Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 9/15 kur. 25-29
  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Pili

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Pili
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtangulizi Atokea
  • Kanisa Lalipiza Kisasi
  • Matokeo ya Uchapaji
  • William Tyndale na Biblia ya Kiingereza
  • Utafiti Waleta Uelewevu wa Wazi Zaidi
  • Tyndale Atafsiri Maandiko ya Kiebrania
  • Biblia Pamoja na Tyndale Chini ya Marufuku
  • William Tyndale—Mwanamume Mwenye Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Biblia ya William Tyndale Kwa Ajili ya Watu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Kutafsiri Biblia Kulikuwa Hatari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Walilipenda Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 9/15 kur. 25-29

Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Pili

Miali ya moto ilipaa juu fueli zaidi na zaidi iliporundikwa kwenye moto mkubwa sana. Lakini huo haukuwa moto wa kawaida. Huo moto mkubwa ulikuwa ukiongezwa Biblia huku makasisi na maaskofu wakitazama. Lakini kwa kununua Biblia ili kuziharibu, askofu wa London bila kujua alimsaidia mtafsiri, William Tyndale, kugharimia chapa zaidi!

Ni nini kilichoongoza kwenye azimio hilo la pande zote mbili za hilo pambano? Katika toleo fulani la mapema, tulifikiria kwa uangalifu historia ya kuchapishwa kwa Biblia hadi mwishoni mwa Enzi za Kati. Sasa twaja kwenye mapambazuko ya enzi mpya wakati ambapo ujumbe na mamlaka ya Neno la Mungu ilikuwa ikikaribia kuwa na matokeo makubwa katika jamii.

Mtangulizi Atokea

John Wycliffe, msomi mstahiki wa Oxford, alihubiri na kuandika kwa njia yenye nguvu dhidi ya mazoea yasiyo ya kimaandiko ya Kanisa Katoliki, akitegemeza mamlaka yake juu ya ‘sheria ya Mungu,’ yaani Biblia. Aliwatuma wanafunzi wake, Waloladi, waende kotekote mashambani Uingereza ili kuhubiria yeyote ambaye angesikiliza, ujumbe wa Biblia katika Kiingereza. Kabla hajafa mwaka wa 1384, alianzisha kutafsiriwa kwa Biblia katika Kiingereza cha siku yake kutoka Kilatini.

Kanisa lilipata sababu nyingi za kumdharau Wycliffe. Kwanza, alilaumu makasisi kwa sababu ya mazidio yao na mwenendo wao usio wa adili. Kwa kuongezea, wengi wa watu waliovutiwa na Wycliffe walitumia vibaya mafundisho yake ili kutetea maasi ya kutumia silaha. Makasisi walimlaumu Wycliffe, hata baada ya kifo chake, ingawa hakuunga mkono kamwe maasi hayo yenye jeuri.

Katika barua aliyomwandikia Papa John wa 23 mwaka wa 1412, Askofu Mkuu Arundel alirejezea “yule jamaa mwenye kustahili kudharauliwa na msumbufu, John Wycliffe, akumbukwaye kuwa mtu mwenye kuchukiza sana, mwana wa yule nyoka wa kale, aliyefananisha kimbele na aliye mwana wa mpinga-Kristo.” Akifikia upeo wa shutumu lake la hadharani, Arundel aliandika hivi: “Ili kujaza kabisa kipimo cha uovu wake, alibuni tafsiri mpya ya maandiko katika lugha ya kienyeji ya kufaa lengo fulani.” Kwa kweli, lililowakasirisha zaidi viongozi wa kanisa lilikuwa kwamba Wycliffe alitaka kuwapa watu Biblia katika lugha yao wenyewe.

Hata hivyo, watu mmoja-mmoja walio mashuhuri walipata Maandiko katika lugha za kienyeji. Mmoja alikuwa Anne wa Bohemia, aliyeolewa na Mfalme Richard wa Pili wa Uingereza mwaka wa 1382. Alikuwa na tafsiri za Kiingereza za Wycliffe za Gospeli, ambazo alijifunza daima. Alipopata kuwa malkia, mtazamo wake wenye upendeleo ulimsaidia kuendeleza kusudi la Biblia—wala si katika Uingereza pekee. Anne aliwatia moyo wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Prague kilicho Bohemia waje Oxford. Huko walijifunza kwa idili vichapo vya Wycliffe na kurudi na baadhi yavyo Prague. Baadaye, kupendwa kwa mafundisho ya Wycliffe kwenye Chuo Kikuu cha Prague kulimtegemeza Jan Hus, aliyejifunza na baadaye kufundisha huko. Hus alifanya tafsiri ya Kicheki yenye kusomeka kutokana na tafsiri ya Kislavoni cha kale. Jitihada zake ziliendeleza matumizi ya kawaida ya Biblia katika Bohemia na nchi jirani.

Kanisa Lalipiza Kisasi

Makasisi walighadhibikia Wycliffe na Hus pia kwa sababu ya kufundisha kwamba yale “maandishi yasiyotoholewa,” Maandiko ya awali yaliyopuliziwa yasiyoongezwa chochote, yalikuwa na mamlaka kubwa zaidi kuliko “fasiri,” yale maelezo marefu ya kidesturi pambizoni mwa Biblia zilizokubaliwa na kanisa. Wahubiri hao walitaka kufanya huo ujumbe usiotoholewa wa Neno la Mungu upatikane kwa mtu wa kawaida.

Hus alikengwa aje mbele ya Baraza la Katoliki la Constance, Ujerumani, mwaka wa 1414 ili kutetea maoni yake, akiahidiwa isivyo kweli kwamba angekuwa salama. Baraza hilo lilifanyizwa na makasisi, maaskofu, na makadinali 2,933. Hus alikubali kukana mafundisho yake ikiwa Maandiko yangeweza kuyathibitisha kuwa yenye makosa. Kwa hilo baraza, suala halikuwa hilo. Kusai kwake mamlaka yao kulikuwa sababu ya kutosha kuwafanya wamchome kwenye mti akiwa hai mwaka wa 1415, alipokuwa akisali kwa sauti kubwa.

Washiriki wa Baraza lilelile pia walifanya tendo la mwisho la kuonyesha lawama yao na tusi lao kwa John Wycliffe kwa kuagiza kwamba mifupa yake ifukuliwe huko Uingereza na kuchomwa. Mwelekezo huo ulikuwa wenye kuchukiza sana hivi kwamba haukutekelezwa hadi mwaka wa 1428, papa alipoamuru ifanywe hivyo. Ingawa hivyo, kama ilivyo sikuzote, upinzani huo mkali haukupunguza bidii ya wapenda kweli wengine. Badala ya hivyo, uliongeza azimio lao la kuhubiri Neno la Mungu.

Matokeo ya Uchapaji

Kufikia mwaka wa 1450, miaka 35 tu baada ya kifo cha Hus, Johannes Gutenberg alianza kuchapa kwa kutumia mashine huko Ujerumani. Kichapo chake kikubwa cha kwanza kilikuwa chapa ya Vulgate ya Kilatini, iliyokamilika wapata mwaka wa 1455. Kufikia mwaka wa 1495 Biblia yote au sehemu yake ilikuwa imechapwa katika Kijerumani, Kiitalia, Kifaransa, Kicheki, Kiholanzi, Kiebrania, Kikatalani, Kigiriki, Kihispania, Kislavoni, Kireno, na Kiserbia—kwa mpangilio huo.

Msomi Mholanzi Desiderius Erasmus alitokeza chapa ya kwanza iliyokamilika ya maandishi ya Kigiriki mwaka wa 1516. Erasmus alitaka kwamba Maandiko “yatafsiriwe katika lugha za watu wote.” Hata hivyo, alisita kuhatarisha kupendwa kwake sana na watu kwa kuitafsiri yeye mwenyewe. Hata hivyo, wengine ambao wangekuwa na ujasiri zaidi wakafuata. Mwenye kutokeza miongoni mwa watu hao mmoja-mmoja alikuwa William Tyndale.

William Tyndale na Biblia ya Kiingereza

Tyndale alielimishwa Oxford na wapata mwaka wa 1521 akaja nyumbani kwa Sir John Walsh awe mfunzi wa watoto wake. Mara nyingi nyakati za mlo kwenye meza ya Walsh yenye vyakula tele Tyndale kijana alikuwa akijadiliana na makasisi wa mahali hapo. Tyndale alipinga kauli zao waziwazi kwa kufungua Biblia na kuwaonyesha maandiko. Punde si punde, akina Walsh wakasadikishwa na yale ambayo Tyndale alikuwa akisema, nao makasisi walialikwa mara chache zaidi na kupokewa bila idili nyingi. Bila shaka, hilo liliwafanya makasisi wamkasirikie zaidi Tyndale na itikadi zake.

Pindi moja wakati wa bishano, mmojawapo wa wapinzani wa kidini wa Tyndale alisisitiza hivi: “Afadhali kuwa bila sheria za Mungu kuliko kukosa sheria za Papa.” Wazia usadikisho wa Tyndale alipojibu hivi: “Namsai Papa na sheria zake zote. Mungu akiniruhusu niishi, kabla ya miaka mingi nitamfanya kijana mwongoza plau ajue mengi zaidi juu ya Andiko kuliko ujuavyo.” Azimio la Tyndale lilikuwa limedhihirika. Baadaye aliandika hivi: “Nilikuwa nimetambua kwa kujionea mwenyewe jinsi ambavyo haikuwezekana kuweka imara watu wa kawaida katika kweli yoyote, isipokuwa andiko liwekwe wazi machoni pao katika lugha zao, ili waweze kuona kiini, utaratibu na maana ya maandishi.”

Wakati huo, bado hakukuwa na Biblia iliyokuwa imechapwa katika Kiingereza. Kwa hiyo mwaka wa 1523, Tyndale alienda London ili kuomba ruhusa na idhini ya Askofu Tunstall ya mradi wa kutafsiri. Akiwa amepata jibu kali na la dharau, aliondoka Uingereza kufuatia kusudi lake, asirudi tena kamwe. Akiwa Cologne, Ujerumani, matbaa yake ya kwanza ilivamiwa, naye Tyndale akaponea chupuchupu akiwa na baadhi ya kurasa zenye thamani ambazo hazikuwa zimejalidiwa. Hata hivyo, akiwa Worms, Ujerumani, angalau nakala 3,000 za “Agano Jipya” lake la Kiingereza zilikamilika. Hizo zilipelekwa Uingereza na zikaanza kugawanywa huko mapema mwaka wa 1526. Baadhi ya hizi ni zile Biblia ambazo Askofu Tunstall alinunua na kuchoma, akimsaidia Tyndale bila kujua aendelee na kazi yake!

Utafiti Waleta Uelewevu wa Wazi Zaidi

Kwa wazi Tyndale alifurahia kazi yake. Kama vile kisemavyo kichapo The Cambridge History of the Bible, “Andiko lilimfanya afurahi, na kuna jambo la haraka na lenye kuchangamsha katika wizani yake linalowasilisha furaha yake.” Mradi wa Tyndale ulikuwa kufanya Maandiko yapatikane kwa mtu wa kawaida katika lugha sahihi na sahili iwezekanavyo. Kujifunza kwake kulimwonyesha maana ya maneno ya Biblia ambayo yalikuwa yamefichwa katika fundisho la kanisa kwa karne kadhaa. Bila kuogofywa na tisho la kifo wala maandishi maovu ya adui wake mwenye nguvu Sir Thomas More, Tyndale alitia ndani ya tafsiri yake mambo aliyogundua.

Akitafsiri kwa kutumia Kigiriki cha awali cha maandishi ya Erasmus badala ya Kilatini, Tyndale alichagua neno “upendo” badala ya neno “wema” ili kuonyesha maana ya neno la Kigiriki a·gaʹpe kikamili zaidi. Pia alitumia “kutaniko” badala ya “kanisa,” “tubu” badala ya “uwe na malipizi,” na “wazee” badala ya “makasisi.” (1 Wakorintho 13:1-3; Wakolosai 4:15, 16; Luka 13:3, 5; 1 Timotheo 5:17, Tyndale) Marekebisho hayo yalimaliza kabisa mamlaka ya kanisa na mazoea ya dini ya kidesturi, kama vile ungamo kwa kasisi.

Hali kadhalika Tyndale alishikilia neno “ufufuo,” akikataa purgatori na kuwa na fahamu baada ya kifo kuwa ni mambo yasiyo ya kibiblia. Kuhusu wafu, alimwandikia More hivi: “Kwa kuwaweka mbinguni, helo, na purgatori, [wewe] waharibu hoja za Kristo na Paulo ambazo zathibitisha ufufuo.” Katika habari hii, Tyndale alirejezea Mathayo 22:30-32 na 1 Wakorintho 15:12-19. Alikuja kuamini kwa usahihi kwamba wafu huendelea kuwa bila fahamu hadi ufufuo wa wakati ujao. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5; Yohana 11:11, 24, 25) Hilo lilimaanisha kwamba mpango wote wa sala kwa Maria na “watakatifu” haukuwa na maana kwa kuwa wakiwa katika hali yao isiyo na fahamu hawangeweza kusikia wala kuingilia kati.

Tyndale Atafsiri Maandiko ya Kiebrania

Mwaka wa 1530, Tyndale alitokeza chapa ya kwanza ya Pentateuki, vile vitabu vitano vya kwanza vya Maandiko ya Kiebrania. Hivyo akawa mtu wa kwanza kutafsiri Biblia katika Kiingereza moja kwa moja kutoka Kiebrania. Pia Tyndale alikuwa mtafsiri wa kwanza wa Kiingereza kutumia jina Yehova. Msomi wa London David Daniell aandika hivi: “Kwa hakika iliwavutia sana wasomaji wa Tyndale kwamba jina la Mungu lilifunuliwa upya.”

Katika kujaribu kwake kupata kuwa wazi, Tyndale alitumia maneno tofauti-tofauti ya Kiingereza ili kutafsiri neno moja la Kiebrania. Hata hivyo, alifuatia muundo wa Kiebrania karibu-karibu. Tokeo ni kwamba ile nguvu yenye usahihi ya Kiebrania yahifadhiwa. Yeye mwenyewe alisema hivi: “Lugha ya Kiebrania yafanana zaidi sana na Kiingereza kuliko ifananavyo na Kilatini. Njia ya kuzisema ni moja; hivi kwamba katika visa vingi wahitaji tu kutafsiri katika Kiingereza, neno kwa neno.”

Mfikio huo sisisi kimsingi, ulitia ladha tafsiri ya Tyndale kwa misemo ya Kiebrania. Lazima baadhi ya misemo hiyo iwe ilionekana kuwa isiyo ya kawaida iliposomwa mara ya kwanza. Lakini, hatimaye Biblia ilipata kujulikana sana hivi kwamba sasa mingi ya misemo hiyo ni sehemu ya lugha ya Kiingereza. Vielelezo vyatia ndani “a man after his own heart” (mtu mwenye kupendeza moyo wake) (kama ilivyo kwenye 1 Samweli 13:14), “passover” (kupitwa), na “scapegoat” (kisingizio). Zaidi ya hilo, wasomaji wa Biblia ya Kiingereza walizoelea mawazo ya Kiebrania, kufanya hivyo kukiwapa ufahamu wa kina ulio bora zaidi wa Maandiko yaliyopuliziwa.

Biblia Pamoja na Tyndale Chini ya Marufuku

Uwezekano wa kusoma Neno la Mungu katika lugha ya mtu mwenyewe ulisisimua. Watu wa kawaida Waingereza waliitikia kwa kununua Biblia zote ambazo zingeweza kuingizwa kimagendo nchini, zikiwa zimefichwa zionekane kama mitumba ya nguo au bidhaa nyinginezo. Wakati uleule, makasisi walifikiria kwa makini kule kupoteza nyadhifa zao kusikoepukika ikiwa Biblia ingekuja kuonwa kuwa mamlaka ya mwisho. Kwa sababu hiyo, hali ya mtafsiri na wenye kumwunga mkono ikawa ya kufa na kupona hata zaidi.

Akifuatwa daima na Kanisa na Serikali, Tyndale aliendelea kufanya kazi mafichoni huko Antwerp, Ubelgiji. Hata hivyo, alitenga siku mbili kwa juma kwa ajili ya aliloita kipisha-wakati—kuhudumia wakimbizi wengine Waingereza, maskini, na wagonjwa. Alitumia nyingi za fedha zake hivyo. Kabla ya kuweza kutafsiri nusu ya pili ya Maandiko ya Kiebrania, Tyndale alisalitiwa kwa ajili ya fedha na Mwingereza aliyejifanya kuwa rafiki. Akifishwa huko Vilvoorde, Ubelgiji, mwaka wa 1536, maneno yake yenye bidii yalikuwa, “Bwana! uyafungue macho ya Mfalme wa Uingereza.”

Kufikia mwaka wa 1538, Mfalme Henry wa Nane alikuwa ameamuru kwamba Biblia ziwekwe katika kila kanisa Uingereza kwa sababu zake mwenyewe. Ingawa Tyndale hakupewa sifa, tafsiri iliyochaguliwa ilikuwa yake hasa. Kwa njia hiyo tafsiri ya Tyndale ikapata kujulikana sana na kupendwa sana hivi kwamba “ikaamua jinsi ambavyo tafsiri [za Kiingereza] zilizofuata zingekuwa.” (The Cambridge History of the Bible) Asilimia ipatayo 90 ya tafsiri ya Tyndale ilinakiliwa moja kwa moja katika King James Version ya mwaka wa 1611.

Kuipata Biblia kwa uhuru kulimaanisha badiliko kubwa kwa Uingereza. Mazungumzo yaliyotegemea Biblia zilizowekwa makanisani yalikuwa machangamfu kwelikweli hivi kwamba nyakati nyingine yalihitilafiana na ibada ya kanisa! “Wazee walijifunza kusoma ili wapate Neno la Mungu moja kwa moja, nao watoto walijiunga na wakubwa wao kusikiliza.” (A Concise History of the English Bible) Kipindi hicho kilikuwa na ongezeko lenye kutazamisha katika ugawanyaji wa Biblia katika nchi na lugha nyinginezo za Ulaya. Lakini kusonga kwa Biblia Uingereza kulitazamiwa kuwa na uvutano wa ulimwenguni pote. Hilo lilitokeaje? Na uvumbuzi na utafiti zaidi umeathirije Biblia tunazotumia leo? Tutamalizia simulizi letu kwa makala itakayofuata katika mfululizo huu.

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Agano Jipya” la Tyndale la mwaka wa 1526—nakala pekee iliyo kamili ijulikanayo iliyoponyoka miali ya moto

[Hisani]

© The British Library Board

[Chati/Picha katika ukurasa wa 26, 27]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Tarehe Muhimu Katika Kupitishwa kwa Biblia

Wakati Wetu

Biblia ya Wycliffe Ilianza (kabla ya 1384)

1400

Hus afishwa 1415

Gutenberg—Biblia ya kwanza kuchapwa karibu 1455

Biblia za Lugha za Kienyeji Zilizochapwa Mapema

1500

Maandishi ya Kigiriki ya Erasmus 1516

“Agano Jipya” la Tyndale 1526

Tyndale afishwa 1536

Henry wa Nane aamuru Biblia ziwekwe makanisani 1538

1600

Biblia ya King James Version 1611

[Picha]

Wycliffe

Hus

Tyndale

Henry wa nane

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki