Sanduku la swali-2
◼ Mafunzo ya Biblia ya familia au mafunzo yanayoongozwa na watoto wadogo wasiobatizwa wa Wakristo walio wakfu yapasa kuripotiwaje?
Kutunza daraka la kufunza watoto njia ya Yehova hutaka wakati na jitihada nyingi upande wa wazazi Wakristo walio wakfu. (Kum. 6:6, 7; Efe. 6:4) Kinachoamua uzito wa daraka walilo nalo wazazi si jambo la kama wakati wote unaohusika utaripotiwa au hautaripotiwa kuwa utumishi wa shambani.
Ripoti ya utumishi wa shambani wa kundi inakusanywa pamoja kuonyesha hasa yale yanayotimizwa katika huduma ya shambani katika kuhubiri habari njema peupe na kuwafunza kweli watu ambao si Mashahidi walio wakfu na kubatizwa. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Hata hivyo, ikiwa mzazi Mkristo aliye wakfu huongoza kwa ukawaida funzo la Biblia la familia, na watoto wasiobatizwa wanahusika, mzazi huyo, awe ni mume au mke anaweza kuripoti jumla isiyozidi saa moja na ziara ya kurudia moja kila juma ambalo funzo limeongozwa na ataripoti funzo moja la Biblia nyumbani kwa mwezi huo. Hivyo ndivyo itakavyokuwa hata kama funzo lenyewe linarefushwa lizidi saa moja kwa safari moja au linaongozwa zaidi ya mara moja kwa juma. Nyakati za ziada za mafunzo au wakati uliotumiwa kufundisha watoto mmoja mmoja hazitatiwa ndani ya ripoti ya utumishi wa shambani, bali zingefaa zionwe kuwa wonyesho wa hamu nyingi ya mzazi ya kutaka kulea watoto katika ujitoaji kimungu.—Mit. 22:6.
Namna gani ikiwa kwa sababu fulani wazazi wanahitaji msaada ili kuingiza sana ile kweli ndani ya mioyo ya watoto wao? Wanaweza kuomba wengine wawape usaidizi unaohitajiwa. Mhubiri mwingine akiombwa atoe usaidizi huo, ingefaa kuzungumza jambo hilo pamoja na mwangalizi-msimamizi au mwangalizi wa utumishi. Ikiwa wazazi ni wapya katika kweli au kwa njia nyingine wanahitaji msaada kwa watoto wao na ingefaa mhubiri mwingine aongoze funzo la Biblia na watoto hao, jambo hilo laweza kufanywa. Ikiwa hivyo, mwenye kuliongoza funzo ataweza kuuhesabu wakati, ziara ya kurudia na funzo lenyewe ikiwa watoto hawajabatizwa.—Ona “Je! Wewe Ndiwe Mshiriki Peke Yako wa Jamaa Uliye Katika Kweli?” katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1980 na “Kuwatendea Vijana Yaliyo Mema” katika toleo hili.—Imechapishwa tena kutoka km-SW 7/83.