Kutegemeza kwa Uaminifu-mshikamanifu Neno la Mungu Lililopuliziwa
“Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu.”—2 WAKORINTHO 4:2.
1. (a) Ni jambo gani limehitajiwa ili kutimiza kazi iliyotajwa kwenye Mathayo 24:14 na 28:19, 20? (b) Biblia ilipatikana kwa kiwango gani katika lugha za watu siku za mwisho zilipoanza?
KATIKA unabii wake mkubwa kuhusiana na wakati wa kuwapo kwake kwa kifalme na umalizio wa mfumo wa kale wa mambo, Yesu Kristo alitabiri hivi: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” Pia aliwaagiza wafuasi wake hivi: “[Fanyeni] wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . [mki]wafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Utimizo wa unabii huo mbalimbali wahusisha kazi nyingi katika kutafsiri na kuchapa Biblia, katika kuwafundisha watu maana yake, na katika kuwasaidia waitumie maishani mwao. Ni pendeleo kama nini kushiriki katika utendaji huo! Kufikia mwaka wa 1914 Biblia au sehemu za Biblia tayari zilikuwa zimechapishwa katika lugha 570. Lakini tangu wakati huo mamia zaidi ya lugha na lahaja kadha wa kadha zimeongezwa, na katika lugha nyingi zaidi ya tafsiri moja zimefanywa zipatikane.a
2. Ni nia zipi tofauti-tofauti zimekuwa na uvutano juu ya kazi ya watafsiri na wachapishaji wa Biblia?
2 Ni kazi ngumu kwa mtafsiri yeyote yule kutafsiri habari kutoka lugha moja na kuifanya ieleweke kwa wanaosoma na kusikia lugha nyingine. Watafsiri fulani wa Biblia wamefanya kazi yao wakifahamu sana kwamba walilokuwa wakitafsiri lilikuwa Neno la Mungu. Wengine wamevutiwa tu na ile kazi ya kisomi yenye kupendeza ya mradi huo. Huenda wakawa waliona yaliyomo katika Biblia kuwa urithi tu wa kitamaduni wenye thamani. Kwa wengine, dini ndiyo kazi-maisha yao, na kuchapisha kitabu chenye jina lao wakiwa watafsiri au wachapishaji ni njia mojawapo ya kupata riziki. Kwa wazi nia zao huwa na uvutano juu ya jinsi wafanyavyo kazi yao.
3. Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya Ulimwengu Mpya ilionaje kazi yake?
3 Taarifa hii iliyotolewa na Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya Ulimwengu Mpya yafaa kuangaliwa: “Kutafsiri Maandiko Matakatifu humaanisha kutafsiri katika lugha nyingine mawazo na semi za Yehova Mungu . . . Hilo ni wazo lenye kufanya mtu afikiri sana. Watafsiri wa kitabu hiki, wamhofuo na kumpenda Mtungaji Mtakatifu wa Maandiko Matakatifu, huhisi daraka la pekee kuelekea Yeye la kupitisha mawazo na matangazo yake kwa usahihi iwezekanavyo. Wao pia huhisi daraka kuelekea wasomaji wanaochunguza ambao hutegemea tafsiri ya Neno lililopuliziwa la Mungu Aliye Juu Zaidi Sana ili wapate wokovu wao udumuo milele. Ni kwa sababu ya kuwa na hisia hiyo ya daraka zito kwamba kwa kipindi cha miaka mingi hiyo halmashauri ya watu waliojiweka wakfu imetokeza New World Translation of the Holy Scriptures.” Mradi wa hiyo halmashauri ulikuwa, kuwa na tafsiri ya Biblia ambayo ingekuwa wazi na yenye kueleweka na ambayo ingeshikamana kwa ukaribu sana na Kiebrania na Kigiriki cha awali hivi kwamba ingeandaa msingi wa ukuzi wenye kuendelea wa ujuzi sahihi.
Jina la Mungu Limepatwa na Nini?
4. Jina la Mungu ni la maana kadiri gani katika Biblia?
4 Mojawapo ya malengo makuu ya Biblia ni kuwasaidia watu wapate kumjua Mungu wa kweli. (Kutoka 20:2-7; 34:1-7; Isaya 52:6) Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake wasali kwamba jina la Baba yake “litakaswe,” lionwe kuwa takatifu, au kutendewa kwa utakatifu. (Mathayo 6:9) Mungu alifanya jina lake la kibinafsi litiwe ndani ya Biblia mara zaidi ya 7,000. Anataka watu walijue jina hilo na sifa za Mwenye jina hilo.—Malaki 1:11.
5. Watafsiri tofauti-tofauti wamelionyeshaje jina la Mungu?
5 Watafsiri wengi wa Biblia wamelistahi kwa moyo mweupe hilo jina la Mungu na wamelitumia kwa upatano katika tafsiri zao. Watafsiri fulani hupendelea Yahweh. Wengine wamechagua aina ya jina la Mungu ambalo limebadilishwa ili lifae lugha yao wenyewe na huku bado likifanana waziwazi na lile lipatikanalo katika maandishi ya Kiebrania, labda aina ambayo yajulikana sana kwa kutumiwa kwa muda mrefu. Biblia New World Translation of the Holy Scriptures hutumia jina Yehova mara 7,210 katika maandishi yenyewe.
6. (a) Miaka ya majuzi, watafsiri wamefanya nini kwa habari ya marejezo kwenye jina la Mungu? (b) Zoea hilo limeenea kadiri gani?
6 Miaka ya majuzi, ijapokuwa watafsiri wa Biblia wamehifadhi majina ya miungu ya kipagani kama Baali na Moleki, kwa ukawaida wenye kuongezeka wanaliondoa jina la kibinafsi la Mungu wa kweli kutoka katika tafsiri za Neno lake lililopuliziwa. (Kutoka 3:15; Yeremia 32:35) Katika vifungu kama vile Mathayo 6:9 na Yohana 17:6, 26, tafsiri ya Kialbania iliyosambaa sana hutafsiri usemi wa Kigiriki “jina lako” (yaani, jina la Mungu) kuwa tu “wewe,” kana kwamba maandishi hayo hayakutaja kamwe jina lolote. Kwenye Zaburi 83:18, The New English Bible na Today’s English Version huondoa jina la kibinafsi la Mungu pamoja na rejezo lolote la uhakika wa kwamba Mungu ana jina. Ijapokuwa jina la Mungu lilionekana katika tafsiri za zamani zaidi za Maandiko ya Kiebrania katika lugha zilizo nyingi, tafsiri mpya zaidi mara nyingi huliondoa au kulitaja pambizoni tu. Hivyo ndivyo ilivyo katika Kiingereza, na pia katika lugha zilizo nyingi za Ulaya, Afrika, Amerika Kusini, India, na visiwa vya Pasifiki.
7. (a) Watafsiri wa Biblia fulani za Kiafrika wanashughulikiaje jina la Mungu? (b) Wewe wahisije juu ya hilo?
7 Watafsiri wa Biblia katika lugha za Kiafrika wanachukua hatua moja zaidi. Badala ya kutumia jina la cheo la Kimaandiko, kama vile Mungu au Bwana, mahali pa jina la Mungu, wanaongeza majina kutoka itikadi za dini ya kienyeji. Katika The New Testament and Psalms in Zulu (tafsiri ya mwaka wa 1986), jina la cheo Mungu (uNkulunkulu) lilitumiwa kwa kubadilashana na jina la kibinafsi (uMvelinqangi) ambalo Wazulu huelewa kuwa hurejezea ‘mzazi mkuu wa kale sana aliyekufa anayeabudiwa kupitia wazazi wa kale wa kibinadamu waliokufa.’ Makala katika gazeti The Bible Translator, la Oktoba 1992, iliripoti kwamba katika kutayarisha Biblia ya Kichichewa itakayoitwa Buku Loyera, watafsiri walikuwa wakitumia jina Chauta likiwa jina la kibinafsi ambalo litachukua mahali pa jina Yehova. Makala hiyo ilieleza kwamba Chauta ni “Mungu ambaye wamemjua na kumwabudu sikuzote.” Hata hivyo, wengi wa watu hao pia huabudu wanazoamini kuwa roho za wafu. Je, ni kweli kwamba ikiwa watu wanasali kwa “Aliye Mkuu Kuliko Wote,” basi jina lolote wanalotumia kumwita huyo “Aliye Mkuu Kuliko Wote” ni ulinganifu halali wa jina la kibinafsi la Yehova, haidhuru chochote kingine kile ambacho ibada yao yaweza kuhusisha? Kwa wazi la! (Isaya 42:8; 1 Wakorintho 10:20) Kuweka jina ambalo huwafanya watu wahisi kwamba itikadi zao za kidesturi kwa hakika ni sawa mahali pa jina la kibinafsi la Mungu hakuwasaidii kusonga karibu zaidi na Mungu wa kweli.
8. Kwa nini kusudi la Mungu la kufanya jina lake lijulikane halikubatilishwa?
8 Yote hayo hayakubadili wala kubatilisha kusudi la Yehova la kufanya jina lake lijulikane. Katika lugha za Ulaya, Afrika, Amerika Kaskazini na Amerika Kusini, nchi za Mashariki, na visiwa vya bahari, bado kuna Biblia nyingi zinazogawanywa ambazo hutia ndani jina la Mungu. Pia kunao Mashahidi wa Yehova wanaozidi 5,400,000 katika nchi na maeneo 233 ambao kwa pamoja hutoa saa zaidi ya bilioni moja kwa mwaka wakiwaambia wengine juu ya jina na kusudi la Mungu wa kweli. Wao huchapa na kugawanya Biblia—ambazo hutumia jina la Mungu—katika lugha zinazosemwa na watu wapatao 3,600,000,000 kati ya idadi yote ya watu wa dunia, kutia na Kiingereza, Kichina, Kirusi, Kihispania, Kireno, Kifaransa, na Kiholanzi. Pia wao huchapa misaada ya kujifunza Biblia katika lugha zijulikanazo na walio wengi wa watu wa dunia. Karibuni Mungu mwenyewe atachukua hatua katika njia ambayo itatimiza kwa kukata maneno tangazo lake la kwamba mataifa ‘watajua ya kuwa yeye ni Yehova.’—Ezekieli 38:23.
Itikadi za Kibinafsi Ziathiripo Tafsiri
9. Biblia huonyeshaje daraka zito walilo nalo wale ambao hushughulika na Neno la Mungu?
9 Wale ambao hutafsiri Neno la Mungu na pia wale ambao hulifundisha wana daraka zito. Mtume Paulo alisema hivi kwa habari ya huduma yake na ile ya washiriki wake: “Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu, bali kwa kufanya kweli iwe dhahiri tukijipendekeza wenyewe kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.” (2 Wakorintho 4:2) Kughushi kwamaanisha kufisidi kwa kuchanganya kitu kigeni au cha kiwango cha chini. Mtume Paulo hakuwa kama wale wachungaji wasio waaminifu wa Israeli katika siku za Yeremia ambao walikaripiwa na Yehova kwa sababu walihubiri mawazo yao wenyewe badala ya aliyosema Mungu. (Yeremia 23:16, 22) Lakini ni jambo gani ambalo limetukia katika nyakati za kisasa?
10. (a) Nia badala ya uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu zimekuwaje na uvutano juu ya watafsiri fulani nyakati za kisasa? (b) Walikuwa wakichukua fungu gani isivyofaa?
10 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, halmashauri ya wanatheolojia na mapasta ilishirikiana na serikali ya Nazi katika Ujerumani ili kutokeza “Agano Jipya” lililofanyiwa marekebisho ambalo lilifuta marejezo yote yenye kupendelea Wayahudi na madokezo yoyote ya nasaba ya Kiyahudi ya Yesu Kristo. Majuzi zaidi, watafsiri waliotokeza The New Testament and Psalms: An Inclusive Version waliegemea upande tofauti, wakijaribu kuondoa madokezo yoyote ya kwamba Wayahudi walikuwa na hatia kuhusiana na kifo cha Kristo. Watafsiri hao walihisi pia kwamba wasomaji wanaotetea haki na masilahi ya wanawake wangefurahi zaidi ikiwa Mungu angetajwa, si kuwa Baba, bali kuwa Baba-Mama na ikiwa Yesu angesemwa kuwa, si Mwana wa Mungu, bali Mtoto wake. (Mathayo 11:27) Walipokuwa wakifanya hivyo, waliondoa kanuni ya ujitiisho wa wake kwa waume na utii wa watoto kwa wazazi. (Wakolosai 3:18, 20) Wafanyizaji wa tafsiri hizo kwa wazi hawakushiriki azimio la mtume Paulo la ‘kutolighushi neno la Mungu.’ Walikuwa wakisahau fungu la mtafsiri, wakichukua wadhifa wa mtungaji, wakitokeza vitabu vilivyotumia kwa faida yake sifa ya Biblia ili kutegemeza kauli zao wenyewe.
11. Mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo huhitilafianaje na yale ambayo Biblia husema juu ya nafsi na kifo?
11 Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kwa ujumla hufundisha kwamba nafsi ya binadamu ni roho, kwamba hiyo huuacha mwili wakati wa kifo, na kwamba haiwezi kufa. Tofauti na hilo, tafsiri za zamani zaidi za Biblia katika lugha zilizo nyingi hutaarifu waziwazi kwamba wanadamu ni nafsi, kwamba wanyama ni nafsi, na kwamba nafsi hufa. (Mwanzo 12:5; 36:6; Hesabu 31:28; Yakobo 5:20) Hilo limewatahayarisha makasisi.
12. Tafsiri za juzi zimefichaje kweli za msingi za Biblia?
12 Sasa tafsiri mpya zaidi hufunika kweli hizi. Jinsi gani? Wao huepuka tu tafsiri ya moja kwa moja ya nomino ya Kiebrania neʹphesh (nafsi) katika maandishi fulani. Kwenye Mwanzo 2:7, huenda wakasema kwamba mtu wa kwanza “akaanza kuishi” (badala ya “akawa nafsi hai”). Au huenda wakarejezea “kiumbe” badala ya “nafsi” katika kisa cha uhai wa wanyama. (Mwanzo 1:21) Katika maandiko kama vile Ezekieli 18:4, 20, wao hurejezea “mtu” au “binadamu” (badala ya “nafsi”) kufa. Labda tafsiri hizo zingeweza kuthibitishwa kuwa za haki kulingana na huyo mtafsiri. Lakini hizo hutoa msaada kiasi gani kwa mtafutaji wa kweli mwenye moyo mweupe ambaye kufikiri kwake tayari kumetawaliwa na mafundisho yasiyo ya kimaandiko ya Jumuiya ya Wakristo?b
13. Tafsiri fulani za Biblia zimefichaje kusudi la Mungu kuhusiana na dunia?
13 Wakijitahidi kutegemeza itikadi yao kwamba watu wote wema huenda mbinguni, huenda watafsiri—au wanatheolojia ambao hurekebisha kazi za watafsiri—wakajitahidi pia kuficha yale ambayo Biblia husema juu ya kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. Kwenye Zaburi 37:11, tafsiri kadhaa husomeka kwamba wanyenyekevu wataimiliki “nchi.” “Nchi” labda ni tafsiri ya neno (ʼeʹrets) litumiwalo katika maandishi ya Kiebrania. Hata hivyo, Today’s English Version (ambayo imeandaa msingi wa kutafsiri katika lugha nyingine nyingi) yafanya mabadiliko zaidi katika tafsiri yake. Ingawa tafsiri hii hutafsiri neno la Kigiriki ge kuwa “dunia” mara 17 katika Gospeli ya Mathayo, kwenye Mathayo 5:5 yatumia fungu la maneno “kile ambacho Mungu ameahidi” mahali pa “dunia.” Bila shaka washiriki wa kanisa hufikiri juu ya mbinguni. Wao hawaarifiwi kwa kufuatia haki kwamba, katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alisema kwamba wenye tabia ya upole, wasikivu, au walio wanyenyekevu “watairithi dunia.”
14. Ni kichocheo gani chenye ubinafsi kilicho dhahiri katika tafsiri fulani za Biblia?
14 Kwa wazi maneno fulani katika tafsiri fulani za Maandiko yamekusudiwa kuwasaidia wahubiri kupata mshahara wa juu zaidi. Ni kweli kwamba Biblia hutaarifu hivi: “Mtenda-kazi astahili mshahara wake.” (1 Timotheo 5:18) Lakini kwenye 1 Timotheo 5:17, ambapo andiko hilo lasema kwamba wanaume wazee wasimamiao katika njia bora wanapaswa “wahesabiwe kustahili heshima maradufu,” heshima pekee ambayo baadhi yao huona kuwa yastahili kutajwa ni ya kifedha. (Linganisha 1 Petro 5:2.) Hivyo, The New English Bible husema kwamba wazee hao “wapaswa wahesabiwe kustahili mshahara maradufu,” nayo Contemporary English Version husema kwamba wao “wastahili kulipwa mara mbili zaidi.”
Kutegemeza Neno la Mungu kwa Uaminifu-Mshikamanifu
15. Twaweza kuamuaje tafsiri za Biblia za kutumia?
15 Yote haya yamaanisha nini kwa habari ya msomaji mmoja-mmoja wa Biblia na kwa wale waitumiao Biblia kuwafundisha wengine? Katika nyingi za lugha zitumikazo sana, kuna zaidi ya tafsiri moja ya Biblia ziwezazo kuchaguliwa. Onyesha ufahamu katika kuteua Biblia utumiayo. (Mithali 19:8) Ikiwa tafsiri haifuatii haki juu ya utambulisho wa Mungu mwenyewe—ikiondoa jina lake kutoka katika Neno lake lililopuliziwa kwa msingi wowote ule—je, yawezekana kwamba watafsiri wamegeuza pia sehemu nyingine za maandishi ya Biblia? Ukiwa na tashwishi juu ya uhalali wa tafsiri fulani, jitahidi kuilinganisha na tafsiri za zamani zaidi. Ikiwa wewe ni mwalimu wa Neno la Mungu, pendelea tafsiri ambazo hushikamana kwa ukaribu na mambo yaliyo katika maandishi ya awali ya Kiebrania na Kigiriki.
16. Sisi mmoja-mmoja twaweza kuonyeshaje uaminifu-mshikamanifu katika matumizi yetu ya Neno la Mungu lililopuliziwa?
16 Sisi sote tukiwa mmoja-mmoja twapaswa kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa Neno la Mungu. Twafanya hilo kwa kuhangaikia vya kutosha yaliyomo katika hilo hivi kwamba, ikiwezekana, twatumia wakati fulani kila siku tukiisoma Biblia. (Zaburi 1:1-3) Twafanya hilo kwa kutumia kikamili maishani mwetu wenyewe yale lisemayo, kujifunza kutumia kanuni na vielelezo vyake vikiwa msingi wa kufanya maamuzi timamu. (Waroma 12:2; Waebrania 5:14) Twaonyesha kwamba sisi ni wateteaji wa Neno la Mungu wenye uaminifu-mshikamanifu kwa kulihubiri kwa bidii kwa wengine. Pia twafanya hilo tukiwa walimu kwa kuitumia Biblia kwa uangalifu, bila kupotoa wala kutanua kamwe yale isemayo ili yafae mawazo yetu. (2 Timotheo 2:15) Yale ambayo Mungu ametabiri yatatukia bila kushindwa. Yeye ni mwenye uaminifu-mshikamanifu katika kulitimiza Neno lake. Na tuwe wenye uaminifu-mshikamanifu katika kulitegemeza.
[Maelezo ya Chini]
a Mwaka wa 1997, United Bible Societies iliorodhesha lugha na lahaja 2,167 ambazo katika hizo Biblia, nzima au sehemu, imechapishwa. Tarakimu hiyo yatia ndani nyingi za lahaja za lugha fulani-fulani.
b Mazungumzo haya yakazia fikira lugha zenye uwezo wa kufanya hilo suala liwe wazi lakini ambazo katika hizo watafsiri huchagua kutofanya hivyo. Msamiati upatikanao huwekea mipaka sana yale ambayo watafsiri wanaweza kufanya katika lugha fulani-fulani. Basi, wafunzi wa kidini wenye kufuatia haki wataeleza kwamba hata ingawa mtafsiri alitumia unamna-namna wa maneno au hata ikiwa alitumia neno lenye vidokezo visivyo vya kimaandiko, neno la lugha ya awali, neʹphesh, hutumiwa kwa wanadamu na wanyama na huwakilisha kitu ambacho hupumua, hula, na kinachoweza kufa.
Je, Wakumbuka?
◻ Ni nia zipi ambazo zimekuwa na uvutano juu ya kazi ya watafsiri wa Biblia nyakati za kisasa?
◻ Kwa nini mielekeo ya tafsiri za kisasa haikubatilisha kusudi la Mungu kuhusiana na jina lake mwenyewe?
◻ Tafsiri fulani hufichaje kweli za Biblia juu ya nafsi, kifo, na dunia?
◻ Twaweza kuonyesha katika njia zipi kwamba sisi hutegemeza Neno la Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Wapaswa kutumia tafsiri ipi ya Biblia?