Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
“Watu Wako Wanajitoa kwa Hiari”
NAAMANI, amiri jeshi Msiria mwenye uweza ana ukoma. Usipotibiwa, ugonjwa huo wenye kuchukiza waweza kuumbua na hata kusababisha kifo. Naamani apaswa kufanya nini? Miongoni mwa walio wa nyumbani mwa Naamani mna msichana mdogo, ‘mfungwa kutoka nchi ya Israeli.’ Msichana huyo asema kwa ujasiri na kumtambulisha Elisha kuwa mmoja awezaye kumponya Naamani.—2 Wafalme 5:1-3.
Kwa sababu ya msimamo wenye ujasiri wa msichana huyo, Naamani amtafuta Elisha naye aponywa. Zaidi ya hayo, Naamani apata kuwa mwabudu wa Yehova! Jambo hilo lililoonwa, ambalo limerekodiwa katika Biblia, lilitukia karne ya kumi K.W.K. (2 Wafalme 5:4-15) Leo, vijana wengi huonyesha ujasiri huohuo wasemapo kwa niaba ya masilahi ya Ufalme. Jambo lililoonwa lifuatalo kutoka Msumbiji lathibitisha hilo.
Nuno mwenye umri wa miaka sita ni mhubiri asiyebatizwa wa habari njema. Hata kabla hajawa mhubiri asiyebatizwa, Nuno alikuwa akiwakusanya watoto katika ujirani wake, atoe sala, na kuwafundisha Biblia, akitumia kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.
Mara nyingi Nuno huamka mapema asubuhi ya Jumamosi na kuikumbusha familia yake hivi: “Leo twaenda katika huduma ya shambani.” Bidii yake kwa ajili ya huduma yaonekana katika njia nyingine pia. Aandamanapo na wazazi wake katika huduma ya barabarani huko Maputo, mara nyingi Nuno huwafikia watu yeye mwenyewe. Kwenye pindi moja kama hiyo, mfanya-biashara alimfikia na kumwuliza: “Kwa nini unauza magazeti haya?” Nuno alijibu hivi: “Siyauzi magazeti, lakini nakubali michango ya kusaidia kulipia gharama za kazi ya kuhubiri.” Huyo mfanya-biashara aliitikia hivi: “Ingawa sipendezwi, navutiwa na mtazamo wako. Ningependa kuchangia kazi hii.”
Kwenye pindi nyingine, Nuno alimfikia mwanamume barabarani na kumtolea kitabu Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje? Huyo mwanamume aliuliza hivi: “Je, wewe husomei kwenye shule ile pale?” “Ndiyo,” Nuno akajibu, “mimi husomea shule hiyo, lakini leo natoa ujumbe muhimu kutoka katika kitabu hiki. Chakuonyesha kwamba waweza kuishi katika ulimwengu mpya ambao Mungu ataleta, kama ionyeshwavyo katika picha kwenye kitabu hiki.” Nuno hakutambua kwamba mwanamume aliyekuwa akizungumza naye alikuwa mwalimu katika shule yake. Huyo mwalimu alikikubali hicho kitabu na sasa yeye hupokea kwa ukawaida Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kutoka kwa Nuno.
Nuno aulizwapo ni kwa nini yeye hupenda kushiriki katika kazi ya kuhubiri, yeye husema hivi: “Nataka kusema na watu na kuwafundisha juu ya Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo.” Huongeza kusema hivi: “Na ikiwa hao watu hawataki kusikiliza, hakuna haja ya kukasirika.”
Ulimwenguni pote, maelfu ya vijana kama Nuno ‘hujitoa kwa hiari’ ili kufundisha na kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu. (Zaburi 110:3) Lakini hilo halitukii tu. Wazazi wawafundishao watoto wao juu ya Yehova tangu utoto sana, wawekao kielelezo kizuri katika huduma, na kufuatia masilahi ya Ufalme kwa bidii watathawabishwa sana.