Sanduku la Swali
◼ Je, wazazi wote wawili wanaweza kuripoti muda unaotumiwa katika funzo la familia la kawaida?
Ingawa akina baba wana daraka la msingi la kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” wazazi wote wawili hushiriki katika kuwazoeza watoto wao. (Efe. 6:4) Biblia inawahimiza hivi watoto: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Met. 1:8) Funzo la Biblia la familia ni sehemu muhimu ya mazoezi ambayo watoto wanapata kutoka kwa wazazi wao.
Zamani, mzazi aliyeongoza funzo la familia pamoja na watoto ambao hawajabatizwa ndiye tu aliyepaswa kuripoti muda aliotumia, hata ikiwa wazazi wote wawili walishiriki katika mazungumzo hayo. Hata hivyo, sasa kuna rekebisho. Ikiwa wakati wa funzo la familia wazazi wote wawili wanashiriki kuwafundisha watoto, basi wote wawili wanaweza kuripoti muda usiozidi saa moja kwa juma kuwa sehemu ya utumishi wao wa shambani. Bila shaka, kwa kawaida wazazi hutumia zaidi ya saa moja kila juma kuwafundisha watoto wao. Kuwazoeza watoto ni jitihada ya kuendelea inayofanywa na wazazi wote wawili. (Kum. 6:6-9) Hata hivyo, ripoti ya utumishi wa shambani ya kila mwezi inapaswa kuonyesha hasa yale yanayotimizwa shambani. Kwa hiyo, wazazi hawapaswi kuripoti zaidi ya saa moja kila juma, hata ikiwa funzo hilo linazidi saa moja, linaongozwa zaidi ya mara moja kwa juma, au ikiwa wazazi wanajifunza na kila mtoto. Ni mzazi mmoja tu atakayeripoti funzo hilo la Biblia la familia na ziara moja tu ya kurudia kwa kila juma ambalo funzo hilo liliongozwa.