Kuwekwa Wakfu kwa Kituo cha Elimu cha Watchtower—Msherehekeo kwa Yehova
TANGU nyakati za kale, misherehekeo yenye furaha imekuwa sehemu ya ibada ya kweli. Baadhi ya misherehekeo iliyofanywa katika Israeli la kale ilichukua muda wa siku nyingi na kuhudhuriwa na maelfu ya waabudu wa Yehova. Kuzinduliwa kwa hekalu la Solomoni kulichukua muda wa siku saba na kufuatwa kwa Msherehekeo wa Vibanda uliochukua muda wa juma zima. Msherehekeo huo uliwapa Waisraeli fursa ya kutafakari jinsi Yehova alivyokuwa ameshughulika nao kwa njia nzuri. Wakarudi nyumbani ‘wakifurahi na kuchangamka moyoni kwa wema wote BWANA aliowafanyia.’—1 Wafalme 8:66.
Yale yaliyotokea Mei 17-22, 1999, kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani, yaliwakumbusha wageni misherehekeo hiyo ya kale yenye furaha. Hilo lilikuwa juma la shughuli za pekee zilizohusu kuwekwa wakfu kwa jengo lenye majumba 28 lililokusudiwa kuendeleza elimu ya Biblia ulimwenguni. Matayarisho yalifanywa ili washiriki wote 5,400 wa makao makuu katika Brooklyn, Wallkill, na Patterson waweze kutembelea sehemu zote za majengo hayo ya Patterson katika juma hilo kuu. Miongoni mwa wageni mlikuwa na zaidi ya wafanyakazi 500 wa zamani walioshiriki katika kazi wakati kituo hicho cha elimu kilipokuwa kikijengwa, wawakilishi kutoka ofisi za tawi 23 za Watch Tower Society, na wengine kutoka makutaniko ya karibu—jumla ya angalau watu 8,100.
Maonyesho Wakati wa Matembezi Yaelimisha
Ili wageni wapate kufahamu kituo hicho cha elimu, mipango ilifanywa ili kuwepo na maonyesho ya pekee, maonyesho ya vidio yenye kuelimisha, na pia watu waweze kutembea wenyewe bila kuongozwa. Katika sebule kuu, wageni walivutiwa mara moja na kigezo cha hekalu lililokuwa Yerusalemu wakati wa huduma ya Yesu duniani. Maonyesho mengine yalionyesha historia ya mapema ya Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, mikusanyiko ya kihistoria, mikutano ya kutaniko, maendeleo yanayofanywa siku hizi katika kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani—mamilioni ya mafunzo hayo yakiongozwa kila juma—na kuonyesha kazi inayofanywa na Idara ya Sheria ili utendaji huo uweze kuendelea kwa kutii amri ya Yesu. —Mathayo 28:19, 20.
Katika ukumbi ulio karibu, unaoweza kutoshea vizuri watu 1,700, wageni waliokuja kwa ajili ya msherehekeo wa kuweka wakfu walionyeshwa vidio iliyochukua muda wa dakika 33 yenye kichwa “Si kwa Nguvu—Bali kwa Roho Yangu!” Vidio hiyo ilionyesha jinsi Kituo cha Elimu cha Watchtower kilivyoanzishwa. Mahoji yalifunua matukio yaliyoonyesha waziwazi jinsi Yehova alivyoelekeza mambo na jinsi alivyobariki jitihada zilizofanywa ili kukamilisha kwa mafanikio kazi hiyo ya miaka 15. Maelfu walishiriki kihalisi katika kazi ya ujenzi. Wakati mmoja katika mwaka wa 1994, kulikuwa na wafanyakazi 526 mahali pa ujenzi, kutia ndani wajitoleaji wa wakati wote wapatao 350, wafanyakazi wa muda 113, na wengine 63 waliosafiri kila siku kuja kusaidia. Wengi zaidi waliunga mkono kazi hiyo kwa kutoa michango. Wote wanatambua kwamba jambo hilo halingewezekana bila roho ya Yehova.—Zekaria 4:6.
Wale waliotembea wangeweza kuona kwamba kazi iliyofanywa kwenye kituo hicho cha elimu ilitilia mkazo kuendeleza ufundishaji wa kimungu. Wonyesho kwenye mlango wa Shule ya Gileadi katika orofa ya kwanza ya jengo la shule ulikazia historia na mambo mazuri ya zamani ya shule hiyo. Shule ya Gileadi imezoeza zaidi ya wanafunzi 7,000 kwa utumishi wa mishonari tangu darasa lake la kwanza mwaka wa 1943 kwenye majengo yake ya kwanza yaliyokuwa South Lansing, New York. Maonyesho kwenye orofa ya pili ya jengo hilo la shule yaonyesha sehemu mbalimbali za Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Shule ya Waangalizi Wasafirio, ambao hupata mafunzo yao katika kituo hicho. Tangu ianzishwe katika Novemba 1995, shule hiyo ya tawi imetoa mafunzo ya hali ya juu kwa washiriki 360 wa Halmashauri ya Tawi kutoka nchi 106.
Wageni walipokuwa wakitembea, walitambua upesi kwamba katika sehemu nyingi, wangeweza kuona mengi zaidi ya maonyesho tu ya picha. Waliweza kuingia katika idara mbalimbali, wakatembelea ofisi na sehemu nyinginezo za kazi, na kufahamu kindani kazi inayofanywa humo. Sehemu yenye kuvutia zaidi ya matembezi hayo ilikuwa jengo la Utayarishaji wa Kaseti na Vidio. Ni vifaa bora kama nini vinavyotumiwa hapo kuendeleza elimu ya Biblia! Kupitia mfululizo wa maonyesho yenye kuarifu na maonyesho mafupi-mafupi ya vidio, wageni walisaidiwa kuelewa jinsi sauti zinavyorekodiwa na jinsi vidio zinavyotayarishwa. Walijifunza kwa kadiri fulani kuhusu utafiti mwingi ambao hufanywa ili kutayarisha vifaa na mavazi ya drama. Waliona jinsi vifaa vinavyotumiwa jukwaani hutayarishwa kwa gharama kidogo na kwa uangalifu mkubwa kuhusiana na mambo madogo-madogo. Waliona jinsi ambavyo muziki hutumiwa kufanya watu waone kana kwamba wamo kikweli katika mandhari wanayoona. Tangu mwaka wa 1990, Sosaiti imetoa vidio kumi katika lugha 41, zinazokazia vichwa mbalimbali vya Biblia mbali na vidio nyingine ambazo zimetolewa kwa ajili ya wale wenye kutumia Lugha ya Ishara ya Marekani.
Wengi waliotembea walienda katika Maabara ya Picha, Idara ya Uchoraji, Idara ya Habari, ambayo hutoa mazoezi ya kompyuta na kusimamia matumizi yake, Idara ya Utumishi, ambayo husimamia utendaji wa makutaniko 11,242 na waangalizi wasafirio 572, Idara ya Kushughulikia Barua, ambapo maswali 14,000 hushughulikiwa kila mwaka. Walivutiwa na utafiti unaofanyiwa barua zinazopelekwa na hangaiko la kweli linaloonyeshwa wale ambao maswali yao yanathibitisha kwamba wanajitahidi kukabiliana na matatizo mazito.
Wengi wa waliotembea waliendelea kumiminika katika mahali pa Huduma za Tafsiri. Walishangaa kujua kwamba katika miaka mitano iliyopita, lugha 102 zaidi ziliongezwa kwa idadi ya lugha ambazo Sosaiti hutumia kutafsiria vichapo vya Biblia. Asilimia 80 hivi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni kote husoma vichapo vya Sosaiti katika lugha nyinginezo mbali na Kiingereza. Ili kutimiza mahitaji yao, kuna wajitoleaji 1,700 wanaofanya kazi katika idara za tafsiri katika nchi 100. Katika maonyesho, Mnara wa Mlinzi ulionekana katika lugha za Amerika, Ulaya, Asia, na Afrika. Wageni waliona Biblia ya New World Translation katika lugha 31. Walipata kujua kwamba vichapo vya Watch Tower sasa vinapatikana katika lugha 332 na kwamba broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? imechapishwa katika lugha 219 kati ya hizo.
Waliotembelea Idara ya Sheria walionyeshwa nyanja mbalimbali za utendaji zinazohitaji kushughulikiwa kisheria ulimwenguni kote. Kwenye vidio moja waliona kesi halisi iliyosikilizwa mahakamani ambapo wakili mmoja Shahidi alikuwa akitoa hoja juu ya kesi iliyohusu kuwekwa damu mishipani. Pia walipata kujua jambo linalofanywa ili habari njema ziweze kuhubiriwa hadharani. (Wafilipi 1:7) Walionyeshwa pia uamuzi ambao mahakama moja ya wilaya ilifanya Machi mwaka huu, ikiliamuru eneo la Oradell, New Jersey, Marekani, libadili sheria zake ili kuondoa takwa la Mashahidi wa Yehova kuwa na kibali na beji wanapotaka kushiriki katika huduma yao ya hadharani ya kwenda nyumba hadi nyumba katika eneo hilo.
Wageni waliona mambo mengi zaidi. Walichunguza maonyesho ya ujenzi katika Karakana ya Kuundia Vitu, wakatembelea jengo la Kuwekea Dawa Maji Machafu, Jengo la Umeme, Jengo la Kuwekea Dawa ya Kulainisha Maji, na karakana nyingi za kazi ya udumishaji miongoni mwa mambo mengine. Ilikuwa fursa ya pekee.
Programu ya Kuweka Wakfu Yakazia Elimu ya Kimungu
Programu ya kuweka wakfu hasa ilikuwa Jumatano, Mei, 19 kuanzia saa 10:00 alasiri. Umati wa watu 6,929 wenye furaha ulitia ndani wafanyakazi wa makao makuu, wageni wa Sosaiti, na wale 372 waliokusanyika kwenye ofisi ya tawi ya Kanada, ambao waliweza kusikiliza programu hiyo kupitia simu.
Wasikilizaji walifurahi sana kusikia maneno yenye kuchangamsha ya ukaribishaji ya Milton G. Henschel, msimamizi wa Watch Tower Society. Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza na mwenyekiti wa programu hiyo, alifuatisha kumkaribisha William Malenfant. Akitoa hotuba juu ya “Mambo Makuu Katika Ujenzi,” yeye aliwahoji ndugu watatu waliokuwa na madaraka muhimu katika ukuzi, ubuni, na ujenzi wa Kituo cha Elimu cha Watchtower. Wakati wa mahojiano hayo, ilisemwa kwamba wakati wa ujenzi wenyewe, wafanyakazi zaidi ya 8,700 wa muda walikuja kwa gharama zao wenyewe ili kufanya kazi kwenye ujenzi huo. Ufundishaji wa kimungu hufanya iwezekane kuwe na muungano na ukarimu ulioje!
Mfululizo wenye kichwa “Elimu ya Kimungu Ulimwenguni Kote” ukafuata. Ulitolewa na washiriki wanne wa Baraza Linaloongoza. John E. Barr alikazia kwamba elimu ya kimungu hutegemea Neno la Mungu, Biblia, ambayo huwatia Wakristo moyo “[waendelee] kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” (Wakolosai 1:10) Daniel Sydlik alizungumzia jinsi ambavyo elimu ya kimungu imepangwa kitheokrasi kuanzia Yesu Kristo aliye kichwa cha kutaniko la Kikristo, hadi kila mshiriki wa udugu wa ulimwenguni kote. (1 Wakorintho 12:12-27) Sehemu mbili za mwisho za mfululizo huo, ambazo zilitolewa na Gerrit Lösch na Carey Barber, zilionyesha jinsi ambavyo elimu ya kimungu huwastahilisha wahudumu wawafikie watu kila mahali na kuwafundisha ili wao pia watembee katika njia ya Mungu.—Isaya 2:1-4; 2 Wakorintho 3:5.
Ili kuwafahamisha wasikilizaji juu ya shule mbalimbali zilizoko katika kituo hicho cha elimu, wafunzi na wengine wanaohusika na utendaji wa shule hizo walikuwa na mazungumzo na pia wakahojiwa. Daraka la kila shule la kutekeleza programu ya elimu ya kimungu ulimwenguni kote lilionyeshwa. Ilitajwa kwamba Shule ya Gileadi hukazia kujifunza kila kitabu cha Biblia, historia ya kisasa ya watu wa Yehova, na matayarisho kwa ajili ya utumishi wa mishonari. Shule ya tawi huhusisha uchunguzi wa hali ya juu na wenye mambo mengi kuhusu nyanja nyingi za utendaji unaohusisha washiriki wa Halmashauri ya Tawi. Shule ya Waangalizi Wasafirio imekusudiwa kutimiza mahitaji ya ndugu wasafirio na pia kuwaandaa kutoa msaada wa kiroho ambao hasa utayanufaisha makutaniko.
Ili kumalizia programu hiyo nzuri, Lloyd Barry wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa “Kujenga na Muumba Wetu Mtukufu.” Alitaja kwamba Muumba, Yehova, hufurahia uumbaji wake wote naye hutualika tufurahi pamoja naye. (Isaya 65:18) Kwa kuwa “yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu,” Yehova Mungu hupewa sifa zote kwa ujenzi huo wote. (Waebrania 3:4) Baada ya kueleza mambo hayo, msemaji alitoa sala ya kutoka moyoni, akikiweka wakfu kwa Yehova, Muumba wetu Mtukufu, Kituo cha Elimu cha Watchtower.a
Yaelekea kwamba sherehe hizo za juma zima zitakumbukwa kwa muda mrefu na wale waliohudhuria. Kwa nini usipange kukitembelea Kituo cha Elimu cha Watchtower? Tuna hakika kwamba utatiwa moyo ukikitembelea kituo hiki katika jitihada zako za kujifunza mengi zaidi juu ya Muumba wetu mwenye upendo na kuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu.
[Maelezo ya Chini]
a Ndugu Barry alimaliza mwendo wake wa kidunia kwa uaminifu Julai 2, 1999. Ona Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1999, ukurasa wa 16.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Ukumbi ukiwa umejaa pomoni na wasikilizaji wa ziada wakiwa katika chumba cha kulia
[Picha katika ukurasa wa 10]
Matembezi yalikuwa sehemu yenye kufurahisha sana