Waweza Kufanya Maendeleo ya Kiroho
THAMANI ya kweli yaweza kuwa ngumu kuitambua. Hivyo ndivyo almasi zilivyo. Ingawa almasi iliyong’arishwa humetameta, almasi ambayo haijang’arishwa hutoa mng’aro hafifu. Hata hivyo, ni wazi kwamba kito kizuri chaweza kupatikana katika sehemu ya ndani kabisa ya almasi ambayo haijang’arishwa.
Wakristo hufanana na almasi ambazo hazijang’arishwa katika njia nyingi. Ingawa tuko mbali na ukamilifu, tuna thamani ya ndani ambayo Yehova huthamini. Kama almasi, sote tuna sifa zetu wenyewe zilizo tofauti. Na kila mmoja wetu aweza kufanya maendeleo ya kiroho, ikiwa hiyo ndiyo tamaa yetu ya kuhisiwa moyoni. Nyutu zetu zaweza kung’arishwa, ili zing’ae kwa wangavu zaidi kwa utukufu wa Yehova.—1 Wakorintho 10:31.
Baada ya kukatwa na kung’arishwa, almasi huwekwa katika kifaa cha kuiunda ambacho huongeza ubora wake wa kurudisha nuru. Vivyo hivyo, Yehova aweza kututumia katika hali, au migawo tofauti ikiwa “[tutavaa] utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—Waefeso 4:20-24.
Huenda isiwe rahisi kufanya maendeleo ya kiroho kama hayo, kama vile ilivyo nadra kwa almasi ambayo haijang’arishwa, kumetameta kama kito. Huenda tukahitaji kujiondolea udhaifu fulani wa muda mrefu, kurekebisha mtazamo wetu kuelekea kuchukua daraka, au hata kujikakamua kutoka katika hali ya kutofanya maendeleo ya kiroho. Lakini twaweza kufanya maendeleo ya kiroho ikiwa kwa kweli twataka kufanya hivyo, kwa kuwa Yehova Mungu aweza kutupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.”—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13.
Yehova Huwaimarisha Watumishi Wake
Kukata almasi huhitaji uhakika ambao hutokana na ujuzi barabara, kwa kuwa mara sehemu ya almasi ambayo haijang’arishwa ikatwapo, kwa kawaida, hiyo hupotea. Sehemu yenye thamani kubwa—nyakati nyingine kufikia asilimia 50 ya jiwe ambalo halijakatwa—lazima ikatwe ili kutokeza muundo uhitajiwao. Sisi pia twahitaji uhakika unaotokana na ujuzi sahihi ili kuunda utu wetu na kufanya maendeleo ya kiroho. Lazima hasa tuwe na uhakika kwamba Yehova atatupa nguvu.
Hata hivyo, huenda tukahisi tumepungukiwa, au tukafikiri kwamba hatuwezi kufanya zaidi. Watumishi waaminifu wa Mungu wa zamani, walihisi hivyo nyakati nyingine. (Kutoka 3:11, 12; 1 Wafalme 19:1-4) Mungu alipompa mgawo wa kuwa “nabii wa mataifa,” Yeremia alisema hivi kwa mshangao: “Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” (Yeremia 1:5, 6) Ingawa hivyo, licha ya unyamavu wake, Yeremia alipata kuwa nabii mwenye ujasiri, aliyewatolea watu wenye uhasama ujumbe mbalimbali ulio wazi. Hilo liliwezekanaje? Alijifunza kumtegemea Yehova. Yeremia aliandika hivi baadaye: “Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea BWANA, ambaye BWANA ni tumaini lake.”—Yeremia 17:7; 20:11.
Hali kadhalika leo, Yehova huwaimarisha wale wenye kumtumaini. Edward,a baba ya watoto wanne, aliyefanya maendeleo ya kiroho polepole, alipata jambo hilo kuwa kweli. Yeye aeleza hivi: “Nilikuwa nimekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka tisa, lakini nilionekana kutofanya maendeleo yoyote ya kiroho. Tatizo lilikuwa kwamba, sikuchochewa sana na sikuwa na uhakika wowote. Baada ya kuhamia Hispania, nilijikuta katika kutaniko dogo ambalo lilikuwa na mzee mmoja tu na mtumishi wa huduma mmoja. Kwa sababu ya huo uhitaji, huyo mzee aliniomba nishughulikie migawo mingi. Nilitetemeka nilipotoa hotuba zangu za kwanza na sehemu za mikutano. Hata hivyo, nilijifunza kumtegemea Yehova. Huyo mzee alinipongeza sikuzote na kunitolea madokezo yenye busara ili nifanye maendeleo.
“Wakati huohuo, niliongeza utendaji wangu wa utumishi wa shambani na kuiongoza familia yangu vyema zaidi kiroho. Tokeo ni kwamba, kweli ilikuwa yenye maana kubwa zaidi kwa familia yote, na nilihisi kuwa nimeridhika zaidi. Sasa mimi ni mtumishi wa huduma, na ninafanya kazi kwa bidii ili kusitawisha sifa za mwangalizi Mkristo.”
“Uvueni Utu wa Zamani”
Kama Edward alivyong’amua, maendeleo ya kiroho huhitaji kumtumaini Yehova. Kusitawisha “utu mpya” ulio kama wa Kristo, pia ni muhimu. Hilo laweza kufanywaje? Hatua ya kwanza ni ‘kuvua’ tabia zile ambazo ni sehemu ya utu wa zamani. (Wakolosai 3:9, 10) Sawasawa na kasoro, kama vile madini yanayokuwa upande wa nje wa almasi, yanavyohitaji kuondolewa ili kuifanya iwe kito chenye kumetameta, ndivyo ambavyo mitazamo ‘iliyo ya ulimwengu’ ihitajiwavyo kutupiliwa mbali ili utu wetu mpya upate kung’aa kwa kupenya.—Wagalatia 4:3.
Mtazamo mmoja kama huo, ni kusita kukubali daraka kwa kuhofu kwamba, mengi mno yatahitajiwa kwetu. Ni kweli, daraka humaanisha kazi, lakini ni kazi yenye kuridhisha. (Linganisha Matendo 20:35.) Paulo alikubali kwamba ujitoaji-kimungu wahitaji kwamba ‘tufanye kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe.’ Alisema kwamba, sisi hufanya hivyo kwa shangwe “kwa sababu tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai,” mmoja ambaye hasahau kamwe kazi tufanyayo kwa niaba ya Wakristo wenzetu na wengineo.—1 Timotheo 4:9, 10; Waebrania 6:10.
Almasi nyingine hupatwa na “mikazo” iliyotokea zilipofanyizwa na zahitaji kushughulikiwa kwa uangalifu. Hata hivyo, kwa msaada wa kifaa cha kupimia almasi, mng’arishaji aweza kupata huo mkazo na aweza kutengeneza hilo jiwe kwa mafanikio. Labda tuna mkazo wa ndani, au dosari ya utu, kwa sababu ya malezi yetu au jambo lenye kufadhaisha lililotupata. Twaweza kufanya nini? Kwanza, twahitaji kukubali hilo tatizo na kuazimia kulishinda kadiri tuwezavyo. Bila shaka yatupasa kujiondolea mzigo wenye kulemea kupitia sala kwa Yehova, labda pia kwa kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa mzee Mkristo.—Zaburi 55:22; Yakobo 5:14, 15.
Mkazo huo wa ndani ulimwathiri Nicholas. “Baba yangu alikuwa mraibu wa alkoholi, naye alifanya dada yangu nami tuteseke sana,” yeye aeleza. “Nilipoacha shule, nilijiunga na jeshi, lakini upesi mwelekeo wangu wa kuasi ukanitia taabani. Wenye mamlaka katika jeshi walinitia jela kwa kuuza dawa za kulevya, na kwenye pindi nyingine nikatoroka. Hatimaye, niliacha jeshi, lakini bado nilikuwa na taabu. Ingawa maisha yangu yalikuwa yamevurugika kwa sababu ya kutumia vibaya dawa na kunywa kupindukia, nilipendezwa na Biblia na nilikuwa na hamu sana ya kuwa na kusudi maishani. Hatimaye, niliwasiliana na Mashahidi wa Yehova, nikabadili mtindo-maisha wangu, na kukubali kweli.
“Hata hivyo, miaka kadhaa ilipita kabla ya kukubali na kushughulikia kasoro fulani katika utu wangu. Nilichukia sana mamlaka na nilikasirika nilipopewa shauri lolote. Ingawa nilitaka kutumiwa kikamili na Yehova, udhaifu huo ulinizuia. Hatimaye, kwa msaada wa wazee wawili wenye uelewevu, nilikubali tatizo langu na kuanza kutumia shauri lao la Kimaandiko. Ingawa pindi kwa pindi uchungu mdogo hutokea, sasa nimedhibiti asili yangu ya uasi. Ninashukuru sana kwa sababu ya njia ya Yehova yenye subira ya kushughulika nami, na kwa msaada wenye upendo wa wazee. Kwa sababu ya maendeleo yangu ya kiroho, hivi karibuni niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma.”
Kama vile Nicholas alivyogundua, kubadili mitazamo yenye kina si jambo rahisi. Huenda tukakabili mwito sawa na huo. Labda sisi ni wenye hisia nyepesi kupita kiasi. Huenda tukawa na lalamiko fulani, au huenda tukawa tunakazia mno kuwa na uhuru. Hivyo, huenda maendeleo yetu ya Kikristo yakawa madogo. Wang’arishaji wa almasi hupata jambo sawa na hilo wanapokata mawe wayaitayo naats. Haya kwa kweli ni mawe mawili yaliyoyeyushwa kuwa jiwe moja wakati wa kufanyizwa kwa almasi. Tokeo ni kwamba, naats yana taratibu mbili za ukuzi zenye kuhitilafiana, ambazo hufanya iwe vigumu sana kuyakata kulingana na mpangilio wa nyuzi. Katika hali yetu, sisi hupata “tabia ya asili” ya roho isiyo tayari ikipigana na “tabia ya asili” ya mwili wetu usio mkamilifu. (Mathayo 26:41; Wagalatia 5:17) Nyakati nyingine, huenda tukawa na mwelekeo wa kuacha hilo pigano kabisa, labda tukitoa sababu kwamba, kutokamilika mbalimbali katika utu wetu, si kwa maana kwa vyovyote. ‘Hata hivyo,’ huenda tukasema, ‘familia yangu na rafiki zangu bado wanipenda.’
Hata hivyo, ikiwa tutatumikia ndugu zetu na kumtukuza Baba yetu wa kimbingu, twahitaji ‘kufanywa upya katika kani inayotendesha akili yetu’ kwa kuvaa utu mpya. Jitihada hiyo yafaa, kama vile Nicholas na wengineo wengi wawezavyo kushuhudia. Mng’arishaji wa almasi ajua kwamba kasoro moja yaweza kuharibu almasi nzima. Hali kadhalika, kwa kupuuza sehemu dhaifu ya utu wetu, twaweza kuharibu sura yetu ya kiroho. Vibaya hata zaidi, udhaifu mkubwa waweza kusababisha kuanguka kwetu kiroho.—Mithali 8:33.
Kama “Moto” Ndani Yetu
Mng’arishaji wa almasi hutafuta kupata moto (mng’aro) ulio ndani ya almasi. Hilo hufanywa kwa kupanga pande zilizokatwa hivi kwamba, zatokeza rangi nyingi. Ndani ya hiyo almasi, nuru yenye rangi nyingi humweka, ikitokeza huo moto ambao hufanya almasi zimetemete. Vivyo hivyo, roho ya Mungu yaweza kuwa kama “moto” ndani yetu.—1 Wathesalonike 5:19; Matendo 18:25; Waroma 12:11.
Lakini namna gani tukihisi uhitaji wa kuchochewa kiroho? Hilo laweza kufanywaje? Twahitaji ‘kuzitafakari njia zetu.’ (Zaburi 119:59, 60) Hilo lingehusisha kuyatambua mambo yapunguzayo mwendo wetu kiroho kisha kuhakikisha ni utendaji gani wa kitheokrasi ambao twahitaji kufuatia kwa bidii zaidi. Twaweza kuongeza kina cha ufahamu wetu wa kiroho kupitia funzo la kibinafsi la kawaida na sala ya bidii. (Zaburi 119:18, 32; 143:1, 5, 8, 10) Isitoshe, kwa kushirikiana na wale wafanyao kazi kwa bidii katika imani, tutaimarisha zaidi azimio letu la kumtumikia Yehova kwa bidii.—Tito 2:14.
Louise, mwanamke mchanga Mkristo, alikiri hivi: “Nilifikiria upainia wa kawaida kwa miaka miwili kabla ya kujiandikisha kuwa painia, au mhubiri wa Ufalme wa wakati wote. Hakuna kitu chochote kilichokuwa kikinizuia, lakini nilikuwa na kawaida ya maisha iliyokuwa rahisi, na sikufanya jitihada yoyote kuiacha. Kisha baba yangu akafa ghafula. Niling’amua jinsi uhai ulivyo wa muda mfupi na kwamba, sikuwa nikiutumia uhai wangu kwa njia iliyo bora zaidi. Kwa hiyo nilibadili mtazamo wangu wa kiroho, nikaongeza utumishi wangu, na kuwa painia wa kawaida. Hasa walionisaidia katika jambo hilo ni ndugu na dada zangu wa kiroho waliounga mkono sikuzote mipango ya utumishi wa shambani, na walioandamana nami kwa kawaida katika huduma. Nimejifunza kwamba hata hali iwe nzuri au mbaya, sisi hushiriki maadili na miradi ya washiriki wetu.”
Kunolewa Kana Kwamba kwa Chuma
Almasi ni vitu vilivyo vigumu zaidi kati ya vitu ambavyo hupatikana duniani. Kwa sababu hiyo, almasi hukatwa kwa almasi nyingine. Hilo huenda likawakumbusha wanafunzi wa Biblia ile mithali isemayo hivi: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” (Mithali 27:17) Uso wa mtu ‘hunolewaje’? Mtu mmoja aweza kufanikiwa kunoa hali ya kiakili na ya kiroho ya mwingine, kama vile kipande cha chuma kiwezavyo kutumiwa kunoa upanga uliotengenezwa kwa chuma kilekile. Kwa mfano, ikiwa tutashuka moyo kwa sababu ya tamauko fulani, kitia-moyo cha mtu mwingine chaweza kuwa chenye kuchangamsha. Hivyo sura yetu yenye huzuni yaweza kubadilika kuwa bora zaidi, na twaweza kuchochewa kwa ajili ya utendaji wenye bidii uliofanywa upya. (Mithali 13:12) Wazee wa kutaniko hasa waweza kusaidia kutunoa kwa kuandaa kitia-moyo na ushauri wa Kimaandiko ili tufanye maendeleo. Wao hufuata kanuni iliyotaarifiwa na Sulemani: “Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima; mfundishe mwenye haki, naye atazidi kuwa na elimu.”—Mithali 9:9.
Bila shaka, mazoezi ya kiroho huchukua muda. Kwa miaka zaidi ya kumi, mtume Paulo alishiriki pamoja na Timotheo uzoefu wake na njia zake za kufundisha. (1 Wakorintho 4:17; 1 Timotheo 4:6, 16) Mazoezi marefu ambayo Musa alimpa Yoshua kwa kipindi cha miaka 40, yalinufaisha taifa la Israeli kwa muda mrefu. (Yoshua 1:1, 2; 24:29, 31) Elisha aliandamana na nabii Eliya labda kwa miaka 6, akipokea mazoezi mazuri kwa ajili ya huduma yake mwenyewe ambayo ingedumu kwa miaka ipatayo 60. (1 Wafalme 19:21; 2 Wafalme 3:11) Kwa kuandaa kwa subira mazoezi yenye kuendelea, wazee hufuata kielelezo cha Paulo, Musa, na Eliya.
Kutoa pongezi ni sehemu muhimu ya kuzoeza. Semi za moyo mweupe za uthamini kwa ajili ya migawo iliyoshughulikiwa vizuri au kwa ajili ya matendo yastahiliyo sifa, huenda yakasukuma wengine watake kumtumikia Mungu kwa ukamili zaidi. Pongezi hujenga uhakika ambao, huandaa kichocheo cha kufanya jitihada ya kushinda udhaifu wetu mbalimbali. (Linganisha 1 Wakorintho 11:2.) Kitia-moyo cha kufanya maendeleo katika kweli pia hutokana na kuwa na juhudi nyingi katika kazi ya kuhubiri Ufalme, na utendaji mwingine wa kikutaniko. (Matendo 18:5) Wazee wawagawiapo ndugu daraka kupatana na maendeleo yao ya kiroho, jambo hilo huwapa wanaume hao uzoefu wenye thamani, na yaelekea litaimarisha tamaa yao ya kufuliza kufanya maendeleo kiroho.—Wafilipi 1:8, 9.
Sababu Nzuri ya Kufanya Maendeleo ya Kiroho
Almasi zimeonwa kuwa zenye thamani. Hivyo ndivyo ilivyo na wale ambao sasa wanashirikiana na familia ya ulimwenguni pote ya waabudu wa Yehova. Kwa kweli, Mungu mwenyewe awaita “vitu vinavyotamaniwa,” au “vyenye thamani,” vya mataifa yote. (Hagai 2:7; kielezi-chini, NW) Mwaka uliopita, watu 375,923 walikuwa Mashahidi wa Yehova waliobatizwa. Ili kushughulikia ukuzi huo, kuna uhitaji wa ‘kupanua hema.’ Kwa kufanya maendeleo kiroho—na kwa kujitahidi kufikia mapendeleo ya utumishi wa Kikristo—yawezekana kuwa na fungu katika kutunza upanuzi huo.—Isaya 54:2; 60:22.
Tofauti na almasi nyingi zenye thamani ambazo huwekwa kwenye stoo za benki zilizo chini ya ardhi, na ambazo ni nadra kuonekana, thamani yetu ya kiroho yaweza kung’aa kwa uangavu. Na tung’arishapo na kudhihirisha sifa zetu za Kikristo kwa ukawaida, twamtukuza Yehova Mungu. Yesu aliwahimiza kwa bidii wafuasi wake hivi: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mathayo 5:16) Bila shaka, hilo hutupatia sababu nzuri ya kufanya maendeleo ya kiroho.
[Maelezo ya Chini]
a Majina-badala yametumiwa katika makala hii.