Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 3/1 kur. 4-7
  • Kwa Nini Yanaomba Msamaha?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Yanaomba Msamaha?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Muungano wa Kidini na Msimamo wa Kiadili
  • Si Wote Wakubalio
  • Hukumu ya Kimungu
  • Makanisa Yaungama
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Je, Kuna ‘Kanisa Moja Tu la Kweli’?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kanisa—Mabadiliko na Mvurugo
    Amkeni!—1993
  • Vatikani 2—Baraka au Laana?
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 3/1 kur. 4-7

Kwa Nini Yanaomba Msamaha?

LILE wazo la kwamba makanisa yapaswa kutubu makosa yao na kujirekebisha yenyewe si jipya. Kamusi Religioni e miti (Dini na Ngano) ya kidini, yasema kwamba ule ushikamanifu-maadili udhaniwao wa kanisa la mapema ulipendeza watu wakati wa Enzi za Kati na uliwaongoza watu wengi waombe marekebisho ya kidini.

Mwaka wa 1523, baada ya Martin Luther kutengana na Roma, Papa Adrian wa Sita alijaribu kuleta muungano kwa kupeleka ujumbe huu kwenye Mkutano wa Kujadili Mashauri ya Kikanisa wa Nuremberg: “Twajua vema kwamba kwa miaka mingi mambo yastahiliyo kukirihiwa yamekusanyika kuzunguka yale Makao ya Papa . . . Tutatumia bidii yote yenye kuendelea ili kurekebisha kwanza kabisa Curia (Baraza la makutaniko, mahakimu, na ofisi ambazo kupitia hizo papa hutawala Kanisa Katoliki) ya Kiroma, ambayo, labda, ndiyo chanzo cha maovu yote haya.” Hata hivyo, kukubali huko, hakukufaulu katika kuponya ule mtengano wala katika kukabili ufisadi katika Curia ya kipapa.

Majuzi zaidi makanisa yamechambuliwa kwa sababu ya kunyamaza kwao kuhusiana na yale Maangamizi Makubwa. Pia yamelaumiwa kwamba hayawazuii washiriki wake wasishiriki katika vita. Mwaka wa 1941, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa ikipamba moto, kasisi aliyeitwa Primo Mazzolari aliuliza hivi: “Kwa nini Roma haijaitikia kwa nguvu kule kuvunjika kwa Ukatoliki kama ilivyokuwa ikifanya, na bado ina desturi ya kufanya hivyo, katika visa vya mafundisho yenye hatari ndogo zaidi?” Mafundisho yenye hatari ndogo zaidi kuliko nini? Huyo kasisi alikuwa akizungumza juu ya utukuzo wa taifa uchocheao vita ambao wakati huo ulikuwa ukiharibu ustaarabu.

Hata hivyo, uhakika ni kwamba hadi majuzi sana, kukubali hatia kwa dini mbalimbali kulikuwa jambo lisilo la kawaida. Mwaka wa 1832, kwa kuitikia watu fulani waliokuwa wakilihimiza Kanisa Katoliki ‘lijiongoe,’ Gregory wa 16 alisema hivi: “Kwa wazi ni jambo la kipuuzi na baya kupendekeza aina fulani ya ‘rekebisho au wongofu’ kwa ajili ya usalama na ukuzi [wa kanisa], kana kwamba lingeweza kuonwa kuwa lenye kasoro.” Namna gani kasoro zilizokuwa mbaya sana zisiweze kukanika? Mikakati mbalimbali ilitwaliwa ili kutolea udhuru kasoro hizo. Kwa mfano, wanatheolojia fulani wameshikilia kwamba kanisa ni takatifu na pia lenye dhambi. Hilo shirika lenyewe lasemwa kuwa takatifu—Mungu akiwa amelihifadhi kutokana na kosa. Hata hivyo, washiriki wake ni wenye dhambi. Hivyo, maovu yafanywapo katika jina la kanisa, hilo shirika lenyewe halipasi kulaumiwa, bali watu mmoja-mmoja waliomo katika hilo kanisa ndio wapasao kulaumiwa. Je, hilo lasikika kuwa lenye kupatana na akili? Halisikiki hivyo kwa Hans Küng, mwanatheolojia wa Katoliki ya Kiroma, aliyeandika hivi: “Hakuna Kanisa kamilifu linaloelea juu ya ulimwengu wa kibinadamu.” Alieleza hivi: “Kanisa lisilo na dhambi za kuungama haliko.”

Muungano wa Kidini na Msimamo wa Kiadili

Huenda ukajiuliza ni matukio gani ambayo yameyaongoza makanisa kuomba msamaha sasa. Mwanzoni, Waprotestanti na Waothodoksi walikubali lawama kwa sababu ya “migawanyiko ya wakati uliopita” miongoni mwa madhehebu tofauti-tofauti. Walifanya hilo kwenye “Imani na Utaratibu,” mkutano wa muungano wa kidini uliofanywa Lausanne, Uswisi, mwaka wa 1927. Kanisa la Katoliki la Kiroma lilifuata kielelezo hicho hatimaye. Hasa tangu wakati huo Vatikani la Pili,a maaskofu wa cheo cha juu, kutia ndani na mapapa, wameomba msamaha kwa ukawaida wenye kuongezeka kwa sababu ya migawanyiko ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa kusudi gani? Yaonekana wanataka muungano zaidi katika Jumuiya ya Wakristo. Mwanahistoria Mkatoliki Nicolino Sarale alitaarifu kwamba katika “mradi [wa John Paul wa Pili] wa ‘maungamo,’ kuna mkakati, nao ni muungano wa kidini.”

Hata hivyo, mengi zaidi ya muungano wa kidini yahusishwa. Leo, historia yenye sifa mbaya ya Jumuiya ya Wakristo yajulikana sana. “Ukatoliki hauwezi kuipuuza tu historia yote hiyo,” asema mwanatheolojia Hans Urs von Balthasar. “Kanisa lake mwenyewe limefanya au limeruhusu kufanywa kwa mambo ambayo bila shaka hatuwezi kuyakubali siku hizi.” Kwa sababu hiyo, papa ameweka tume ya “kueleza rekodi mbovu ya kanisa ili . . . msamaha uweze kuombwa.” Basi, sababu nyingine ya kanisa kunuia kushiriki katika kujichambua yaonekana kuwa tamaa ya kupata tena msimamo wake wa kiadili.

Vivyo hivyo, mwanahistoria Alberto Melloni, akieleza juu ya ombi la kanisa la kutaka msamaha, aandika hivi: “Kihalisi, liombwalo wakati mwingine ni kuahirisha mashtaka ya lawama.” Ndiyo, Kanisa Katoliki laonekana kuwa lajaribu kupuuza ule mzigo wenye kulemea wa dhambi za wakati uliopita ili lipate tena ustahilifu wake katika mahakama ya kauli ya watu wote. Ingawa hivyo, kwa kufuatia haki lazima isemwe kwamba laonekana kuhangaikia zaidi kufanya amani na ulimwengu badala ya kufanya amani na Mungu.

Tabia hiyo hutukumbusha Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli. (1 Samweli 15:1-12) Alitenda kosa lenye kuhuzunisha, nalo lilipofunuliwa, kwanza alijaribu kujitetea—kutoa udhuru wa kosa lake—kwa Samweli, nabii mwaminifu wa Mungu. (1 Samweli 15:13-21) Hatimaye, mfalme alilazimika kukiri hivi kwa Samweli: “Nimefanya dhambi; maana nimeihalifu amri ya BWANA.” (1 Samweli 15:24, 25) Ndiyo, alikubali kosa lake. Lakini maneno yake yafuatayo kwa Samweli yafunua kilichokuwa cha kwanza kabisa akilini mwake: “Nimekosa; lakini uniheshimu sasa, nakuomba, mbele ya wazee wa watu wangu, na mbele ya Israeli.” (1 Samweli 15:30) Kwa wazi, Sauli alihangaikia zaidi msimamo wake katika Israeli kuliko kupatanishwa na Mungu. Mtazamo huo haukutokeza msamaha wa Mungu kwa Sauli. Je, wafikiri mtazamo huohuo utatokeza msamaha wa Mungu kwa makanisa?

Si Wote Wakubalio

Si wote wakubalio kwamba makanisa yapaswa kuomba msamaha waziwazi. Kwa kielelezo, idadi fulani ya washiriki wa Katoliki ya Kiroma huhisi kutostarehe wakati ambapo papa wao huomba msamaha kwa sababu ya utumwa au awarudishiapo sifa njema “wazushi” kama vile Hus na Calvin. Kulingana na vyanzo vya Vatikani, hati iliyopelekwa kwa makadinali ikipendekeza “uchunguzi wa dhamiri” katika historia ya Ukatoliki ya mileani iliyopita ilichambuliwa na makadinali waliokuwa wakihudhuria baraza la papa na makadinali lililofanywa Juni 1994. Hata hivyo papa alipotaka kutia ndani sehemu ya msingi ya pendekezo hilo katika waraka wa papa, kadinali Mwitalia Giacomo Biffi alitoa taarifa ya pasta ambamo alithibitisha: “Kanisa halina dhambi yoyote.” Hata hivyo, alikubali hivi: “Kuomba msamaha kwa sababu ya makosa ya kanisa ya karne zilizopita . . . kwaweza kutumika kutufanya tuwe wenye kukubalika zaidi.”

“Kuungama dhambi ni mojawapo ya habari yenye kubishaniwa zaidi katika Kanisa Katoliki,” asema mwelezaji wa Vatikani Luigi Accattoli. “Papa akikiri makosa ya wamishonari, kuna wamishonari ambao hupinga hilo kwa nia njema.” Zaidi, mwandishi wa habari wa Katoliki ya Kiroma aliandika hivi: “Ikiwa kwa kweli papa ana wazo lenye kuhofisha hivyo juu ya historia ya Kanisa, ni vigumu kuelewa jinsi yeye awezavyo kulionyesha Kanisa lilo hilo kuwa mhusika mkuu mwenye kutokeza wa ‘haki za kibinadamu,’ ‘mama na mwalimu’ ambaye yeye peke yake aweza kuongoza jamii ya binadamu kuingia katika mileani ya tatu yenye matumaini mema kwelikweli.”

Biblia huonya dhidi ya wonyesho wa nje wa toba ambao huchochewa na aibu tu ya kupatikana katika kosa. Kwa kawaida aina hiyo ya toba haiongozi kamwe kwenye badiliko la muda mrefu la mwenye kutubu. (Linganisha 2 Wakorintho 7:8-11.) Toba yenye thamani machoni pa Mungu huandamana na “matunda yafaayo toba”—yaani, uthibitisho wa toba ya weupe wa moyo.—Luka 3:8.

Biblia husema kwamba mwenye kutubu na kuungama lazima aache matendo maovu, aache kuyafanya. (Mithali 28:13) Je, hilo limetendeka? Baada ya maungamo yote ya makosa yaliyofanywa na Kanisa Katoliki la Kiroma na makanisa mengine, ni nini kilichotokea katika zogo za wenyewe kwa wenyewe za hivi majuzi katika Afrika ya kati na Ulaya Mashariki, ambako idadi kubwa ya “Wakristo” ilihusika? Je, makanisa yalitenda yakiwa kani ya kuleta amani? Je, viongozi wao wote walisema kwa muungano dhidi ya maovu ambayo washiriki wao walikuwa wakitenda? La. Kwani, baadhi ya wahudumu wa kidini hata walishiriki katika uchinjaji huo!

Hukumu ya Kimungu

Katika kusema juu ya maungamo ya papa ya kurudia-rudia, Kadinali Biffi aliuliza hivi kwa kukejeli: “Kwa ajili ya dhambi za kihistoria, je, haingekuwa afadhali kwetu sote kungojea hukumu ya ulimwengu wote mzima?” Hukumu ya wanadamu wote inakaribia. Yehova Mungu ajua vema matukio yote maovu katika historia ya dini. Upesi vya kutosha, atawatoza hesabu wenye hatia. (Ufunuo 18:4-8) Kwa sasa, je yawezekana kupata aina ya ibada isiyotiwa doa na hatia ya damu, kutovumilia kwenye kuua kimakusudi, na uhalifu mwingine mbalimbali ambao makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanaomba radhi kwa sababu yake? Ndiyo.

Twaweza kufanyaje hivyo? Kwa kutumia kanuni iliyotaarifiwa na Yesu Kristo: “Kwa matunda yao mtawatambua.” Rekodi ya historia, ambayo dini fulani zingependa isahaulike, hutusaidia kutambulisha wale ambao Yesu aliwaita “manabii wasio wa kweli” na pia wale ambao wametokeza “matunda bora.” (Mathayo 7:15-20) Hao ni nani? Twakualika ujigundulie kwa kuichunguza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Pata kuona ni nani leo wanaojaribu kufuata Neno la Mungu badala ya kutafuta kudumisha msimamo wenye uvutano ulimwenguni.—Matendo 17:11.

[Maelezo ya Chini]

a Baraza la 21 la muungano wa kidini lilikutana katika vipindi vinne huko Roma kuanzia 1962-1965.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Makanisa yanaomba radhi kwa kusababisha maovu kama hili

[Hisani]

The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki