Muungano wa Ulimwengu—Utakujaje?
KAMA jengo lililochakaa ambalo limeharibiwa vibaya na wapangaji wasiojali, mfumo wa ulimwengu wa sasa wafaa kwa jambo moja tu—kubomolewa na mwingine kuchukua mahali pake. Haya si maoni mengine tu ya wenye kutabiri juu ya kukaribia kwa maafa. Kulingana na Biblia, hayo ndiyo maoni pekee ya kihalisi. Kwa nini?
Misingi ya utaratibu wa ulimwengu wa sasa si salama. Jengo lote limejawa na mchwa na mbao zenye kuoza. Miimo ya feleji inashika kutu. Kuta zinazotegemeza zimedhoofika. Paa inabonyea. Ufundibomba wavuja. Mfumo wa umeme una kasoro na ni hatari. Wakaaji hupigana bila kukoma na husababisha uharibifu katika jengo lote wakiwa na nia ya kudhuru wengine. Rasilimali yote na mazingira yake yamejaa wadudu na huenda yakatokeza kifo au madhara mabaya.
“[Ku]cheza Dansi Ukingoni mwa Kaburi”
Kwa sababu ya mapambano ya kisiasa yasiyo koma, pupa, uchokozi, na uhasama wa kijamii na kikabila ulio na msingi imara, “jamii yote ya kibinadamu,” kama vile Gwynne Dyer alivyosema, “inacheza dansi ukingoni mwa kaburi.” Ulimwenguni kote, vikundi vya wachache wenye kuazimia—vikundi-vishawishi, wapigania-uhuru, magenge ya wahalifu, maharamia wa kimataifa, na wengineo—hufuatia mipango yake ya ubinafsi na huonekana kuwa na uwezo wa kuangamiza uwezekano wowote wa amani ulimwenguni vikitaka. Vikiwa kama wapangaji wenye mvurugo, vyaweza kufanya maisha ya wengine wote yawe yenye taabu.
Hata hivyo, kulingana na wafafanuzi wengi, vikundi vya upinzani au watu mmoja-mmoja wasiotawalika hawako peke yao katika kuzuia muungano wa ulimwengu. Lile taifa lenye kujitawala ndilo kizuizi kikubwa. Mataifa huru, asema mwandishi wa shughuli za vita, S. B. Payne, Jr., huwako katika “hali ya mchafuko wa kimataifa.” Hayo hufanya lolote lile ambalo hufaa zaidi masilahi yake ya kitaifa, kwa kujali kidogo au kutojali kabisa wengine. Tokeo ni kwamba, katika historia yote “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, chapa ya 1952.
Ni kweli, serikali fulani za kitaifa zimefaulu kwa kiasi fulani kupigana na ukosefu wa haki na uonevu, ndani ya mipaka ya maeneo yake na, kwa kiasi fulani, katika kiwango cha kimataifa. Pindi kwa pindi zimeanzisha kadiri fulani ya muungano wa kimataifa. Lakini hata wakati ambapo mataifa fulani yameungana ili kutenda dhidi ya taifa lenye uchokozi, mara nyingi shaka kwamba walitenda kutokana na kujipendeza wala si kutokana na kujali kikweli hali-njema ya wengine huendelea kuwako. Uhalisi ni kwamba serikali za kibinadamu hazina suluhisho kamili na lenye kudumu kwa ukosefu wa muungano ulimwenguni. Gwynne Dyer aeleza hivi: “Dhana ya kwamba mataifa yote ya ulimwengu yataungana pamoja ili kuzuia au kuadhibu uchokozi wa taifa-pinzani ni kanuni nzuri, lakini ni taifa au mataifa gani ambayo huamua taifa lenye uchokozi, na nani hulipia gharama za fedha na uhai ambazo huenda zikahitajiwa ili kulifanya hilo taifa-pinzani lenye uchokozi liuache?”
Bila shaka, uchokozi wa taifa lolote dhidi ya jingine wawezekana tu wakati ambapo raia walio wengi wa taifa hilo chokozi hawapingi uchokozi huo. Historia huonyesha tena na tena kwamba si katika “taifa-pinzani” fulani tu kwamba raia wametegemeza viongozi wao, wawe sawa au wasiwe sawa. Kwa hakika, wapangaji wa dunia walio wengi wamefanya hivyo. Wamefuata “uwongo, fitina na propaganda, bila kufikiri,” kama gazeti Time lilivyoeleza, zitokazo kwa viongozi wengi wa kisiasa na wa kidini.
Utukuzo wa taifa umewasha harara za watu ambao vinginevyo wangekuwa wenye kusababu na wenye huruma na umewasababisha kufanya uhalifu wa kinyama dhidi ya wanaume, wanawake, na watoto wa taifa jingine. Kwa kielelezo, kwa kurejezea Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mwanahistoria J. M. Roberts aeleza hivi: “Mojawapo ya mambo tata ya mwaka wa 1914 ni kwamba katika kila nchi idadi kubwa ya watu, wa vyama vyote, imani na ukoo, kwa kushangaza, waonekana kuwa wameenda vitani kwa kupenda na kwa furaha.” Je, watu wamejifunza somo tangu wakati huo? La! Uovu wa “kutukuza taifa bila kufikiri,” kama vile mwandishi wa habari Rod Usher alivyouita, waendelea kuharibu nafasi yoyote ile ya kuwa na muungano wa ulimwengu.
Kani Kutoka Nje Zafanya Kazi
Hata hivyo, kuna kizuizi kikubwa zaidi kwa muungano wa ulimwengu. Biblia hufunua kwamba kani kutoka nje zafanya kazi. Kani hizo zatambulishwa kuwa Shetani Ibilisi na vibaraka wake, roho waovu. Kulingana na Biblia, Shetani ni “mungu wa huu mfumo wa mambo [ambaye] amepofusha akili za wasioamini,” ili “habari njema yenye utukufu juu ya Kristo” isiwavutie.—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9.
Bila shaka, jambo hilo haliwaweki watu mmoja-mmoja huru na daraka la vitendo vyao wenyewe. Lakini laeleza ni kwa nini serikali za kibinadamu haziwezi kamwe kuanzisha ulimwengu wenye muungano kikweli. Maadamu Shetani Ibilisi aendelea kuwako, atawaathiri wanaume na wanawake wakuze zile ambazo Biblia huziita “kazi za mwili,” kutia na ‘uadui, zogo, magomvi na migawanyiko.’—Wagalatia 5:19-21.
Serikali ya Ulimwengu
Basi, suluhisho ni nini? Miaka ipatayo mia saba iliyopita, yule mshairi na mwanafalsafa Mwitalia aliyejulikana sana, Dante alionyesha jibu. Alitoa hoja kwamba serikali ya ulimwengu pekee ndio ingeweza kuhakikisha amani na muungano wa wanadamu. Kwa watu wengi tumaini la kuwa na serikali ya ulimwengu ya namna yoyote ni udanganyo tu, si jambo wawezalo kuwa na uhakika halisi nalo. “Serikali ya ulimwengu,” amalizia mtungaji, Payne, aliyetangulia kutajwa, “haiwezi kupatikana katika pindi hii ya historia.” Kwa nini? Kwa sababu ingeibidi serikali yoyote ya ulimwengu yenye kufaulu itoe uhakikisho kamili wa mambo mawili ambayo yaonekana kupita kabisa uwezo wa mwanadamu, yaani “serikali ya ulimwengu itakomesha vita na kwamba serikali ya ulimwengu haitakuwa mamlaka ya tufeni pote yenye kuonea.”
Ni jambo la hakika kwamba hakuna serikali ya kibinadamu itakayofanya hivyo wakati wowote. Hata hivyo, Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo waweza na utaondoa vita vyote. (Zaburi 46:9, 10; Mathayo 6:10) Kwa kweli, utaondoa wachochezi wa vita. Nabii Danieli huonyesha kwamba mwishoni mwa wakati uliowekwa na Mungu wa utawala wa kibinadamu juu ya dunia, utawala wa kibinadamu “[unge]kuwa ufalme uliogawanyika” kama “chuma [ambacho] kimechanganyika na udongo wa matope.” (Danieli 2:41-43) Hilo lingetokeza kuvunjika-vunjika kisiasa na mapambano yasiyoepukika. Na bado, Danieli asema kwamba Ufalme wa Mungu “utavunja falme [au serikali] hizi zote [zenye kufuatia utukuzo wa taifa na zisizo na muungano] vipande vipande,” ukisimamisha mahali pa hizo Ufalme wake mikononi mwa Yesu Kristo ambao umengojewa kwa muda mrefu.—Danieli 2:44.
Lingekuwa jambo la ubatili kutokeza mazingira yafaayo kwa watu ikiwa dunia ingeendelea kukaliwa na watu mmoja-mmoja wenye kupora ambao wangefuliza kufanya maisha yawe yenye taabu kwa wengine. Hata hivyo, “watenda mabaya wataharibiwa.” (Zaburi 37:1, 2, 9, 38; Mithali 2:22) Kwa sababu hiyo, Kristo ataondoa wote ambao hukataa viwango vya Mungu kwa kupenda au kuunga-mkono mamlaka za kilimwengu zenye machafuko. Atawaharibu wale wote wanaoharibu sayari hii. Mungu aahidi “kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18.
Hilo halitakuwa aina fulani ya uonevu wa tufeni pote. Yesu Kristo atatenda “kwa ajili ya kweli na upole na haki” atenganishapo wema na wabaya. (Zaburi 45:3, 4; Mathayo 25:31-33) Wala si tendo hasi na lenye kuharibu tu, utumizi mbaya wa mamlaka. La! Si kana kwamba jengo fulani zuri, la kihistoria litaharibiwa na mwendelezaji rasilimali mwenye pupa. Tendo hili litakuwa zaidi kama kuharibiwa kwa jengo ovyo lililooza ili kuandaa mazingira safi, yenye kupendeza.
Lakini namna gani juu ya kani za kutoka nje ambazo zimesababisha ukosefu huo wa muungano wakati uliopita? Je, zitakuwa huru kujipenyeza katika mfumo huo mpya hivi kwamba wakaaji wataanza upya ule utaratibu wenye kuharibu, kupigana na wakaaji wenzao na kufanya maisha yawe yenye taabu kwa kila mtu? Hakika sivyo. Kufukuzwa na kurekebishwa huko ni kwa mwisho na ni kamili. “Mateso hayatainuka mara ya pili.”—Nahumu 1:9.
Biblia hulinganisha kuharibiwa kwa mwisho kwa Shetani na kuteketezwa kwa takataka. Yasema kwamba “Ibilisi aliyekuwa aki[w]aongoza vibaya [wakaaji wa dunia] alivurumishwa ndani ya ziwa la moto na sulfa.” (Ufunuo 20:10) Ni ishara yenye nguvu kama nini! Wazia, uharibifu ambao haulinganishwi tu na chombo kidogo cha kuteketezea chenye uwezo mdogo tu bali walinganishwa na ziwa zima la moto, lenye kula kabisa na kuondoa kila kitu ambacho ni kiovu na chenye kuchafuliwa kisiweko. Hakuna yeyote, wala mwanadamu wala roho mwovu, atakayeruhusiwa kuendelea kufanya mambo ambayo hutisha utaratibu wa ulimwengu wote mzima, ambayo yavunja viwango vya Mungu vya mema na mabaya, au ambao husababisha maumivu kwa binadamu-mwenzi wao. Wote wenye kuharibu muungano watakuwa wameondolewa!—Zaburi 21:9-11; Sefania 1:18; 3:8.
Watu Wenye Muungano Kutoka Katika Mataifa Yote
Waokokaji wa usafishaji huo mkubwa watakuwa “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:9) Hawatagawanywa na tofauti za kitaifa na za kikabila. Watakuwa wamejifunza kuishi pamoja katika upatano wenye amani. (Isaya 2:2-4) Lililo la ajabu hata zaidi, waokokaji hao wataungwa na wapangaji wa hii sayari wa wakati uliopita watakaorudishwa kuwa wakaaji wa dunia iliyosafishwa kupitia uandalizi wa ajabu sana wa ufufuo.—Yohana 5:28, 29.
Je, ungependa kuishi katika ulimwengu kama huo? Wale tu ambao hushikamana sana na matakwa ya Mungu ndio watakaofanya hivyo, na matakwa yake yaonyeshwa wazi katika Biblia. (Yohana 17:3; Matendo 2:38-42) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze yale ambayo Mungu hutaka ili uweze kutumaini kuonea shangwe uhai milele katika ulimwengu wenye muungano kikweli.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Serikali mikononi mwa Yesu Kristo itatoa uhakikisho kamili wa ulimwengu wenye muungano