Je! Unathamini Tengenezo la Yehova la Kidunia?
TAZAMA almasi nzuri sana iliyokatwa vizuri, nawe waona nini? Kito ambacho kwa kweli ni kitu chenye uzuri. Sasa chunguza almasi hiyo kupitia darubini, nawe waona nini? Yaelekea kuna mikwaruzo, nyufa, vitu vinginevyo vilivyo ndani ya fuwele hiyo, au hitilafu nyingine.
Je! ungeharibu au kutupilia mbali almasi hiyo kwa sababu tu ya jinsi inavyoonekana chini ya darubini? Bila shaka sivyo! Ebu ondoka kwenye darubini, na bado waweza kuthamini uzuri na mn’gao usio wa kawaida unaoifanya itokeze miongoni mwa vito vingine.
Kama almasi, tengenezo la Yehova la kidunia latokeza katika njia nyingi. Hakuna tengenezo jingine duniani linaloonea shangwe uhusiano wa kindani pamoja na Muumba. Katika barua kwa Wakristo wa karne ya kwanza, waliofurahia tumaini la kimbingu, mtume Petro alirejezea uhusiano huo wa kipekee. Yeye alisema hivi: “Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.” (1 Petro 2:9) Leo umati mkubwa wa “kondoo wengine,” walio na tumaini la uhai wa milele duniani, wamejiunga na wale wanaobaki wa “taifa takatifu” katika kumwabudu Mungu. (Yohana 10:16) Pamoja vikundi hivyo viwili vinafanyiza tengenezo linalotokeza kama kito chenye uzuri na chenye mng’ao usio wa kawaida.
Epuka Kuwaona Wengine kwa Jicho Lenye Kuchambua
Lakini ni lazima tutambue kwamba washiriki wa tengenezo hili la ulimwenguni pote ni wanadamu wasiokamilika. Kwa hiyo, nini kingetukia ikiwa tungeliangalia kupitia darubini ya ufananisho? Naam, tungepata mielekeo yenye dhambi na makosa ya kiutu katika watu mmoja mmoja walio sehemu yalo.—Warumi 3:23.
Mtume Paulo alikubali kwamba alikuwa na makosa kama hayo. Alisema hivi: “Mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya.” (Warumi 7:21) Kila Mkristo hupatwa na pambano hilo hilo. Wote hufanya makosa. Isitoshe, hakuna budi kwamba wengi huteseka kwa sababu ya makosa ya mtu mwingine. Je! twapaswa kushuka moyo au kupoteza maoni yetu mazuri kuhusu wengine wakati makosa na kutokamilika kwa Wakristo wenzetu kunapofunuliwa? Je! hilo lapasa kupunguza uthamini wetu wa tengenezo la Yehova? Bila shaka sivyo! Bali, twapaswa kupata maoni ya ujumla kama vile kuondoka kwenye darubini, na kuacha kukazia fikira kutokamilika kwa watu mmoja mmoja.
Maandiko huorodhesha sifa kadhaa ambazo zingetambulisha wale ambao juu yao roho takatifu hutenda kazi. Nyingine zazo ni “upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi.” (Wagalatia 5:22, 23) Tofauti na hilo, matengenezo ya kidini, kisiasa, na kibiashara ya ulimwengu huu mara nyingi huonyesha yale ambayo Biblia hurejezea kuwa matendo ya mwili: “uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.” (Wagalatia 5:20, 21) Hivyo, kama almasi ing’aayo miongoni mwa miamba ya kawaida, watu wa Yehova hutokeza kati ya ulimwengu uliopotoka kiroho.—Mathayo 5:14-16.
“Kuunganika kwa Kufaa Katika Akili Moja”
Sehemu moja yenye kutokeza sana ya almasi ni muundo wayo wa kiatomi wenye kifungo cha ukaribu sana na chenye nguvu. Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kidunia huonyesha umoja usio na kifani katika mafundisho na udugu. Wale walio sehemu ya tengenezo hilo hutii himizo linalopatikana ka-tika Biblia katika 1 Wakorintho 1:10, NW, linalotaarifu hivi: “Sasa mimi natia moyo ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana yetu Yesu Kristo kwamba imepasa ninyi nyote kusema kwa mwafaka, na kwamba imepasa kusiwe migawanyiko mwenu ninyi, bali kwamba ninyi mpate kuunganika kwa kufaa katika akili moja na katika mstari mmoja wa fikira.”
Mashahidi wa Yehova wameshinda pia ubaguzi wa rangi na kiburi cha kitaifa. Wakiwa na “hekima itokayo juu,” wao ‘hawana ubaguzi.’ (Yakobo 3:17, HNWW) Tunampa Yehova utukufu kwa yale ambayo ametimiza kuhusu jambo hili katika tengenezo ambalo washiriki walo ni wanadamu wasiokamilika.
Tofauti na hilo, gazeti The Christian Century, likiongea kuhusu mwaka wa 1990, lilitaarifu kwamba “zaidi ya wakati mwingine wowote ulimwengu ulionekana kuwa umegawanywa na vikundi vya kidini na maoni ya kikabila na ya kitaifa yaliyofungamana sana na imani za kidini. Kutoka India hadi Ulaya na kutoka Mashariki ya Kati hadi Pasifiki, dini yenye kuchangamana na utii kwa mambo ya kikabila na kitaifa—mara nyingi huwa na matokeo ya kisiasa yenye kubadilika-badilika ghafula.” Kwa wazi, wale wanaotaka kumtumikia Mungu wanaweza kugeukia tu tengenezo lile moja linaloonea shangwe roho na baraka za Yehova.
‘Kama Almasi Ilivyo, Ndivyo Nilivyofanya Kipaji Chako’
Almasi ndicho kitu kilicho kigumu zaidi kipatikanacho kiasili anachojua mwanadamu. Biblia hurejezea utumizi wa almasi katika kukwaruza au kuchonga vitu vigumu. (Yeremia 17:1) Angalia pia, maneno ya Yehova kwa Ezekieli: “Tazama, nimeufanya uso wako kuwa mgumu juu ya nyuso zao, na kipaji cha uso chako kuwa kigumu juu ya vipaji vya nyuso vyao. Kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume, ndivyo nilivyokifanya kipaji chako.” (Ezekieli 3:8, 9) Yehova alimpa Ezekieli nia ngumu kama almasi iliyomwezesha kutoa unabii kwa watu wenye shingo ngumu.—Ezekieli 2:6.
Vivyo hivyo leo, Yehova amewapa watu wake ugumu wa mfano wa almasi wakabilianapo na upinzani mkubwa. Mashahidi wa Yehova wamevumilia kupigwa marufuku kisheria, kushambuliwa na watu wenye ghasia, kuuawa bila hukumu ya sheria, kupigwa, kufungwa gerezani isivyo haki, kuteswa, hata kuuawa. Hata hivyo, wameonyesha imani yao kuwa isiyoweza kuvunjwa.
“Watumishi Wangu Watafurahi”
Biblia ilitabiri wakati ambao watu wangekuwa “wenye mfano wa utauwa” lakini wangethibitika kuwa wenye ‘kukana nguvu zake.’ (2 Timotheo 3:1-5) Gazeti moja la habari linaripoti kwamba “Waprotestanti, Wakatoliki ya Kiroma na Wayahudi wote huhangaikia mpunguo” ulio katika makanisa na masinagogi yao. Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova, ni wanafunzi wa Biblia wenye bidii. Kwa idadi zenye kuongezeka, wote, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, huhudhuria mikutano kadhaa ya kila juma, kwa idadi zinazoongezeka. Barua moja iliyopelekwa kwa gazeti moja lilitaarifu kuhusu wao kwamba “dini yao ni kitu chenye thamani zaidi walicho nacho, hangaiko lao la pekee ni kuishiriki na wengine.”
Mwelekeo kama huo hufanya tengenezo la Yehova litokeze kama almasi yenye thamani kubwa. Na sifa inamwendea Yule ambaye huwaimarisha na kuwaongoza watu wasiokamilika kupitia roho takatifu yake.
Nabii Isaya alitabiri hivi: “Bwana MUNGU [Yehova, NW] asema hivi, Tazama, watumishi wangu watakula . . . Tazama, watumishi wangu watakunywa . . . Tazama, watumishi wangu watafurahi . . . Tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo.”—Isaya 65:13, 14.
Leo tunaona utimizo wa unabii huo. Mungu hutunza watu wake katika njia isiyo ya kawaida! Kwa hiyo, ikiwa unashirikiana nao, usikubali kufikiri kokote kusikofaa kukunyang’anye shangwe yako. Angalia tengenezo zima nawe ukumbuke: Hakuna tengenezo jingine duniani linaloonea shangwe utunzaji na ulinzi wa Mungu wa upekee. Usiache kamwe kuthamini sana pendeleo lako la kuwa sehemu yalo.