Ni Nini Linalowapata Vijana?
HABARI njema au habari mbaya—wataka kusikia ipi kwanza? Waulizwapo swali hilo, watu wengi huchagua kusikia habari mbaya kwanza wakitarajia kwamba habari njema zitadumu akilini.
Tuchunguzapo linalowapata vijana, fikiria kwanza hali ya sasa. Kwa kawaida watu wenye umri mkubwa zaidi hueleza kwamba vijana leo si kama vijana wa wakati uliopita. Kwa upande ule mwingine, vijana huonea uchungu dokezo lolote la kwamba hawafikii viwango vya mwaka-jana. Hata hivyo, wachunguzaji makini wa jamii ya binadamu hukubali kwamba vijana wa leo wako tofauti.
Tofauti Jinsi Gani?
Ingawa watu kwa ujumla huamini kwamba vijana wapaswa kuwa na adabu nzuri, kuwa na hisi ya kuchukua madaraka, na kuwastahi wengine, mara nyingi uhalisi haufikii hayo. Kulingana na uchunguzi uliochapishwa katika gazeti la habari The Independent la London, vijana “[wana]kuza ‘roho mpya ya uasi’ dhidi ya ulimwengu ambao waona kuwa umewatamausha sana.” “Roho [hiyo] mpya ya uasi” yaonekana katika matokeo ya uchunguzi yaonyeshayo kwamba vijana wengi zaidi wa siku ya kisasa hawataki kujiona kuwa “wenye busara na wenye kuchukua madaraka.” Afadhali waonwe kuwa “wasiotulia na wasiotabirika.”
Kwa kielelezo, katika Uingereza, uhalifu uliorekodiwa—ambao mwingi wake ulifanywa na vijana—uliongezeka mara kumi kati ya mwaka wa 1950 na mwaka wa 1993. Ongezeko la matumizi mabaya ya dawa na alkoholi lafanana na ongezeko la uhalifu. Wakati uleule, lasema gazeti The Times la London, karibu nchi zote ambazo zimesitawi zimeona “maongezeko makubwa katika miparanganyo ya kisaikolojia na ya kijamii miongoni mwa vijana tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili.” Kulingana na David J. Smith, profesa wa elimu-jinai, miparanganyo hiyo “[hai]husiani na hali ya uhitaji au ukwasi wenye kuongezeka katika njia yoyote sahili.” Utafiti waonyesha kwamba tofauti kubwa zaidi sasa ni dhahiri kati ya vijana na watu wenye umri mkubwa zaidi.
Leo watoto na matineja wachanga hukabili mkazo unaoongezeka. Visa vya kujaribu au kufanikiwa kujiua, vimekuwa mambo ya kawaida. Majaribio ya kujiua ya watoto wenye umri wa chini ya miaka 12 yaliongezeka maradufu kwa muda unaopungua miaka kumi, laripoti gazeti Herald la Glasgow, Scotland. Watoto wenye umri mkubwa zaidi huruhusu kukata tumaini kuwachochee kujiua. Hilo gazeti laeleza hivi: “Majaribio ya kujiua ni matokeo mabaya zaidi ya kuongezeka kwa matatizo ya kiakili katika vijana yanayoelekea sana kushinda msaada wanaotolewa.”
Ni Nani Mwenye Lawama?
Watu wazima huona likiwa jambo rahisi kuwalaumu vijana kwa sababu ya maoni ya vijana “yaliyopotoka.” Hata hivyo, kusema kweli kabisa, je, watu wazima hawana sehemu kubwa ya lawama kwa sababu ya yale yanayotukia leo miongoni mwa vijana? Kukandamizwa na marika, kupuuzwa na wazazi, kukosekana kwa vigezo vya kuiga ambavyo vijana waweza kutumaini, ni mambo ambayo hutajwa mara nyingi kuwa sababu ya tabia iliyopotoka ya vijana. “Mshuko-moyo wa watu kwa ujumla uko vilevile ulivyokuwa miaka 30 iliyopita,” adai Profesa Sir Michael Rutter, mkuu wa Medical Research Council Child Psychiatry Unit ya Uingereza. “Lakini,” aongeza kusema hivi, “kutukia kwa mshuko-moyo miongoni mwa matineja na vijana kumeongezeka sana. . . . Bila shaka kuvunjika kwa familia huchangia; si talaka tu, lakini viwango vya kawaida vya kutopatana na kupambana miongoni mwa watu wazima.”
Mtafiti mmoja adai kwamba vijana “[wana]kataa desturi.” Kwa nini? “Kwa sababu njia za kidesturi hazitumiki tena kamwe.” Kwa kielelezo chukua maoni yanayobadilika ya madaraka ya kijinsia. Wanawake wengi vijana wakubali vitabia vilivyo vya kiume zaidi vya uchokozi wa kutumia nguvu na vya ujeuri, huku wanaume vijana wakikubali vitabia vya kike. Jinsi ilivyo tofauti na kawaida za wakati uliopita!
Lakini kwa nini twaona mabadiliko haya makubwa sasa? Na kuna habari njema gani kuhusu vijana leo? Vijana waweza kuwaje na wakati ujao salama? Makala yetu inayofuata yachunguza majibu ya maswali hayo.