Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 4/1 kur. 20-25
  • Nilijifunza Kweli ya Biblia Katika Rumania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nilijifunza Kweli ya Biblia Katika Rumania
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nyakati Zenye Matatizo
  • Kutamani Kwangu Kweli ya Biblia
  • Kweli ya Biblia Yaenea Katika Rumania
  • Hadi Marekani
  • Huduma Yetu ya Mapema Katika Marekani
  • Rekebisho Nililohitaji
  • Kuweza Hali Wakati wa Mshuko wa Kiuchumi
  • Kudumisha Imani Yetu
  • Familia Yetu Yenye Uaminifu Katika Rumania
  • Kweli Bado Ni Yenye Thamani Kwangu
  • Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi
    Amkeni!—2005
  • Furaha Isiyo na Kifani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Nilipata Utajiri wa Kweli Katika Australia
    Amkeni!—1994
  • Njaa ya Kiroho Katika Rumania
    Amkeni!—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 4/1 kur. 20-25

Nilijifunza Kweli ya Biblia Katika Rumania

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GOLDIE ROMOCEAN

Mwaka wa 1970, nilitembelea watu wa ukoo katika Rumania kwa mara ya kwanza katika miaka karibu 50. Watu waliishi chini ya utawala wa Kikomunisti wenye kuonea, nami nilionywa mara kwa mara kuwa mwangalifu juu ya yale niliyosema. Hivyo basi, niliposimama katika ofisi ya serikali katika kijiji chetu cha nyumbani, ofisa alinisihi sana niondoke nchini mara moja. Kabla ya kueleza ni kwa nini, acheni nisimulie jinsi nilivyojifunza kweli ya Biblia katika Rumania.

NILIZALIWA Machi 3, 1903, katika kijiji cha Ortelec kaskazini-magharibi mwa Rumania karibu na mji wa Zalău. Tuliishi katika mazingira yenye kupendeza. Kulikuwa na maji safi na hewa safi. Tulikuza chakula chetu wenyewe na hatukupungukiwa na chochote kimwili. Katika miaka yangu ya mapema, nchi ilikuwa yenye amani.

Watu walikuwa wa kidini sana. Kwa hakika, familia yetu ilishirikiana na dini tatu tofauti. Mmojawapo wa nyanya zangu alikuwa Mkatoliki wa Kiothodoksi, yule mwingine alikuwa Mwadventisti, na wazazi wangu walikuwa Wabaptisti. Kwa sababu sikukubaliana na yoyote ya dini zao, familia yangu ilisema kwamba ningekuwa mwatheisti. ‘Ikiwa kuna Mungu mmoja,’ niliwaza ‘lazima kuwe na dini moja tu—wala si tatu katika familia moja.’

Mambo niliyoyaona katika dini yalinisumbua. Kwa kielelezo, kasisi alizuru nyumba mbalimbali ili kukusanya haki za kanisa. Watu walipokosa fedha za kutoa, alichukua blanketi zao za sufu zilizokuwa nzuri zaidi badala ya fedha. Katika kanisa Katoliki, nilimtazama nyanya akipiga magoti kusali mbele ya picha ya Mariamu. ‘Kwa nini asali kwa picha?’ nikawaza.

Nyakati Zenye Matatizo

Baba alienda Marekani mwaka wa 1912 ili kuchuma fedha za kulipa deni. Baadaye kidogo vita ilitokea, na wanaume wa kijiji chetu waliondoka kwenda kupigana—ni wanawake, watoto, na wanaume wazee tu waliobaki. Kijiji chetu kilitawaliwa na Hungaria kwa muda fulani, lakini wakati huo askari-jeshi wa Rumania walirudi na kutwaa hicho kijiji tena. Walituamuru kuondoka mara moja. Hata hivyo, katika halahala na vurugu za kupakia mizigo na watoto katika gari la kuvutwa na ng’ombe, niliachwa nyuma. Eleweni kwamba, mimi ndiye nilikuwa mkubwa zaidi katika watoto watano.

Nilikimbilia kwa jirani, mwanamume mzee aliyebaki nyuma, naye akaniambia hivi: “Nenda nyumbani. Funga milango yako, na usiruhusu yeyote aingie ndani.” Nilitii haraka. Baada ya mlo wa mchuzi wa kuku na wali uliofungiwa ndani ya majani ya kabichi zilizopikwa, ambao ulikuwa umeachwa katika halahala za kuondoka, nilipiga magoti kando ya kitanda changu na kusali. Upesi nikalala fofofo.

Nilipofungua macho yangu kulikuwa mchana, nikasema hivi: “O, asante Mungu! Niko hai!” Kuta zilijaa matundu ya risasi, kwa kuwa risasi zilifyatuliwa usiku kucha. Mama alipong’amua kwamba sikuwa pamoja nao katika kijiji kilichofuata, alituma mwanamume kijana aliyeitwa George Romocean, aliyenipata na kuniunganisha tena na familia yangu. Upesi tuliweza kurudi katika kijiji chetu cha nyumbani na kuanza kuishi huko tena.

Kutamani Kwangu Kweli ya Biblia

Mama yangu alinitaka nibatizwe kuwa Mbaptisti, lakini sikutaka kufanya hivyo kwa sababu singeweza kuamini kwamba Mungu mwenye upendo angechoma watu milele katika helo. Huku akijaribu kunieleza, mama alisema hivi: “Ni sawa, ikiwa ni wabaya.” Lakini nilimjibu hivi: “Ikiwa wao ni wabaya, basi waharibu lakini usiwatese. Siwezi hata kutesa mbwa au paka.”

Nakumbuka kwamba katika siku moja yenye kupendeza wakati wa masika, nilipokuwa na umri wa miaka 14, mama aliniambia nipeleke ng’ombe malishoni. Nilipokuwa nikilala nyasini kando ya mto, kukiwa na msitu katika mandharinyuma, niliangalia angani na kusema hivi: “Mungu, najua kwamba wewe uko; lakini sipendi zozote za dini hizi. Lazima uwe na moja iliyo nzuri.”

Naamini kikweli kwamba Mungu alisikia sala yangu kwa sababu katika kiangazi hichohicho cha 1917, Wanafunzi wa Biblia wawili (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) walikuja kijijini kwetu. Walikuwa makolpota, au wahudumu wa wakati wote, na walikuja kwenye kanisa la Baptisti wakati ibada ilikuwa ikifanywa.

Kweli ya Biblia Yaenea Katika Rumania

Miaka michache kabla, mwaka wa 1911, Carol Szabo na Josif Kiss, waliopata kuwa Wanafunzi wa Biblia huko Marekani, walirudi Rumania kuanzisha kweli ya Biblia huko. Walikaa katika Tîrgu-Mureş, kilometa zinazopungua 160 kusini-mashariki mwa kijiji chetu. Baada ya miaka michache, kihalisi mamia ya watu waliitikia ujumbe wa Ufalme na kuanza huduma ya Kikristo.—Mathayo 24:14.

Basi, wakati hao Wanafunzi wawili wa Biblia waliokuwa vijana walipokuja kwenye kanisa la Baptisti katika kijiji chetu cha Ortelec, George Romocean, ijapokuwa alikuwa na umri wa miaka 18 tu, alikuwa akiongoza ibada na alikuwa anajaribu kueleza maana ya Waroma 12:1. Hatimaye, mmojawapo wa wale makolpota alisimama na kusema hivi: “Ndugu, marafiki, mtume Paulo anajaribu kutuambia nini hapa?”

Niliposikia hayo, nilisisimuka sana! ‘Lazima wanaume hawa wanajua jinsi ya kuifafanua Biblia,’ nikawaza. Lakini walio wengi wa wale waliokuwako walipiga kelele hivi: “Manabii wa uwongo! Tunawajua nyinyi ni nani!” Ghasia ilifuata. Lakini wakati huo babake George alisimama na kusema hivi: “Nyamazeni kimya nyinyi nyote! Hii ni roho ya aina gani—aina ile inayotokana na kulewa pombe? Ikiwa wanaume hawa wana jambo fulani la kutuambia na hamtaki kusikiliza, ninawaalika nyumbani mwangu. Yeyote ambaye ataka kuja amekaribishwa.”

Kwa kusisimuka, nilikimbia nyumbani na kumwambia mama yaliyokuwa yametendeka. Nilikuwa mmojawapo wa wale waliokubali mwaliko kwenda nyumbani kwa Romocean. Jinsi nilivyosisimuka jioni hiyo kujifunza katika Biblia kwamba hakuna helo iwakayo moto na kuona katika Biblia yangu mwenyewe ya Kirumania jina la Mungu, Yehova! Hao makolpota walipanga Mwanafunzi mmoja wa Biblia azuru nyumbani kwa Romocean kila Jumapili kutufundisha. Kiangazi kilichofuata, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa, nikiwa na umri wa miaka 15.

Hatimaye, karibu familia nzima ya Prodan na familia ya Romocean zilikubali kweli ya Biblia, zikajiweka wakfu kwa Yehova. Wengine wengi kijijini kwetu walifanya hivyo pia, kutia ndani wenzi wa ndoa ambao nyumba yao ilitumika kama kanisa la Kibaptisti hapo zamani. Baadaye waliigeuza kuwa mahali pa Wanafunzi wa Biblia kukutana ili kufanya funzo. Kweli ya Kimaandiko ilienea haraka katika vijiji vilivyokuwa karibu, na kufikia mwaka wa 1920 kulikuwa watangazaji wa Ufalme karibu 1,800 katika Rumania!

Hadi Marekani

Tulikuwa na hamu kushiriki yale tuliyokuwa tumejifunza pamoja na baba yangu, Peter Prodan. Lakini, kwa kushangaza, kabla ya kupata fursa ya kuandika, tulipokea barua kutoka kwake akituambia kwamba alikuwa amekuwa mtumishi wa Yehova aliyebatizwa. Alikuwa amejifunza na Wanafunzi wa Biblia katika Akron, Ohio, na alitaka sisi sote tujiunge naye huko Marekani. Hata hivyo, mama alikataa kuondoka Rumania. Kwa hiyo, mwaka wa 1921, nikitumia fedha alizokuwa amenitumia baba, nilijiunga naye Akron. George Romocean na ndugu yake mkubwa walikuwa tayari wamehamia Marekani mwaka uliotangulia.

Nilipowasili Ellis Island, New York kwa meli, ofisa wa idara ya wahamiaji hakujua jina la Kiingereza linalolingana na langu, Aurelia. kwa hiyo, yeye alisema hivi: “Jina lako ni Goldie.” Hilo limekuwa jina langu tangu wakati huo. Muda mfupi baada ya hapo, katika Mei 1, 1921, George Romocean nami tulioana. Mwaka mmoja hivi baadaye, baba alirudi Rumania na katika 1925 akamleta huko Akron dada yangu mchanga, Mary. Kisha baba alirudi Rumania ili awe na mama na wengine wa familia waliobaki.

Huduma Yetu ya Mapema Katika Marekani

George alikuwa mtumishi wa Yehova mwenye uaminifu-mshikamanifu na mwenye kujitoa sana. Kati ya mwaka wa 1922 na 1932, tulibarikiwa kupata binti wanne wenye kupendeza—Esther, Anne, Goldie Elizabeth, na Irene. Kutaniko la Kirumania lilianzishwa katika Akron, na mwanzoni mikutano ilifanyiwa nyumbani kwetu. Hatimaye, mwakilishi wa makao makuu ya Wanafunzi wa Biblia katika Brooklyn, New York, alizuru kutaniko letu kila baada ya miezi sita na kukaa nasi.

Jumapili nyingi tulihubiri siku nzima. Tulipakia chakula cha mchana na mifuko yetu ya vitabu, tukaweka wasichana ndani ya gari letu aina ya Model T Ford, na kutumia hiyo siku kuhubiri katika eneo la mashambani. Kisha jioni, tulihudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi. Wasichana wetu wakaja kupenda kazi ya kuhubiri. Mwaka wa 1931, nilikuwapo Columbus, Ohio, Wanafunzi wa Biblia walipokubali kirasmi kutumia jina Mashahidi wa Yehova.

Rekebisho Nililohitaji

Miaka michache baadaye, nilimkasirikia Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society wakati huo. Shahidi aliyekuwa amebatizwa karibuni alihisi kwamba Ndugu Rutherford alikuwa ameshughulika naye isivyo haki, kwa kutomsikiliza vya kutosha. Nilihisi kwamba, Ndugu Rutherford alikuwa na makosa. Hivyo, Jumapili moja dada yangu Mary na mume wake, Dan Pestrui, walitutembelea. Baada ya chakula cha jioni Dan alisema hivi: “Acheni tujitayarishe kwenda mkutanoni.”

“Hatuendi mikutano tena kamwe,” nikasema. “Tumemkasirikia Ndugu Rutherford.”

Dan alifumbata mikono yake nyuma, ndipo akasema hivi: “Je, ulimjua Ndugu Rutherford ulipobatizwa?”

“Bila shaka la,” nikajibu. “Unajua nilibatizwa Rumania.”

“Kwa nini ulibatizwa?” akaniuliza.

“Kwa sababu nilijifunza kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, na nilitaka kujiweka wakfu kumtumikia,” nikajibu.

“Usisahau kamwe jambo hilo!” akajibu. “Namna gani ikiwa Ndugu Rutherford angeacha kweli, je ungeiacha?”

“La kamwe, la kamwe!” nikasema. Hilo lilinisaidia kurudia fahamu zangu, na kusema hivi: “Kila mtu ajitayarishe kwenda mikutanoni.” Nasi hatujaacha tangu wakati huo. Nilimshukuru Yehova kama nini kwa rekebisho lenye upendo la shemeji yangu!

Kuweza Hali Wakati wa Mshuko wa Kiuchumi

Wakati wa Mshuko wa Kiuchumi katika miaka ya 1930, hali zilikuwa ngumu. Siku moja George alifika nyumbani kutoka kazini akiwa mwenye huzuni sana, akanijulisha kwamba alikuwa ameachishwa kazi yake kwa muda kwenye kiwanda cha mpira. “Usiwe na wasiwasi,” nikasema, “tuna Baba tajiri mbinguni, naye hatatuacha.”

Siku hiyohiyo George alikutana na rafiki aliyekuwa na kikapu kikubwa cha viyoga. George alipojua mahali rafiki yake alikuwa amevichuma, alikuja nyumbani na viyoga vingi. Ndipo akatumia dola zetu tatu za mwisho kununua vikapu vidogo. “Ungeweza kufanyaje hivyo,” nikauliza, “tukiwa na wasichana wadogo wanaohitaji maziwa?”

“Usiwe na wasiwasi,” akajibu, “fanya tu nisemavyo.” Kwa majuma machache yaliyofuata, tulikuwa na kiwanda kidogo nyumbani kwetu, tukisafisha na kupakia viyoga. Tuliviuza kwenye mikahawa yenye viwango vya juu na kuleta nyumbani faida ya kati ya dola 30 hadi 40 kwa siku, fedha nyingi kwetu wakati huo. Mkulima aliyetupatia ruhusa ya kuchuma hivyo viyoga kutoka kwa malisho yake alisema kwamba alikuwa ameishi hapo kwa miaka 25 na hakuwa amepata kamwe kuona viyoga vingi hivyo. Kabla ya muda mrefu kile kiwanda cha mpira kilimrudisha George kazini tena.

Kudumisha Imani Yetu

Mwaka wa 1943 tulihamia Los Angeles, California, na miaka minne baadaye tulifanya makao katika Elsinore. Tulifungua duka la vyakula hapo, na washiriki wa familia yetu nzima walifanya kazi humo kwa zamu. Wakati huo, Elsinore ulikuwa mji mdogo tu wenye watu wapatao 2,000, nasi tulilazimika kusafiri kilometa 30 kwenda mji mwingine kwa ajili ya mikutano yetu ya Kikristo. Nilikuwa mwenye furaha jinsi gani kuona kutaniko dogo likianzishwa katika Elsinore mwaka wa 1950! Sasa kuna makutaniko 13 katika eneo hilohilo.

Mwaka wa 1950 binti yetu Goldie Elizabeth (ambaye walio wengi leo humjua kuwa Beth) alifuzu kutoka Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower katika South Lansing, New York, na kupewa mgawo kwenda Venezuela akiwa mishonari. Mwaka wa 1955 binti yetu mchanga zaidi, Irene, alifurahi kwamba mume wake alialikwa kutumikia akiwa mhudumu asafiriye katika kazi ya mzunguko. Kisha mwaka wa 1961, baada ya kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme katika South Lansing, New York, walitumwa Thailand. Nyakati nyingine niliwakosa sana binti zangu hivi kwamba nililia, lakini ndipo nilipowaza, ‘Hivyo ndivyo nilivyotaka wafanye.’ Kwa hiyo niliuchukua mfuko wangu wa vitabu na kwenda katika kazi ya kuhubiri. Sikuzote nilirudi nyumbani nikiwa mwenye furaha.

Mwaka wa 1966 mume wangu mpendwa, George, alipatwa na mshtuko wa akili. Beth, aliyekuwa amerudi kutoka Venezuela kwa sababu ya matatizo ya afya, alisaidia kumtunza. George alikufa mwaka uliofuata nami nilifarijiwa na uhakika wa kwamba alikuwa amebaki mwaminifu kwa Yehova na alikuwa amepokea thawabu yake ya kimbingu. Baadaye Beth alienda Hispania kutumikia mahali ambako uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi. Binti yangu mkubwa zaidi, Esther, alipatwa na kansa na kufa mwaka wa 1977, na mwaka wa 1984, Anne alikufa kutokana na leukemia. Kila mmoja alikuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova.

Kufikia wakati wa kifo cha Anne, Beth na Irene walikuwa wamerudi kutoka katika migawo yao ya kuhubiri ya kigeni. Walikuwa wamesaidia kuwatunza dada zao, nasi sote tulihuzunika sana. Baada ya muda niliwaambia wasichana wangu hivi: “Sawa, tosha! Tumewafariji wengine kwa ahadi za Biblia zenye thamani. Sasa lazima tujiruhusu kufarijiwa. Shetani ataka kutunyang’anya shangwe yetu katika kumtumikia Yehova, lakini hatuwezi kumruhusu.”

Familia Yetu Yenye Uaminifu Katika Rumania

Dada yangu Mary nami tulifanya hiyo safari yenye kustahili kukumbukwa kutembelea familia yetu katika Rumania mwaka wa 1970. Mmojawapo wa dada zetu alikuwa amekufa, lakini tuliweza kutembelea ndugu yetu John na dada yetu Lodovica, waliokuwa bado wanaishi katika kijiji cha Ortelec. Kufikia wakati wa ziara yetu, baba na mama walikuwa wamekufa, wakiwa wamebaki waaminifu kwa Yehova. Wengi walituambia kwamba baba alikuwa nguzo kutanikoni. Hata baadhi ya vitukuu wake katika Rumania ni Mashahidi sasa. Tulitembelea watu wa ukoo wengi upande wa familia ya mume wangu waliokuwa wamebaki bila kuondoleka katika kweli ya Biblia.

Mwaka wa 1970, Rumania ilikuwa chini ya utawala mkatili wa Kikomunisti wa Nicolae Ceauşescu, na Mashahidi wa Yehova walikuwa wananyanyaswa vibaya sana. Flore, mwana wa kiume wa ndugu yangu John, na wengine wa watu wa ukoo wangu vilevile, walitumia miaka mingi katika kambi za mateso kwa sababu ya imani yao ya Kikristo, na ndivyo binamu wa kwanza wa mume wangu, Gábor Romocean. Si ajabu kwamba wakati tulikabidhiwa kupeleka barua kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova New York, ndugu zetu wa Rumania walisema wangekuwa na wasiwasi hadi wapate kusikia kwamba tulitoka nchini kwa usalama!

Tulipong’amua kwamba wakati wa kutumika wa visa zetu ulikuwa umekwisha, tulienda kwenye ofisi ya serikali katika Ortelec. Ilikuwa Ijumaa alasiri, na hapo kulikuwa na ofisa mmoja tu kazini. Akijua tuliyekuwa tukitembelea na kwamba mpwa wetu wa kiume alikuwa amekuwa katika kambi ya mateso, alisema hivi: “Wanawake, ondokeni hapa!”

“Lakini hakuna gari la moshi linaloondoka leo,” dada yangu akajibu.

“Haidhuru,” akasema kwa hima. “Chukueni basi. Chukueni gari la moshi. Chukueni teksi. Tembeeni kwa miguu. Ondokeni hapa tu haraka mwezavyo!”

Tulipoanza kuondoka, tuliitwa tena na kuarifiwa kwamba gari la moshi la kijeshi ambalo halikuwa limeratibiwa lilikuwa linakuja saa 12:00 jioni. Jinsi jambo hilo lilivyothibitika kuwa uongozi wa Mungu! Katika gari la moshi la kawaida, hati zetu zingechunguzwa tena na tena, lakini kwa kuwa gari hilo la moshi lilikuwa likisafirisha wafanyakazi wa jeshi na ni sisi wawili tu tuliokuwa raia ndani yalo, hakuna yeyote aliyeomba kuona pasipoti zetu. Labda walidhani kwamba tulikuwa nyanya za baadhi ya hao maofisa.

Tuliwasili Timisoara asubuhi iliyofuata, na kwa msaada wa rafiki ya mtu wa ukoo, tuliweza kupata visa. Siku iliyofuata tulikuwa tumeondoka nchini. Tulirudi nyumbani na kumbukumbu nyingi tuzipendazo na zisizosahaulika juu ya ndugu na dada zetu Wakristo wenye uaminifu-mshikamanifu katika Rumania.

Miaka kadhaa baada ya ziara yetu ya Rumania, tulisikia habari za hapa na pale juu ya utendaji wa kuhubiri kutoka nyuma ya Pazia la Chuma. Hata hivyo, tulitumaini kwamba ndugu na dada zetu Wakristo wangebaki wakiwa waaminifu-washikamanifu kwa Mungu wetu—hata hali ziweje. Na kwa kweli wamefanya hivyo! Ilikuwa ni furaha iliyoje kujua kwamba Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria kuwa tengenezo la kidini katika Rumania katika Aprili 1990! Kiangazi kilichofuata tulipendezwa na ripoti juu ya mikusanyiko iliyofanywa Rumania. Kwani, watu zaidi ya 34,000 walihudhuria katika majiji manane, na 2,260 walibatizwa! Sasa kuna watu zaidi ya 35,000 wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri katika Rumania, na mwaka uliopita 86,034 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Kweli Bado Ni Yenye Thamani Kwangu

Kwa miaka michache, niliacha kushiriki mifano kwenye Ukumbusho. Niliona ndugu wenye kustahili sana ambao hawakushiriki, nikasababu hivi: “Kwa nini Yehova angenipa mimi pendeleo la kuwa mtawala mwenzi pamoja na Mwana wake mbinguni wakati wengine ni wasemaji wenye ufasaha hivyo?” Lakini nilipokosa kushiriki, nilihisi nimevurugika sana. Ni kana kwamba nilikuwa ninakataa kitu fulani. Baada ya kujifunza sana na dua katika sala, nilianza kushiriki tena. Amani na shangwe ilinirudia tena, na hazijapata kuniacha kamwe.

Ijapokuwa siwezi tena kuwa na uwezo wa kuona vya kutosha ili kusoma, mimi husikiliza kila siku kaseti za Biblia na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Bado mimi hushiriki pia katika kazi ya kuhubiri. Kwa kawaida mimi huangusha magazeti kati ya 60 na 100 kila mwezi, lakini tulipokuwa na kampeni ya pekee ya kuangusha gazeti la Amkeni! mwezi wa Aprili uliopita, niliangusha magazeti 323. Kwa msaada kutoka kwa binti zangu, naweza kushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Nina furaha kwamba naweza kuendelea kutia moyo wengine. Karibu kila mtu kwenye Jumba la Ufalme huniita nyanya.

Nifikiriapo ile miaka ipatayo zaidi ya 79 ya kumtumikia Yehova, namshukuru kila siku kwamba aliniruhusu kujua kweli yake yenye thamani na kutumia maisha yangu katika utumishi wake. Ninashukuru sana kwamba nimeishi kuona utimizo wa unabii mzuri ajabu wa Biblia uliotabiri kukusanywa kwa watu wa Mungu wenye mfano wa kondoo katika siku hizi za mwisho.—Isaya 60:22; Zekaria 8:23.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Dada yangu Mary na baba wakiwa wamesimama, na mimi, George, na binti zetu Esther na Anne

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na binti zangu Beth na Irene, na mume wa Irene na wavulana wao wawili, wote wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki