Kunufaika Kutokana na Utii kwa Agizo la Kimungu
1 Tunavyozidi kutazama upumbavu wa aina ya binadamu isiyotii, ndivyo tunavyozidi kuthamini jinsi lilivyo jambo lenye manufaa kutii agizo la kimungu. Falsafa ya ulimwengu ya tenda lako mwenyewe imesababisha kuteseka kwingi kusikohitajiwa kwa wafuasi wayo. Hata hivyo, Yesu Kristo aliweka kigezo kwa Wakristo. Biblia inaonyesha kwamba sikuzote yeye alitii Baba yake, na kwa sababu ya mwendo huu wenye uaminifu alithawabishwa sana.—Yn. 8:29; Ebr. 5:8; Flp. 2:7-11.
2 “Kunufaika Kutokana na Utii kwa Agizo la Kimungu” ndicho kichwa cha programu ya siku ya kusanyiko la pekee kwa mwaka wa utumishi wa 1989. Madokezo yanayofaa na shauri kwa wakati unaofaa vitatolewa ili kusaidia sisi katika pande mbalimbali za maisha ya Kikristo. Mathalani: Wazazi wanaweza kusaidia watoto wao jinsi gani ili washike ukweli kwa uthabiti na kuufanya uwe wao wenyewe? Kila mshiriki wa jamaa anaweza kufanya nini ili aongeze shangwe yake katika kutumikia Yehova? Kila mshiriki wa kundi anaweza kufanya jambo gani ambalo litamnufaisha yeye binafsi na tengenezo kwa ujumla? Haya ndiyo baadhi ya mambo yatakayozungumziwa katika programu ya siku ya kusanyiko la pekee.
3 Fikira zitaelekezwa kwenye umaana wa kufuata agizo la kimungu tunapokabili mitihani ya utii wa Kikristo kuhusiana na waajiri-kazi na tunaposhughulika na mamlaka zilizo kuu. Kwa sababu ya kuzungukwa na jamii ya watu yenye kuvunja sheria, lazima Wakristo wawe waangalifu ili wadumishe rai ya Kimaandiko kuelekea mamlaka na kuepuka mielekeo isiyofaa ambayo imeenea ulimwenguni leo.
4 Marekebisho fulani yanafanywa katika ratiba ya programu. Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1989, muhtasari wa Mnara wa Mlinzi utaonyeshwa kwenye programu, iwe itafanywa Jumamosi au Jumapili. Hii inamaanisha kwamba makundi ambayo yatakuwa na siku ya kusanyiko la pekee Jumamosi hayataratibu Funzo la Mnara wa Mlinzi au mkutano wa watu wote siku inayofuata. Badala yake wazee watapanga kuwe na kutoa ushuhuda sana kama kikundi.
5 Maelezo yenye uthamini yamesikika kuhusu jinsi siku ya kusanyiko la pekee la kwanza ilivyothibitika kuwa. Wengi walitiwa moyo na kutiwa nguvu kwa agizo zuri la kiroho juu ya funzo la kibinafsi la Biblia na habari zinazohusu maendeleo ya tengenezo.
6 Bila shaka programu ya siku ya kusanyiko la pekee kwa ajili ya mwaka wa utumishi wa 1989 itakuwa yenye manufaa kubwa pia kwetu sisi kadiri tunavyojitahidi kuiga Kielelezo kikuu chetu, Yesu Kristo. Usikose sehemu yoyote yayo. Na tuendelee sote kunufaika kutokana na utii kwa agizo la kimungu.—Ebr. 10:23-25.