Biblia ya William Tyndale Kwa Ajili ya Watu
ILIKUWA siku moja katika Mei katika mwaka 1530.a Ua wa kanisa la St. Paul katika London ulijaa umati wa watu. Badala ya kusongamana kwenye vibanda vya wauza vitabu na kubadilishana habari za karibuni zaidi na kupiga domo kama kawaida, umati huo wa watu ulionekana kuwa umefadhaika. Moto ulikuwa ukiwaka kwa ngurumo katikati ya ua huo. Lakini haukuwa moto mkubwa wa sherehe ya kawaida. Wanaume fulani walikuwa wakitia katika moto huo vitabu vilivyojaa vikapuni. Ilikuwa sherehe ya kuchoma vitabu!
Wala hivyo havikuwa vitabu vya kawaida. Zilikuwa Biblia—“Agano Jipya“ na Pentatuki za William Tyndale—za kwanza kabisa kuchapwa katika lugha ya Kiingereza. Kwa kushangaza, Biblia hizo zilikuwa zikichomwa kwa agizo la Askofu wa London, Cuthbert Tunstall. Kwa kweli, yeye alikuwa ametumia kiasi kikubwa mno cha fedha kununua nakala zote ambazo angeweza kupata. Ni jambo gani baya lingeweza kuwa katika Biblia hizo? Ni kwa sababu gani Tyndale alizifanyiza? Na kwa sababu gani wenye mamlaka walifanya yote wawezayo kuziondolea mbali?
Biblia—Kitabu Kilichofungwa
leo, ni jambo rahisi kwa kulinganisha kununua Biblia. Lakini hivyo si ndivyo imekuwa sikuzote. Hata katika Uingereza wa karne ya 15 na mapema mwa karne ya 16, Biblia ilionwa kuwa mali ya kanisa, kitabu cha kusomwa tu wakati wa ibada ya watu wote na kuelezwa na makasisi peke yao. Hata hivyo, yaliyosomwa, kwa kawaida yalikuwa katika Biblia ya Kilatini, ambayo watu wa kawaida hawangeweza ama kufahamu ama kuwa na pesa za kutosha kununua. Hivyo, yale waliyojua juu ya Biblia yalikuwa hadithi tu na masomo ya kiadili yaliyofundishwa na viongozi wa kanisa.
Lakini si watu wa kawaida tu waliokuwa hawajui Biblia. Kama ambavyo imeripotiwa, wakati wa utawala wa Mfalme Edward wa Sita (1547-53), askofu mmoja wa Gloucester alipata kujua kwamba miongoni mwa viongozi wa kanisa 311, 168 wao hawangeweza kurudia kutaja zile Amri Kumi na 31 hawakujua mahali wangezipata katika Biblia. Arobaini hawangeweza kurudia kusema ile Sala ya Bwana na karibu 40 hawakujua mwanzilishi wayo. Kweli, John Wycliffe alikuwa ametokeza Biblia katika Kiingereza katika 1384, na fafanusi za sehemu mbalimbali za Maandiko, kama vile vitabu vya Injili na Zaburi, zilikuwako katika lugha hiyo. Hata hivyo, kwa kweli Biblia ilikuwa kitabu kilichofungwa
Hali kama hizi zilimfanya Tyndale aazimie kuifanya Biblia ipatikane kwa watu wenye kusema lugha ya Kiingereza. “Mimi nilifahamu jinsi lilivyokuwa jambo lisilowezekana kuimarisha watu wa kawaida katika ukweli wo wote.“ akaandika, “isipokuwa Andiko liwekwe wazi mbele ya macho yao katika lugha yao wenyewe.“
Lakini kwa kutafsiri Biblia katika Kiingereza, Tyndale alijiletea ghadhabu ya wenye mamlaka. Kwa sababu gani? Kwa sababu mapema kama 1408 baraza la viongozi wa kidini lilikutana katika Oxford, Uingereza, kuamua kama watu wa kawaida wanapaswa kuruhusiwa kuwa na nakala za Biblia katika lugha yao wenyewe kwa matumizi ya kibinafsi. Uamuzi huo ulisoma hivi, kwa sehemu: “Kwa hiyo sisi tunaamuru na kuagiza, kwamba kuanzia sasa na kuendelea hakuna mtu asiyeruhusiwa atakayetafsiri sehemu yo yote ya Andiko takatifu katika Kiingereza au lugha nyingine yo yote . . . chini ya adhabu ya kutengwa na ushirika kukubwa zaidi, mpaka tafsiri hiyo itakapokubaliwa ama na askofu wa jimbo hilo, ama baraza la mkoa kama hali hiyo itakavyotaka.
Zaidi ya karne moja baadaye, Askofu Tunstall alitumia amri hii katika kuchoma Biblia ya Tyndale, ingawa Tyndale alikuwa ametafuta kibali cha Tunstall mapema.b Katika oni la Tunstall, tafsiri ya Tyndale ilikuwa na makosa 2,000 na kwa hiyo ilikuwa “yenye kudhuru, yenye kukashifu, na yenye kutongoza akili nyepesi.“ Lakini je! huo ulikuwa udhuru upande wa askofu kumpa kaki ya kuichoma? Je! kweli Tyndale alikuwa mtafsiri asiyefaa, asiye na elimu inayohitajiwa kabisa ya mwanachuo katika Kiebrania, Kigiriki, na Kiingereza? Tyndale alikuwa mtafsiri mwenye kufaa kadiri gani?
Tyndale—Je! Alikuwa Mtafsiri Asiyefaa
Ijapokuwa ufahamu wa Kiebrania na Kigiriki wakati huo haukuwa kama ulivyo leo, ufahamu wa Tyndale wa lugha hizi ulilingana na ule wa wanachuo walio wengi wa wakati wake. Kinachofanya kazi ya tafsiri ya Tyndale iwe yenye kutokeza ni kwamba yeye hakuchunguza to tafsiri ya Kilatini ya Vulgate na ya Kijeremani ya Luther. Yeye alichunguza maandishi ya Kigiriki ya kwanza-kwanza yaliyochapishwa kwa mara ya kwanza katika 1516 na Erasmus. Pia Tyndale hakusahau kusudi lake: kufanya Maandiko yawe rahisi vya kutosha kusomwa na watu wa kawaida kufikia hata “kivulana alimaye shamba kwa plau.“ Kwa hiyo mtindo na mwandiko wake na ufasaha wa maneno ni mwepesi na wazi, hata hivyo ni wenye nguvu. Na mwendo wake wenye shauku bila shaka unaonyesha furaha ambayo alipata kwa kufanya kazi hiyo ngumu.
Hivyo ni kweli kusema kwamba “Tyndale alikuwa mtafsiri ambaye kwa kawaida uamuzi wake ulikuwa mzuri. Akifanya kazi katika hall mbaya isivyo kawaida, kulingana na maendeleo ya maarifa ya lugha za Kibiblia katika siku zake, yeye alitokeza tafsiri ambazo ziliweka kiolezo kwa watafsiri wote wa Kiingereza waliofuata.“—The Making of the English Bible, cha Gerald Hammond, kurasa 42, 43.
Tafsiri Sahihi
Katika mambo ya usahihi Tyndale pia aliweka kiwango cha juu. Kwa mfano, katika kutafsiri kutoka Kiebrania, yeye alijaribu kuwa halisi ilivyowezekana huku akidumisha mtindo wa Kiingereza rahisi, wenye ufasaha. Yeye alikuwa mwangalifu hata kudumisha elezo kamili la Kiebrania pamoja na kurudia-rudia mara nyingi kwalo kwa neno “na“ katika kuunganisha fungu la maneno baada ya jingine katika sentensi. (Ona Mwanzo sura ya 33 katika King James Version, ambayo inatumia karibu maneno yote ya Tyndale.) Yeye aliangalia sana maneno yanayotangulia na kufuata na akaepuka kuongezea au kuondolea maandishi ya kwanza kabisa, ingawa ufafanusi ndio uliofuatwa na walio wengi wa watafsiri wa wakati wake
Uteuzi wa maneno wa Tyndale ulikuwa pia wa uangalifu na sahihi. Kwa mfano, yeye alitumia “upendo“ badala ya “fadhili,“ “kundi“ kwa “kanisa,“ na “mzee“ badala ya “kasisi“ mahali ilipofaa. Hilo lilikasirisha wachambuzi kama Sir Thomas More kwa sababu ilibadilisha maneno ambayo yalikuwa yamepata kuheshimiwa sana kupitia mapokeo. Mahali maandishi ya kwanza-kwanza yalipotaka kurudiwa kwa neno, Tyndale alikuwa mwangalifu kulirudia. Kutoa mfano: Kwenye Mwanzo 3:15, tafsiri yake ilisema mara mbili juu ya ‵kukanyagaʼ kunakofanywa na uzao wa mwanamke na yule nyoka.c
Tyndale ndiye pia aliyechukua daraka la kuingiza jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, katika Biblia ya Kiingereza. Kama asemavyo mwandikaji J. F. Mozley, Tyndale alilitumia katika tafsiri yake ya “Agano la Kale mara zaidi ya ishirini.“
Katika kutazama nyuma kwenye matokeo ya jitihada za Tyndale na sifa zazo zenye kudumu, kadirio hili la kisasa linaeleza vizuri kazi yake kwa ufupi: “Uaminifu, unyofu, wa Tindale, na ukamilifu wake wenye uangalifu mwingi, uhalisi wake rahisi, urahisi wa ajabu wa vifungu vya maneno yake, muziki wenye kiasi wake, yameyapa mamlaka matumizi yake ya maneno ambayo yamekuwa na uvutano juu ya tafsiri zote za baadaye. . . Sehemu tisa katika kumi za Agana Jipya la Authorized New Testament [King James Version] zingali za Tindale, na yaliyo bora zaidi yangali ni yake.“—The Bible in Its Ancient and English Versions, ukurasa 160.
Kazi ya Tyndale Si ya Bure
Ili aepuke mateso ya wenye mamlaka, Tyndale alikimbilia bara la Ulaya aendeleze kazi yake huko. Lakini mwishowe alikamatwa. Kwa kuonekana kuwa na hatia ya uzushi, alinyongwa na kuchomwa moto akiwa amefungiwa penye mti katika Oktoba 1536. Sala yake ya mwisho ilikuwa: “Bwana, ufungue macho ya Mfalme wa Uingereza.“ Yeye hakujua hata kidogo jinsi hali hiyo ingebadilika upesi sana. Katika Agosti 1537, muda ulio chini wa mwaka mmoja baada ya kifo cha Tyndale, Mfalme Henry wa Nane alitoa ruhusa kwa Biblia inayojulikana kwa kawaida kuwa Biblia ya Mathayo. Yeye aliagiza kwamba inapaswa kuuzwa na kusomwa bila vizuizi katika milki yake.
Ni ipi iliyokuwa Biblia ya Mathayo? Profesa F. F. Bruce anaeleza hivi: “Inapochunguzwa kwa kweli inaonekana kuwa Pentatuki ya Tyndale, tafsiri ya Tyndale ya vitabu vya kihistoria vya Agano la Kale kufika 2 Nyakati . . . tafsiri ya Coverdale ya vile vitabu vingine vya Agano la Kale na Apokreifa, na Agano Jipya la Tyndale la 1535.“ Hivyo, mwandikaji huyo anaendelea kusema, “lilikuwa tendo kubwa la haki . . . kwamba Biblia ya kwanza ya Kiingereza kuchapishwa chini ya ruhusa ya kifalme ikawa Biblia ya Tyndale (kufikia mahali tafsiri ya Tyndale ilipokuwa imefika), hata ingawa lilikuwa bado si jambo lenye busara kuishirikisha na jina la Tyndale hadharani.“
Katika muda wa miaka mingine michache, mambo yangebadilika kabisa. Wakati chapa ya tafsiri ijulikanayo kama Great Bible —ambayo ni Biblia ya Mathayo iliyosahihishwa—ilipotolewa katika 1541 na amri ikatolewa iwekwe katika kila kanisa katika Uingereza, ukurasa wenye jina ulitia ndani maneno haya: “Imesimamiwa na kuchunguzwa kwa amri ya mtukufu mfalme, na mababa waheshimiwa sana katika Mungu Cuthbert askofu wa Duresme, na Nicholas askofu wa Rochester.“ Ndiyo, huyo ‘Askofu wa Durhamʼ alikuwa si mwingine ila Cuthbert Tunstall, aliyekuwa hapo kwanza Askofu wa London. Yeye ambaye alikuwa amepinga vikali sana kazi ya Tyndale alikuwa sasa akitoa kibali cha kutolewa kwa Great Bible, kazi ambayo kwa asili ingali ni ile ya Tyndale
Kutambuliwa Mwishowe
Huenda ikashangaza leo kusoma juu ya ubishi kama huo juu ya Biblia na chuki kwa watafsiri wayo. Lakini labda jambo la kutokeza zaidi ni uhakika wa kwamba, ijapokuwa jitihada zao, wapinzani hawakuweza kuzuia Neno la Mungu lisiwafikie watu wa kawaida. “Majani yaka aka, ua lanyauka;“ akasema nabii Isaya, “bali neno la Mungu wetu litasimama milele.“—Isaya 40:8.
Tyndale na wengine walifanya kazi uvuli wa kifo ukiwa unaningʼinia juu ya vichwa vyao. Lakini kwa kufanya Biblia ipatikane kwa watu wengi katika lugha zao za kienyeji, walifungua mbele yao taraja, si la kifo, bali la uzima wa milele. Kama alivyosema Yesu Kristo: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.“ (Yohana 17:3) Kwa hiyo, sisi na tulithamini sana na kujifunza kwa bidii Neno la Mungu.
[Maelezo ya chini]
a Matukio yanayofanana na hayo ambayo yameelezwa hapa yalikuwa yametukia katika 1926 na katika nyakati nyingine.
b Kwa mazungumzo zaidi juu ya maisha na kazi ya Tyndale, ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Januari 1, 1982, kurasa 10-14.
c Watafsiri wengi wa kisasa wanakosa kuangalia kitenzi cha Kiebrania kinachorudiwa hapa pamoja na maana ile ile yacho. Kwa hiyo badala ya “-chubua . -chubua“ (New World Translation; Revised Standard Version), wanatumia “-ponda .. -piga“ (The Jerusalem Bible; New International Version), “-ponda -uma“ (Todayʼs English Version), “-kanyaga-piga“ (Lamsa), au “-ponda . . . -otea“ (Knox).).
[Hisani katika ukurasa wa 21]
From an old engraving in the Bibliothèque Nationale