Kufanya Mambo Yanayohitajiwa Sana Ili Kupendeza Mungu
1 Kupendeza Muumba wetu ni jambo la maana kwetu sisi, kwa kuwa “Yehova hupata raha katika wale wanaomwogopa yeye.” (Zab. 147:11, NW) Tamaa yetu ni kupendeza Mungu wa kweli, kama alivyofanya Henoko. (Ebr. 11:5) Kuna mambo yanayohitajiwa sana ambayo lazima tufanye. Hayo yangetia ndani ‘kushika mwiko wa damu,’ kulingana na agizo la kimungu ambalo limeandikwa katika Mdo. 15:28, 29, NW. Kama utakavyokumbuka, jambo hili lilizungumziwa hivi karibuni kwenye “Tumaini Katika Yehova” Mikusanyiko ya Wilaya ya 1987.
2 Kulazwa hospitalini, hasa wakati wa dharura, kunaweza kutokeza hali ambazo zinatahini imani na ushikamanifu wetu sana. Matayarisho yapaswa kufanywa kimbele ili kupunguza matatizo ambayo huenda yakatokea. Mathalani, ni jambo la muhimu kwamba sikuzote ubebe kadi mpya ya kitiba ambayo imejazwa vizuri na kutiwa sahihi. Hatua nyingine ya hadhari ambayo ni ya maana sana ni kuhakikisha kwamba daktari wako amepashwa habari mapema, ikiwa inawezekana, kwamba msimamo wetu kuhusu swali la damu hauwezi kubadilika.
ZUNGUMZA NA DAKTARI WAKO
3 Ripoti zinaonyesha kwamba wengine wamekuwa wazembe kuzungumza na daktari wao mapema, kabla ya dharura kutokea. Ingawa huenda wakawa wamempasha habari daktari wao kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova, walikosa kueleza vizuri msimamo wao kuhusu matumizi ya damu, nao hawakujua kama yeye ataheshimu mapendezi yao. Ikiwa wewe una daktari nawe hujazungumza naye kibinafsi kuhusu mambo haya, unapaswa kufanya hivyo unapomtembelea tena. Ikiwa haionekani kwamba wewe utatembelea daktari wako karibuni, inapendekezwa kwamba ujitahidi kufanya miadi mapema ifaavyo
4 Kwenye “Tumaini Katika Yehova” Mkusanyiko wa Wilaya, madokezo yenye mafaa yalitolewa kuhusu mambo ambayo unapaswa kuzungumza pamoja na daktari wako, pia njia ambayo jambo hili lapaswa kufanywa. Mkazo ulitiwa kwenye uhitaji wa kuonyesha staha kwa cheo cha madaktari, si kuwa wenye kushindana au kuonyesha mwelekeo wa kuwa wakubwa. Kumwendea kwa njia hiyo isiyofaa kungekuwa kwenye kukosa hekima na kwa kujishinda mwenyewe. Tukilinganishwa na daktari wetu, huenda tukawa wastadi katika Neno la Mungu, lakini tunapaswa kumpa heshima anayostahili akiwa stadi katika mambo ya kitiba. (1 Pet. 2:17) Tafadhali msizungumze mambo ya ulaji unaofaa na matibabu mengine yasiyo ya kitiba pamoja na madaktari wa kitiba kuhusiana na msimamo wetu juu ya damu. Maoni yako ya kibinafsi kuhusu mambo hayo huenda yakasababisha wakose kuona uhakika wa kwamba msimamo wako kuhusu matumizi ya damu kwa msingi ni wa Kimaandiko.
MAMBO YA KUSEMA
5 Unapotembelea daktari wako wakati ujao, mwambie kwamba una jambo fupi lakini la maana sana la kuzungumza pamoja naye kabla ya kuzungumza sababu yo yote ya kitiba ya kuzuru kwako. Kisha zungumzia mambo manane yaliyoonyeshwa kwenye “Tumaini Katika Yehova” mkusanyiko: (1) Unathamini ustadi wake na uhusiano mzuri wako pamoja naye akiwa daktari wako. (2) Una sadikisho kubwa ambalo anapaswa kujua. (3) Kwa sababu za kidini huwezi kamwe kutiwa damu mishipani, hata wakati wa dharura. (4) Unatambua kwamba huenda hili ukatatanisha mambo, huwezi kubadili msimamo huu wa adili. Unatumaini atatoa utibabu mzuri katika hadi hii, sawa na wanavyofanya madaktari wengine wengi. (5) Hii inahusu pia daktari mwingine ambaye huenda yeye akapanga ili akutunze. (6) Wewe utakubali hatari ya ziada na utatia sahihi fomu za kufunguliwa, nawe unaomba kwamba msimamo wako uandikwe kwenye maandishi ya afisini na hospitalini. (7) Mpe nakala ya makala iliyochapishwa tena kutoka jarida la kitiba katika Amkeni! ya Juni 22, 1982 (Kiingereza), kurasa 25-7. (8) Unathamini nafasi ya kueleza msimamo huu, ambao ni wa maana sana kwako sasa na wakati ujao. Mambo haya manane yatolewe kifupi, katika njia isiyo ya kubishana, yenye uzito, na ya kuonyesha uthamini. Kundi lenu litakuwa limepokea nakala za makala ya kitiba iliyochapishwa tena.
6 Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba jitihada hizi za mapema kuelekea kufanyiza uhusiano mzuri pamoja na madaktari na kuwafahamisha waziwazi msimamo wako ni wenye msaada sana wakati dharura inapotokea. Ikiwa msimamo wako wa uthabiti unatolewa katika njia yenye heshima, inaelekea kwamba daktari wako atakuwa mwenye ufahamu na mwenye ushirikiano. Kutii kwetu amri za Yehova kutapendeza Yeye nako kutatokeza baraka Yake yenye kuendelea.