‘Vuka Uende Makedonia Ukasaidie’
1 Wengi wetu twafahamu maneno yaliyonukuliwa juu na hali zinazoyazunguka. (Mdo. 16:6-10) Paulo na Barnaba walipenda watu. Utayari wao wa kujitoa wenyewe ulikuwa dhahiri kwa matendo yao. Twaona utayari huohuo miongoni mwa watumishi wa Yehova leo. (Zab. 110:3) Wengi wamehamia makutaniko ili wasaidie kuhubiri maeneo yasiyohubiriwa mara nyingi na wawe chanzo cha kitia moyo. Kama Paulo na Barnaba, wale ambao wamefanya hivyo wamebarikiwa kwelikweli.
2 Hatupaswi kufikiria kwamba kuhamia kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa ni kwa nchi nyingine peke yazo. Tungependa kutia moyo roho hii pia katika eneo letu. Pamoja na kuwa na ndugu na mapainia waliowekwa rasmi wanaofikiria juu ya jambo hili, tuna mahitaji pia ya familia na dada waliokomaa katika makutaniko mengine. Wote waweza kuunga mkono kutaniko na kusaidia kuhubiri eneo hilo.
3 Mtazamo unaofaa ni wa maana katika kuamua kuhamia kutumikia palipo na uhitaji mkubwa. Kuhama kwetu kwapaswa kuwa kwa sababu ya kutaka kusaidia. Ndugu mmoja, pamoja na mke na mtoto wake, ambao wametumia miaka mingi kutumikia katika makutaniko yenye uhitaji wa msaada, alisema hivi: “Usijaribu kugeuza kutaniko lifae mapendezi yako ya kibinafsi,” yeye akasema, “lakini fanya kazi nalo, ukimtegemea Yehova upate kazi, nyumba na kadhalika. Uwe tayari kukubali Anayoandaa.” Madokezo mazuri!
4 Pia kumbuka kwamba katika sehemu nyingi ambapo msaada wahitajiwa, kazi ya kuajiriwa huenda isiwe rahisi kupata, gharama ya nyumba na mahitaji mengine ya lazima huenda yakawa ghali. Lazima mtu afikirie kwa sala kabla ya kuhama. Hesabu gharama. (Luka 14:28) Ni jambo la maana kumgeukia Yehova, ukiwa peke yako au mkiwa familia, kumwomba mwelekezo wake na mwongozo. Na litakuwa jambo la maana kila mshiriki wa familia aunge mkono mpango huo. Je, mko tayari kujidhabihu na kufanya marekebisho katika maisha yenu?
5 Unapaswa kufanya nini ukiamua kuhamia kutaniko jipya? Kwanza pitia yaliyoandikwa katika kitabu Huduma Yetu kurasa 112 na 113. Kisha waweza kumwandikia mwangalizi wa mzunguko atakayepanga orodha ya makutaniko yanayohitaji msaada katika mzunguko huo, akionyesha kama kuna uhitaji wa wazee, watumishi wa huduma, mapainia wa kawaida, familia na kadhalika. Halafu ukitaka kuhamia kutaniko jingine andika barua kwa halmashauri ya utumishi ya kutaniko lako. Kisha, wao wataipeleka kwa mwangalizi wa mzunguko. Ukitaka kuhamia kutaniko lililo nje ya mzunguko wako halmashauri ya utumishi itapelekea Sosaiti barua itakayoipeleka kwa mwangalizi wa mzunguko huo.
6 Huenda wengine wakaweza kuhamia kwa muda mfupi maeneo yaliyo na uhitaji mkubwa wakati wa kampeni ya eneo lililo pekee katika miezi ya Julai hadi Septemba. Ikiwa waweza kujitegemeza mwenyewe na kuhamia eneo lililo pekee, tafadhali andikia Ofisi kupitia Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lako. Ndipo Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itaandaa pendekezo na kupelekea Ofisi barua. Tafadhali onyesha katika barua yako ni eneo gani unalotaka kuhubiri. Ikiwa unatoka kwenye sehemu ambapo kweli haijafika, huenda ukataka kwenda huko kwa muda mfupi hali zako zikiruhusu, uhubiri huko. Hata unaweza kupanga na watangazaji kadhaa waandamane nawe. Ndiyo, habari njema lazima ihubiriwe kwanza. (Mk. 13:10) Makutaniko mengine yalianzishwa kwa njia hiyo na kwa baraka za Yehova twataka kufikia watu wengi kabla mwisho haujaja.
7 Wakati uliobaki wa mfumo huu wa zamani unapoisha, ni vizuri kama nini tukisaidia ndugu zetu na watu wenye mioyo yenye kufuatia haki ambao bado wanaona kiu ya kweli. Twatoa sala kwa ajili yenu kuhusu jambo hili la maana. Yehova na aandae mwongozo tufanyapo kazi katika kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Mdo. 4:29.