Kutafsiri Biblia Kulikuwa Hatari
KUTAFSIRI Biblia kulianza zamani za kale. Katika karne ya tatu K.W.K. wanafunzi wa Kiyahudi (sabini na wawili, kulingana na mapokeo) walianza kutafsiri vitabu vitano vya Musa, yaani Pentateuch, kutoka Kiebrania kuviingiza katika Kigiriki. Tangu wakati huo watafsiri wa Biblia wamepingwa vikali mara kadha, hasa na wakuu wa dini. Ikawapasa kujiacha wataabishwe na hata wauawe kwa ajili ya kazi yao.
Hatuwezi kueleza kirefu sana vile Biblia ilivyotafsiriwa katika mojawapo ya lugha nyingi ambazo zinapatikana sasa, yote au sehemu yake, kwa sababu ni hadithi ndefu sana. Kwa hiyo, tutaangalia kisehemu tu cha hadithi hiyo inayoonyesha jitihada za kwanza zenye hatari zilizofanywa ili kutafsiri Biblia katika lugha mbili kubwa—Kiingereza na Kichina.
BIBLIA KATIKA KIINGEREZA
Tafsiri ya kwanza ya Kiingereza ilitokezwa karne ya kumi na nne ilipokuwa ikimalizika. Jina Wycliffe linashikamanishwa na tafsiri hiyo iliyotegemea Vulgate ya Kirumi. Leo haijulikani John Wycliffe aliitafsiri mpaka wapi. Walakini, ni hakika kwamba kazi ya kutafsiri ilipingwa vikali sana. Wycliffe na wenzake walichukiwa vibaya sana na wakuu wa dini. Lakini, linaloshangaza ni kwamba Wycliffe hakufa kwa sababu walimchochea fitina bali aliuawa na ugonjwa wa kupooza.
Baada ya hapo wakuu wa dini waliendelea kupinga nakala zisifanywe juu ya tafsiri ya Wycliffe. Mwishowe, mwaka wa 1408, viongozi wa dini walipokutana katika Oxford kwa agizo la Askofu Mkuu, Arundel, walikataza Maandiko Matakatifu hayo ya Kiingereza yasitumiwe. Ingawa viongozi hao wa dini walikataza jambo hilo, tafsiri hiyo moja tu iliyopatikana katika Kiingereza iliendelea kunakiliwa. Hiyo yahakikishwa na nakala karibu 200 za tafsiri hiyo ambazo zingali ziko leo (na nyingi kati yazo zilinakiliwa baada ya mwaka 1420). Wycliffe alichukiwa sana hata masalio yake yalichimbuliwa mwaka 1428 yakachomwa kisha mavumbi yake yakatupwa ndani ya mto Swift.
Biblia ilianza kutafsiriwa kutoka lugha za asili (si kutoka Vulgate ya Kirumi) kuingia katika Kiingereza mapema katika karne ya kumi na sita. William Tyndale ndiye aliyeanza kazi hii. Tyndale alikwenda London akitumainia kuungwa mkono na Askofu Cuthbert Tunstall. Lakini hakuungwa mkono.
Ingawa Tyndale aliendelea kukaa London, karibuni alijua kwamba viongozi wa dini hawakutaka atafsiri Biblia Uingereza. Kwa hiyo alielekea Ujeremani mwaka 1524. Huko, katika Cologne, tafsiri yake ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (yaitwayo na watu “Agano Jipya”) ilianza kuchapwa. Mahakimu wa Cologne walipopashwa habari hizo, waliikomesha kazi hiyo. Tyndale aliondoka upesi kuelekea Worms, ambako Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliweza kumalizwa kuchapwa. Baada ya muda mfupi nakala za tafsiri hiyo ziliuzwa Uingereza. Wakati huo Tyndale alikuwa akiendelea kuchunguza mambo aliyotafsiri na kuzidi kutafsiri.
Wakuu wa dini katika Uingereza walikasirika sana. Mei 4, 1530, nakala za tafsiri ya Tyndale ziliteketezwa kwa moto katika St. Paul’s Cross, London. Kuelekea mwisho wa Mei amri ya kifalme, yenye kuungwa mkono na wakuu wa dini, ilisema tafsiri za Tyndale za Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki zilikuwa kati ya vitabu hatari na ikasema: “Zichukieni, zichukieni kiasi cha kutapika; msizishike, zipelekeni kwa wakuu wanaosema wapelekewe.” Kwa habari ya wasiotii, amri iliendelea kusema hivi: “Wakuu wa kanisa, waliokabidhiwa kazi ya kuangalia nafsi zenu, wanapaswa kuwalazimisheni, na mkuu wenu apaswa kuwaadhibu na kuwarudi.” Jitihada nyingi zilifanywa kuharibu tafsiri hizo katika Uingereza na nchi nyinginezo.
Sababu moja iliyofanya Tyndale apingwe vikali hivyo ni kwamba yeye hakufuata maneno ya kidini, bali alitumia maneno yaliyoeleza maana halisi ya lugha ya asili. Kwa mfano, yeye alitumia neno “kundi,” si kanisa; “mwangalizi,” si askofu, na “upendo,” si fadhili. Wakuu wa dini hawakupendezwa na vile Tyndale alivyotumia maneno yaliyokaribiana na Kigiriki cha asili. Tyndale hata alikuwa ameonyesha nia ya kubadili lo lote ambalo lingeweza kuwa kosa au ambalo lingeweza kutafsiriwa kwa njia yenye kufahamika zaidi. Lakini, wakuu wa dini hawakutaka hata kidogo Biblia isomwe na watu wa kawaida, kwa sababu hawakutaka watu hao wakatae maelezo yao ya kidini.
Baada ya muda mfupi kazi ngumu za Tyndale zilikomeshwa. Mtu mmoja aliyeitwa Phillips alijisingizia kuwa rafiki yake kisha akamsaliti kwa adui. Halafu Tyndale alitiwa gerezani katika jumba la kifalme la Vilvorde, karibu na Brussels. Katika Septemba wa 1536 alinyongwa akateketezwa kwa moto.
Ndivyo yalivyokoma maisha ya mwanafunzi hodari ambaye alifanya kazi ngumu zilizotoa uongozi wa kutafsiri Biblia katika Kiingereza karibu miaka 400 iliyofuata. Tyndale alikuwa amefanya kazi kwa kuhatirisha maisha yake, si kwa kusudi la kujipatia heshima wala sifa wala cheo, bali kwa kusudi la kufanya Neno la Mungu lipatikane na mwanadamu wa kawaida.
BIBLIA KATIKA KICHINA
Mwaka 1807, karibu miaka 271 baada ya Tyndale kuuawa, Robert Morrison, mmisionari Mprotestanti, alifika Canton, China. Baada ya muda mfupi alianza kutafsiri Biblia katika Kichina. Morrison alijua Kichina kidogo lakini alihitaji msaada zaidi aielewe lugha hiyo. Ilikuwa vigumu kupata msaada huo, kwa sababu kutafsiri Biblia katika Kichina kulikuwa hatari, na adhabu yake ilikuwa kifo. Hata hivyo Morrison alifaulu akapata msaada wa wanafunzi wawili Wachina. Mmoja wao aliogopa sana kukamatwa na kufa kifo cha polepole, akiumizwa-umizwa, hata akawa akichukua sumu ili akikamatwa ajiue mwenyewe.
Wakati huo wageni waliruhusiwa kuingia mji wa Canton miezi sita tu kwa mwaka, na hiyo ililazimisha Morrison kuondoka-ondoka baada ya kila miezi sita. Wakati huo Morrison alikuwa akikaa katika kisiwa cha Macao. Alipokubali kufanya kazi ya kutafsiri katika kampuni iliyoitwa East India Company, aliweza kurudi Canton.
Mchana, wakati Morrison alipokuwa akifanyia East India Company kazi, aliangalia biashara na kutafsiri kamusi ya Kichina kwa Kiingereza na kupanga sarufi ya Kichina. Usiku yeye na wasaidizi wake Wachina walitafsiri Biblia.
Mwaka 1810 kitabu cha Matendo katika Kichina kilichapwa kutokana na mbao za kutengenezwa kwa mikono. Kwa kuwa Morrison hakutaka mbao hizo zichukuliwe na watu wabaya, Morrison alizifukia alipofunga safari ya kwenda Macao. Alikata tamaa sana wakati aliporudi baada ya miezi sita akakuta mchwa wamezila mbao hizo.
Ijapokuwa kulikuwa na matatizo na vipingamizi, mwaka 1814 Morrison alisaidiwa na mmisionari mwingine, William Milne, wakamaliza kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kufika mwaka 1818 Biblia yote ilikuwa imetafsiriwa.
Kutafsiri Biblia kumekuwa hatari kweli kweli. Watafsiri kama Tyndale na Morrison walikuwa na moyo na ushujaa, na walikuwa na nia ya kustahimili ijapokuwa vipingamizi vilikuwa vikubwa sana. Wao walitenda kupatana na mapenzi ya Mungu kwamba watu wote wanapaswa kuwa na nafasi ya kupata ‘maarifa sahihi ya kweli.’—1 Tim. 2:3, 4, NW.