Mashahidi wa Yehova Watafanya Mikusanyiko ya Kimataifa
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linapanga kufanya mikusanyiko ya kimataifa katika 1998. Tangazo hilo lilipokewa kwa itikio lenye idili kwenye mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, uliofanywa katika Jumba la Kusanyiko la Jiji la Jersey siku ya Jumamosi, Oktoba 5, 1996.
Pamoja na mikusanyiko ya wilaya ya kawaida, mikusanyiko ya kimataifa kadhaa itafanywa Amerika Kaskazini katikati ya mwaka wa 1998. Yatarajiwa kwamba mikusanyiko hiyo itaunganisha mamia ya maelfu ya Mashahidi kutoka sehemu nyingi za dunia. Ili kuwezesha nchi nyingi iwezekanavyo kuwakilishwa, kila moja ya zile ofisi za tawi zaidi ya 100 za Watch Tower Society itakuwa na wajumbe kadhaa kwa ajili ya jiji hususa la mkusanyiko wa kimataifa katika Amerika Kaskazini.
Kwa wazi, si wote ambao wangependa kusafiri hadi Amerika Kaskazini watakaoweza kufanya hivyo. Hata hivyo, huenda ikawezekana kwa maelfu ya watu kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa karibu zaidi na kwao. Mipango inafanywa kwa ajili ya mikusanyiko ya kimataifa kufanywa katika nchi mbili au tatu za Ulaya na mingine katika Afrika, Asia, Amerika ya Latini, Pasifiki Kusini, na Karibea.
Kwenye wakati ufaao, ofisi za tawi za Sosaiti zitajulisha makutaniko katika maeneo yazo juu ya jiji au majiji ya mkusanyiko ambako yamealikwa. Habari juu ya tarehe mbalimbali za mkusanyiko na mipango ya kuwachagua wajumbe itatolewa. Wale wafikiriao kujaza fomu za maombi kwa ajili ya uteuzi wa wajumbe huenda wakataka kuanza kuhifadhi kiasi fulani cha fedha zao wakitarajia matukio hayo ya pekee.
Mashahidi wa Yehova wote ulimwenguni pote wanaweza kutazamia kilicho akibani kwenye mikusanyiko hiyo ya kimataifa ya mwaka wa 1998. Mikusanyiko ya wilaya katika nchi zote itakuwa na programu ileile.