Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 9/15 kur. 21-24
  • Jinsi ya Kudumisha Shangwe Katika Utumishi wa Wakati Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kudumisha Shangwe Katika Utumishi wa Wakati Wote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukabiliana na Kutamaushwa
  • Kupatana na Wengine
  • Katika Afya Mbaya
  • Kudumisha Shangwe Kujapokuwa Ubaridi wa Watu
  • Kitia-Moyo Kutoka kwa Wengine
  • Shangwe ya Yehova—Ngome Yetu
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kuthamini Sana Mapendeleo ya Utumishi Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 9/15 kur. 21-24

Jinsi ya Kudumisha Shangwe Katika Utumishi wa Wakati Wote

UTIMIZO wa unabii wa Biblia waonyesha wazi kwamba twaishi katika siku za mwisho za huu mfumo usiomcha Mungu. Wakijua hilo, watumishi wa Yehova Mungu hutumia wakati mwingi wawezavyo kulingana na uwezo wao wakieneza habari njema za Ufalme wake. Zaidi ya Mashahidi wa Yehova 600,000 wamepanga maisha yao ili kushiriki utumishi wa wakati wote. Baadhi yao ni wapiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote wanaoitwa mapainia. Wengine ni wajitoleaji wa Betheli kwenye makao makuu ya Watch Tower Society au ofisi zake za tawi. Hata wengine ni wamishonari na waangalizi wasafirio.

Biblia huonyesha kwamba siku za mwisho, kungekuwako “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Maandishi ya Biblia ya Kigiriki hutumia usemi ambao waweza kutafsiriwa kuwa “nyakati zilizowekwa zilizo kali.” Kwa sababu hiyo, haimpasi mtu yeyote kutazamia maisha yasiyo na taabu katika siku yetu. Kwa baadhi ya wahudumu Wakristo, matatizo huonekana kuwa makubwa sana hivi kwamba wanaweza kujiuliza, ‘Naweza kuendelea na utumishi wa wakati wote, au lazima niache?’

Ni hali zipi zinazoweza kumsababisha mtu akadirie tena hali yake akiwa painia, mjitoleaji wa Betheli, mwangalizi asafiriye, au mishonari? Labda kuna tatizo kubwa la kiafya. Labda mtu wa jamaa aliye mzee-mzee au mgonjwa ahitaji utunzi wa daima. Huenda ikawa wenzi waliooana wanaanza familia. Yeyote anayeacha utumishi wa wakati wote kwa sababu hizo na kwa sababu ya madaraka ya Kimaandiko hahitaji kuona aibu kwa sababu ya marekebisho aliyofanya.

Hata hivyo, vipi ikiwa mtu anapanga kuacha utumishi wa wakati wote kwa sababu ya kukosa shangwe? Labda painia aona itikio kidogo katika huduma yake na kuuliza, ‘Kwa nini niendelee na mtindo-maisha wangu wa kujidhabihu ilhali watu wachache sana wanasikiliza?’ Labda mjitoleaji wa Betheli hafurahii sana mgawo wake. Au yawezekana kwamba afya mbaya yenye kusumbua, ijapokuwa haifanyi utumishi wa painia usiwezekane, mwishowe yamomonyoa furaha ya mtu. Watu hao wanaweza kudumishaje shangwe yao? Na tufikirie vile baadhi ya wahudumu wazoefu wanavyosema.

Kukabiliana na Kutamaushwa

Anny, anayetoka Uswisi, alihudhuria Watchtower Bible School of Gilead mwaka wa 1950. Alitazamia kupata mgawo wa mishonari nchi ya ng’ambo. Alipopewa tena mgawo wa kufanya kazi Betheli huko Ulaya, Anny alitamaushwa. Hata hivyo, alikubali mgawo wake katika Idara ya Tafsiri naye bado anafanya kazi hiyo. Alishindaje kutamaushwa kwake? “Kulikuwa na bado kuna kazi nyingi ya kufanywa. Hisia zangu na mapendeleo yangu si ya maana kama hiyo kazi,” aeleza Anny.

Tukitamauka kwa sababu ya mgawo wetu, labda twaweza kusitawisha mtazamo wa Anny. Mapendeleo yetu ya kibinafsi si ya umaana mkubwa. Linalostahili kuangaliwa sana ni kwamba namna zote za madaraka zinazohusiana na kuendeleza ujumbe wa Ufalme zishughulikiwe. Mithali 14:23 hutuambia kwamba “katika kila kazi mna faida.” Bila kujali tumepewa mgawo upi, kuufanya kwa uaminifu huchangia kutimizwa kwa kazi ya Ufalme. Na kunaweza kuwa na uradhi mkubwa—naam, shangwe—katika kazi hiyo ya kupewa na Mungu.—Linganisha 1 Wakorintho 12:18, 27, 28.

Kupatana na Wengine

Utumishi wa wakati wote hutia ndani kukutana na watu wa aina zote—katika huduma ya shambani, kwenye Betheli, katika makao ya mishonari, au mwangalizi asafiriye anapotembelea kutaniko baada ya kutaniko. Kwa sababu hiyo, shangwe hutegemea sana kupatana vizuri na wengine. Hata hivyo, ‘nyakati zilizo kali’ zilizotabiriwa kwa siku hizi za mwisho huweka mkazo mkubwa katika mahusiano ya kibinadamu. Mhudumu anaweza kuepukaje kupoteza shangwe yake, hata mtu akimkasirisha? Labda twaweza kujifunza jambo fulani kutoka kwa Wilhelm.

Wilhelm alikuwa mshiriki wa familia ya Betheli huko Ulaya mwaka wa 1947. Baadaye, alitumia wakati katika kazi ya painia na katika utumishi akiwa mwangalizi asafiriye. “Mke wangu nami tuonapo mambo tunayoona si sawa au yanayotusumbua kibinafsi, sisi humwambia Yehova jinsi tunavyohisi kisha twamwachia mambo ayatatue,” aeleza Wilhelm.—Zaburi 37:5.

Labda wewe mwenyewe umekuwa ukisumbuliwa na tabia ya Mkristo mwenzako aliyekuzungumzia bila staha au bila kufikiri. Kumbuka kwamba sisi sote hujikwaa mara nyingi katika usemi wetu. (Yakobo 3:2) Kwa hiyo kwa nini usitumie hali hiyo ikuvute karibu zaidi na “Msikiaji wa sala”? (Zaburi 65:2, NW) Sema na Yehova kuhusu hilo jambo, kisha uliache mikononi mwake. Mungu akitaka kufanya mabadiliko, atafanya hivyo. Wale wanaoishi katika makao ya mishonari huenda wakahitaji kukumbuka hilo mkazo ukitokea kuhusiana na mambo hayo, kwa kuwa hilo litawasaidia wadumishe shangwe yao katika utumishi wa Yehova.

Katika Afya Mbaya

Watu wachache hufurahia afya nzuri isiyo na ugeugeu. Hata wale wanaoonwa kuwa na kipindi bora zaidi maishani wanaweza kupatwa na mshuko-moyo au maradhi. Afya mbaya hulazimisha wengine kuacha utumishi wa wakati wote, lakini baadaye wao hufanya kazi bora kabisa wakiwa wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, wengine, wanaweza kuendelea na utumishi wa wakati wote ijapokuwa afya mbaya. Kwa mfano, fikiria Hartmut na Gislind.

Hartmut na Gislind ni wenzi waliooana ambao wametumia miaka 30 wakiwa mapainia, wamishonari, na katika kazi ya kusafiri. Wote wawili wamepatwa na magonjwa mabaya sana ambayo nyakati nyingine yamewaacha wakiwa wamechoka kimwili na kihisia-moyo. Hata hivyo, wamefanya kazi bora kabisa na wameweza kuwatia moyo wengine ambao wanapatwa na majaribu kama hayo. Wanatoa ushauri gani? “Tazama wakati ujao na si uliopita. Tumia vizuri kabisa kila hali. Huenda kila siku ikaleta fursa moja tu ya kumsifu Yehova. Tumia fursa hiyo, na uifurahie.”

Fikiria kisa cha Hannelore. Ametaabishwa na ugonjwa wenye kurudia-rudia katika miaka yake 30 akiwa painia, mishonari, katika kazi ya kusafiri akiwa na mume wake, na katika utumishi wa Betheli. Hannelore asema hivi: “Nakazia fikira suala lililozushwa na Shetani—kwamba wanadamu wanamtumikia Yehova iwapo tu kufanya hivyo ni rahisi kwao. Kwa kuvumilia majaribu, naweza kuwa na sehemu katika kumthibitisha Shetani kuwa mwongo.” Hilo laweza kuwa kichocheo kikubwa sana. Kumbuka kwamba uaminifu-mshikamanifu wako binafsi kwa Yehova unapojaribiwa hilo ni jambo la maana kwake.—Ayubu 1:8-12; Mithali 27:11.

Unapojaribu kufanya uamuzi wenye usawaziko kuhusu afya yako, fikiria kwa uangalifu mambo mawili ya unabii wa Yesu Kristo kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo. Yesu alitabiri magonjwa ya kuambukiza mahali pamoja baada ya pengine. Pia alisema hivi: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:3, 14; Luka 21:11) Yesu alijua kwamba siku za mwisho, wafuasi wake wangeshindana na ugonjwa. Lakini anang’amua kwamba kazi ya kuhubiri ingefanywa si na watu wanaofurahia afya nzuri tu bali pia na watu wanaopatwa na magonjwa mabaya. Tukiweza kuendelea na utumishi wa wakati wote ijapokuwa afya isiyo nzuri, Yehova hatasahau upendo tunaoonyesha kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10.

Kudumisha Shangwe Kujapokuwa Ubaridi wa Watu

Mtazamo wetu waweza kuathiriwa na jinsi watu wanavyoitikia kazi ya kuhubiri Ufalme. “Hata mapainia huona likiwa jambo gumu kuanzisha mazungumzo na mwenye nyumba,” akasema mhudumu mmoja mzoefu. “Sisi sote lazima tujitahidi kudumisha shangwe yetu.” Ndiyo, ubaridi wa watu waweza kupunguza shangwe yetu katika utumishi wa shambani. Kwa hiyo painia ambaye hupata ubaridi kwa ukawaida anaweza kudumishaje shangwe yake? Wahudumu wazoefu wanatoa madokezo yafuatayo ambayo yamejaribiwa na kutahiniwa.

Ubaridi huleta ugumu, lakini hauhitaji kumaanisha ushinde. Wenyewe, ubaridi ulioenea si sababu ya kuacha utumishi wa wakati wote. Twaweza kudumisha shangwe yetu tukabilipo ubaridi ikiwa twaweka kando wakati wa kutosha wa funzo la Maandiko la bidii yenye kuendelea. Hayo ‘hutuandalia vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema,’ nazo hutia ndani kusema na wale wasiosikiliza habari njema. (2 Timotheo 3:16, 17) Ijapokuwa watu hawakutaka kumsikiliza Nabii Yeremia, hilo halikumzuia. (Yeremia 7:27) Tunapojifunza Biblia kwa msaada wa vichapo vya Kikristo, twaweza kunufaika zaidi tukiangalia mawazo yanayoimarisha imani yetu na kutusaidia tukabiliane na ubaridi.

Tukikubali kwamba ubaridi ni ugumu, acheni tuchunguze mtazamo wetu kuelekea wale tunaowahubiri. Kwa nini wana ubaridi? Mathalani, sababu moja ya ubaridi ulioenea sehemu za Ulaya, ni rekodi mbaya ya dini isiyo ya kweli. Watu hawahisi tena kamwe kwamba dini ina mahali maishani pao, wala hawaitaki kamwe. Twahitaji kuwa wenye kunyumbulika, tukiongea na watu kuhusu mambo yanayowaathiri, kama vile ukosefu wa kazi ya kuajiriwa, afya, uhalifu, kutovumilia, mazingira, na tisho la vita.

Katika maneno yetu ya ufunguzi kwa mwenye nyumba, huenda tukataja jambo la kupendeza watu wa kwetu. Ndivyo alivyojaribu kufanya Dietmar alipokuwa akihubiri katika kijiji ambacho alikuwa na mafanikio kidogo. Mkazi mmoja alitaja kwamba kijiji hicho kilikuwa kimepatwa na jambo la huzuni kubwa siku moja kabla ya hapo. Baada ya hapo, katika kila mlango, Dietmar alionyesha sikitiko la moyo mweupe kuhusu jambo hilo la huzuni kubwa. “Kwa ghafula, watu wakaanza kuongea,” akasema. “Hilo jambo la huzuni kubwa lilikuwa katika akili ya kila mmoja. Nilikuwa na mazungumzo mazuri sana siku hiyo kwa sababu nilionyesha kupendezwa na maisha yao.”

Twahitaji kuwatolea watu ushahidi wa Ufalme popote tunapowapata. Ushahidi wa vivi hivi waweza kuwa na matokeo, nasi twaweza kujizoeza wenyewe katika utendaji huu kwa kutumia madokezo yanayotolewa katika vichapo vyenye kutegemea Biblia nyumbani. Shangwe yaweza kutokana na maneno machache ya kirafiki au kutokana na kumwangushia mwenye nyumba nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ikiwa tumefanya ziara za kurudia na kuanza kuongoza funzo la Biblia na mtu anayependezwa, twaweza kupata kurejezewa mtu mwingine kwa kuuliza: “Wajua mtu yeyote ambaye angependa kujifunza Biblia?” Hilo laweza kuongoza kwenye kuanzisha funzo jingine la Biblia. Kwa vyovyote vile, na tuwe wenye mtazamo mzuri, tukimtegemea Yehova kwa kusali, bila kuruhusu ubaridi utuvunje moyo.

Kitia-Moyo Kutoka kwa Wengine

Jürgen na Christiane wamekuwa wakipainia na kushiriki katika kazi ya kusafiri kwa miaka zaidi ya 30. Wakati mmoja walikuwa na mgawo uliohusisha kuhubiri katika eneo ambalo watu walio wengi walikuwa na ubaridi na wenye vichwa vigumu. Jinsi Jürgen na mke wake walivyotamani kitia-moyo! Ingawa hivyo, kwa sababu fulani, wengine katika kutaniko hawakuitikia uhitaji wao.

Kwa hiyo Jürgen anajua kwa kujionea mwenyewe kwamba “baadhi ya mapainia wana wakati mgumu. Wanahitaji kitia-moyo kingi kutoka kwa wazee na wahubiri wengine.” Mungu alimwambia Musa amtie moyo na kumwimarisha Yoshua. (Kumbukumbu la Torati 3:26-28) Na Wakristo wanapaswa kuwa vyanzo vya kitia-moyo wao kwa wao. (Waroma 1:11, 12) Wahubiri wa Ufalme wanaweza kutia moyo wale walio katika utumishi wa wakati wote kwa maneno yenye kujenga na kwa kujiunga nao katika huduma mara kwa mara.

Shangwe ya Yehova—Ngome Yetu

Wakristo ambao wametumia maisha yao karibu yote wakiwa mapainia au wamishonari, wakitumikia Betheli, au wakizuru makutaniko katika kazi ya kusafiri wamegundua kwamba matatizo yaliyo mengi si ya muda mfupi, lakini mengine ni yenye kudumu. Hata matatizo machache ambayo hayaonekani kuisha hayapaswi kutunyang’anya shangwe yetu. Ramon, ambaye ametumikia katika mgawo wa kigeni kwa miaka zaidi ya 45, adokeza kwamba wakati wowote matatizo yatuhuzunishapo, “twapaswa kufikiria baraka nyingi tulizo nazo na kuhusu maelfu ya wengine ambao wanapatwa na magumu makubwa zaidi.” Kwa kweli, waabudu wenzetu ulimwenguni pote wanapatwa na mateso, na Yehova anatujali sisi sote kwelikweli.—1 Petro 5:6-9.

Kwa hiyo basi, hali zetu za kibinafsi zituruhusupo kushiriki katika utumishi wa wakati wote na kubaki katika huo, na tudumishe shangwe yetu kwa kumtegemea Baba yetu wa kimbingu. Yeye hutia nguvu watumishi wake, na sisi sote twapaswa kukumbuka kwamba ‘shangwe ya Yehova ni ngome yetu.’—Nehemia 8:10, NW.

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Hisia zangu na mapendeleo yangu si ya maana kama hiyo kazi”

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Sisi humwambia Yehova jinsi tunavyohisi kisha twamwachia mambo”

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Tumia vizuri kabisa kila hali. Huenda kila siku ikaleta fursa moja tu ya kumsifu Yehova”

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Kwa kuvumilia majaribu, naweza kuwa na sehemu katika kumthibitisha Shetani kuwa mwongo”

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Baadhi ya mapainia wana wakati mgumu. Wanahitaji kitia-moyo kingi kutoka kwa wazee na wahubiri wengine”

[Picha katika ukurasa wa 24]

‘Twapaswa kufikiria baraka nyingi tulizo nazo’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki