Onesiforo—Mfariji Jasiri
“WAWEKENI akilini wale walio katika vifungo vya gereza kama kwamba mmefungwa pamoja nao, na wale wanaotendwa vibaya.” (Waebrania 13:3) Mtume Paulo alipoandika maneno hayo wapata mwaka wa 61 W.K., yeye mwenyewe alikuwa tayari amefungwa kwa zaidi ya wakati mmoja na alikuwa afungwe tena kabla ya kifo chake akiwa mfia-imani. (Matendo 16:23, 24; 22:24; 23:35; 24:27; 2 Wakorintho 6:5; 2 Timotheo 2:9; Filemoni 1) Umuhimu ulikuwako wakati huo, kama ulivyoko sasa, kwa makutaniko kushughulikia waamini wenzao wanaopatwa na majaribu ya imani yao.
Mwanafunzi mmoja wa karne ya kwanza aliyekuwa mwangalifu hasa kwa uhitaji huo alikuwa Onesiforo. Alimzuru Paulo wakati wa kifungo chake cha pili huko Roma. Kumhusu, huyo mtume aliandika hivi: “Bwana na awaruhusu kuwa na rehema watu wa nyumbani mwa Onesiforo, kwa sababu mara nyingi aliniletea kiburudisho, naye hakuwa mwenye kuaibikia minyororo yangu. Kinyume chake, hilo, alipotukia kuwa huko Roma, alinitafuta kwa bidii yenye kuendelea na kunipata.” (2 Timotheo 1:16, 17) Je, umewahi kuchukua wakati ili kufikiria kwa uzito lile ambalo maneno hayo machache yamaanisha kwa kweli? Yaelekea kufanya hivyo kutaongeza uthamini wako kwa Onesiforo. Utaona kwamba alikuwa mfariji jasiri.
Kifungo cha Pili cha Paulo
Baada ya kufunguliwa kutoka kifungo chake cha kwanza, Paulo alikuwa katika jela la Roma tena lakini akiwa chini ya hali tofauti. Wakati wa kifungo chake cha kwanza, marafiki wake waliweza kumfikia katika nyumba yake mwenyewe iliyopangishwa, na alionekana mwenye hakika kwamba kufunguliwa kulikuwa karibu. Sasa akiwa ameachwa na walio wengi, kufia imani kulionekana kama kwakaribia.—Matendo 28:30; 2 Timotheo 4:6-8, 16; Filemoni 22.
Wakati huo Paulo alikuwa gerezani wapata mwaka wa 65 W.K. Karibu mwaka mmoja mapema—Julai 64 W.K.—moto ulikumba Roma, ukisababisha uharibifu mkubwa sana katika maeneo 10 kati ya maeneo 14 ya jiji. Kulingana na Tacitus mwanahistoria Mroma, Maliki Nero alishindwa “kufutilia mbali ile itikadi yenye kusumbua kwamba huo moto mkubwa ulikuwa tokeo la agizo fulani. Kwa sababu hiyo, ili aepuke tangazo hilo baya juu yake mwenyewe, Nero aliishtaki na kuitesa vikali zaidi jamii iliyochukiwa kwa sababu ya matendo yake yenye kuchukiza, ambayo watu wa kawaida waliiita Wakristo. . . . Vifo vyao vilitekelezwa katika njia yenye madharau sana. Wakiwa wamefunikwa ngozi za hayawani, waliraruliwa na mbwa na kuangamia, au walipigiliwa misumari misalabani, au wakahukumiwa kutupwa kwenye miali na kuchomwa, ili watumike wakiwa mmuliko wakati wa usiku, nuru ya mchana ilipoisha.”
Ilikuwa ni katika hali kama hiyo na kukiwa na matazamio hayohayo kwamba Paulo alijikuta gerezani tena. Haishangazi kwamba alishukuru sana kwa sababu ya ziara za rafiki yake Onesiforo! Lakini acheni tutazame hali hiyohiyo kwa maoni ya Onesiforo.
Kumzuru Paulo Mfungwa
Yaonekana, familia ya Onesiforo iliishi huko Efeso. (2 Timotheo 1:18; 4:19) Haielezwi kama Onesiforo alikuwa amekuja kwenye jiji kuu la hiyo milki kwa shughuli zake mwenyewe au alikuja kihususa kumzuru Paulo. Kwa vyovyote, huyo mtume alisema hivi: ‘Alipotukia kuwa katika Roma, mara nyingi Onesiforo aliniletea kiburudisho.’ (2 Timotheo 1:16, 17) Kiburudisho cha aina gani? Ingawa huenda ikawa msaada wa Onesiforo ulitia ndani kusaidia kimwili, kwa wazi kuwapo kwake kulitumika pia kukiwa dawa ya kumwimarisha na kumtia moyo Paulo. Kwa hakika, tafsiri fulani husomeka hivi: “Mara nyingi alinichangamsha,” au “mara nyingi amenifariji.”
Kutimiza tamaa ya kumzuru mfungwa Mkristo katika Roma wakati huo kulitokeza magumu. Tofauti na siku za kifungo cha Paulo cha kwanza, kwa wazi Wakristo Waroma walikuwa wameshindwa kumpata. Katika jiji kubwa kama Roma, halikuwa jambo rahisi kumpata mfungwa mmoja asiye mashuhuri miongoni mwa hesabu kubwa ambayo lazima ilikuwa imefungwa kwa makosa mbalimbali. Kwa sababu hiyo, utafutaji wenye bidii yenye kuendelea ulihitajika. Msomi Giovanni Rostagno afafanua mambo kwa njia hii: “Huenda ikawa magumu yalikuwa ya namna nyingi. Zaidi ya yote, busara isiyo na kifani ilihitajika katika huo utafutaji. Huenda ikawa kukusanya habari hapa na pale na kuonekana kuwa na hangaiko la kupata jela ambalo lilimzuilia mfungwa shupavu wa zamani aliyehusika katika uhalifu mwingi sana kuliamsha kushuku kusikostahili.”
Mwandishi P. N. Harrison afafanua waziwazi hali hiyohiyo, akisema hivi: “Yaonekana kuwa twaona kidogo tu uso mmoja wenye kusudi miongoni mwa umati wenye kutembea kwa miguu, na kwa upendezi ulioamshwa twamfuata mtu huyu asiyejulikana kutoka pwani za mbali za Bahari ya Aegea, azungukapo kupitia njia za mzingo za barabara asizozijua, akibisha milango mingi, akifuatilia kila kidokezi, akiwa ameonywa juu ya kujihatarisha lakini akiwa ameazimia asiache utafutaji wake; hadi katika gereza fulani isiyo dhahiri ambapo sauti aijuayo yamsalimia, na amtambua Paulo akiwa amefungwa kwenye askari-jeshi Mroma kwa minyororo.” Ikiwa mahali hapo palikuwa kama jela za Roma, yamkini palikuwa mahali penye baridi, giza, na pachafu, ambapo palikuwa na wingi wa minyororo na wa taabu za kila namna.
Lilikuwa jambo hatari kutambuliwa kuwa rafiki wa mfungwa kama Paulo. Lilikuwa jambo hatari hata zaidi kufuliza kumzuru. Kujitambulisha waziwazi kuwa Mkristo kulikuwa ni kujihatarisha kukamatwa na kuuawa kwa kuteswa. Lakini Onesiforo hakuridhika na kumzuru mara moja au mara mbili. Wala hakuaibikia wala kuogopa kufanya hivyo “mara nyingi.” Kwa kweli Onesiforo aliishi kulingana na maana ya jina lake, “Mchukuzi wa Faida,” akiandaa msaada wenye ujasiri na wenye upendo kujapokuwa hatari mbalimbali.
Kwa nini Onesiforo alifanya hayo yote? Brian Rapske asema hivi: “Gereza lilikuwa si mahali pa kuteseka kimwili tu, bali pia mahali pa hangaiko kubwa kwa sababu ya mikazo lililomletea mfungwa. Katika mazingira kama hayo, kule kuwapo kimwili na vitia-moyo vya maneno vya wasaidiaji vingeweza kumsaidia mfungwa kihisia-moyo.” Kwa wazi, Onesiforo aling’amua hayo na kwa ujasiri akashikamana na rafiki yake. Lazima Paulo alithamini msaada huo kama nini!
Ni Nini Lililompata Onesiforo?
Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo aliwapelekea watu wa nyumbani mwa Onesiforo salamu na kusema hivi juu yake: “Bwana na amruhusu kupata rehema kutoka kwa Yehova katika siku ile.” (2 Timotheo 1:18; 4:19) Wengi hufikiri kwamba hayo maneno “katika siku ile” yarejezea siku ya Mungu ya hukumu na hivyo kukata kauli kwamba Onesiforo alikuwa amekufa. Ikiwa ilikuwa hivyo, labda “Onesiforo alikuwa amejasiria kuingia ndani ya makazi haya na huenda ikawa alikamatwa wakati wa ziara yake ya mwisho, na kulipia . . . adhabu kwa maisha yake,” adokeza P. N. Harrison. Bila shaka, huenda ikawa Onesiforo alikuwa mbali na nyumbani tu, au huenda ikawa Paulo alimtia ndani katika salamu alizoipelekea nyumba yake nzima.
Watu fulani huamini kwamba kuna maana ya pekee katika taarifa hii: “Bwana na amruhusu kupata rehema kutoka kwa Yehova katika siku ile.” Wao huhisi kwamba maneno hayo hutetea uhalali wa sala za kuomba kwa niaba ya nafsi zilizoondoka ambazo zinaishi na labda kuteseka katika makao fulani ya kiroho. Hata hivyo, wazo kama hilo lahitilafiana na lile fundisho la Kimaandiko kwamba wafu hawajui neno lolote. (Mhubiri 9:5, 10) Hata ikiwa Onesiforo alikuwa amekufa, Paulo alikuwa tu akionyesha matamanio kwamba rafiki yake angepata rehema kutoka kwa Mungu. “Tuna haki ya kuwaonyesha watu wote matamanio hayo,” asema R. F. Horton. “Lakini kuwaombea wafu, na kuwatolea Misa, ni wazo ambalo liko mbali sana na akili ya [mtume].”
Acheni Tuwe Wafariji Wenye Uaminifu-Mshikamanifu
Iwe kwa hakika Onesiforo alipoteza uhai wake alipokuwa akimsaidia Paulo au la, bila shaka aliuhatarisha ili kumpata huyo mtume na kumzuru gerezani. Hakuna shaka kwamba Paulo alithamini tegemezo na kitia-moyo chenye kuhitajiwa sana alichopata kutoka kwa Onesiforo.
Wakristo wenzetu wapatwapo na jaribu, mnyanyaso, au kifungo, huenda tukaweza kuwafariji na kuwatia moyo. Kwa hiyo na tusali kwa niaba yao na kufanya kwa upendo yote tuwezayo ili kuwasaidia. (Yohana 13:35; 1 Wathesalonike 5:25) Kama Onesiforo, na tuwe wafariji jasiri.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Onesiforo alimfariji kwa ujasiri mtume Paulo aliyekuwa gerezani