi za mtunga-zaburi: “Nitamsifu BWANA muda ninaoishi, nitamwimbia Mungu wangu ningali ni hai.”—Zaburi 146:2.
[Maelezo ya chinis]
a Rapsodi ni muziki uliobainishwa katika sehemu mbalimbali na roho ya uhuru. Mara nyingi rapsodi zilitukuza matukio au mashujaa.
b Wakorintho wa Kwanza 14:15 laonekana kuonyesha kwamba kuimba kulikuwa sehemu ya kawaida ya ibada ya Wakristo wa karne ya kwanza.
c Baadhi ya nyimbo katika kitabu chetu cha wimbo cha sasa, Mwimbieni Yehova Sifa, zimedumisha ule ulinganifu wa sauti wenye sehemu nne kwa manufaa ya wale wanaofurahia kuimba sehemu za ulinganifu wa sauti. Hata hivyo, nyimbo nyingi zimepangwa ili kuwa na mfuatano wa piano na zilipewa mpangilio wa kimuziki unaojaribu kuhifadhi asili za kimataifa za huo muziki mbalimbali. Kutunga sauti zenye ulinganifu kwa ajili ya nyimbo zilizoandikwa bila ule ulinganifu wa sauti wenye sehemu nne kamili huenda ukaandaa uongezeo wenye kupendeza kwenye kuimba kwetu mikutanoni.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
MADOKEZO KADHAA YA KUIMBA VIZURI ZAIDI
1. Shika kitabu cha wimbo kikiwa juu uimbapo. Hilo lamsaidia mtu apumue kikawaida zaidi.
2. Pumua kwa uzito mwanzoni mwa kila fungu la maneno.
3. Kukifungua kinywa wazi zaidi kuliko kawaida mwanzoni kutaongeza kiasili kiasi cha sauti na mlio wa sauti.
4. Zaidi ya yote, kazia fikira hisia ya wimbo unaoimbwa.