Je, Yehova Hutaka Mengi Mno Kutoka Kwetu?
“BWANA [“Yehova,” “NW”] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”—MIKA 6:8.
1. Huenda ni kwa nini watu fulani hawamtumikii Yehova?
YEHOVA hutaka jambo fulani kutoka kwa watu wake. Lakini baada ya kusoma maneno yaliyo juu yaliyonukuliwa katika unabii wa Mika, huenda ukaamua kwamba matakwa ya Mungu ni ya kiasi. Hata hivyo, wengi hawamtumikii Muumba Mtukufu wetu, na wengine waliomtumikia wakati fulani wameacha kufanya hivyo. Kwa nini? Kwa sababu wanadhani kuwa Mungu anataka mengi mno kutoka kwetu. Je, ni kweli? Au labda mtazamo wa mtu kwa yale atakayo Yehova una kasoro fulani? Simulizi moja la kihistoria huandaa ufahamu wenye kina kwa habari hii.
2. Naamani alikuwa nani, na nabii wa Yehova alimtaka afanye nini?
2 Mkuu wa majeshi ya Siria, Naamani, alikuwa na ukoma naye akaelezwa kuwa kuna nabii wa Yehova nchini Israeli awezaye kumponya. Kwa hiyo, Naamani na msafara wake wakasafiri mpaka Israeli nao hatimaye wakafika nyumbani kwa Elisha nabii wa Mungu. Badala ya kuondoka nyumbani mwake amlaki mgeni wake mashuhuri, Elisha alituma mtumishi amwambie Naamani: “Enenda ukaoge katika Yordani mara saba, na nyama ya mwili wako itakurudia, nawe utakuwa safi.”—2 Wafalme 5:10.
3. Kwa nini hapo mwanzoni Naamani alikataa kufanya yale aliyotaka Yehova?
3 Ikiwa Naamani angefuata takwa lililotolewa na nabii wa Mungu, angeponywa ugonjwa wenye kuchukiza. Kwa hiyo je, Yehova alikuwa akitaka mengi mno kutoka kwake? Sivyo. Ingawa hivyo, Naamani hakutaka kufanya yale aliyotaka Yehova. “Je! Abana na Farpari, mito ya Dameski, si bora kuliko maji yote ya Israeli?” akateta. “Je, siwezi kujiosha ndani yake, na kuwa safi?” Kwa hayo, Naamani akaenda zake kwa hasira.—2 Wafalme 5:12.
4, 5. (a) Naamani alipewa thawabu gani kwa utii wake, naye aliitikiaje alipoipokea? (b) Tutachunguza nini sasa?
4 Ni nini hasa lililokuwa tatizo la Naamani? Si kwamba takwa hilo lilikuwa gumu mno asiweze kulitimiza. Watumishi wa Naamani wakamwambia kwa busara: “Kama yule nabii angalikuambia kutenda jambo kubwa, usingalilitenda? je! si zaidi basi, akikuambia, Jioshe, uwe safi?” (2 Wafalme 5:13) Tatizo lilikuwa maoni ya Naamani. Aliona kuwa hakupewa heshima anayostahili na kwamba alitakwa afanye jambo ambalo yaonekana aliliona kuwa lisilo na maana na linalomvunjia heshima. Hata hivyo, Naamani aliitikia shauri la busara la watumishi wake naye akajitosa mara saba ndani ya Mto Yordani. Wazia shangwe yake ‘nyama ya mwili wake iliporudi ikawa kama nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi’! Akashukuru sana. Isitoshe, Naamani akatangaza kuwa tangu wakati huo, hangeabudu mungu mwingine ila Yehova.—2 Wafalme 5:14-17.
5 Kwa muda wote wa historia ya binadamu, Yehova amewataka watu wafuate kanuni mbalimbali. Twakuomba uchunguze baadhi ya kanuni hizo. Uzichunguzapo, jiulize jinsi ambavyo ungaliitikia ikiwa Yehova angalikutaka ufanye mambo hayo. Baadaye, tutachunguza yale ambayo Yehova hutaka kwetu leo.
Yale Aliyotaka Yehova Wakati Uliopita
6. Wenzi wa kibinadamu wa kwanza walitakwa wafanye nini, nawe ungaliitikiaje maagizo hayo?
6 Yehova aliwaagiza wenzi wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa, wazae watoto, waitiishe dunia na wanyama pia. Pia, mwanamume huyo na mkewe walibarikiwa kwa kupewa makao makubwa yaliyo kama bustani. (Mwanzo 1:27, 28; 2:9-15) Lakini wakapewa sharti. Hawakupaswa kula matunda ya mti fulani, mmoja kati ya miti mingi yenye kuzaa matunda katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 2:16, 17) Je, hiyo ilikuwa kutaka mengi mno? Je, hungalifurahia kutimiza mgawo huo, huku ukitazamia kuishi milele katika afya kamilifu? Ingawa mshawishi alikuja katika bustani, je hungalikataa ubishi wake? Nawe hukubali kwamba Yehova alikuwa na haki ya kuweka sharti moja sahili?—Mwanzo 3:1-5.
7. (a) Noa alipewa kazi gani, naye alikabili upinzani gani? (b) Wewe unaonaje yale ambayo Yehova alimtaka Noa afanye?
7 Baadaye, Yehova alimtaka Noa ajenge safina ya kuokolea watu kutoka kwa furiko la duniani kote. Ukizingatia ukubwa wa safina, kazi hiyo haikuwa rahisi nayo labda ilifanywa kukiwa na dhihaka na uhasama mwingi. Ingawa hivyo, lilikuwa pendeleo lililoje kwa Noa kuokoa nyumba yake, mbali na wanyama! (Mwanzo 6:1-8, 14-16; Waebrania 11:7; 2 Petro 2:5) Ikiwa ungalipewa kazi kama hiyo je, ungalijitahidi kuikamilisha? Au je, ungalikata kauli kwamba Yehova anataka mengi mno kutoka kwako?
8. Abrahamu alitakwa afanye nini, na kufuata kwake takwa hilo kulitoa kielezi cha nini?
8 Mungu alimtaka Abrahamu afanye jambo gumu sana, akimwambia: “Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa.” (Mwanzo 22:2) Kwa kuwa Yehova alikuwa ameahidi kwamba Isaka, asiyekuwa na uzao wakati huo, angepata uzao, imani ya Abrahamu katika uwezo wa Mungu wa kumrudisha Isaka kwenye uhai ilijaribiwa. Abrahamu alipofanya jaribio la kumchinja Isaka, Mungu alimhifadhi mwanamume huyo mchanga. Tukio hilo lilitoa kielezi cha Mungu kumtoa Mwana wake mwenyewe kwa ajili ya wanadamu na kisha kumfufua.—Mwanzo 17:19; 22:9-18; Yohana 3:16; Matendo 2:23, 24, 29-32; Waebrania 11:17-19.
9. Kwa nini Yehova hakuwa akitaka mengi mno kutoka kwa Abrahamu?
9 Huenda wengine wakafikiri kuwa Yehova Mungu alikuwa akitaka mengi mno kutoka kwa Abrahamu. Lakini je, alitaka mengi mno? Je, kweli lingekuwa jambo lisilo la upendo kwa Muumba wetu, awezaye kufufua wafu, kututaka tumtii hata ikiwa hilo lingefanya tufe kwa muda mfupi? Yesu Kristo na wafuasi wake wa mapema hawakuona hivyo. Walikuwa tayari kuteswa kimwili, hata kufa, ili kufanya mapenzi ya Mungu. (Yohana 10:11, 17, 18; Matendo 5:40-42; 21:13) Ikiwa hali zingekuhitaji ufanye hivyo, je, ungefanya vivyo hivyo? Fikiria baadhi ya mambo ambayo Yehova alitaka kwa wale waliokubali kuwa watu wake.
Sheria ya Yehova kwa Israeli
10. Ni nani walioahidi kufanya yote aliyotaka Yehova, naye aliwapa nini?
10 Wazao wa Abrahamu kupitia Isaka mwanaye na mjukuu wake Yakobo, au Israeli, waliongezeka wakawa taifa la Israeli. Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri. (Mwanzo 32:28; 46:1-3; 2 Samweli 7:23, 24) Punde baadaye, wakaahidi kufanya lolote alilotaka Mungu kutoka kwao. Walisema hivi: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” (Kutoka 19:8) Kwa kuzingatia nia ya Waisraeli ya kutawaliwa naye, Yehova alilipa taifa hilo sheria zaidi ya 600, kutia ndani Amri Kumi. Baadaye, sheria hizi za Mungu, zilizotolewa kupitia Musa, zikaja kuitwa tu Sheria.—Ezra 7:6; Luka 10:25-27; Yohana 1:17.
11. Kusudi moja la Sheria lilikuwa nini, na ni zipi baadhi ya kanuni zilizosaidia kulitimiza?
11 Kusudi moja la Sheria lilikuwa kuwalinda Waisraeli kwa kuwapa kanuni nzuri zenye mwongozo juu ya mambo kama vile maadili ya kingono, shughuli za kibiashara, na malezi ya watoto. (Kutoka 20:14; Mambo ya Walawi 18:6-18, 22-24; 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Kanuni juu ya namna ya kuwatendea wanadamu na wanyama pia zilitolewa. (Mambo ya Walawi 19:18; Kumbukumbu la Torati 22:4, 10) Matakwa yaliyohusu misherehekeo ya kila mwaka na kukutana kwa ajili ya ibada yalisaidia kuwalinda watu hao kiroho.—Mambo ya Walawi 23:1-43; Kumbukumbu la Torati 31:10-13.
12. Ni nini lililokuwa kusudi kuu la Sheria?
12 Mtume Paulo alionyesha kusudi kuu la Sheria, akiandika: “Iliongezwa kufanya mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu [Kristo] iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19) Sheria iliwakumbusha Waisraeli kwamba si wakamilifu. Kwa kufaa, basi, walihitaji dhabihu kamilifu ambayo ingeondoa dhambi zao kabisa. (Waebrania 10:1-4) Kwa hiyo, Sheria ilikusudiwa kuwatayarisha watu wamkubali Yesu, aliyekuwa Mesiya, au Kristo. Paulo aliandika hivi: “Sheria imekuwa mfunzi wetu ikiongoza kwa Kristo, ili tupate kutangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani.”—Wagalatia 3:24.
Je, Sheria ya Yehova Ilikuwa Yenye Kulemea?
13. (a) Watu wasio wakamilifu waliionaje Sheria, na kwa nini? (b) Je, kweli Sheria ilikuwa yenye kulemea?
13 Ingawa Sheria ilikuwa “takatifu na ya uadilifu na njema,” wengi waliiona kuwa yenye kulemea. (Waroma 7:12) Kwa sababu Sheria ilikuwa kamilifu, Waisraeli hawangeweza kutimiza kiwango chake cha juu. (Zaburi 19:7) Hiyo ndiyo sababu mtume Petro aliiita “nira ambayo baba zetu wa zamani wala sisi hatukuweza kuhimili.” (Matendo 15:10) Sheria yenyewe bila shaka haikuwa yenye kulemeza, na watu walinufaika kwa kuitii.
14. Ni vielelezo gani vichache vionyeshavyo kwamba Sheria ilitimiza kusudi lenye manufaa mengi kwa Waisraeli?
14 Kwa kielelezo, chini ya Sheria, mwizi hakufungwa bali alipaswa kufanya kazi ili alipe maradufu au zaidi kile alichoiba. Hivyo mwathiriwa hakupata hasara yoyote, wala watu waliofanya kazi kwa bidii hawakutwikwa mzigo wa kutegemeza mfumo wa jela. (Kutoka 22:1, 3, 4, 7) Vyakula hatari vilipigwa marufuku. Nyama ya nguruwe yaweza kuambukiza minyoo isipopikwa vya kutosha, na sungura waweza kuambukiza ugonjwa wa viini vya sumu. (Mambo ya Walawi 11:4-12) Vivyo hivyo, Sheria ilikuwa ulinzi kwa kukataza kugusa mizoga. Ikiwa mtu angegusa maiti, alitakiwa aoge na kufua mavazi yake. (Mambo ya Walawi 11:31-36; Hesabu 19:11-22) Kinyesi kilipasa kufukwa, na hilo liliwalinda watu dhidi ya kuenea kwa viini vya maradhi, ambavyo wanasayansi wamevigundua katika karne za juzijuzi tu.—Kumbukumbu la Torati 23:13.
15. Ni nini kilichowalemea Waisraeli?
15 Sheria haikutaka mengi mno kutoka kwa watu. Lakini watu waliojichukulia daraka la kuifasiri Sheria walitenda kinyume. Kuhusu kanuni walizoweka, kichapo A Dictionary of the Bible, kilichohaririwa na James Hastings, chataarifu hivi: “Kila amri ya Biblia ilizungukwa na kanuni nyingi zisizo na maana. . . . Kwa hiyo jitihada ilifanywa kudhibiti kwa njia ya Sheria kila jambo linalowazika, na kudhibiti bila huruma mwenendo wote wa binadamu kwa utaratibu mkali wa utendaji. . . . Dhamiri ilikandamizwa; nguvu iliyo hai ya neno la Mungu ikabatilishwa na kuzuiwa chini ya kanuni nyingi mno za nje.”
16. Yesu alisema nini juu ya kanuni na mapokeo yenye kulemea ya viongozi wa kidini?
16 Yesu Kristo aliwashutumu viongozi wa kidini walioweka kanuni nyingi mno, akisema: “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” (Mathayo 23:2, 4) Alisema kuwa kanuni na mapokeo yenye kulemea yaliyotungwa na wanadamu, pamoja na utaratibu wenye mambo mengi wa kujisafisha, ‘vilibatilisha neno la Mungu.’ (Marko 7:1-13; Mathayo 23:13, 24-26) Ingawa hivyo, hata kabla Yesu hajaja duniani, walimu wa kidini katika Israeli walikuwa wakipotosha yale atakayo Yehova hasa.
Yale Atakayo Yehova Hasa
17. Kwa nini Yehova hakufurahia dhabihu za kuteketezwa za Waisraeli wasio na imani?
17 Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng’ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume.” (Isaya 1:10, 11) Kwa nini Mungu hakufurahia dhabihu alizoamuru mwenyewe katika Sheria? (Mambo ya Walawi 1:1–4:35) Kwa sababu watu hawakumheshimu. Kwa hiyo walipewa onyo hili: “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.” (Isaya 1:16, 17) Je, hayo hayatusaidii kufahamu yale atakayo Yehova kwa watumishi wake?
18. Yehova alikuwa akitaka nini hasa kwa Waisraeli?
18 Yesu alionyesha yale atakayo Mungu hasa. Alifanya hivyo alipoulizwa swali hili, “Ni ipi iliyo amri kubwa zaidi sana katika ile Sheria?” Yesu akajibu: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri kubwa zaidi sana na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Juu ya amri mbili hizi Sheria yote yaning’inia, na Manabii.” (Mathayo 22:36-40; Mambo ya Walawi 19:18; Kumbukumbu la Torati 6:4-6) Nabii Musa alitoa hoja hiyohiyo alipouliza hivi: “BWANA, Mungu wako, anataka nini kwako, ila umche BWANA, Mungu wako, na kwenda katika njia zake zote, na kumpenda, na kumtumikia BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote; kuzishika amri za BWANA na sheria zake, ninazokuamuru leo, upate uheri?”—Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; 15:7, 8.
19. Waisraeli walijaribuje kuonekana watakatifu, lakini Yehova aliwaambia nini?
19 Licha ya makosa yao, Waisraeli walitaka kuonekana watakatifu. Ingawa Sheria ilitaka watekeleze mfungo kwenye Siku ya Kufunika pekee, walianza kufunga mara nyingi. (Mambo ya Walawi 16:30, 31) Lakini Yehova aliwakemea, akisema: “Je! saumu [“mfungo,” NW] niliyoichagua, siyo ya namna hii? kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Je! siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?”—Isaya 58:3-7.
20. Yesu aliwakemea wanafiki wa kidini kwa sababu gani?
20 Waisraeli hao wenye kujifanya waadilifu walikuwa na tatizo linalofanana na la wanafiki wa kidini, ambao Yesu aliwaambia hivi: “Nyinyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na jira, lakini mmepuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu. Ilikuwa lazima mambo haya kuyafanya, na bado kutopuuza yale mambo mengine.” (Mathayo 23:23; Mambo ya Walawi 27:30) Maneno ya Yesu yanatusaidia kufahamu yale hasa atakayo Yehova kutoka kwetu, sivyo?
21. Nabii Mika alitoaje muhtasari wa yale Yehova anayotaka na asiyotaka kutoka kwetu?
21 Ili kubainisha yale anayotaka na asiyotaka Yehova kutoka kwetu, Mika nabii wa Mungu aliuliza: “Nimkaribie BWANA na kitu gani, na kuinama mbele za Mungu aliye juu? Je! nimkaribie na sadaka za kuteketezwa, na ndama za umri wa mwaka mmoja? Je! BWANA atapendezwa na elfu za kondoo waume, au na elfu kumi za mito ya mafuta? Je! nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza kwa kosa langu, mzao wa mwili wangu kwa dhambi ya roho yangu? Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”—Mika 6:6-8.
22. Yehova alitaka nini hasa kwa wale waliokuwa chini ya Sheria?
22 Hivyo basi, Yehova alitaka nini hasa kwa wale walioishi chini ya Sheria? Ni wazi kuwa walipaswa kumpenda Yehova Mungu. Isitoshe, mtume Paulo alisema hivi: “Sheria nzima husimama ikiwa imetimizwa katika usemi mmoja, yaani: ‘Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” (Wagalatia 5:14) Vivyo hivyo, Paulo aliwaambia Wakristo huko Roma: “Apendaye binadamu-mwenziye ametimiza sheria. . . . Upendo ndio utimizo wa sheria.”—Waroma 13:8-10.
Si Mengi Mno
23, 24. (a) Kwa nini isiwe kamwe vigumu mno kwetu kufanya atakayo Yehova? (b) Sasa tutachunguza nini?
23 Je, haituvutii kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo, mwenye kufikiri, na mwenye rehema? Mwana mzaliwa-pekee wake, Yesu Kristo, alikuja duniani kutukuza upendo wa Mungu—kufahamisha watu jinsi walivyo wenye thamani kwa Yehova. Akitoa kielezi cha upendo wa Mungu, Yesu alisema kuhusu shore wenye hali ya chini: “Hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua.” Basi akamalizia hivi: “Msiwe na hofu: nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Mathayo 10:29-31) Kwa hakika, haipaswi kamwe kuwa vigumu mno kwetu kufanya lolote atakalo Mungu huyu mwenye upendo!
24 Ingawa hivyo, Yehova hutaka nini kwetu leo? Na kwa nini wengine huona kana kwamba Mungu hutaka mengi mno? Kwa kuyachunguza maswali hayo, twapaswa tuone kwa nini ni pendeleo zuri mno kufanya yale atakayo Yehova.
Waweza Kujibu?
◻ Kwa nini huenda wengine wakakataa kumtumikia Yehova?
◻ Matakwa ya Yehova yamebadilikaje kwa muda wa miaka mingi?
◻ Sheria ilitimiza makusudi gani?
◻ Kwa nini yale atakayo Yehova kwetu si mengi mno?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kanuni zenye kutungwa na wanadamu, kama vile utaratibu wenye mambo mengi wa kusafisha, zimefanya ibada iwe yenye kulemea